RAIA MWEMA: Waziri Mkuu avuruga mpango wa Lowassa

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
Mwandishi Wetu

6 Jul 2011

pinda-lowassa.jpg


MAJIBU ya wiki iliyopita ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda bungeni, yanaweza kuwa yamevuruga hoja ya waziri mkuu aliyejiuzulu kwa kashfa ya kampuni ya kufua umeme ya Richmond, Edward Lowassa, inayotafsiriwa kuwa ililenga kuvuruga Serikali ya Rais Jakaya Kikwete.

Mbali ya majibu hayo ya Pinda bungeni, kuna taarifa za kuwa Serikali imejipanga kimkakati kuzima mipango inayoashiria kuivuruga na kuichafua, ikiwa ni pamoja na kufanya maamuzi ambayo yanatokana na hali ya kuwa sasa uvumilivu unakaribia ukomo.

Kiasi cha wiki moja iliyopita, akishangiliwa sana bungeni, Lowassa alisema Serikali ilikuwa inaumwa ugonjwa wa kutokutoa maamuzi na akaitaka ifanye maamuzi hata kama ni mabaya kwa vile alisema ni bora kufanya uamuzi hata kama ni mbaya kuliko kukaa bila kufanya uamuzi.

Lakini katika majibu yake kwa Lowassa, na wengine waliochangia kwenye mjadala wa Hotuba yake ya Bajeti ya mwaka 2011/2012, Waziri Mkuu Pinda alisema si tu Serikali hii ya awamu ya nne iliyopata kufanya maamuzi magumu, bali serikali zote zilizotangulia zimepata kufanya maamuzi magumu, lakini yakizigatia "busara na umakini". Baadhi ya wachunguzi wa mambo, wakitafsiri alichokisema Lowassa, wameiambia Raia Mwema kwamba hoja yake ililenga kuhimili vishindo dhidi ya upepo mbaya unaovuma dhidi yake ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) anakotakiwa, yeye na wenzake kadhaa, kujiuzulu nyadhifa zao.

Uamuzi mgumu
Alisema Pinda kuhusu Serikali kufanya maamuzi magumu: "Maamuzi (magumu) haya ni sehemu ya maisha ya Serikali katika kutekeleza majukumu yake kwa dhana ya uwajibikaji wa pamoja (collective responsibility) kupitia Baraza la Mawaziri. Tunachohitaji ni kuvumiliana. Kuvuta subira, kwani mambo mema hayataki haraka. Tutaamua na tutafanya".

Akianisha maeneo karibu 12 ambayo Serikali imepata kufanya maamuzi, Waziri Mkuu Pinda alisema: "Serikali ya awamu ya nne imekuwa ikifanya maamuzi thabiti na magumu, lakini kwa busara na tahadhari ili kutenda haki na kwa kuzingatia uwezo wa Serikali ili kulinda maslahi ya wananchi kudumisha amani. Katika kufanya maamuzi hayo, Serikali imekuwa makini kuzingatia sheria, kanuni na taratibu.
"Tunatambua kuwa moja ya sifa za kiongozi ni kuweza kufanya maamuzi. Tunayo historia ya viongozi ambao tunawakumbuka kwa maamuzi yao kwa Taifa hili.

"Mfano mzuri, ni Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Wakati wa uongozi wake, moja ya maamuzi magumu ambayo aliyafanya na tunayakumbuka ni kuruhusu nchi yetu kuingia katika harakati za kusaidia nchi za Bara la Afrika ambazo zilikuwa hazijapata uhuru".


Alitaja mifano ya nchi zilizofaidika na uamuzi mgumu wa Mwalimu Nyerere kuwa ni pamoja na Angola, Afrika Kusini, Msumbiji, Namibia na Zimbabwe.
Aliongeza: "Vilevile, tunakumbuka uamuzi mgumu uliofanywa na Baba wa Taifa kuwasaidia ndugu zetu wa Uganda kujikomboa kutoka kwenye Utawala wa Dikteta Iddi Amin. Lakini pia tunakumbuka uamuzi mzito uliofanywa na Baba wa Taifa kuhusu vita dhidi ya walanguzi, uamuzi ambao ulisababisha baadhi ya wafanyabiashara kutupa bidhaa barabarani."

