Soma ushuhuda wa wakulima
Wakulima waeleza matatizo
Wakulima kutoka Iringa, Babati, Morogoro na maeneo mbalimbali ya nchi waliozungumza na JAMHURI, wamesema kuwa matrekta hayo ya URSUS yanawasumbua kwa kiasi kikubwa na wanapata shaka iwapo yataweza kufanya kazi kwa miaka miwili na zaidi.
Martine Qamary Ori wa Babati, Manyara, ameliambia JAMHURI kuwa betri mbovu, rimu zimevunjika, breki, wiring, taa zinazimika, cable ya accelerator (chapuzi) imekatika, gearbox inavujisha mafuta.
Athumani Hemed Kazikubwa – Kilindi, amesema pini ya kati ya kwenye kifua cha trekta inachomoka, wakati trekta linalima wanarudishia.
Ibrahim George Voniatis wa Ndanda, Mtwara, anasema kuhusu tairi za mbele: “Inakuwa kama vile unatembelea ‘tyubu’, yaani miba kidogo tu, tunakuta umepata pancha, hilo ndilo tatizo kubwa ambalo naliona.” Amenunua tairi za mbele mpya kwa Sh 400,000 na akaongeza: “Wiring ilikuwa inasumbua ile ya mwanzo ya 4wheel, honi switch inakataa, switch ya taa, switch… tairi hizi ni za Ulaya, hazifai hapa kwetu.”
Peter William Hhayuma, Mwenyekiti wa URSUS Tractors Family, katika maeneo ya Hanang, Karatu, Babati, Mbulu na Itigi, umoja ambao una wanachama 50, anasema: “Hili tatizo la rimu linachangiwa na adjustment ya jembe wakati unalima.
“NDC kwa sababu ni wageni na hiki chombo hawakuwa na wataalamu wa kuendesha haya matrekta, lakini mafundi wa vijijini kwa sababu ni wazoefu wamebaini, kuwa kisu cha nyuma kimenyooka, wamekipindisha kwa kukata shafti, unaipindisha ili iweze kuvuta, usipofanya hivyo unailazimisha kwenda kwenye system (mfumo) ambayo siyo.
“Oil kuvuja, kuna matatizo ya uvujaji na hilo linachangiwa katika hali ya ufungaji, zinakuja kuungwa hapo Dar es Salaam, kuna uzembe katika hatua za ufungaji ninavyoona mimi… ni kwamba chombo chako unapochukua, hata kama ungechukua gari mpya ukaamua kuanza nayo kwa kudhani kuwa ni mpya unakwenda mbele lazima itakuletea shida.
“Kununua nati, bolti… la kwangu, uvujaji ulikuwa kwenye tela nyuma, ilikuwa kumbe kuna seal kule nyuma imekufa, lakini kwa sababu ilikuwa kwenye ‘guarantee’ waliruhusu tuitengeneze.”
Wakulima wanalipa asilimia 10 ya bei ya kununulia trekta hiyo iliyopata msamaha wa kodi na kukabidhiwa trekta, hivyo 75HP inauzwa wastani wa Sh milioni 56 na ya 50HP inauzwa Sh milioni 45. “Mrejesho wake ni miaka 4, unarejesha bila riba, na mwaka wa 5 ndipo unalipa 10%. Kwa kweli huu ni ukombozi kwa mkulima, maana benki nyingine mpaka upeleke hati.
“Katika mpango huu unapeleka barua ya kijiji, kata au mkurugenzi wako anayekufahamu unakopeshwa trekta… kwa hiyo inarahisishia wakulima, baada ya kuona kwamba hili jambo ni zuri, watu tumeamua kuanzisha umoja na kama kuna tatizo mawasiliano yetu mtu anapiga simu unawajulisha huko NDC.
“Yalikuwa na tatizo la matumizi ya mafuta, kwenye system ya mafuta suala la injector kwenye chombo kilichopo kwenye guarantee huwezi kugusa, akatushauri fundi wetu kwamba tufanye adjustment, huyu kijana sasa hivi NDC wamempeleka Mwanza, Mafinga kurekebisha matatizo ya matrekta haya.”
sent from toyota Allex