Baada ya kuusoma uchambuzi wa mwandishi mahiri wa makala nchini ndugu Mwigamba, nimeona nilete jamvini hiki alichokisema kuhuhiana na waziri wetu mkuu na si mwingine bali ni Mhe. Mizengo Pinda.
Binafsi uchambuzi huu nimeuona ni sahihi kwa kuzingatia virejea vilivyotumiwa na Mwigamba katika makala yake kutoka gazeti la Tanzania Daima (3 Machi, 2010). Kauli za Pinda kweli zinapoteza msimamo wake kufaa kuwatumikia wananchi. Soma hapa chini makala yenyewe na kisha toa maoni yako.
"KAMA nilivyopata kusema huko nyuma, sipendi kushabikia kitu haraka haraka. Hata gazeti ninalolipenda kuliko yote (Tanzania Daima) lilipoanza kutolewa na habari motomoto nilijipa muda wa kuangalia utendaji wake na hatimaye nikaona hili ndilo gazeti hasa linalofaa kusomwa na Watanzania wenye uchungu na nchi yao.
Vivyo hivyo walipoanza wale waliojiita wapambanaji dhidi ya ufisadi, niliwastadi kwanza na hatimaye nikawaeleza kwamba wote ni ‘wasanii'.
Mapema kabla ya hapo nilikuwa nimemstadi yule aliyewahi kupewa majina adhimu kama ‘chaguo la Mungu', ‘tumaini lililorejea', naye hatimaye nikawaeleza kuwa ni ‘msanii'. Na mifano mingine mingi ambayo naamini wasomaji wa muda mrefu wa Kalamu ya Mwigamba wataikumbuka.
Ni kawaida yangu hiyo ambayo ilinifanya nijipe muda kidogo wa kumstadi aliyeteuliwa kushika nafasi ya waziri mkuu baada ya Edward Ngoyay Lowassa kujiuzulu.
Huyu si mwingine, ni Mizengo Kayanza Peter Pinda. Waziri Mkuu anayesadikika kutokuwa fisadi katika enzi hizi za tawala za kifisadi. Binafsi nakubali kwamba sikuwahi na mpaka leo sijawahi kusikia kama Pinda naye ni fisadi. Lakini sikutaka kushabikia alipoteuliwa na kusema taifa limepata waziri mkuu bora eti kwa kuwa tu si fisadi.
Nilipenda nione atalitumikiaje taifa na kwa kuwa yeye si fisadi atautumiaje mwanya huo kulisafisha taifa dhidi ya ufisadi.
Haitoshi kusimama tu pembeni na kusema ‘mimi si mla rushwa na kama nikila rushwa leo Mungu anichukue'. Usipokula rushwa huku ukiwalinda wala rushwa na wewe ni mla rushwa.
Tunaweza kukufananisha na wezi wakuu ambao wakitaka kuiba huwatumia wengine kwenda kuiba ili kama ni kukamatwa wakamatwe wao.
Pinda alianza vizuri kwa kauli (kama ilivyo kawaida ya Serikali ya Awamu ya Nne). Alituahidi kwamba wezi wote (sisi tukajumuisha waliohusika na EPA bila kujali nafasi zao, Richmond, IPTL, TRL, Kiwira, Buzwagi, n.k) kwamba watachukuliwa hatua za kisheria.
Wadanganyika tukadhani huyu anaweza kuwa kama Nyerere ama Sokoine. Hawa walikuwa watu safi. Ilipofika kuwashughulikia wahalifu kama wala rushwa, mafisadi, wahujumu uchumi na kila aina ya watu kama hao, hawakuogopa. Hawakufikiria kwamba "Nikifanya hivi na mimi nitaumbuliwa kwamba mbona wewe pia ulifanya hivi au vile.''
Lakini ikaja kubainika kwamba Pinda si wa vile. Kwa ujumla naweza kumwita mheshimiwa Pinda kuwa ni ‘Mr. Mimi Simo'. Kazi yake ni kujilinda tu na yeye asiitwe fisadi. Ndiyo maana akawahi kujitetea kwamba siku akichukua rushwa Mungu amchukue.
Inasikitisha kuona waziri mkuu anayesifika kwa kuwa mtu safi anakuwa wa kwanza kudai kwamba walioiba fedha kupitia EPA ni watu hatari kiasi kwamba serikali ikiwakamata nchi itayumba.
Halafu wakati huo huo wadanganyika wanatamba kwamba serikali ya Kikwete inapiga vita rushwa ndiyo maana mafisadi wamefikishwa mahakamani, wakitolea mfano wale watuhumiwa wa kesi za EPA. Nawauliza mnaompa sifa hizo rais wenu, mmeona nchi imeyumba?
Kama haijayumba basi eleweni wezi wa EPA hawajafikishwa mahakamani maana waziri mkuu alishasema wakikamatwa hao nchi itayumba. Huwezi kujua, labda tukisema kwamba walioshiriki wizi wa EPA wote wakamatwe tutajikuta baraza zima la mawaziri kwa maana ya mawaziri, waziri mkuu, makamu wa rais na rais, halafu nusu ya wabunge na spika wao, ongeza waziri mkuu mstaafu na rais mstaafu wote watapelekwa mahakamani.
