Rai Ya Jenerali

mstahiki

JF-Expert Member
Jul 14, 2007
308
5
Maneno ya J.Ulimwengu
-----------------------------------------------------------------
UKWELI wa vyama vyetu kuwa bandia umedhihirishwa na matendo ya wanasiasa wetu wenyewe. Ukitazama mwenendo wa wanasiasa wa nchi za Magharibi utabaini kwamba uanachama aghalab ni jambo la maisha mazima ya mhusika, kwa maana kwamba kama anajiunga na chama akiwa na umri wa miaka 18 basi mwelekeo ni kwamba atakuwa mwanachama wa chama hicho hadi kufa.

Pasi na shaka, hawakosi wachache ambao wataudhiwa na jambo, watashawishiwa na hali inayojitokeza, watarubuniwa kwa mvuto wa mtu, watahama chama, lakini hawa ni wachache mno, na ni nadra kuwakuta katika ngazi za uongozi.

Viongozi wahamaji huhama na vyama vyao, kwa maana ifuatayo: Chama kimekuwa na mtazamo wa kifalsafa wa aina fulani kwa karne nzima, lakini hali ya kisiasa na kiuchumi imebadilika kiasi kwamba mtazamo uliozoeleka ndani ya chama hicho haukubaliki tena na wala haukiwezeshi chama hicho kushika madaraka. Ili ìkwenda na wakatiî na ili kuchagulika tena, kiongozi (mara nyingi mpya) au kundi la uongozi (jipya vile vile) hujitokeza na kutetea mabadiliko ambayo yanaonekana kama hayakwepeki.

Iwapo wanachama walio wengi hawatashawishika na mwito huo wa uongozi mpya, watawafukuzilia mbali na kuwachagua wapya. Iwapo watashawishika watawaunga mkono, na chama hicho (si viongozi) kitahama kutoka mwelekeo mmoja kwenda kwenye mwelekeo mwingine. Isitoshe, mwelekeo huo mpya mara nyingi hauna tofauti bayana mno na ule wa zamani, na wananchi wa kawaida wataona mambo yanakwenda kama yalivyokuwa tangu zama. Ni wachambuzi tu, na wadaku wengine, ndio wanaobaini kwamba ingawa mlio ni ule ule lakini manju mpya kabadili mdundo.

Hiyo ndiyo hali iliyotokea Uingereza wakati akina Anthony Blair, Gordon Brown, Peter Mandelson na Alastair Campbell wanaingia madarakani, baada ya miaka 18 ya kuishi uhamishoni kisiasa. Mabadiliko yaliyofanywa na viongozi hawa wapya wa “New Labour” yalifuata mlolongo wa ubishi ndani ya chama chao ambao ulikuwa umeendelea tangu enzi za Hugh Gaitskell mwaka 1959, kiini cha ubishi huo kikiwa ni kuendelea ama kutoendelea na kile kilichojulikana kama Kifungu Namba Nne cha katiba ya chama, ambacho kilitaka umiliki wa pamojaí wa mali ya taifa, msimamo uliotokana na nguvu kubwa iliyokuwa imehodhiwa na vyama vya wafanyakazi ndani ya Labour.

Toka enzi za Gaitskell hadi kufikia mabadiliko yaliyofanywa na akina Blair katikati ya miaka ya 1990, ilitokea mivutano ya kila aina, sehemu ya chama ikitaka kufanya mabadiliko makubwa ya kiitikadi ili chama kivutie na kichagulike, huku wengine wakisisitiza kwamba kuchagulika peke yake hakuwezi kukawa sababu ya kuachana na misimamo ya kimsingi. Rejea maneno ya Harold Wilson, mwaka 1964: ìWalikuwa wanataka tufute Kitabu cha Mwanzo (Genesis) kutoka kwenye Biblia".

Inajulikana kwamba mabadiliko yaliyofanywa na akina Blair yalibadilisha sura ya siasa za Uingereza kwa kupunguza makali ya vyama vya wafanyakazi na kukifanya chama cha Labour kisitofautiane sana na mahasimu wao wa Conservative, kiasi kwamba Tony Blair akawa anaitwa “Tory” Blair. Kwa hakika wanasiasa wa Conservative walimtuhumu Blair kwa ëwizi wa sera.í Alichokitaka Blair kikawa, akatwaa madaraka na sera zake madarakani zikawa hazina tofauti kubwa na zile za Conservative, si nyumbani wala katika masuala ya kimataifa (tazama kasheshe la Iraq.)

Mojawapo ya mambo muhimu tunayojifunza katika simulizi hii fupi ni kwamba chama kizima kilikuwa kinaingia katika mabadiliko kwa mjadala miongoni mwa wanachama wake na miongoni mwa viongozi wao. Ingawaje kulikuwa na misigano muhimu ya kiitikadi miongoni mwao, lakini mjadala ulikuwa wa wazi na wa kuambiana ukweli, kadri kila upande ulivyoyaona masuala yaliyokuwa mezani, na kadri hali ilivyobadilika kutoka kipindi kimoja hadi kingine. Wanachama walijua na baadhi wakashiriki katika mjadala, lakini pia umma wa Uingereza uliojali kujua nini kinatendeka ulifuatilia.

