Komeo
JF-Expert Member
- May 3, 2011
- 2,498
- 1,171
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akisalimiana na Mbunge wa viti Maalumu Chadema, Mheshimiwa Upendo Peneza, katika mkutano wa hadhara uliyofanyika Ruangwa Mjini, akiwa kwenye ziara ya kikazi ya siku nne Mkoani Lindi, Julai 12, 2017. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
MBUNGE wa Viti Maalumu kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Upendo Peneza amewaomba wananchi waliombee Taifa liendelee kuwa na amani pamoja na kuwaombea viongozi wa kisiasa, wawe na uvumilivu ili wazidi kusonga mbele kimaendeleo.
Alisema hayo juzi katika mkutano wa hadhara katika Uwanja wa Shule ya Msingi Likangara wilayani Ruangwa wakati wa ziara ya Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa mkoani Lindi.
“Wananchi wa Ruangwa nawatakia maisha mema ili mzidi kusonga mbele, tuombee amani ya nchi yetu na mtuombee viongozi tuwe na uvumilivu wa kisiasa,” alisema mbunge huyo kijana kutoka mkoani Geita, ambaye bungeni anaongoza Chama cha Wabunge Vijana.
Mbali na Peneza, pia mkutano huo ulihudhuriwa na wabunge wengine ambao ni Hassan Masala (Nachingwea – CCM), Zubery Kuchauka (Liwale - CUF), Hassan Kaunje (Lindi Mjini – CCM) na Hamida Abdallah (Viti Maalumu – CCM).
Kwa pamoja, wabunge hao walisema lengo la kushiriki kwenye ziara hiyo ni kuunga mkono jitihada zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano katika kuwaletea wananchi maendeleo.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Godfrey Zambi aliwataka wananchi kuhakikisha wanaendelea kudumisha na kuilinda amani iliyopo kwa sababu ndiyo inayowawezesha kufanya shughuli zao za kimaendeleo.
Alisema licha ya kuwepo kwa matukio machache ya uhalifu yanayojitokeza katika baadhi ya maeneo, vyombo vya ulinzi na usalama kwa kushirikiana na mikoa jirani, limejizatiti kukabiliana na wahalifu wa aina yoyote kwa mtu mmoja mmoja au vikundi.