Ni dhahiri basi waliofikishwa mahakamani ni mfano tu wa watuhumiwa lakini watuhumiwa wenyewe wako mitaani.
Hatuhitaji waziri mkuu wa namna hii. Waziri mkuu wa kuogopa nchi kuyumba hatumhitaji kabisa. Unadhani wakati wa Operesheni Wahujumu Uchumi iliyoendeshwa na hayati Moringe Sokoine nchi haikuyumba.
Kwa wale waliokuwa na akili tayari wakati wa operesheni hiyo miaka ya 80 hawakumbuki jinsi bidhaa zilivyoadimika madukani. Kwa sababu nyingi zilitupwa baharini, kwenye maziwa na mito.
Kununua kilo ya sukari, ilimbidi mtu awahi na kupanga jiwe la kumshikia nafasi kwenye foleni ili afanye kwanza shughuli zingine na baadaye akirejea anasimama kwenye nafasi ya jiwe. Lakini hicho kilikuwa kipindi cha mpito na baadaye nchi ikatengemaa.
Kama Sokoine angeogopa nchi kuyumba, uhujumu ungeendelea na wachache wangeendelea kustawi kwa hasara ya wengi kama ilivyo leo kwamba mafisadi wengi wanastawi huku wanyonge wengi wakiendelea kuumia.
Waziri mkuu anayeogopa kusafisha mafisadi amefeli.
Lakini kuna kauli nyingi tu za Pinda ambazo zinazua maswali. Fikiria kwa mfano anaulizwa swali anajibu kwa kusema ‘mimi nadhani kwa pressure hii ya wananchi itafikia mahali itamlazimu tu DPP kuwataja wamiliki wa Kagoda, anakuta mahali watendaji wa chini yake wameboronga anasema, ‘mimi nadhani kuna haja watumishi wa umma kuwatumikia wananchi' ama anasema ‘jamani hammwogopi hata Mungu?'
Mahali ambapo anatakiwa kutoa tamko juu ya jambo fulani la kitaifa tena mara nyingi kaulizwa akiwa bungeni, yeye anasema ‘mimi nadhani'. Nani sasa aje atoe tamko?
Kweli mbunge mmoja akikuita baba wa kufikia atakuwa amekosea? Maana uwaziri mkuu unaonekana kwamba haukuwa nafasi yako wewe uliwekwa tu kuziba nafasi na kuonyesha kwamba ndani ya nyumba kuna mwanaume baada ya baba mwenye nyumba kufariki (kujiuzulu)!
Hata namna Waziri Mkuu Pinda alivyokuwa akitoa taarifa juu ya utekelezaji wa serikali wa maazimio 23 ya Bunge kuhusu kadhia ya Richmond alionekana kabisa kuwa baba wa kufikia ambaye hataki kuleta mabadiliko isije ikaonekana kana kwamba ndiye aliyemuua "baba mwenye nyumba'' ili yeye ashike ubaba.
Nimesukumwa kuandika makala hii na kauli ambazo zimetolewa hivi karibuni na Mheshimiwa Pinda akiwa ziarani mkoani Tabora na kunukuliwa na vyombo vya habari. Kwanza aliripotiwa akiwa Igunga jimboni kwa Rostam Aziz.
Akiwa huko alimmwagia sifa Rostam Aziz na kisha kuwataka wananchi wa Igunga waachane na mambo yanayoendelea bungeni.
Ni kama alikuwa akimpigia debe Rostam Aziz kwamba ni mbunge mzuri na kuwataka wananchi wa Igunga waachane na yanayosemwa bungeni, ni sawa na kuwaambia "nyie mchagueni tu tena, ni mtu safi na yale yanayozungumzwa bungeni juu ya kashfa za ufisadi ni uongo.''
Waziri mkuu unayejua jinsi mbunge unayetembelea jimbo lake alivyochafuka hata kama umegoma kumfikisha mahakamani (pengine ni mmojawapo wa watakaoyumbisha nchi akikamatwa), lakini madhari keshachafuka mbele ya jamii, kwa nini umtetee hadharani?
Kwani Mheshimiwa Pinda angesema tu kwamba nawapongeza wananchi wa Igunga pamoja na mbunge wenu kwa kufanikisha moja, mbili, tatu, kungekuwa na shida gani?
Waziri mkuu alitaka wabunge wanaogombana na Rostam ndani ya Bunge juu ya ufisadi na kufanya vyombo vya habari kila siku viripoti kwamba ‘bifu' la Richmond kati ya Sitta na Rostam halijaisha, wajifikirieje?
Wachukulie kwamba kiongozi wa shughuli za serikali bungeni yuko upande wa watuhumiwa wa ufisadi na si wale wanaopiga vita ufisadi? Na anataka sisi Watanzania tumweleweje? Kwamba pale kwenye hicho kiti cha kufikia ndiyo hivyo tena, hawezi kuwasahau waliomwachia?
