MWENYEKITI wa chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia, amezidi kuwasha moto mkoani Mtwara, baada ya kuwataka wananchi wa mkoa huo kuichukia kwa vitendo CCM.
Alisema kuwa hata kama CCM bado wana nia ya kuendelea kutawala nchi, katika kipindi hiki wananchi hawana sababu ya kuendelea kukiunga mkono kwa kuwa kimekuwa chanzo cha kudorora kwa uchumi wao.
Mbatia aliyasema hayo mjini Tandahimba mkoani Mtwara juzi wakati akihutubia mkutano wa hadhara katika moja ya mikutano yake ya kukijenga chama mkoani hapa.
CCM siyo chama cha kucheka nacho, lazima muonyeshe chuki za waziwazi, lazima sasa muwaambie CCM basi kwa sababu kimeshindwa kutimiza wajibu wake.
Nawaambieni ukiona kitu kinakuudhi kama CCM, kemea, kama ukishindwa kukemea basi chukia, onyesheni kwa dhati kwamba mnaichukia. Unaweza kuwadanganya watu wachache kwa wakati wote lakini kamwe huwezi kuwadanganya watu wote kwa wakati wote, alisema Mbatia.
Kwa mujibu wa Mbatia, siku ya mwisho Mungu atawahukumu wanadamu kutokana na matendo yao waliyotenda duniani na kwamba hivyo hivyo atawahukumu Watanzania kwa kuendelea kuiunga mkono CCM wakati haina sifa ya kuendelea kuwa madarakani.
Kuanzia sasa CCM ijue kwamba tuko tayari kuishtaki kwa Mungu kutokana na matendo yake na kama hatatusikia, basi tuko tayari kwa mapambano hadi tutakapopata haki zetu, alisema.
Katika hatua nyingine, aliitaka serikali itamke wazi kuwa imeshindwa kuwatafutia soko la korosho wakulima wa Mtwara kwa kuwa haiwezekani kila mwaka wakulima hao wanapata hasara wakati zao hilo ndilo wanalolitegemea.
Naye Katibu Mwenezi wa chama hicho ambaye pia ni Mbunge wa Kasulu Mjini, Moses Machali, aliwashangaa wakazi wa Tandahimba kuwa maskini wakati hawana sababu ya kuwa katika hali hiyo.
JamiiForums uses cookies to help personalise content, tailor your experience and to keep you logged in if you register.
By continuing to use this site, you are consenting to our use of cookies.