Nikimtafakari Jaji Sinde Warioba Simumalizi (5)
Katika sehemu iliyopita niliendelea kutoa ufafanuzi kadiri nilivyomsikiliza na kutafakari yale aliyoeleza Mh. Jaji Warioba. Nilieleza kuwa katika rasimu ya pili ya katiba (ya Jaji Warioba) wananchi walitaka kuwawajibisha wabunge wasiokaa katika majimbo yao, na walitaka kuwawajibisha wakishindwa kuwawakilisha wananchi waliowachagua. Hitaji hili la wananchi liliwekwa katika rasimu ya pili ya katiba ya wananchi (ya Jaji Warioba). Lakini katika rasimu ya katiba pendekezwa (ya Sitta, Chenge na CCM) wameondoa. Badala yake wamewapa madaraka vyama vya siasa, na bunge la JMT kuwawajibisha wabunge wao. Niliel;eza kuwa jambo hili haikubaliki na ni moja ya sababu kubwa kuikataa katiba pendekezwa ya Sitta, Chenge na CCM. Katika sehemu hii ninatoa ufafanuzi kuhusu maoni ya wananchi kuhusu ukomo wa ubunge na mawaziri kutokuwa wabunge. Katika rasimu ya pili ya katiba ya wananchi (ya Jaji Warioba) maoni ya wananchi kuhusu ukomo wa ubunge na mawaziri kutokuwa wabunge yalingizwa katika rasimu ya pili ya katiba (ya Jaji Wariona) lakini yakaondolewa rasimu ya katiba pendekezwa (ya Sitta, Chenge na CCM).
Kadiri ya maoni ya wananchi, walitaka ukomo wa kuwa ubunge uwe vipindi vitatu. Lakini bunge maalumu la Sitta, Chenge na CCM wameondoa kabisa ukomo wa ubunge. Pia wameondoa maoni ya wananchi ya kutaka mawaziri wasiwe wabunge. Kuondolewa kwa maoni ya wananchi kuhusu mawaziri kutokuwa wabunge kuna maana kuwa serikali itaendelea kuwa sehemu ya bunge. Hii ina maana kuwa bunge litashindwa kuisimamia serikali ipasavyo kwa vile wabunge mawaziri wanakuwa na conflict of interest. Na kwa hiyo inadumaza uwajibikaji wa serikali kwa bunge na kwa wananchi pia kwa sababu kinadharia wabunge ni wawakilishi wa wananchi.
Kuondolewa kwa maoni ya wananchi kuhusu mawaziri kutokuwa wabunge, inatoa ujumbe kuwa serikali haitaki kuwajibika kwa wananchi kama ilivyo kwa wabunge kukataa kuwajibika kwa wananchi (kumbuka maoni yao ya kutaka kuwawajibisha wabunge wasiokaa majimboni mwao yameoendolewa katika rasimu ya katiba pendekezwa ya Sitta, Chenge na CCM). Mambo haya mapya ya wananchi kuondolewa katika katiba pendekezwa ni sababu nyingine ya kuikataa katiba hiyo ya Sitta, Chenge na CCM.
Katika sehemu inayofuata nitaendelea kutoa ufafanuzi wa mambo mapya yaliyopendekezwa na wananchi na kuwekwa katika rasimu ya pili ya katiba ya wananchi (ya Jaji Warioba) lakini yakaondolewa katika rasimu ya katiba pendekezwa ya Sitta, Chenge na CCM.
Nikimtafakari Warioba Simumalizi (6)
Katika sehemu iliyopita nilielezea kuwa kadiri ya ufafanuzi wa Jaji Warioba, katika rasimu ya katiba pendekezwa ya Sitta, Chenge na CCM, wameondoa hitaji la wananchi la kuwa na vipindi vitatu vya ukomo wa ubunge. Nilieleza pia kuwa katika rasimu ya katiba pendekezwa ya CCM wameondoa maoni ya wananchi ya kutaka mawaziri wasiwe wabunge. Nilieleza kuwa kuondolewa kwa maoni ya wananchi tafsiri yake ni kuwa wabunge, mawaziri na serikali kwa ujumla hawataki kuwajibika kwa wananchi wanaowaweka madarakani.
Katika sehemu hii ninamtafakari zaidi Warioba kuhusu maoni ya wananchi juu ya mgombea binafsi, juu ya tume huru ya uchaguzi, na kuhusu muungano wa serikali tatu. Katika rasmu ya pili ya katiba ya wananchi (ya Jaji Warioba) maoni ya wananchi kuhusu uwepo wa mgombea binafsi katika ngazi mbalimbali yalizingatiwa na kuingizwa kwenye rasimu ya pili. Katika rasimu hiyo ya pili, mgombea huru anaruhusiwa na halazimiki kuwa mwanachama wa chama cha siasa wala halazimiki kupitishwa na chama cha siasa. Katika rasimu ya katiba pendekezwa ya CCM, mgombea binafsi amewekewa mashariki magumu, ikiwemo hitaji la kupitishwa na chama cha siasa, mashariki ambayo yanaondoa na kuzuia maoni ya wananchi kuhusu uwepo wa mgombea binafsi. Kadiri nilivyoelewa ufafanuzi wa Warioba na ninavyokumbuka ni kuwa tume huru ya uchaguzi imezingatiwa katika rasimu ya katiba pendekezwa ya CCM kama ilivyopendekezwa na tume ya Warioba kwa kuzingatia maoni ya wananchi.
