Tunatarajia kuona ustaarabu mkubwa uwanjani leo Send to a friend Saturday, 05 March 2011 09:58
Kocha wa Simba,Patrick Phiri
LEO ni leo. Ni siku ambayo pambano la watani wa jadi Simba na Yanga ambalo limesubiriwa kwa muda mrefu litafanyika kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Kama kawaida ya mechi hiyo, tunatarajia pambano hilo litakuwa la ushindani mkubwa kwa kuwa kila timu kati ya hizo mbili inataka pointi tatu muhimu ili kujiweka katika mazingira mazuri ya kutwaa mafasi ya juuya ubingwa wa Tanzania Bara.
Pambano hilo ambalo linatarajiwa kuhudhuria na mashabiki 57,558 kulingana na makisio ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) wakati wa kutangaza viingilio vya mchezo huo, linatarajiwa pia kipimo cha ubora wa soka katika nchi yetu.
Viingilio hivyo kama vilivyowekwa na TFF kwa ajili ya kushuhudia pambano hilo vinaonyesha kuwa watu wa rika, hali zote za kimaisha wataweza kujitokeza ili kuona na kuzishangilia timu zao.
Tunaamini kuwa viingilio hivyo vya aina sita, yaani Sh 3,000, 5,000, 7,000, 10,000, 20,000 na 30,000 vitawawezesha mashabiki wengi kujitokeza na kuona mchezo huo.
Tumeambiwa kwamba kuelekea pambano hilo, timu za Simba amao ni wageni na Yanga , wenyeji ziliweka kambi zao maalum kule Zanzibar na Bagamoyo.
Tunaamini kuwa kutokana na maandalizi hayo makubwa yaliyofanywa na timu zote mbili wadau wa mchezo huo wategemee kuona mchezo mzuri kiufundi na ule wa haki kutoka kwa waamuzi ambao wamekabidhiwa jukumu la kusimamia mchezo huo.
Pamoja na mategemeo ya kuona soka ya kiwango cha juu kutoka kwa timu hizo mbili chini ya Sam Timbe (Yanga) na Patrick Phiri wa Simba, hatutaona mchezo wa kukamiana na ambao unaondoa ladha ya soka ambayo inatarajiwa na mashabiki wengi.
Tunamshauri mwamuzi achezesha bila upendeleo, azingatie sheria na kanuni 17 zinazosimamia mchezo huo ili kuepuka kuharibu pambano na kutupiwa lawama.
Kwa upande wa mashabiki, tunatarajia mashabiki wengi wa soka watajitokeza kushuhudia pambano hilo watatimiza wajibu wao ipasavyo, lakini hatutarajii kushuhudia kuona vitendo vyovyote vya kihuni.
Tunasema hivyo kwa sababu matukio ya nyuma ya mechi baina ya timu hizo yamekuwa ya vurugu, uhuni, uharibifu wa mali katika viwanja kiasi cha kuharibu sifa nzuri ya umaarufu wa mchezo huo.
Tunatambua kwamba zinapocheza Simba na Yanga mashabiki wao huonyesha hisia zao za juu za kuzipenda timu zao, lakini vitendo viovu hatuvikubali hata kidogo.
Tunashauri vyombo vya dola, hasa polisi kuwa makini na kazi zao, waache kuwa mashabiki, walinde amani, utulivu katika mchezo na kuwachukulia hatua wale wote wanaobainika kuvuruga mchezo huo kwa njia moja au nyingine.
Tunawasihi mashabiki wote kwamba hatutarajii kuona kutoka kwao lugha za matusi na wavunjifu wowote wa amani na kuwaonya wale wote ambao hupenda kushiriki vitendo hivyo kwa kuwarushia waamuzi chupa za maji au vitu vingine vingine wadhibitiwe, wachukuliwe hatua.
Tunatarajia mashabiki wote watakaojitokeza uwanjani kuwa makini na kujiepusha na uharibifu wa viti au kwenda vyooni na kujisaidia ovyo, kuharibu masinki ya kunawia wakitambua kwamba huo sio ustaarabu wala uungwana.
Tunawashauri mashabiki wanapoingia uwanjani waheshimu taratibu zote kwenye uwanja huo siyo mzuri wa kisasa na kuheshimu kanuni kama zilivyowekwa na TFF na kuachana na mazoea.
Tunawakumbusha TFF katika pambano la leo kuwe na ulinzi mkali nje na ndani ya uwanja ili kuhakikisha usalama wa mashabiki, mali zao na kupunguza vitendo viovu vikiwamo vya wizi na udokozi.
Kwa upande wa wachezaji wa Simba na Yanga, wawe kioo na mfano kwa nidhamu, watoe burudani kwa mashabiki na wakitambua kwamba wanajiuza kwa kuonekana katika televisheni ikiwamo ya Supersport ya Afrika Kusini na Star TV.
Comments
0
#1 hassan 2011-03-05 10:16 Watanzania wengine huwa hawaendi mpirani hadi kwanza wabugie unga au wavute bangi. Kwa mtu mwenye akili zake timamu ni vigumu kung`oa viti vya kukalia au kuingia na chupa za mikojo uwanjani.
Quote