Maana kuna kauli nyingine ambayo nimeisikia kwa marafiki zangu maana sikufuatilia Bunge siku ya kuzungumzia Richmond na kuahirisha vikao vya Bunge.
Inasemekana kuna kauli aliitoa Pinda kwamba, "Wenzetu waliojiuzulu kwa kashfa ya Richmond walifanya hivyo kwa kuwajibika tu, na inshallah iko siku watarejea madarakani.'' Kweli sikuisikia kwa masikio yangu kama hakuitamka basi namwomba radhi waziri mkuu mapema kabisa, maana sina uhakika.
Lakini kama aliitamka kweli na baadhi yenu wasomaji mmeisikia, basi nachelea kusema katika mawaziri wakuu wote waliopita, Pinda ni waziri mkuu aliyefeli kuliko wote.
Kumbe hapo kamshikia mwenye nafasi yake aliyekwenda likizo iko siku atarudi ‘inshallah'? Kumbe ndiyo maana hataki ‘ku-act'? Anaogopa kwa sababu yeye anakaimu tu uwaziri mkuu? Huyu anatufaaje?
Halafu kama vile kashtuka, alipofika Urambo jimboni kwa Samuel Sitta (kimsingi ndiye hasimu mkubwa wa Rostam Aziz), akammwagia sifa nyingi na kuwaeleza wananchi wa Urambo kwamba Sitta anafanya kazi nzuri sana (ya kumbana Rostam?) bungeni. Msomaji niliposema huyu ni Mr. Mimi Simo unanielewa sasa? Ni waziri mkuu wa kusema mimi simo bwana (kwenye ugomvi wao).
Anaona kama ugomvi wa Sitta na Rostam (mmoja akiwakilisha wapinga ufisadi na mwingine watuhumiwa wa ufisadi) yeye kama waziri mkuu hana upande wowote. Eti yeyote kati ya hao ni mzuri kwake.
Alipofika kwa Rostam alitaka aonekane yuko naye. Kumbe hata yeye kama kiongozi wa shughuli za serikali bungeni anaona kabisa naonewa!
Akasahau kwamba wakati huo Sitta alimwangalia kwa jicho tofauti. Kwamba kumbe yuko na watuhumiwa wa ufisadi!
Kufika kwa Sitta akamwonyesha kwamba yeye anakubaliana kabisa kwamba mafisadi hawafai na vita dhidi ya ufisadi ni vita takatifu. Hata kama mafisadi ni wabunge wenzetu, mheshimiwa spika washughulikie na kama mjumbe wa halmashauri kuu ya chama tawala pigania wavuliwe nyadhifa zao zote ndani ya chama.
Akasahau wakati huo yule mwingine anamwangaliaje. Huyu ni waziri mkuu wa ajabu. Waziri mkuu rangi mbili hatufai. Tunahitaji waziri mkuu rangi moja.
Akisema anapiga vita ufisadi hatajali nani ni fisadi. Amini usiamini kama wakati ule mawaziri wenzake na Sokoine ama mawaziri wakuu wastaafu wangekuwa wahujumu uchumi wangekiona cha moto.
Alikuwa hatazami usoni anapolitetea taifa. Na alikuwa mtendaji. Akiona jambo linastahili tamko la waziri mkuu hakuwahi kuwalilia watendaji wa chini yake wamkumbuke Mungu ama wawahurumie wananchi wao kama alivyofanya Pinda ziarani katika mkoa mmoja ambapo watendaji waliwanyima wananchi huduma ya maji kwa makusudi ili wayanunue kwao kwa bei kubwa.
Si alitoa tamko ama agizo ambalo lilihitaji utekelezaji bali pia alihakikisha anafuatilia utekelezaji wa agizo lake. Jambo ambalo hata Lowassa alijaribu sana kulifanya.
Sokoine, Salim, Lowassa na wengineo, hawakuwa mawaziri wakuu wa mimi nadhani. Nakumbuka hata Sumaye wanafunzi walipozidi kunyanyaswa na wenye daladala aliwahi kuagiza kama mwenye daladala anaona kupakia wanafunzi kwa shilingi 50 ni hasara, aache biashara hiyo!
Lakini huu uwaziri mkuu wa Pinda una kasoro kubwa. Amefeli na usafi wake wa kutokuwa fisadi haujatusaidia chochote pamoja na juhudi zake zote za kutangaza mali zake na kuitwa waziri mkuu maskini, tunataka kuona nafasi ya uwaziri mkuu ikitumika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo.
Namalizia kwa kukuuliza Pinda, unapomaliza uwaziri mkuu wako, una nini unachojivunia katika miaka mitatu uliyoshikilia nafasi hiyo ambacho wananchi watakukumbuka nacho? Ni kulilia albino bungeni halafu ukawaacha wakaendelea kuuawa? Niishie hapo leo."