Awali Msigwa akinukuu taarifa mbalimbali na historia, alikuwa amesema hivi juu ya haki za Wamasai huko Ngorongoro;
UKIUKWAJI WA HAKI ZA WAMAASAI
HIFADHI YA ENEO LA NGORONGORO
Mheshimiwa Spika,
Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro na Loliondo ni moja ya maeneo ya asili ya jamii za Wamaasai. Kwa mujibu wa taarifa za kitafiti za ekolojia ya maeneo haya, Wamaasai wameishi katika maeneo hayo tangu karne ya kumi na nane. Kabla ya mwaka 1959 eneo hili lilikuwa ni sehemu ya maeneo ya Serengeti-Ngorongoro ambayo yalikuwa yakikaliwa na wafugaji wa Kimaasai. Mwaka 1959 Serikali ya kikoloni iliigawanya Serengeti-Ngorongoro baada ya kuanzishwa kwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti upande wa magharibi, na Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro upande wa milima ya mashariki ya eneo la ekolojia la Serengeti-Ngorongoro.
Wafugaji wa Kimaasai waliokuwa wakiishi katika maeneo ya Seronera, Moru na Sironet katika upande wa magharibi waliondolewa katika maeneo hayo na kuhamishiwa Hifadhi ya Eneo la Ngoroongoro na Loliondo. Hata hivyo, Serikali ya kikoloni iliahidi kwamba haki za Wamaasai juu ya ardhi za maeneo walikohamishiwa zitapewa kipaumbele na kulindwa na Serikali. Kwa mujibu wa taarifa rasmi ya kikao cha Baraza la Kutunga la Sheria (LEGCO) cha siku ya Jumatatu ya tarehe 17, Novemba 1953, Gavana wa Tanganyika wa wakati huo alisema yafuatayo: Wakati eneo hili lilipotangazwa kuwa hifadhi ya taifa, ilitambuliwa kwamba kulikuwa na watu waliokuwa na haki za asili za machungio ya mifugo na maji ndani ya mipaka yake na kwamba haitawezekana kuwaondoa watu hawa kwa nguvu.
Kauli hii ya Serikali ilitiliwa nguvu na Waraka wa Serikali Na. 1 wa 1956 (Government Sessional Paper No. 1 of 1956) uliochapishwa kufuatia kuongezeka kwa shinikizo la mashirika ya uhifadhi ya kimataifa yaliyokuwa yanataka Wamaasai wafukuzwe katika maeneo ya Serengeti-Ngorongoro: Kuanzishwa kwa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti chini ya Sheria ya Wanyamapori na baadaye kuundwa kwake upya chini ya Sheria ya Hifadhi za Taifa hakukuathiri kwa namna yoyote haki zilizokuwepo za mtu yeyote ndani au juu ya ardhi za Hifadhi. Badala yake, haki hizo sio tu kwamba zililindwa wazi wazi, bali pia Wamaasai waliokuwa tayari wanaishi ndani ya eneo la Hifadhi walipewa ahadi chanya na Serikali kwamba haki zao hazitavurugwa bila ridhaa yao.
Kufuatia kuchapishwa kwa Taarifa ya Tume ya Uchunguzi juu ya Ngorongoro iliyoongozwa na Sir Barclay Nihill aliyekuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Afrika Mashariki, iliyopendekeza Wamaasai wafukuzwe Serengeti na pia katika maeneo ya Kreta za Ngorongoro na Empakaai, Serikali ya kikoloni ilirudia msimamo wake kuhusu haki za Wamaasai wa Serengeti-Ngorongoro katika Waraka wa Serikali Na. 6 wa 1956 (Government Sessional Paper No. 6 of 1956): Mapendekezo ya kuwa na maeneo tengefu katika Kreta hizo mbili hayakukubalika. Yanaashiria kuondolewa kwa Wamaasai kutoka kwenye maeneo haya mawili. Haikuonekana sawa sawa kuomba ridhaa ya Wamaasai kuachia haki zao ndani ya Kreta hizo mbili wakati huo huo wakiwa wanaachia haki zao ndani ya Hifadhi yenyewe.
Mheshimiwa Spika,
Ahadi za kulinda haki za ardhi za Wamaasai wa Serengeti-Ngorongoro ziliendelea kutolewa kwa nyakati tofauti na viongozi wa ngazi za juu wa Serikali ya kikoloni ya Tanganyika. Hivyo basi, katika kikao cha Baraza la Kutunga Sheria cha tarehe 25 Aprili 1956, Gavana Sir Richard Turnbull aliliambia Baraza hilo kwamba: Wakati Hifadhi ya Taifa ya Serengeti ilipoanzishwa mwaka 1940, ahadi rasmi zilitolewa na Serikali hii kwa Wamaasai. Hii haimaanishi kwa kabila lote la Wamaasai bali wale waliokuwa na haki za kisheria au za asili katika eneo hilo. Nina uhakika kabisa kwamba hakuna mtu yeyote anayeweza kutegemea Serikali hii, au Serikali yoyote ya Kiingereza kuvunja ahadi zake rasmi. Imekuwa ni lazima, kwa hiyo, kupata ridhaa ya Wamaasai kwa ajili ya mabadiliko yanayopendekezwa.
