Mengine yaliyo jiri haya hapa....ukistaajabu ya Mussa!
Uchaguzi wa UWT watawaliwa na rushwa-Nipashe, 22nd October 2012
Na Sharon Sauwa
Rushwa imeendelea kutawala chaguzi za Chama Cha Mapinduzi (CCM), baada ya uchaguzi wa Umoja wa Wanawake wa chama hicho (UWT), kulalamikiwaa kugubikwa na vitendo vya rushwa.
Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa rushwa hiyo ilianza kutolewa kabla ya wajumbe kuwasili mjini Dodoma huku mmoja wa wagombea nafasi ya uenyekiti akiwagawia baadhi ya vigogo wa mikoa Sh. 500,000.
Fedha za rushwa zilikuwa zikitolewa katika nyumba za kulala wageni na katika moja ya nyumba ya kigogo mmoja serikalini siku moja kabla ya uchaguzi.
Rushwa hiyo inadaiwa kutolewa katika nyumba za wageni waliofikia wajumbe hao na pia katika vyoo vya ukumbini kwa mbinu za hali ya juu bila kugundulika.
Habari zinasema kuwa mbali na viongozi wenye ushawishi kupatiwa fedha hizo kabla siku ya uchaguzi, wajumbe wa mkutano huo waligawiwa Shilingi 150,000 kwa nyakati tofauti.
"Unaona hiyo misururu mirefu ya kuingia vyooni, hawa wote hawana nia ya kwenda katika haja ndogo bali wamekwenda kupokea fedha ya chai," alisema mmoja wa wajumbe aliyeonyesha kukerwa na vitendo hivyo juzi ambayo ilikuwa siku ya uchaguzi.
Uchunguzi zaidi umebaini kuwa wajumbe hao walikuwa wakiingia wawili wawili chooni ili kupeana rushwa hizo bila maofisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuwabaini.
Hata hivyo, mmoja wa maofisa wanaodaiwa wa Takukuru alisikika akisema: "Nyie mnaingia wawili wawili vyooni kufanya nini huko, tupo hapa msidhani hatupo."
Aidha, kiwango cha fedha kilikuwa kikibadilika kulingana na nyakati na ugumu za zoezi lenyewe la uchaguzi huku baadhi ya wajumbe waliokuwa wakionekana wagumu kukubali kumchagua mgombea huyo wanadaiwa kupewa dau la juu la Shilingi 500,000.
Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali, Ijumaa jioni, wajumbe walikuwa wakifuatwa katika nyumba za kulala wageni na teksi ili kugawiwa fedha hizo.
"Ijumaa usiku kila mjumbe alipata Shilingi 100,000 na ilipofika na asubuhi (juzi), tulipewa tena Shilingi 50,000 kama pesa ya kunywa chai," alisema mmoja wa wajumbe ambaye alionekana kukerwa na rushwa katika uchaguzi huo.
Pia, mgombea mmoja anadaiwa kubeba wapambe kutoka mikoa ya Dar es Salaam, Morogoro na Pwani na kuwagharamia kwa siku mbili mfululizo kwa kuwapa posho na usafiri.
"Hayo mabasi unayoyaona yamekodiwa na mmoja wa mgombea kuja kumpigia kampeni mkoani hapa," alisema mwanachama mwingine ambaye alikataa kutajwa jina lake gazetini.
Licha ya kupewa fedha hizo, baadhi ya makada wanaomuunga mkono mmoja wa wagombea, walifadhili baadhi ya wagombea kwa kununua vinywaji katika baa mbalimbali za mjini hapa.
"Hizi hapa fedha alizotoa kulipia vinywaji mtakavyokunywa leo," alisikika mmoja wa makada akiwaambia wenzake juzi katika moja ya baa zilizopo karibu na ukumbi uliokuwa ukifanyika uchaguzi huo wa Chuo cha Mipango.
Uchunguzi pia ulibaini kuwepo kwa baadhi ya makada wanaotengeneza mtandao wa urais wa mwaka 2015 mjini hapa ambao walionekana wakihaha kuwashawishi wajumbe wa mkutano huo kumpigia kura mmoja wa wagombea wa mtandao huo katika nafasi za uenyekiti.
Baadhi ya makada ambao wamekuwa wakichukizwa na rushwa, wameonyesha kukata tamaa ya kuomba nafasi za uongozi ndani ya chama kutokana hatua chaguzi kugubikwa na rushwa.
"Mimi sina fedha, kushinda katika uchaguzi itakuwa ni ngumu maana siku hizi kama huna fedha hata kama una sifa huwezi kushinda katika uchaguzi wowote," alisema kada mmoja.
Akizungumza na NIPASHE kwa njia ya simu jana, Kamanda wa Takukuru mkoani Dodoma, Eunice Mmari, alisema hawajamkamata mtu yeyote kuhusiana na rushwa.
Alisema ingawa walikuwa wakipokea taarifa kutoka kwa makada mbalimbali wa CCM kwamba kuna watu walikuwa wakitoa rushwa vyooni, lakini alipokwenda hakuweza kuwaona.
"Mimi mwenyewe nilikuwa hapo ukumbini jana (juzi), na nilimsikia Mama Kilango (mmoja wa wagombea katika nafasi ya uenyekiti wa UWT, Anne Kilango Malecela" akilalamika kuna watu wanatoa rushwa vyooni," alisema Mmari na kuongeza kuwa:
"Niliamua kwenda mwenyewe vyooni, lakini sikufanikiwa kumkuta mtu, hata huko gesti (nyumba ya kulala wageni) tulisikia taarifa kuwa kuna watu wanatoa rushwa katika moja ya vyumba tulipokwenda hatukufanikiwa kumkuta mtu."
Alisema waliweka maofisa 18 katika eneo la Chuo cha Mipango mahali panapofanyika uchaguzi huo, lakini hawakuweza kumkamata mtu hata mmoja.
"Rushwa siku hizi inatolewa kwa teknolojia, wanaweza kuwa wanatumia simu za mkononi labda ni rahisi kuwanasa kama mtu atakwambia sasa anakwenda kupewa rushwa na fulani ili muweke mtego," alisema Mmari.