Naunda Takukuru yangu kupambana na TAKUKURU

Mzito Kabwela

JF-Expert Member
Nov 28, 2009
18,857
7,615
Siandiki uchochezi huu kwa sababu mjomba wangu kashindwa kura za maoni ndani ya CCM, naamini familia yetu haitateseka kwani alichochuma akiwa mbunge aliniambia kinatutosha kula kwa miaka 50 ijayo. Ndiyo maana hata wakati wa kutangaza matokeo mjomba hakulia wala kudondoka kama wengine.

Sema yaliyojitokeza wakati wa mchakato wa kuteuliwa kwenye chama chake ndiyo yaliyonisikitisha, hata ungekuwa wewe yangekuuma. Mara tatu kwa macho yangu nilimuona mjomba pamoja na uzee wake akitimua mbio kukimbia asinaswe na maofisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini waliokuwa wakimfuatilia kila kona.

Wakati mwingine namlaumu mjomba kwa kutokunisikiliza, maana nilimshauri asigombee tena, upepo wa kijijini ulikuwa umegeukia upande wa mpinzani wake ambaye hata wakati akitoa rushwa majini yalimkinga asionwe na vijana wa Dk. Edward Hosea waliokuwa na kazi ya kukamata hata bahasha tupu za kaki, na ole wako wakukute una vijisenti kwenye mkoba wako.

Ni kweli kwamba mjomba hakulia aliposhindwa, lakini mimi nimeshindwa kuyazuia machozi yangu kwa kuwa nahisi sitakuwa na mbwembwe tena mitaani kwa vile nilizoea kujivuna kwa wadhifa wa ‘anko’ wangu, hivyo jambo la kupoteza nafasi ya ubunge lililomtokea ndugu yake maana limeniathiri sana. Nimeshawataarifu baadhi ya marafiki zangu na hapa nilipo naendelea kupokea salamu za pole.

Si vibaya hata wewe msomaji ukanihurumia licha ya kutokupa fungu kwenye marupurupu aliyopewa mjomba kwa kazi yake. Lakini jambo ambalo sitaki watu waniulize ni, KWA NINI MJOMBA WANGU KASHINDWA? Kwa hili niko radhi kurudia wazimu wangu wa zamani wa kuchapana makonde, maana ni swali la kejeli, lililojaa uonevu na linaloumiza sana.

Acheni kunihoji hivyo, maana mtanikumbusha jinsi TAKUKURU walivyokuwa wanamkimbiza mjomba na kumwacha mpinzani wake ‘akishea’ unafiki na wapiga kura ambao walinunuliwa kwa lengo la kumwangusha anko kwenye nafasi yake. Ahaaa…mnasingizia majini yaliwapofusha macho kiasi cha kupita nyuma ya nyumba ya mpinzani na kutowakamata waliokuwa wanakunywa bia za bure!

Ikiwa ndivyo, kuanzia leo natangaza vita na ‘majini’ hayo yaliyowapofusha TAKUKURU kiasi cha kuwafanya wasione makosa na rushwa za wagombea wengine kwenye majimbo na kumwandama mjomba wangu peke yake. Lakini pia naunda takukuru yangu kupambana na TAKUKURU, kwa vile nimegundua kulikuwa na njama za wazi za kuwawezesha baadhi ya wagombea kushinda na wengine kushindwa, siropoki nina ushahidi.

KWANZA, TAKUKURU wa Hosea hawa hawa waliokuwa majimboni nchi nzima walikiri kuwahoji baadhi ya wagombea kwa kutumia umbeya na fununu za mitaani, huku wakivamia kwenye nyumba za wagombea usiku kwa kuongozwana maneno ya kuambiwa. Kibaya zaidi hata walipofika kwenye nyumba hizo na kukuta milango imefungwa hawakusita kuwaita waandishi wa habari na kuwaeleza issues zilizojaa maswali.

