Mazingile mwanambiji yanayomkabili Warioba

Kakke

JF-Expert Member
Dec 4, 2010
1,883
1,482
[h=1][/h]Posted on May 10, 2012 by zanzibaryetu
Mwenyekiti wa Tume ya Katiba, Jaji Joseph Warioba

Ahmed Rajab
TUME ya Katiba, chini ya uwenyekiti wa Jaji Joseph Warioba, imekwishaanza kujipanga na kujipangia namna itavyokuwa inafanya kazi. Kwa mujibu wa sheria ya kuundwa kwa Tume hiyo kazi yake kubwa itakuwa ni kupita kila pembe ya Tanzania kwa madhumuni ya kukusanya maoni ya wananchi kuhusu Katiba mpya ya taifa, kuyachambua maoni hayo na kuyaratibu.
Hadi sasa hatujui ni mwongozo gani utakaofuatwa na Tume hiyo katika kuendesha shughuli zake. Nielewavyo ni kwamba kwa sasa wajumbe wa Tume wanaipima hali ya mambo ilivyo nchini kuhusu mchakato mzima wa Katiba mpya.
Mengi bado hayajulikani kuhusu namna Tume hiyo itakavyofanya kazi zake lakini nafikiri kwamba kufikia mwisho wa wiki au mwanzoni mwa wiki ijayo Warioba ataweza kutueleza jinsi Tume yake itakavyoanza kuendesha shughuli zake.
Jambo la kwanza la kutiwa maanani ni kwamba itakuwa muhali kwa wajumbe wote wa Tume kufuatana pamoja kwenda kila mahala. Watabidi wagawane sehemu watazokwenda; hawa wende huku na wengine wende kwengine. Vikundi vya Tume vitakuwa vya mchanganyiko wa watu kutoka Bara na wale wa kutoka Visiwani.
Kwa ufupi, Tume ya Katiba ina kazi mbili: mosi, kushauriana na wananchi na kujua wanasema nini kuhusu Katiba na pili, kuyatathmini maoni ya wananchi na kutoa mapendekezo.
Juu juu kazi hiyo inaonyesha kuwa ni rahisi na isiyokuwa na utata. Si jambo gumu kutega masikio na kuyasikiliza maoni ya watu ila labda pale wenye kutega masikio wanapokuwa na masikio ya kufa. Na sidhani kwamba wajumbe wa Tume ya Katiba ni watu wa sampuli hiyo.
Tatizo litazuka katika kuyachambua na kuyaratibu hayo maoni ya wananchi ambayo lazima yatakuwa ni yenye kutofautiana na kukinzana. Tatizo kubwa zaidi litazuka pale wajumbe wa Tume watapokaa kitako wakawaza na kuwazua na kuyatathmini maoni watayoyapata na kutoa mapendekezo.
Hapo patahitajika uadilifu wa hali ya juu kabisa katika kuyapambanua maoni hayo na kuyapanga. Uadilifu huo utahitajika kwa sababu lazima patatolewa maoni ambayo hayatowapendeza wale wenye kujiona kwamba wao ndio wenye uamuzi wa mwisho juu ya mustakabali wa taifa.
Hayo yako bayana zaidi huko Zanzibar ambako tayari tunasikia sauti kubwa zikipazwa kuupinga mfumo wa sasa wa Muungano, sauti ambazo baadhi ya wakubwa wanataka zizimwe. Bado haijulikani lini Tume itafunga safari yake ya kwanza kwenda Zanzibar kusikiliza maoni ya wananchi.
Warioba aliwakuna wengi alipotamka kwamba Tume yake haitofanya kazi kwa shinikizo za mtu yeyote au za kikundi chochote. Ijapokuwa hadi sasa hatujui ni mwongozo gani Tume hiyo itaufuata ni jambo la kutia moyo kuona kwamba Warioba ametoa hakikisho hilo. Ni jambo la kutia moyo kwa sababu endapo atajiachia ashinikizwe basi naye anaweza akawapotosha wajumbe wa Tume yake kwa kuwapitisha kwenye mazingile mwanambiji ya kichaka cha huo mchakato wa kulipatia taifa Katiba mpya.
Nikizungumzia yanayojiri Zanzibar wananchi wengi wa huko wanaisubiri kwa hamu kubwa Tume ya Katiba kwani itawapa fursa ya kutoa maoni yao juu ya aina ya Katiba waitakayo na hususan juu ya mfumo wa Muungano wanaoutaka. Wanaipata fursa hiyo kutokana na ile sheria iliyouanzisha huu mchakato wa Katiba mpya.
Sheria hiyo hiyo inatambua kwamba Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni Muungano wa nchi mbili tofauti, yaani Tanganyika (au Tanzania-Bara) na Zanzibar. Utambuzi huo ndio msingi wa Tume ya Katiba yenye wajumbe 32 (tukimjumlisha mwenyekiti na kaimu wake), iwe na wajumbe 16 kutoka Bara (Tanganyika) na 16 wengine kutoka Zanzibar.
Hii ni hatua muhimu sana kwa sababu labda hii ni mara ya mwanzo Zanzibar inawakilishwa inavyostahili katika taasisi za Muungano tangu Muungano wenyewe uundwe miaka 48 iliyopita. Ni matarajio ya wengi kwamba kwa vile Zanzibar inawakilishwa vilivyo kwenye Tume hiyo basi maslahi yake yatalindwa na wajumbe wa Tume watokao Visiwani.
