Pinda ahusishwa mgogoro wa ardhi Mpanda

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
Sunday, 05 August 2012 01:14


Elias Msuya, Mpanda

WAZIRI Mkuu, Mizengo Pinda ameingizwa katika mgogoro wa ardhi unaotaka vijiji 23 kuhamishwa katika maeneo vilipo, wilayani Mpanda Mkoa wa Katavi, kupisha Mradi wa Jumuiya ya Kuhifadhi na Kusimamia Matumizi ya Rasilimali ya Ubende (Ubende WMA).


Hata hivyo, akijibu tuhuma hizo, Msaidi wa Waziri Mkuu, Charles Kanyanda alisema: “Si kweli kwamba Waziri Mkuu anachochea mgogoro wa ardhi. Kabla ya Ubende kuanza wanavijiji walishirikishwa na walikubali kutenga maeneo yao.

Tatizo pale ni kwamba, jambo hilo limechukua muda mrefu na kumekuwa na ongezeko kubwa la watu.” 

Kayanda alisema kuwa, Waziri Mkuu alishauri pande zote zikutane ili wazungumze upya na kuongeza kuwa, mazungumzo yameshaanza katika Kijiji cha Upingo.


Uchunguzi uliofanywa na Mwananchi Jumapili unaonyesha kuwa, zaidi ya kaya 5,000 zilizoko kwenye vijiji hivyo Mkoa mpya wa Katavi, zinatakiwa kuhama ili kupisha mradi huo.

Pinda ambaye pia ni Mbunge wa Mpanda Mashariki ni mjumbe wa Bodi ya Wadhamini ya Ubende WMA, inayoongozwa na Mwenyekiti wa CCM wilayani Mpanda, Sebastian Kapufi.

Wajumbe wengine ni pamoja na aliyekuwa Mbunge wa Mpanda Magharibi, Abdallah Sumry, aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Rukwa, Anna Lupembe na Ofisa Mstaafu Maliasili, Patrick Mwanakusha.

Jumuiya hiyo iliyoanzishwa mwaka 2005 ikiwa na vijiji 10 ambavyo ni Itenka A na B, Kakese, Kapanda, Kapalamsenga, Matandalani, Mbugani,
Sibwesa na Stalike sasa vimeongezeka na kufikia vijiji 23.

Wanavijiji hao wanalalamika kuwa, Waziri Mkuu na baadhi ya viongozi wilayani humo kutaka kuwapora ardhi yao kwa kuweka mipaka ya mradi huo katika maeneo wanayoishi bila kuwashirikisha.

Wanavijiji
Baadhi ya watu kutoka vijiji hivyo wamelalamika kuwa, Pinda kama mbunge wao na viongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpanda hawakuhamisha wakati kuamua kuchukua maeneo yao kwa ajili ya Mradi huo wa Ubende WMA.

Suala hilo pia liliibuka hivi karibuni katika mikutano iliyofanywa na Taasisi ya Haki Ardhi katika baadhi ya vijiji hivyo. Katika mkutano uliofanyika Kijiji cha Itenka A, baadhi ya wanavijiji walimlaumu Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.

“Mwaka 2010, Waziri Mkuu akihutubia mkutano hapa kijijini alisema Jumuiya ya Ubende. Jina la ubende ni tamu, lakini sasa ni chungu.

Tulishangilia wakati likitambulishwa kwetu hasa waliposema watakuwa wakibadilisha viongozi kila baada ya miaka mitatu, lakini tunashangaa
viongozi hao wamebadilika kuwa miungu watu,” alisema Alex Yumbu.


Naye Peter Fungamwango alisema kwamba iwapo nafasi hizo za Wajumbe wa Bodi ya Ubende WMA ingekuwa ni ya kuchaguliwa kwa kura, basi wasingemchagua tena Pinda.

“Mwaka 2004, viongozi wa wilaya walikuja, wakasema tutenge maeneo ya kufugia, pori la akiba, maeneo ya kilimo na makazi na Waziri Mkuu pia alikuja kuhimiza,” alisema Fungamwango.

Kwa upande wake Nesta Masebu wa kijiji hicho alipinga madai kuwa wanavijiji wanaopinga mradi huo ni wahamiaji.

“Mwaka 2005 walipokuja kuanzisha jumuiya ile, tukaikubali, lakini walipokuja kuweka mipaka hawakutushirikisha kabisa na ndicho tunacholalamika,” anasema Masebu.