Kwetu hali ni tofauti. Nimetaja mifano kama Mwai Kibaki wa Kenya na Bingu wa Mutharika wa Malawi, ambao wote wawili waliingia madarakani wakibebwa na chama fulani, lakini baadaye wakaondoka, kila mmoja kwa staili yake na kujitengenezea utaratibu mwingine wa kichama.

Alipokabiliwa na hali ya kutoelewana baina yake na rais aliyemtangulia, Bakili Muluzi (ambaye alikuwa bado ni mwenyekiti wa chama na ambaye Mutharika alianza kumpeleleza kwa makosa ya ufisadi wakati akiwa madarakani), Mutharika akajitoa katika chama, akaanzisha cha kwake na akaendelea kutawala bila kuwa na mbunge hata mmoja mwanzoni, ingawa alianza kujikusanyia wabunge mmoja baada ya mwingine.

Kilichofuata ni wabunge wa chama cha Muluzi na wasihirika wao kufanya kampeni za kutaka kumshitaki Mutharika bungeni (impeachment), kampeni ambazo zimeshindikana hadi leo kwa sababu Mutharika yu madarakani na anaweza kutumia vyombo vya dola na nyenzo vinazompa kuwapiga dana-dana mahasimu wake. Mpaka leo wanazungushana.

Kwa majirani zetu wa Kenya nako, akina Kibaki, Raila Odinga, Kalonzo Musyoka, Charity Ngilu na wengine wamekuwa wakicheza ëmchezo wa kalinge kanyama,í wakihama vyama ama kuunda vipya ama kutengeneza ushirika na wenzao katika hali inayomfanya hata mfuatiliaji makini ashindwe kujua kwa uhakika nani yuko chama gani.

Hatimaye tunajua kwamba kundi moja kubwa limejitengenezea kile kinachoitwa Muungano wa Chungwa (ODM), jingine linajiita Chama Cha Umoja wa Kitaifa (PNU), na kingine ni Chungwa-Kenya (ODM-K). KANU, ambayo ndiyo ilitawala Kenya hadi mwaka 2002 sasa hivi i ‘hoi bin taaban’, na upo uwezekano wa kweli ikajikuta katika pipa la taka la historia muda si mrefu kutoka sasa, hasa kama uongozi wenyewe ni huu wa bwana mdogo Uhuru Kenyatta.

Iwapo KANU itafifia hadi kupotea haitakuwa ya kwanza kupatwa na mkasa huo, kwani tumekwisha kuona jinis UNIP iliyotawala Zambia tangu Uhuru hadi mwaka 1991 ilivyomomonyoka hadi kuwa kikundi kidogo kisichokuwa na mwelekeo wa kisiasa wala tamaa ya kupata ushindi tena. Hii ni pamoja na ukweli kwamba mwanzilishi wake, Kenneth Kaunda bado yu hai, ni mwenye siha ya kuridhisha na amebaki na heshima yake katika jamii ya Zambia na ya kimataifa.

Nchini Senegal, chama kilichopigania Uhuru, Parti Socialiste du Senegal cha Leopold Sedar Senghor, nacho kimekumbwa na tatizo hilo hilo baada ya kushindwa na Abdoulaye Wade, na hivi sasa kimo katika hatari ya kufutika kabisa. Barani Afrika vyama vya aina hii ni vingi mno, na sababu yake ni ile niliyokwisha kuielezea, kwamba si vyama halisi, kwa sababu havina misingi ya kifalsafa bali ni mipangilio iliyobuniwa kwa ajili ya (kwanza) kupata Uhuru kutoka kwa mkoloni na (pili) kubakia madarakani, hata kwa mbinde, huku wakuu wakigawana madaraka na mapato ya taifa.

Hata baadhi ya majina ya vyama hivi yanatupa fununu ya silika ya vyama vyenyewe, kama vile Rassemblement du Peuple Togolais cha Gnassingbe Eyadema (rassemblement inatafsirika kama ëmkusanyikoí), au Mouvement Populaire de la Revolution, cha Mobutu Sese Seko, movement ikiwa na maana ya ëharakati.í Haishangazi kwamba vyama hivi viwili, vilivyokuwa ni makundi yanayoshabihiana kabisa na kundi lo lote la kigaidi, vilijiwekea misingi ya kuchekesha: kwa mfano, kwamba kila raia wa Zaire au Togo, pamoja na watoto ambao hawajazaliwa bado, alikuwa ni mwanachama!

Rai yangu ya msingi hapa ni kwamba Waafrika tumekubali kuiga mambo ya watu wengine bila kuyaelewa, tukakumbatia dhana za asasi zisizokuwa na uhusiano nasi, na matokeo yake ni kwamba tumekuwa kama tunda lisilokuwa na mti, au mbweko usiokuwa na mbwa. Kwa kushindwa kujenga asasi zinazofanana na utamaduni wetu na zinazozingatia uzoefu wetu kama Waafrika, tunajikebehi wenyewe kwa kutenda mambo yasiyo halisi.

Uzoefu wetu kama Watanzania utatupa mwanga zaidi kuhusu hili.

Itaendelea.
 
Back
Top Bottom