Waziri Mkuu Pinda alisema pia kwamba yapo maeneo mengi ya maamuzi mazito ambayo yamefanywa na uongozi wa awamu ya pili na awamu ya tatu. Akasema awamu ya nne imepata na inafanya mamuzi magumu.

Pinda alisema Serikali ya awamu ya nne imekamilisha miradi yote 27 ya barabara
kuu zilizoanzishwa na Rais mstaafu, Benjamin Mkapa.


"Tumesimamia ujenzi na ukamilishaji wa miradi ya maji nchini, tumefanya maamuzi mazito katika kuwalinda watu wenye ulemavu wa ngozi na tumefanikiwa.


"Tumeondoa mpasuko wa kisiasa Zanzibar, tumefanya maamuzi magumu ya kukubali
kuanzisha Serikali ya Umoja wa Kitaifa katika Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.


"Tumefanya maamuzi ya kupanua na kushamiri kwa Demokrasia Nchini kwa kiwango kikubwa. Nadhani, hii ndilo linasababisha baadhi yetu sasa tunajisahau na kuanza kutumia maamuzi hayo visivyo. Tunahamasisha maandamano huku tukijisifu kwamba huo ndio uzalendo.


"Tumefanya maamuzi ya kuruhusu Uhuru mkubwa wa Vyombo vya Habari. Mtu anaandika anachotaka, na uhuru wa kusema lolote. Hivi karibuni tumefanya uamuzi wa kuruhusu kuanzisha mchakato wa Kupata Katiba Mpya. Hili nalo siyo jambo dogo hata kidogo," alisema Pinda na kuongeza kuwa;

"Lakini pia katika awamu hii ndipo tumefanya maamuzi mazito sana ya kuvunja Baraza la Mawaziri kufuatia kujiuzulu kwa aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa. Hili nalo halikuwa jambo jepesi hata kidogo. Inataka moyo!"


Amani na utulivu

Katika maelezo yake kwa wabunge, Waziri Mkuu Pinda alizungumzia pia haja ya kudumisha amani na utulivu nchini akieleza kwamba kwa wabunge wengi kuzungumzia suala la amani na utulivu ni uthibitisho kuwa nchi inahitaji amani na utulivu.

Alisema Pinda: "Suala la amani na utulivu ni urithi ambao waasisi wa Taifa hili walituachia. Tangu tupate Uhuru suala hili lilikuwa ni ajenda muhimu sana ya Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere ndani na nje ya nchi kila alipokuwa.


"Alisisitiza amani kwa nchi jirani. Alisisitiza amani kwa nchi zote za Bara la Afrika na duniani kote. Msisitizo wake mkubwa ulikuwa, utulivu, amani na maendeleo ya watu kwani alitambua kwenye amani kutakuwa na maendeleo ya watu na kwenye maendeleo ya watu kutakuwa na amani.


"Amani ni mazingira wezeshi ya kusaidia kila mmoja wetu kufanya shughuli zake za kijamii na kiuchumi. Ni dhahiri kwamba bila Amani hatuwezi kuwa na Maendeleo.

Bila amani hatuwezi kuwa na uzalishaji na kwamba bila Amani hatuwezi kuwa na uhuru wa kikatiba wa kuishi. Kwa msingi huo, ni lazima tutumie urithi huu tulioachiwa na Baba wa Taifa kwa kulinda nchi yetu idumu katika amani na utulivu.


"Si busara kuingiza mbegu za kuashiria uvunjifu wa amani katika kizazi cha sasa. Vilevile, ni jukumu letu sote kuendelea kuwakanya baadhi ya viongozi wanaoanza kupanda mbegu mbaya kwa vijana na hasa wa vyuo vya elimu ya juu."