Jambo lingine jipya lililopendekezwa na wananchi na kuzingatiwa na tume ya katiba ya Warioba lakini likondolewa na bunge la katiba la Sitta na Chenge na CCM ni kuwa na nchi moja yenye serikali tatu. Katika rasimu ya katiba pendekezwa ya CCM wameweka serikali 2. Cha ajabu ni kuwa Zanzibar wamepewa mambo mengi kuwa huru ikiwemo kujiunga na jumuiya za kimataifa, lakini kulingana na rasimu ya CCM, ni serikali ya Muungano ndiyo yenye mamlaka kamili. Hata Jumuiya ya Afrika Mashariki kadiri ya rasimu ya CCM, Zanzibar haiwezi kujiunga nayo. Kibaya zaidi, mambo kama ardhi ambayo siyo ya Muungano yameingizwa katika rasimu ya katiba pendekezwa ya CCM. Hii inamaana kuwa serikali ya Muungano itakuwa na jukumu ya kusimamia na kuongelea masuala ya ardhi ya Zanzibar katika jumuiya ya Afrika Mashariki. Na ikumbukwe kuwa kwa Zanzibar kupewa uhuru wa kujiamulia mambo mengi, Tanzania bara ndiyo inabaki kuwa ndiyo serikali ya muungano. Hii inamaana kuwa CCM inauvunja muungano. Kwa lugha rahisi ni kuwa Tanzania bara inavaa koti la muungano. Na kwa kweli siyo koti, sasa imekuwa kanzu. Kwa nini ni kanzu? Imekuwa kanzu kwa sababu pamoja na Zanzibar kupewa kwa kudanganywa mmbo mengi ya kujiamulia, vyanzo vya mapato ya serikali ya muungano vimeainishwa katika rasimu ya CCM kuwa ni ushuru na kodi. Kwa hiyo serikali ya muungano itakuwa na jukumu la kukusanya kodi na ushuru Zanzibar na Tanzania bara. Na wakati huohuo Tanzania bara imevaa kanzu ya Muungano. Hivyo, Zanzibar inakuwa tegemezi kimapato kwa Tanzania bara ili kuendesha serikali ya Zanzibar. Hivyo uhuru inaopewa Zanzibar, unanyang'anywa tena na Tanzania bara (iliyovaa koti la muunganoi) kwa kuondolewa mamlaka ya kukusanya kodi na ushuru kwa kuendesha serikali yake. Katika rasimu ya Warioba, mamlaka za serikali tatu zimetenganishwa na koti la muunganio ambalo Tanzania bara inavaa kwa sasa limevuliwa. CCM, wakaondoa, wakaona waivishe Tanzania bara kanzu ya muungano.
Suala hili la kuondolewa kwa uwezo wa Zanzibar kukusanya kodi na ushuru katika kuendesha serikali ya Zanzibar, linaongeza kero za muungano na linauweka muungano katika hatari ya kuvunjika. Sababu ni kwamba kodi na ushuru ndiyo ilikuwa kero ya kwanza kabisa ya muungano mwaka 1964. Na kero hii iliondolewa kwa kuirudishia Zanzibar mamlaka ya kukusanya kodi na ushuru ili kuendesha serikali yake. Mapendekezo ya CCM, yana maana kuwa Tanganyika iliyovaa koti la muungano inakuwa inaitawala Zanzibar, maana haina mamlaka ya kukusanya kodi na ushuru kuendelesha serikali yake. Suala lingine ni kuwa katika serikali ya muungano, tume ya Warioba ilipendekeza mawaziri na manaibu mawaziri wasiozidi 40, CCM wameweka mawaziri wengi zaidi. Tume ya Warioba ilipendekeza wabunge wa muugano wasiozidi 75, CCM wameweka wabunge zaidi ya 300. Tume ya Warioba ilipendekeza makamu wa raisi watatu. Katika rasimu ya katiba ya CCM kuna makamu ya rais watano. Utaona kuwa gharama za kuendesha serikali ya muungano zimeongezeka kwa sababu ya wingi wa mawaziri, wabunge na makamu wa raisi katika rasimu ya katiba pendekezwa ya CCM, ukilinganisha ka rasimu ya katiba ya wananchi (ya Jaji Warioba).
Kwa ufupi ni kwamba asilimia zaidi ya 80% ya mambo mapya Sita (6) yaliyopendekezwa na wananchi na ambayo hayakuwepo katika katiba ya sasa, lakini yaliwekwa katika rasimu ya pili ya katiba ya wananchi (ya Jaji Warioba) yameondolewa katika katiba pendekezwa ya Sitta, Chenge na CCM. Pia, mapendekezo ya CCM, yameifanya Tanzania bara ivae kanzu ya muungano badala ya koti, na hivyo Tanzania bara itakuwa inaitawala Zanzibar kwa sababu serikali ya Zanzibar itakuwa tegemezi kifedha kwa vile kodi na ushuru vitasimamiwa na serikali ya muungano (Tanzania bara iliyovaa kanzu ya muungano). Hizi ni sababu nyingine za kuikataa rasimu ya katiba pendekezwa ya Sitta, Chenge na CCM. Katika sehemu inayofuata nitaeleza namna jina la Baba wa Taifa, Julius Kambarage Nyerere linavyotumika vibaya kuhalalisha katiba pendekezwa ya Sitta, Chenge na Warioba.