“Tulisikia mgombea fulani anagawa pesa kwa wapiga kura nyumbani kwake, tulikwenda, lakini tukakuta mlango umefungwa” Nukuu ya mmoja wa maofisa wa TAKUKURU iliyoandikwa hadi kwenye magazeti. Nyingine “Tulimhoji mgombea ubunge jimbo la ….baada ya kusikia kutoka kwa wasamaria wema kwamba anagawa pesa.” Naomba tutafakari maneno hayo ili tuone kama hawa TAKUKURU hawastahili kuundiwa Takukuru nyingine ya kuwachunguza.

PILI, kwa masikio yangu nimesikia TAKUKURU wakijinasibu kumkamata mgombea mmoja akiwa na bahasha za kaki zikiwa tupu na shilingi zipatazo milioni moja alizodaiwa kutaka kuzitumia kuwahonga wapiga kura wake.

Ok, hilo sikatai kuwa ni jambo zuri, lakini kisheria mtuhumiwa atashitakiwa kwa kosa gani la kukutwa na bahasha, je akiwaonesha duka lake la vifaa vya ofisini maarufu kama stationary na kudai bahasha hizo ni za dukani utetezi wa kisheria utakuwaje?
Najaribu kuhoji kasoro ndogo za matukio ya rushwa ambayo tayari yameshalalamikiwa na wahusika kwamba,yalilenga kuwadhoofisha kisiasa wakati wa mchakato wa kuwapata wawakilishi wa Chama Cha Mapinduzi kuelekea uchaguzi mkuu mwaka huu.

Hivi ni lini katika historia ya TAKUKURU imewahi kutangaza hadharani kuwahoji watuhumiwa wa rushwa kwa kusikia tu kuwa wanajihusisha na rushwa. Mara zote sisi kama waandishi tumekuwa tukiambiwa na TAKUKURU tusubiri upepelezi wa matukio fulani ambayo jamii inahisi kuna mianya ya rushwa! Leo hisia zimekuwa habari kwenye magazeti.

Naweza kuonekana kichaa kwa uchochezi huu, lakini kama maneno ya kuambiwa yanatosha kumtia hatiani au kuwa sababu ya watu kuhojiwa na habari zao kutangazwa, basi TAKUKURU wapitie taarifa za Tume ya Jaji Joseph Warioba kuhusu mianya ya rushwa mahakamani, polisi, hospitali na kwenye taasisi za umma, na za wananchi ambazo walizibainisha na wakapelekewa tena zikiambatanishwa na majina, wawahoji watuhumiwa hao na wawaite waandishi wawaambie fulani na fulani tumewahoji kwa saa mbili kwa sababu tuliambiwa na wananchi kuwa ni wala rushwa pale TRA.

Ikifanyika hivyo, sitakuwa na shida na chombo hiki cha kuzuia rushwa nchini, tofauti na hapo watachunguza mambo yao na chombo changu kitawachunguza wao kuona kama hawakuchukua rushwa kwenye rushwa, kwa lengo la kuwabeba baadhi ya watu kwa maslahi yao.
Najua wahusika mmechukia kwa vile nimeponda juhudi zenu, msinihukumu ila tambueni mimi ni mtanzania ninayelilia haki ya wengi na sitoacha kusema yale yenye maslahi kwa taifa.

Juzi dada yangu Ananilea Nkya Mkurugenzi wa TAMWA, kaka yangu Absalom Kibanda na Muhingo Rweyemamu walinifundisha ujasiri kuhusu hatima ya nchi yetu hasa kwenye masuala haya ya uchaguzi. SASA NINATAMBUA NINA JUKUMU LA KUFANYA KWA TAIFA.

Mwisho nitabiri kwamba, kasi ya rushwa iliyokuwa inatikisa nchi kwenye uchaguzi ndani ya CCM itapungua tutakapokuwa tumeanza kampeni za vyama vingi, sababu MENO YA MBWA HAYATAFUNANI. Mbwembwe za wagombea na hali ya kupakana matope kwenye vyombo vya habari hazitakuwepo, kisa nitawaambieni baadaye, ngoja nimchunguze huyu anayekuja asijekuwa katumwa kunikamata!

GPL
 
Back
Top Bottom