Utawala bora

Katika majumuisho yake ambayo yamechapishwa kwa ukamilifu katika toleo hili,
Waziri Mkuu pia alizungumzia Serikali kufuata mfumo wa utawala bora.


Alisema Pinda: "Kambi ya Upinzani imetoa maelezo kuhusu ukiukwaji wa misingi ya utawala bora umeendelea kukithiri nchini kwa kiasi kikubwa na kwamba TAKUKURU ina uwezo mdogo wa kuchunguza kesi na kufungua mashtaka.


"Niseme tu kwamba, nchi hii inaongozwa kwa utawala wa sheria. Kuna taasisi zimeundwa na zinafanya kazi yake kwa umakini mkubwa na wale wote wanaokiuka sheria wanachukuliwa hatua za kisheria. Kuhusu uwezo wa TAKUKURU, chombo hiki kinafanya kazi kubwa na katika mazingira magumu. Sote tunafahamu ilivyo vigumu kushugulikia masuala ya rushwa kwa kuwa watoaji na wapokeaji wanatumia mbinu mbalimbali na wanafanya biashara hiyo kwa kificho kikubwa. "Pamoja na changamoto zote hizo, katika kipindi cha mwaka 2008 hadi 2010, jumla ya malalamiko 17,752 yalipokewa na si 14,426 kama yalivyotajwa na Mheshimiwa Freeman Mbowe. Na kati ya hayo, malalamiko yaliyohusu rushwa ni 2,682. Kati ya malalamiko hayo, TAKUKURU ilichunguza na kukamilisha majalada 2,973 kwa maana kwamba malalamiko yote yaliyohusu rushwa yalichunguzwa na mengine 291 ya miaka ya nyuma yalifanyiwa kazi pia.

"Aidha, kwa kipindi cha mwaka 2008 hadi 2010, jumla ya kesi zilizoamuliwa na mahakama zilikuwa 382 na kati ya hizo, Jamhuri ilishinda kesi 139 na washtakiwa walifungwa. Kesi zilizoshinda ni asilimia 36.4 na si asilimia 22.2 kama alivyoeleza Mheshimiwa Mbowe.


"Ni vyema ikahafamika pia kwamba sheria haibagui wala kuweka makundi ya walalahoi na vigogo kwenye rushwa na wala hakuna tofauti kati ya rushwa ndogo na rushwa kubwa. Rushwa ni rushwa tu. "Pengine kinachojitokeza ni kwamba rushwa ndogo ushahidi unaweza kupatikana kwa haraka wakati kesi kubwa wakati mwingine, ushahidi wake huchukua muda mrefu, na wakati mwingine huhitaji kuupata ushahidi nje ya nchi na hivyo kesi kuchukua muda mrefu zaidi."

Muungano wa Bara na Visiwani

Akizungumzia hoja za Muungano, Waziri Mkuu Pinda alisema zilijitokeza hoja mbalimbali kuhusiana na Muungano ambao ni kielelezo kikubwa cha mahusiano ya kidugu na ya kijadi ya pande zote mbili.

Alisema Muungano ni mzuri sana na kwamba wananchi wa pande zote mbili wanaishi na kufanya kazi zao bila kuulizana wanakotokea na kwamba inafurahisha sana unapowakuta Watanzania wa Zanzibar wakifanya biashara zao Rukwa, Mbeya, Simanjiro na kwingineko na vivyo hivyo, unawakuta Watanzania Bara wakifanya shughuli zao Micheweni, Kiembesamaki na kwingineko kwa upande wa Zanzibar.