Naye Kadami Khamis wa Kijiji cha Mwamkulu alisema kuwa mwaka 2005, halmashauri ya wilaya hiyo ilitambulisha jumuiya hiyo kwa wanavijiji, lakini kabla hawajakaa sawa, walishangaa kuona mipaka imeshawekwa na Katiba ya Jumuiya imeshatungwa, bila kuwashirikisha.

Mwananchi mwingine Charles Mbuli alishangaa kuitwa mgeni katika eneo hilo akieleza kuwa alihamia hapo tangu mwaka 1968.

“Nilikuja hapa kama mvuvi wa samaki mwaka 1968 nikiwa bado kijana, na baada ya jumuiya ya Ubende kuanzishwa, tunaitwa eti wahamiaji,” alisema.


Diwani

Diwani wa Kata ya Kapalamsenga, Joseph Moses alisema kuwa, wakati mradi huo ulipoanzishwa katika eneo hilo wananchi hawakupewa taarifa za kutosha na kwamba sasa wanashangaa kuona kuwa ulikuwa wa kuwataka kuhama.

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya kufuatilia mgogoro huo, Michael Wamalwa alisema malalamiko ya wanavijiji yameshawasilishwa katika ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpanda.

Halmashauri ya Mpanda

Wakati baadhi ya viongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpanda wakiwaita wanavijiji hao kuwa ni wahamiaji waliovamia eneo la hifadhi hiyo, baadhi ya nyaraka za halmashauri zinaonyesha kuwa hawakushirikishwa wakati wa kuweka mipaka ya hifadhi.

Uchunguzi umebaini kuwa, muhtasari wa kikao kilifanyika Mei 17 mwaka huu ulieleza kuwa chanzo cha mgogoro huo ni kutowashirikisha wananchi.

“Chanzo kikuu cha mgogoro huo kwa mujibu wa taarifa za kikao ni ‘wananchi kutoshirikishwa wakati wa kuweka mipaka hiyo. Endapo wananchi watashirikishwa sehemu kubwa ya mgogoro huo itakuwa imetatuliwa,” inaeleza sehemu ya muhtasari huo ambao gazeti hili uliona.

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri

Kwa upande Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Tiberana Justine alisema kuwa, wananchi walikubaliana na mipango ya jumuiya hiyo.

“Tunazo nakala za muhtasari wa vijiji vyote vilivyokubali jumuiya hiyo na ramani pia ipo. Hata hivyo, hatua za mwisho tulikabidhi kwa uongozi wa jumuiya hiyo,” alisema Justine na kuongeza:

“Hata hivyo, maeneo yale yana rutuba nyingi, hivyo kuna wahamiaji wengi kutoka mikoa ya Shinyanga, Mwanza na Tabora wakiwa na fedha nyingi. Hao ndiyo wanaoidhoofisha jumuiya hiyo.”

Alisema kuwa wanavijiji wanaopinga jumuiya ya hifadhi hiyo ni wahamiaji wanaotoka mikoa jirani na wamevamia maeneo yaliyopimwa kwa kupewa na viongozi wa vijiji alishindwa kutoa ushahidi wa maelezo hayo.


“Hatuna ushahidi wa kutosha, ila kwa mfano tulisema watu wasiingie na mifugo, lakini wameingia na sasa tunachukua hatua.


Eneo la Mpanda ni kubwa mno, ni sawa na nchi za Rwanada na Burundi yaani kilometa za mraba 45 sawa na mikoa ya Kilimanjaro na Tanga, ni vigumu mno kuidhibiti.”

Alidai kuwa mgogoro huo ni wa kisiasa hasa kwa kuwa Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo, Sebastian Kapufi ni Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Mpanda na aliwahi kugombea ubunge wilayani lakini hakufanikiwa.

Utata wa Katiba ya jumuiya
Wanavijiji hao walidai kuwa licha ya kutowashirikisha katika kutunga Katiba ya jumuiya hiyo, viongozi wao wanadaiwa kuivunja.

Kwa mfano Ibara ya 20(5) ya katiba hiyo inasema kuwa mwenyekiti wa jumuiya hiyo atafanya kazi kwa miaka mitatu kabla ya kuitisha uchaguzi mwingine, lakini uchunguzi wa gazeti hili umeonyesha kuwa mwenyekiti aliyepo, Sebastian Kapufi hajawahi kuitisha uchaguzi mwingine tangu alipochaguliwa


Utata mwingine umejitokeza kwenye Ibara ya 9 ya Katiba hiyo inaeleza kuwa hata kama kijiji kikijitoa katika jumuiya hiyo, hakitaruhusiwa kukomboa eneo lake.

Alipoulizwa kwa njia ya simu juu ya madai hayo, Kapufi alisema: “Sifanyi kazi kwa jinsi hiyo. Kwa sasa mimi nipo Dar es Salaam kwenye shughuli zangu, panga ratiba uje kuniona.