Miaka miwili baadae Gavana Turnbull alirejea kauli yake hiyo wakati akifungua Mkutano wa 34 wa Baraza la Kutunga Sheria tarehe 14 Oktoba, 1958: Nadhani ni lazima nichukue fursa hii kusisitiza kwamba kwa misingi yote ya haki na nia njema hakuna Serikali itakayofikiria kuwaondoa Wamasai kutoka maeneo yote ya hifadhi za wanyama za Serengeti na Nyanda za juu za Kreta. Kama inavyojulikana, baadae Serikali ya kikoloni iliingia mkataba na Wamaasai ambapo Wamaasai walikubali kuhama kutoka maeneo yao ya Sironet, Moru na Seronera ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na kuhamia kwa eneo jipya la Hifadhi ya Ngorongoro. Kwa maneno ya Gavana Turnbull,
uhifadhi wa eneo la Ngorongoro utajengwa kuzunguka nguzo ya maslahi ya wenyeji wa eneo hilo.
Na katika mwaka ambao Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro ilianzishwa, yaani 1959, Gavana Turnbull alisisitiza msimamo wa Serikali yake juu uhifadhi wa Ngorongoro kujengwa kwa kuzingatia maslahi ya wakazi wake katika hotuba aliyoitoa mbele ya Halmashauri ya Wilaya ya Maasai mwezi Agosti 1959: Nataka kuweka wazi kwenu wote kwamba ni nia ya Serikali kuendeleza Crater kwa maslahi ya watu na matumizi yake, wakati huo huo Serikali inakusudia kulinda hifadhi ya wanyama katika eneo hilo, pamoja na kuwepo kwa mgongano wa jamii na serikali bado serikali inathamini na kuheshimu shughuli za jamii na haitaingilia shughuli za wafugaji wa Kimaasai.
Mheshimiwa Spika,
Makubaliano kati ya Serikali ya kikoloni na Wamaasai wa Serengeti-Ngorongoro yalikuwa ndio msingi wa kutungwa kwa Sheria ya Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro ya 1959. Sheria hiyo iliweka msingi kwamba eneo hilo litakuwa ni eneo la matumizi mseto wa rasilmali ambako Wamaasai wataruhusiwa kuishi na kutumia maeneo ya Ngorongoro kwa ajili ya malisho ya mifugo yao. Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro (NGorongoro Conservation Area Authority, NCAA) ilipewa majukumu ya kisheria ya kuhifadhi maliasili za eneo hilo na pia kuwaendeleza Wamaasai kiuchumi.
Hata hivyo, Mheshimiwa Spika, kwa mingi Serikali ya Tanzania imeshiriki katika ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu za Wamaasai wa Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro na Loliondo katika Wilaya ya Ngorongoro. Serikali pia imekiuka wajibu wake wa kuwaendeleza Wamaasai wa Ngorongoro kama ilivyotakiwa kwa mujibu wa Sheria ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro. Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa mwaka 1995 na Shirika la Misaada la Denmark (DANIDA), licha ya NCAA kupokea mamilioni ya fedha za kigeni kutokana na utalii unaoendeshwa katika Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro, umaskini katika familia za Kimaasai ulifikia hatua ambayo 50% ya kaya zao zilikuwa na chini ya mifugo saba kwa kaya ambacho kinachukuliwa kuwa chini ya kiwango cha kujikimu kiuchumi wakati 40% ya kaya hizo zilichukuliwa kuwa ni fukara kwa maana ya kuwa na chini ya mifugo miwili kwa kaya.
Miaka karibu ishirini baadaye, hali ya kiuchumi na kijamii ya Wamaasai wa Ngorongoro imekuwa ni mbaya zaidi kuliko ilivyokuwa wakati wa utafiti huo wa DANIDA. Ushahidi wa suala hili ni Taarifa ya Tume ya Uchunguzi ya CCM iliyoundwa na Katibu Mkuu wa CCM Abdulrahman Kinana na kuongozwa na Naibu Katibu Mkuu, Tanzania Bara, Mh. Mwigulu Nchemba iliyosambazwa jana tarehe 29 Aprili 2013.
Wajumbe wengine wa Tume hiyo ni pamoja na Mbunge wa Longido Mh. Lekule Laizer, Mbunge wa Simanjiro Mh. Christopher ole Sendeka na Mbunge wa Viti Maalum na Katibu wa CCM Mkoa wa Arusha Mh. Mary Chatanda. Ukimwacha Mh. Chatanda, wajumbe wengine wa Tume hiyo ni wajumbe wa NEC ya CCM. Kwa vyovyote vile, taarifa ya Tume hiyo ya uchunguzi inahitaji kupewa uzito na umuhimu wa kipekee kutokana na uzito kichama wa wajumbe walioiandaa.