"Hii inathibitisha Muungano huu ni wa wananchi. Nchi kubwa duniani zenye uchumi mkubwa zimeungana na zinaendelea kuongeza nchi nyingine ili kupanua Muungano wao. Sote tumeshuhudia hili kwa kuendelea kuona Umoja wa Ulaya ukiongeza wanachama zaidi. Ninaomba sana tuige mfano wa nchi hizo. Muungano wetu utatusaidia kujiimarisha kiuchumi.


"Kama alivyowahi kusema Mwalimu Nyerere, hakuna atakayeendelea na kupewa sifa kwa kutengana. Ni muhimu kuimarisha Muungano huu. Hizi chokochoko ndogo ndogo zilizoanza kujitokeza ni vyema tukazikemea zisiendelee.


"Serikali imesisitiza sana umuhimu wa viongozi wa pande zote mbili kutembeleana na kubadilishana uzoefu. Binafsi nilifanya ziara Zanzibar mwaka 2009 na kutembelea Mikoa yote na nilijifunza mengi sana. Ninawahakikishia waheshimiwa wabunge kule Zanzibar niliona miradi mingi inatekelezwa kwa kuzingatia kigezo cha value for money". Ili kuendelea kuimarisha Muungano wetu, ninaendelea kusisitiza kuwa kuna kila sababu ya pande zote mbili kuendelea kutembeleana kujifunza zaidi.


"Muungano wowote ule lazima ukumbane na changamoto na majaribu mengi kwa nyakati tofauti. Changamoto hizo inabidi zitatuliwe kwa diplomasia ya aina yake na utulivu wa hali ya juu. Mijadala tunayoiendesha kuhusu Muungano ni vyema iendeshwe bila jazba kwani ninaamini tunaweza tukafikia muafaka kwa kuzungumza bila kunyoosheana vidole," alisema.


Alisisitiza ya kuwa wananchi na viongozi watapata nafasi ya kutoa mawazo yao kuhusu masuala ya Muungano wakati wa mchakato wa maandalizi ya Katiba mpya ambayo ni fursa ya kuboresha na kuimarisha Muungano.


Uwekezaji katika kilimo

Waziri Mkuu Pinda alizungumzia pia uwekezaji mkubwa katika kilimo akisema kwamba azma ya Kilimo Kwanza ina lengo kubwa la kuongeza uzalishaji na tija kwa wakulima wakubwa na wadogo.

Alisema Serikali imelenga pia kuikaribisha sekta binafsi kwenye kilimo kwa lengo la kuongeza thamani ya mazao na kusaidia wakulima wadogo kiteknolojia na masoko ya mazao yao na kwamba programu ya SAGCOT ni moja ya mikakati ya kukuza na kuendeleza kilimo ili kiwe kweli uti wa mgongo wa Taifa.


"Ofisi yangu inaandaa semina kwa ajili ya waheshimiwa wabunge ya kufafanua zaidi kuhusu programu hii na kupata maoni na shauri wenu," alisema.


Nidhamu ya matumizi ya Serikali

Akizungumzia uamuzi wa Serikali kuhusu mapato na nidhamu ya matumizi ya serikali, Waziri Mkuu Pinda, alisema Serikali imeanza kushughulikia ushauri wa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na Kamati za Bunge za Hesabu za Serikali Kuu (PAC), Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) na Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC).

Katika hatua nyingine, aliagiza wizara zote, wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya na wakurugenzi wa halmashauri zote kutekeleza maelekezo yote ya CAG. Ili kudhibiti kwa nguvu zaidi matumizi ya Serikali, Pinda ameagiza CAG mara anapogundua eneo lenye matumizi mabaya ya fedha za umma, apeleke majina ya wabadhirifu hao moja kwa moja kwenye vyombo vya dola badala ya kusubiri hadi taarifa yake iwasilishwe bungeni.

Ameagiza pia wizara na taasisi zote zinazotakiwa kukaguliwa, wahasibu wawe wameweka hesabu zao vizuri ikiwamo kumbukumbu za hesabu na vitabu vya fedha vyote na risiti zote za malipo pamoja na maelezo ya malipo yaliyofanyika wakati Mkaguzi wa Nje kutoka CAG anapopita na sio kuanza kuzitafuta wakati huo.

