NEC: kuizuia kadi ya kupigia kura ya mtu mwingine ni kinyume cha Sheria

Mwakaboko King

JF-Expert Member
Apr 22, 2015
1,099
207
TUME ya Taifa ya Uchaguzi imewatahadharisha watu wanaochukua kadi za kupigia kura za wenzao na kuzizuilia au kubaki nazo kuwa ni kinyume cha Sheria.
Hayo yamesema na Mkurugenzi wa Huduma za Kisheria wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Emmanuel Kawishe wakati akitoa elimu ya mpiga kura katika halmashauri ya manispaa ya Bukoba na Shinyanga hivi karibuni.

Alisema kifungu cha 88 cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi kinasema kuwa ni kosa la jinai kwa mtu kuchukua kadi ya mpiga kura mwingine na kuiziulia, kukataa kuirudisha au kubaki nayo kwa uzembe.

Kawishe alifafanua kuwa kumekuwa na malalamiko kwamba inapofikia karibu na kipindi cha uchaguzi, baadhi ya watu wanachukua kadi za wapiga kura wengine na kuzizuia kinyume cha Sheria.

Hata, hivyo alisema kutokana na kutoa elimu ya mpiga kura kupitia mikutano na kuhudhuria maonesho mbalimbali, baadhi ya wananchi wameelewa umuhimu wa kadi hizo na kuahidi kutoampa mtu kadi zao za kupigia kura.

“Kwa hiyo katika jambo hilo tumekuwa na mrejesho ambo ni chanya lakini tunachowaomba ukiandikishwa tunza kadi yako ya mpigia kura” alisema Bw. Kawishe na kuongeza kuwa, “Jambo la pili mwananchi usikubali mtu achukue kadi yako ya mpigia kura na wala usitumie kadi yako ya mpiga kura kwenye kuchukulia dhamana sehemu yoyote”

“Kwa sababu itakwenda kuchukulia dhamana alafu utashindwa kwenda kupiga kura unapofika wakati wa kupiga kura, mwananchi ajue kwamba kupiga kura ni haki yake”

Alisema mtu aliyejiandikisha asipokwenda kupiga kura anakosa haki ya kuchagua kiongozi anayemtaka na badala yake anawaacha wenzako wakuchagulie kiongozi.

“Unaacha kupiga kura alafu baadaye anakuja kulalamika unasema huyu kiongozi simtaki kumbe kura moja inatosha kubadilisha matokeo ya eneo zima” alisema.

Hivyo aliwasihi wananchi waendelee kuzingatia amani katika uchaguzi na kuwashukuru kwa jinsi uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 na uchaguzi mdogo uliofanyika Januari 22 mwaka huu kwa jinsi ulivyokuwa na amani na utulivu.

”Kwa kweli Watanzania tutambue kuwa amani ni yetu sisi sote na sisi ndio tutakaoilinda hiyo amani tuiweke Tanzania yetu kwanza alafu sisi baadaye” aliwakumbusha Watanzania.

Akijibu swali la mmoja wa wanafunzi wa shule ya Sekondari ya Bukoba aliyehoji anayepoteza kadi ya mpiga kura anachukuliwa hatua gani kumuwajibisha, Kawishe alisema hakuna hatua yoyote inayochukuliwa dhidi yake.

Alifafanua kuwa wale wote wanaopoteza kadi ya mpiga kura wanatakiwa wafike kwenye kituo cha uboreshaji wa daftari la wapiga kura na kujieleza na watapatiwa kadi nyingine.

CHANZO: Raia Mwema.
 
Back
Top Bottom