Kwa mujibu wa Taarifa ya Tume ya Mwigulu Nchemba: Kutokana na ukosefu wa ardhi ya kuendeshea shughuli za kiuchumi, umaskini umekithiri miongoni mwa wakazi wa Ngorongoro kiasi cha kupelekea wakuu wa familia kukimbia familia zao. Ukosefu wa ardhi unaopelekea umaskini kukithiri ni wa kutengeneza na Serikali hii ya CCM kwani kati ya km2 14,036 ambazo ndio eneo lote la Wilaya ya Ngorongoro, km2 8281 au 59% zimechukuliwa na Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro wakati km2 870 au 6% zimechukuliwa na Hifadhi ya Misitu ya Nyanda za Juu Kaskazini. Maeneo ya wanyamapori na malisho ya mifugo ni km2 3916 au 30%, wakati maeneo ya kilimo ni km2 435 au 3% ya eneo lote la Wilaya hiyo.
Katika miaka ya mwanzo 2000, NCAA ilipiga marufuku kilimo cha mazao ya chakula katika maeneo ya Nainokanoka na Endulen ambayo yako ndani ya Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro. Matokeo ya sera hizi za kuwanyanganya wananchi wa Ngorongoro ardhi kwa ajili ya mifugo yao na kupiga marufuku kilimo yamekuwa, kwa mujibu wa Taarifa ya Tume ya Mwigulu Nchemba, ni ... tatizo ... sugu la njaa isiyoisha katika Tarafa ya Ngorongoro.
Taarifa hiyo inafafanua zaidi: Wananchi wa Ngorongoro wana njaa ya muda mrefu ambayo haijapatiwa ufumbuzi. Wananchi hawa hawaruhusiwi kulima ndani ya Hifadhi hivyo hutegemea mgawo wa chakula toka Mamlaka ya Hifadhi. Ahadi ya Rais Dokta Kikwete kuwa Serikali ya CCM itashughulikia suala la kilimo cha kujikimu ambacho kingewasaidia Wamaasai kujipatia chakula, ahadi hiyo haijatekelezwa licha ya ukweli kwamba ... Mamlaka ya Hifadhi imeshindwa kuwapatia chakula.
Hivyo, kama walivyosema Profesa Issa G. Shivji na Dr. Wilbert Kapinga katika kitabu chao The Maasai Rights in Ngorongoro, Tanzania, Serikali ya Tanzania, kwa kupitia Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, imekiuka sio tu haki za binadamu za Wamaasai wa Ngorongoro, bali pia imeshindwa kutekeleza wajibu wake wa kuwaendeleza Wamaasai hao kama inavyotakiwa na sheria. Kwa maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, hiki ndio chanzo cha migogoro ya ardhi ya muda mrefu na isiyomalizika kati ya Wamaasai na Serikali ya CCM na mashirika yake ya uhifadhi wa wanyamapori.
Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaamini kwamba njia pekee ya kutatua matatizo ya kiuchumi na kijamii ya Wamaasai na migogoro juu ya haki zao za ardhi na rasilmali, ni sharti Serikali iweke utaratibu mpya utakaoruhusu Wamaasai kufaidika na rasilmali za wanyamapori katika maeneo yao kwa kiwango kikubwa zaidi kuliko ilivyo sasa. Kama inavyosema Taarifa ya Tume ya Mwigulu Nchemba, kuwapatia wananchi wa Ngorongoro mgawo wa shilingi bilioni moja wakati mapato ya Mamlaka ya Hifadhi ni zaidi ya shilingi bilioni 51 kwa mwaka ni dhihaka na kuwapuuza.
Aidha, utaratibu wa uhifadhi unaosisitiza binadamu na mifugo yao kuondolewa katika maeneo ambayo wameishi pamoja na wanyamapori kwa karne nyingi hauna msingi wowote kisayansi na umepitwa na wakati. Kama walivyowahi kusema watafiti Homewood na Rodgers katika kitabu chao The Maasailand Ecology: Pastoralist Development and Wildlife Conservation in Ngorongoro, Tanzania, hakujawahi kuwa na sababu za msingi za kisayansi za kuwakataza wafugaji wa Kimaasai kutumia rasilmali asili za Serengeti-Ngorongoro kwa ajili ya mifugo yao.
Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali kutoa kauli rasmi mbele ya Bunge hili tukufu kama bado kuna sababu zozote za kuendelea kuwazuia wafugaji wa Kimaasai wa Ngorongoro na Loliondo kutumia maeneo ya malisho ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na maeneo ya Kreta za Ngorongoro, Olmoti na Empakaai na vile vile katika Hifadhi ya Msitu wa Nyanda za Juu za Kaskazini ili kukabiliana na matatizo ya ukosefu wa malisho na maji ya mifugo hasa hasa wakati wa kiangazi.