Hayo bila ya shaka yatategemea juu ya msimamo utaochukuliwa na wajumbe wa Katiba – ama wa kila mmoja wao binafsi au wa pamoja kama kundi la Wazanzibari walioteuliwa na Rais wa Tanzania baada ya kupendekezwa na Rais wa Zanzibar na kwa ridhaa yake. Wajumbe hao wataiwakilisha Zanzibar mpaka utapopatikana mfumo mpya wa uhusiano baina ya Tanganyika na Zanzibar, mfumo ambao utapatikana kwa makubaliano ya pande hizo mbili ama juu ya msingi wa Katiba au, kama Wazanzibari wengi wanavyotaka, juu ya msingi wa mikataba baina ya nchi mbili, kila moja ya nchi hizo ikiwa na uhuru na mamlaka kamili ya kuendesha shughuli zake za ndani na ya nje ya nchi.
Wajumbe wa Tume kutoka Zanzibar wana fursa isiyo na kifani ya kuhakikisha kwamba Wazanzibari wanaupata mradi wao na hivyo kujenga msingi madhubuti wa uhusiano wa karibu na wa kindugu baina ya Tanganyika na Zanzibar. Wazanzibari wanataraji kwamba uhusiano huo mpya utaziwezesha nchi hizo mbili ziheshimiane na zitambue kwamba kila mojawao ni sawa na mwenziwe. Kwa lugha ya mitaani wanachotaraji Wazanzibari wengi ni kwamba hakuna nchi itayojaribu ‘kuionea’ nyingine kwa misingi ya ukubwa wa eneo la nchi au nguvu za kijeshi.
Inavyoonyesha ni kwamba wengi wa Wazanzibari wamekwishaamua wanataka nini kitokee utapomalizika mchakato huu wa Katiba. Wanachotaka ni kuiona serikali yao inarejeshewa mamlaka yake kamili yatayoiwezesha kuyatanzua matatizo ya kiuchumi na kijamii yaliyoikumba nchi yao kwa muda wote huu wa miaka 48 tangu ulipoundwa Muungano.
Kwa sasa serikali hiyo imelemaa kwa sababu haina uwezo wa kuyalinda ipasavyo maslahi ya Zanzibar kwa vile wanaamini ya kwamba shughuli zote za utawala zilizo muhimu na za kimsingi zimehaulishwa kwenye Serikali ya Muungano kwa mujibu wa Katiba ya sasa ya Jamhuri ya Muungano.
Tatizo ni kwamba Katiba hiyo yenyewe haikutungwa kihalali na wananchi hawakuwa na usemi wowote katika utungwaji wake. Matokeo yake, na huu ndio ukweli unaowachoma Wazanzibari, Serikali ya Zanzibar imegeuka kuwa sawa na ‘serikali ya mkoa’ au serikali ya manispaa. Ndio maana hakuna ushahidi kwamba Serikali ya Tanzania inashiriki katika maendeleo ya Zanzibar au kwamba inatenga fungu la fedha za Serikali ya Muungano kwa maendeleo ya Zanzibar. Kwa hakika, tunaweza kusema kwamba hiyo ndiyo sababu moja kubwa inayowafanya Wazanzibari wawe wanaupinga vikali Muungano na wanasubiri tu fursa itayowawezesha kuyamwaga rasmi na hadharani malalamiko yao.
Wajumbe wa Zanzibar katika Tume ya Katiba wameteuliwa kuiwakilisha Zanzibar kama wenzao walivyoteuliwa kuiwakilisha Tanzania-Bara. Uteuzi huo unaainisha kwamba wakuu wa Tanzania wanaelewa wazi kwamba ile iliyokuwa Tanganyika ina maslahi yaliyo tofauti na yale ya Zanzibar. Hivyo, wajumbe wa Bara katika Tume watautetea msimamo wa Tanganyika na haitostaajabisha endapo watataka mfumo wa Muungano uliopo sasa uendelee vivi hivi ulivyo baada ya kutiwa viraka vya hapa na pale.
Wenzao kutoka Zanzibari watakuwa na jukumu gumu zaidi la kuhakikisha kwamba maoni ya Wazanzibari wengi yanaheshimiwa na kuwasilishwa kwa njia itayowaridhisha. Maoni hayo ni yenye kutaka pawepo mageuzi makubwa zaidi na ya kimsingi katika mfumo wa Muungano.
Kadhalika ni wazi kwamba umma wa Zanzibar unaofuatilia mchakato huu kwa shauku kubwa utakuwa unawaangalia kwa macho mawili wajumbe Wakizanzibari walio katika Tume ya Katiba.
Ili waweze kuyatetea maslahi ya Zanzibar, wajumbe Wakizanzibari watawajibika wafanye kazi kwa pamoja na itakuwa jambo zuri iwapo wataongozwa na Serikali ya Umoja wa Kitaifa ya Zanzibar. Serikali hiyo nayo inawajibika iwe na msimamo ulio sawa na ule wa Wazanzibari wengi juu ya Muungano, hasa kwa vile Zanzibar inajigamba kuwa ni yenye utawala wa kidemokrasia wenye kuongozwa na matakwa ya Wazanzibari.
 
Back
Top Bottom