Polisi wapiga stop maandamano ya CUF

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, limezuia maandamano ya Chama cha Wananchi (CUF) yaliyoandaliwa kufanyika leo kwa lengo la kuwasilisha kwa Waziri wa Katiba na Sheria, Celina Kombani, rasimu ya mapendekezo ya Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Hata hivyo, chama hicho kimesisitiza kuwa maandamano hayo yako palepale na yataanzia Buguruni Sheli jijini Dar es Salaam.
Amri ya kuzuia maamndamano hayo, ilitangazwa na Kamanda wa Polisi wa Kanda hiyo, Suleiman Kova jana wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.
Kova alisema wamefikia uamuzi huo baada ya kukutana na viongozi wa CUF ofisini kwake jana na kukubaliana maandamano hayo yasifanyike kwa vile yatavuruga amani.
" Hivyo, mtu yeyote asishiriki maandamano hayo kama yatafanyika kwani yatakuwa ni kinyume cha sheria," alisema.
Alisema kabla ya kukutana na viongozi wa CUF, aliwasiliana na Waziri Kombani kujiridhisha kama anazo taarifa za kuombwa kupokea maandamano hayo, lakini akamjibu kuwa hana taarifa.
Katika barua yake kwa CUF jana, Kova alisema kuwa ofisi yake iliwasiliana na Ofisi ya Waziri Kombani na kuelezwa kuwa waziri huyo hakuwa na habari kuhusiana na maandamano hayo na kwamba hakuwa amejiandaa kuyapokea.
“Katika barua yako ulisema, nanukuu: “Kwa kuwa Waziri Mkuu wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania ameshatangaza kuwa serikali inatafakari juu ya namna gani katiba mpya itaandaliwa au namna nyingine yoyote”. Kwa hiyo hii inaonyesha hakuna upinzani juu ya jambo hilo, hivyo maandamano hayo hayana sababu ya kufanyika ili kuishinikiza serikali,” ilieleza barua ya Kova kwenda kwa Naibu Katibu Mkuu CUF bara Julius Mtatiro.
Kova alisema taarifa za kiintelejensia walizonazo zinaonyesha kuwa maandamano hayo hayataisha kumalizika kwa usalama kwani upo uwezekano wa kutokea uvunjifu wa amani na kwamba wavunjifu wa amani wanaweza kutokea ndani au nje ya maandamano/ mkutano huo.
“Ili kuhakikisha hali ya usalama na amani iliyopo inaendelea na kwa mamlaka niliyopewa chini ya kifungu 43 (1-6) cha sheria za polisi na Polisi wasaidizi sura 32 kama ilivyorekebishwa mwaka 2002, nasitisha maandamano na mkutano huo,” alieleza Kova katika barua hiyo ambayo aliisambaza kwa vyombo vya habari jana jioni na kuongeza:
“Yeyote atakayekiuka maagizo haya, Jeshi la Polisi litawajibika kuchukua hatua kali za kisheria. Endapo hamtaridhika na maamuzi tuliyoyatoa, sheria inawaruhusu kukata rufaa kwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi na si vinginevyo.”
Wakati Kova akisema hivyo, Mtatiro, alisema maandamano yaliyoandaliwa na chama chake leo, yatafanyika kama yalivyopangwa.
Mtatiro alisema kitendo cha polisi kuyazuia, kimelenga kukihujumu chama chake (CUF) na demokrasia.
Mtatiro alisema jana mchana waliitwa na Kamanda huyo ofisini kwake, wakadhani kuwa alikuwa anataka kuwaelekeza namna watakavyowadhibiti watu wao wakati wa maandamano.
Alisema walipofika na kukutana naye, walishangaa kuona anawaeleza juu ya uamuzi wa polisi wa kuzuia maandamano yao kufanyika.
" Hatukukubaliana chochote na Kova kutokana na sababu (za kuzuia maandamano) kuziona kuwa ni za upuuzi,” alisema Mtatiro na kuongeza:
" Tuliachana vizuri (na Kamanda Kova). Hatukumuambia kuwa hatutandamana au tutaandamana."
Alisema barua ya kuiarifu polisi kuhusu maandamano na ile ya kumuomba Kombani kupokea rasimu ya mapendekezo hayo ya Katiba mpya, zilipelekwa Desemba 21, mwaka huu.
Alisema wanashangazwa kuona wakijibiwa na polisi siku moja kabla ya siku waliyopanga kufanya maandamano hayo.
Alisema wanachotaka ni Waziri huyo kupokea rasimu yao ya mapendekezo ya Katiba hiyo na si kutoa tamko lolote.
Alisisitiza kuwa kamwe hawawezi kutii amri hiyo ya polisi kwani wametumia zaidi ya Sh. Milioni 12 kuandaa maandamano hayo na hawako tayari kuona demokrasia ikivunjwa.
" Kwa hiyo, tunasema maandamano yetu yako palepale, kuanzia saa 2.00 asubuhi na yataanzia palepale Buguruni Sheli. Na mimi ndiye nitakayeyaongoza. Kama ni kupigwa risasi niwe wa kwanza kupigwa," alisema Mtatiro.
Alipoulizwa sababu za maandamano hayo kutoongozwa na Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, Mtatiro alisema kiongozi huyo kwa sasa yuko safarini, ingawa hakueleza amesafiri kwenda wapi.
Maandamano hayo yalitangazwa na Profesa Lipumba Ijumaa iliyopita jijini Dar es Salaam kwa waandishi wa habari akisema lengo lake ni kudai katiba hiyo mpya na kuundwa kwa tume huru ya uchaguzi.
Lipumba alisema maandamano hayo yangehusisha wanachama na wasio wanachama wa CUF kuanzia makao makuu ya chama hicho Buguruni hadi katika ofisi za Wizara ya Katiba na Sheria kisha kufuatiwa na mkutano wa hadhara katika Viwanja vya Mnazi Mmoja.
" Kama mnakumbuka, tulianza kupiga kelele kwa muda mwingi kuwa katiba ya nchi ibadilishwe na iundwe tume huru ya uchaguzi, na sasa imezaa matunda kwani hivi sasa viongozi wa dini, wanaharakati wa haki za binadamu, viongozi wa vyama vya siasa, viongozi wastaafu, vyama vya wanafunzi na wafanyakazi pamoja na Watanzania wengine kwa ujumla nao wanazungumzia suala hilo, ni vyema serikali ikaheshimu kilio cha wananchi walio wengi na kuweka mchakato shirikishi wa kupata katiba mpya," alisema Lipumba.
Alisema kwa kuanzia rais kwa kushauriana na wadau wengine ateue tume ya kuratibu mapendekezo ya katiba ambayo itaongozwa na na Mtanzania anayeheshimika nchini, Jaji Mkuu mstaafu, Barnabas Samata, Jaji Mstaafu Robert Kisanga au Profesa Issa Shivji na kuwa katika muda usiozidi miezi 12 watoe ripoti na kuishauri serikali utaratibu utakaotumiwa kuipata katiba itakayokuwa na uhalali wa juu wa kumilikiwa na Watanzania wote.
CHANZO: NIPASHE
 
Back
Top Bottom