RC Mwanri asimamisha likizo watumishi wapambane na Corona

Analogia Malenga

JF-Expert Member
Feb 24, 2012
5,011
9,879
Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri, amesimamisha kwa muda likizo za watumishi wakiwemo wa idara za afya ili waendelee kuunganisha nguvu katika kusaidia jamii kampeni za mapambano dhidi ya virusi vya Covid-19.

Hatua hiyo inalenga kuhakikisha kuwakuwepo na wataalamu wa kutosha katika maeneo yote, ambao wataendelea kutoa elimu ya kujikinga na kudhibiti ugonjwa wa corona usiingie mkoani Tabora.

Mwanri alitoa kauli hiyo jana wilayani Uyui na Nzega wakati wa ziara yake ya kukagua vituo na zahanati zilizoandaliwa kwa washukiwa wa ugonjwa wa corona.

Alisema kipaumbele hivi sasa ni kuhakikisha tahadhari zote zinachukuliwa ili wakazi wa Mkoa wa Tabora waendelee kuwa salama kwa kuzingatia maelekezo ya wataalamu wa afya na viongozi wa kitaifa.

Aidha Mwanri alizitaka halmashauri zote za Mkoa wa Tabora kutumia redio zilizopo na magari ya matangazo kupeleka elimu maeneo mbalimbali ya wananchi kuhusu kujikinga na virusi vya Covid-19.

“Tumieni magari yenye vipaza sauti kupita katika mitaa mbalimbali kutoa elimu ya kujikinga wakati wote…na pia wataalamu nendeni katika redio zote zilizopo mkoani Tabora kupeleka ujumbe ambao utawasaidia wananchi kuepuka kupata maambukizi ya corona,” alisema Mwanri.

Katika hatua nyingine, Mwanri ameziagiza halmashauri zote kuhakikisha magari yote yanayosafirisha abiria ndani na nje ya Mkoa wa Tabora yanapuliziwa dawa kabla ya safari ili kuwakinga abiria na uwezekano wa kupata corona.

MTANZANIA
 
Back
Top Bottom