Waufukweni
JF-Expert Member
- May 16, 2024
- 4,393
- 14,500
Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam linawashikilia watu 15 kwa tuhuma za kukutwa wakitumia namba za SSH 2530 kwenye magari. Kukamatwa kwa watuhumiwa hao ni sehemu ya utekelezaji onyo la kutotumia namba hizo baada ya Septemba Mosi, 2025.
Awali, Jeshi la Polisi Tanzania kupitia Msemaji wake David Misime, lilipiga marufuku matumizi ya namba hizo kwenye magari na kutoa hadi Septemba 1, 2025 wahusika wawe wamezitoa.
Alisema kuwa baadhi ya watu wamekuwa wakibandika namba hizo kwenye magari yao kinyume na sheria, jambo ambalo lilizua sintofahamu kwa watumiaji wengine.
“Mtu yeyote anayebandika namba hizo baada ya kufuatiliwa kwenye mifumo ya usajili, itahesabika hilo ni kosa la kisheria na atakayekamatwa atakuwa na kosa la kuendesha chombo cha moto bila usajili wa namba rasmi,” alisema Misime.
Leo Alhamisi Septemba 4, 2025 na Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro amesema wamefanikiwa kuwatia mbaroni watu 10 huku msako ukiendelea.
Kwa mujibu wa Kifungu cha 13(1) cha Sheria ya Usalama Barabarani, Sura ya 168 Marejeo ya Mwaka 1973 yaliyofanyiwa marekebisho mwaka 2023, mtu yeyote anayeendesha chombo cha moto bila kuwa na usajili rasmi na namba halali za usajili anatenda kosa la jinai.