KIM KARDASH
JF-Expert Member
- Sep 21, 2011
- 5,139
- 1,139
Waziri Mkuu, Mh Pinda kushoto, akiwa na Mama Fatuma Karume kulia. Katikati ni Nahodha wa Yanga, Nadir Haroub 'Cannavaro' nje ya ukumbi wa Bunge, Dodoma leo. |
Na Mahmoud Zubeiry, Dodoma
MABINGWA wa soka Afrika Mashariki na Kati, Yanga SC ya Dar es Salaam asubuhi ya leo wameonyesha Kombe lao ubingwa wa michuano hiyo, maarufu kama Kombe la Kagame katika ukumbi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mjini Dodoma.
Mheshimiwa Spika, Mama Anna Makinda baada ya kumaliza kikao cha asubuhi alianza kutambulisha wageni mbalimbali waliotembelea Bungeni leo na ukumbi wa Bunge uliripuka kwa shangwe nzito, alipofikia kuwatambulisha mabingwa hao wa Kagame.
Mama Anna Makinda, alianza kwa kuwatambulisha viongozi wa Yanga, Wajumbe wa Baraza la Wadhamini, Mama Fatuma Karume, Francis Kifukwe na Mwenyekiti wa klabu hiyo, Yussuf Manji, Makamu wake, Clement Sanga na Wajumbe wengine kabla ya kukiinua kikosi kizima wafalme wa soka kwa nchi 12 barani Afrika.
Wakati wa zoezi hilo, Wabunge ambao ni wapenzi wa Simba, mahasimu wa jadi, wa Yanga, wakiongozwa na Mwenyekiti wa Wekundu hao wa Msimbazi, Alhaj Ismail Aden Rage, walianza kuwabeza wapinzani wao hao, kwa kuwakumbushia kipigo cha mabao 5-0 walichowapa katika mchezo uliopita wa Ligi Kuu.
Lakini hiyo haikuzuia sherehe za Yanga kuendelea hadi nje ya ukumbi wa Bunge, ambako Wabunge na Mawaziri wakiongozwa na Waziri Mkuu, Mheshimiwa Mizengo Pinda walipiga picha na wachezaji, viongozi na Kombe lao hilo.
Wabunge wengine na Mawaziri, ambao ni wapenzi wa Simba wakiwemo Naibu Waziri wa Habari Utamaduni na Michezo, Mh. Amos Makala, Mbunge wa Kinondoni, Iddi Azam na Mbunge wa Kondoa Kusini, Juma Nkamia nao pia walijumuika kupiga picha na Yanga.
Baada ya hapo, wachezaji wa Yanga na viongozi walikwenda kwenye ukumbi mdogo wa Bunge kukutana na Uongozi wa Tawi la klabu hiyo, Bungeni chini ya Mwenyekiti wake, Mohamed Hamisi Misanga uliochaguliwa Julai 31, mwaka huu ambako huko Mama Karume alizindua rasmi tawi hilo.
Yanga, waliotwaa Kombe hilo mara mbili mfululizo sasa, wachezaji wake waliwasili usiku wa jana na baadhi ya viongozi, Wajumbe wa Kamati ya Utendaji, Titus Osoro, Mohamed Bhinda na George Manyama pamoja na Katibu Mkuu, Celestine Mwesigwa na Meneja, Hafidh Suleiman, wakati Mwenyekiti, Yussuf Manji na Makamu wake, Clement Sanga na Wajumbe wengine waliwasili mapema leo.
Kwa upande wa timu, wachezaji walifika pia jana na makocha wasaidizi, Freddy Felix Minziro na Mfaume Athumani Samatta, wakati kocha Mkuu, Mbelgiji Tom Saintfiet alikuja leo pamoja na viongozi hao wakuu na Wajumbe wa Baraza la Wadhamini, Francis Mponjoli Kifukwe na Mama Fatuma Karume.
Yanga ilitwaa Kombe la Kagame kwa mara ya pili mfululizo wiki iliyopita, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kwa kuifunga Azam FC mabao 2-0, ambayo yalitiwa kimiani na Hamisi Kiiza Diego Milito na Said Bahanuzi Spider Man.
Hiyo kwa ujumla ilikuwa mara ya tano mfululizo, Yanga inatwaa Kombe hilo, baada ya awali kuchukua mwaka jana, wakiifunga Simba katika fainali bao 1-0, Uwanja wa Taifa mfungaji Kenneth Asamoah ambaye ametemwa, ingawa siku hiyo Kiiza pia alifunga bao safi, ambalo refa alilikataa.
Yanga ilichukua kwa mara ya kwanza Kombe hilo, mwaka 1975 ikiifunga tena Simba katika fainali, mabao 2-0 wafungaji Sunday Manara Computer na Gibson Sembuli (sasa marehemu) Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
Ikachukua tena mwaka 1993, Uwanja wa Nakivubo, Kampala, Uganda kwa kuifunga SC Villa mabao 2-1, yaliyotiwa kimiani na Said Nassor Mwamba Kizota (sasa marehemu) na Edibily Jonas Lunyamila.
Ilichukua tena mwaka 1999, ikiifunga tena SC Villa, Uwanja wa Nakivubo, kwa penalti 5-3, kufuatia sare ya 1-1 ndani ya dakika 120, Yanga ikisawazisha bao kupitia kwa Lunyamila, baada ya Hassan Mubiru kutangulia kuifungia Villa, siku hiyo Manyika Peter akicheza penalti mbili za Waganda.