WAZIRI wa Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, ambaye pia anaomba CCM impitishe kuwa mgombea urais katika Uchaguzi Mkuu baadaye mwaka huu, Bernard Membe amekiri kwamba katika kinyang'anyiro cha urais ndani CCM, mtu anayemnyima usingizi ni Waziri Mkuu Mizengo Pinda.
Alisema kuwa Waziri Mkuu Pinda ni mchapakazi, asiye mbinafsi, mwadilifu, mvumilivu sana mwenye hekima na busara ya hali juu, mwanasheria aliyebobea na ndiye mwalimu aliyemfundisha kazi.
"Wengine wote hawanitishi nitawagonga lakini nikifika kwa Pinda itabidi nipumue kwanza...kwa hiyo mimi na Pinda ni pacha nikishindwa mimi nitamuunga mkono lakini akishindwa naamini ataniunga mkono, ndio maana hata wakati nakuja huku nimewasiliana naye akanieleza nenda na amenisaidia nimepata wadhamini wa kutosha," alisema.
Membe aliwaasa baadhi ya wanaCCM kuacha kuwashangilia kila mgombea anayepita kuomba udhamini kwa kuwa si wote wana sifa kwani wenye sifa stahiki ni yeye na Waziri Mkuu Pinda.
Chanzo: Habari Leo