Hakuna siri tena.Kila kitu kinaonekana. Tume ya Taifa ya Uchaguzi-NEC iko taabani.Taabani kiutendaji.Hadi sasa kuna sintofahamu kuhusu mustakabali wa Kura ya Maoni. Haiko wazi kama itafanyika au la.Yote hayo ni kwa sababu ya NEC. NEC inajikongoja, tena kwa kutambaa, katika kuandikisha wapiga kura. Ndiyo kwanza uandikishwaji kwa njia ya mashine za BVR umefanyika kwa majaribio Kawe na kuzinduliwa Njombe.
Hakukuwa na dalili zozote za kufanikisha uandikishaji huo. Huku Kura ya Maoni ikipangwa kufanyika Aprili 30 mwaka huu, na kampeni za kuipigia chapuo Katiba Inayopendekezwa ikiendelea, NEC haioneshi dalili za kuendana na muda huo. Leo, Waziri wa Katiba na Sheria, Dr.Asha-Rose Migiro ametangaza kugawa rasmi nakala za Katiba Inayopendekezwa. Serikali imetangulia mbele na NEC imebaki nyuma.
NEC inapaswa pia kutoa elimu ya uraia kuhusu Katiba Inayopendekezwa. Muda nao ndiyo unazidi kuyoyoma. Kimahesabu, NEC inapaswa kumaliza uandikishaji na uhakiki wa wapigakura hadi kufikia mwisho wa mwezi huu. Ili, utakapoanza mwezi Aprili elimu ya uraia ianze kutolewa. Kama hiyo haitoshi, NEC ndio watakaosimamia uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu. Hakuna dalili zozote za kuanza matayarisho ya zoezi hilo linalobeba mustakabali wa Tanzania yetu kwa miaka mitano ijayo.
NEC ya Jaji Lubuva imechoka.Iko hoi.Kama yabidi,ifumuliwe na kuundwa upya. Bunge litakaloanza kesho liweke hoja ya dharura mezani kuhusu NEC na Uchaguzi Mkuu wa Oktoba kabla mambo hayajaharibika. NEC isaidiwe kwa kurekebishwa. Ama sivyo,madhara ya kimaumivu ya kisiasa kwa kila mwanademokrasia hayatavutia. Wabunge,kazi ni kwenu!
Mzee Tupatupa wa Lumumba, Dar es Salaam