"Serikali imewakumbusha maafisa wahasibu kuhifadhi kumbukumbu za hesabu za malipo vizuri ili ziwepo tayari wakati wote na sio kuzitafuta wakati ukaguzi unafanyika. Serikali itaendelea kusimamia kikamilifu usimamizi wa mapato na matumizi ya serikali kwa umakini mkubwa," alisema Pinda.

Kupitia upya uamuzi wa bomoa bomoa

Waziri Mkuu alisema bomoa bomoa imekuwa kero kubwa kwa wananchi hasa wanapowekewa alama za "X" kwenye nyumba zao kabla ya barabara kujengwa.

"Serikali itatafakari upya kuhusu mfumo mzuri wa utekelezaji wa suala hili. Hata hivyo, natoa tahadhari kwa wananchi wote kuzingatia sheria za barabara na kuepuka kujenga kwenye hifadhi za barabara. "Matatizo yanayotokana na ubomoaji kama fidia, alama za X na mengineyo yatatazamwa upya katika mwaka huu wa fedha ili kuona njia nzuri na isiyowaumiza wananchi katika utekelezaji," alisema.

Wafugaji kulipwa fidia

Pinda alikumbusha kuwa alipokuwa akifunga Bunge la mwisho la bajeti mwaka jana, Rais Kikwete aliahidi kuwapa kifuta machozi wafugaji walipoteza mifugo yote kutokana na ukame mkali Arusha na hasa Monduli na Longido.
"Napenda kuliarifu Bunge lako kwamba, Serikali imetenga jumla ya sh bilioni 8.7, kama fidia ya kupoteza mifugo. Utaratibu wa kulipa fidia hiyo umekamilika. Ni matarajio kwamba wahusika watapata kifuta machozi chao wakati wowote kuanzia sasa.

Maslahi ya madiwani

Kuhusu maslahi ya madiwani Waziri Mkuu aliahidi serikali kufanya utaratibu maalumu na kueleza uwekezakano wa madiwani kulipwa Sh kati ya 200,000 hadi 300,000 kuanzia mwaka ujao wa fedha.
Lakini mbali na kuwaahidi, alitaka wawe wepesi kusimamia shughuli za maendeleo kwenye kata wanazoongoza na hasa kutembelea miradi ya ujenzi ili kutathimini thamani halisi ya fedha.
 
Kwa kweli dawa ya moto ni moto. Jamaa alidhani huu ni wakati wa kupata credit na kurejesha nuru yake ambayo ilififishwa na matendo yake dhidi ya waliompa dhamana ya uongozi na ambao ilikuwa awarudie tena na kuwaomba wampe ridhaa.

Kuna dhana imejengeka kwamba jamaa alikuwa mfanyakazi hodari na kuutaja mradi wa shule za kata (ambazo hazikuanza na yeye maana zimekuwepo toka wakati wa Mkapa) na mradi wa ziwa victoria (ambao kadhalika ni uasisi wa serikali ya wamu ya tatu tena kwa ufadhili unaotokana na mikataba ya Kikwete akiwa waziri wa Mambo ya Nje) kama vigezo vya utendaji bora. Maamuzi mabaya anayodhani yeye kwamba yana unafuu ni yale ya kuileta ByWater na baadae kuitimua na baadae kuiingiza nchi katika madeni ya kulipa gharama za wakili kuitetea serikali. Ndiyo hayo yaliyogubika utata wa Richmond. Mwalmu alikataa maamuzi ya kukurupuka pale aliposema bora madini yetu yasichimbwe, kuliko kuchimbwa halafu yasinufaishe wananchi. Pinda mapigo haya yanatakiwa yaendelee, ili huyu bwana asipate sehemu ya kupumbazia wananchi wakati bado wana deni naye.
 
Back
Top Bottom