Aliongeza “Nenda kwenye ‘reliable sources’, (vyanzo sahihi) utapata taarifa, kachunguze uhakikishe watakuambia… Unajua ninyi waandishi wa habari huwa hamjali, mnachojua ninyi ni kuuza magazeti tu, siyo usahihi wa taarifa, hatuendi hivyo…”

Maelezo wa WWF

Kwa upande wake ofisa wa Mfuko wa Kimataifa wa Hifadhi ya Wanyamapori (WWF), Pellage Kauzeni alisema wamepewa jukumu la kusimamia hifadhi hiyo mwaka 2009 baada shirika ya GTZ la Ujerumani na Africare kushindwa.

“Sisi tumepewa jukumu la kusimamia hifadhi hii na Serikali. Tunafanya kazi na Wizara ya Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Maliasili na Utalii na Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira) na tunashuka hadi ngazi za chini. Sisi ni tunaunga mkono juhudi za kutunza mazingira, siyo watekelezaji,” alisema Kauzeni.


Alisema kuwa tangu walipofika wamekuwa wakifanya tathmini ya mipaka iliyowekwa tangu mwaka 2004 na kuhamasisha wananchi kukubali hifadhi hiyo.

Hata hivyo, alilalamikia upinzani mkali waliokumbana nao katika vijiji hivyo na kwamba, wanaoleta upinzani ni wahamiaji.

“Asilimia 75 ya wamavijiji walioko kule ni wahamiaji. Idadi ya watu haiongezeki kwa kuzaliana, bali wahamiaji. Kuna kikundi cha watu wanane wanaopinga juhudi za maendeleo vijiji,” Kagezi alisema na kungeza:
“Tulishamwambia Mkuu wa Mkoa wa Rukwa kuwa, kama sisi ndiyo wenye makosa tutafunga ofisi na kuondoka...”

Maelezo ya wabunge
Mbunge wa Mpanda Magharibi, Ibrahim Kakoso alisema kuwa hoja hiyo alishaifikisha bungeni akipinga hifadhi hiyo.

“Hiyo ‘issue’ (suala) nilishaifikisha bungeni ni ya muda mrefu. Mimi sikubaliani na hifadhi hiyo… Ilianza na kijiji kimoja cha Sibwesa katika jimbo langu, lakini sasa vimeshakuwa vijiji vitano na watu wameongezeka mno. Tulikubaliana kukutana na mkuu wa mkoa na viongozi wa wilaya kujadili kwa sababu vijiji hivyo wanavitambua na hifadhi pia wanaitambua,” alisema Kakoso.

Akizungumzia ushiriki wa Waziri Mkuu Pinda, Kakoso alisema alishamhusisha na walikubaliana kuyazungumza.

“Hata mimi nilishamuuliza Waziri Mkuu kwa nini ameendelea kuwa mjumbe wa bodi wakati wananchi wanamlalamikia, akasema kuwa hapo zamani maeneo hayo hayakuwa na watu. Hata hivyo, alisema tutakutana ili tuangalie maslahi ya wananchi,” alisema Kakoso.

Naye Mbunge wa Mpanda Kati, Said Arfi alisema hakubaliani na mradi wa hifadhi hiyo hasa kwa kuwa ni ya muda mrefu na mambo yamebadilika.

Alitoa mfano kuwa Kata ya Kakese, haikuwamo kwenye hifadhi wakati wa makubaliano mwaka 2005, lakini sasa imeingizwa.


“Suala hili nilishauliza swali bungeni na sasa nimeshaongea na Waziri wa Maliasili na Utalii ameahidi kunipa majibu wakati wa kujadili bajeti ya wizara hiyo,” Arfi alisema. 

Kuhusu Waziri Mkuu Pinda, alisema aliingizwa katika Bodi ya Mradi huo kwa kuwa wakati ule alikuwa Mbunge wa Mpanda Mashariki, hivyo aliingia kwa nafasi hiyo.
 

Hata Mtoto wa Mkulima sasa ni Mbabe wa kuchukua Ardhi za Wananchi? Jamani ni wakati wa kuwapumzisha CCM

Kidogo toka kwenye UONGOZi; Wamelewa na UONGOZI...

Wanachota Mali; Wanabeba Mali... Yaani Madhambi yoyote ni Mali kwao
 
Habari chochezi kwa watu wanaohitaji uchochezi ili siku zisonge!!!
Siku uchochezi utakapokoma watajigundua na kukosa soko la kuuza bange polisi
 
Back
Top Bottom