Tusisahahu haya maneno ya wenye uchungu na TAIFA LAO!
Na Dunstan Bahai
``...Urithi wetu umegeuka kuwa mali ya wageni, na nyumba zetu kuwa mali ya makafiri. Tumekuwa yatima waliofiwa na baba, mama zetu wamekuwa kama wajane.
Tunakunywa maji yetu kwa fedha, kuni zetu twauziwa.
Watufuatao wako juu ya shingo zetu, tumechoka tusipate raha yoyote Baba zetu walitenda dhambi hata hawako, na sisi tumeyachukuwa maovu yao. Watumwa wanatutawala, hakuna mtu wa kutuokoa na mikono yao.
``Twapata chakula kwa kujihatarisha nafsi zetu, kwa sababu ya upanga wa nyikani. Ngozi zetu ni nyeusi kama tanuu, kwa sababu ya hali ya njaa ituteketezayo Wakuu hutungikwa kwa mikono yao, nyuso za wazee hazipewi heshima.
``... Wazee wameacha kwenda langoni, na vijana kwenda ngomani. Furaha ya mioyo yetu imekoma, michezo yetu imegeuka maombolezo.
``Mbona watusahau siku zote, na kutuacha muda huu mwingi. We Bwana, utugeuze kwako nasi tutageuka, zifanye mpya siku zetu kama siku za kale. Isipokuwa wewe umetukataa kabisa, nawe una hasira nyingi sana juu yetu,`` hayo ni baadhi maneno ya Bibilia yanayopatikana kwenye kitabu cha Maombolezo sura ya 5:1-22.
Nimelazimika kunukuu sehemu hiyo ya Biblia kama kitabu kitakatifu, kuonyesha maonyo yaliyotolewa wakati wa zamani na dhuluma iliyopo sasa duniani, hasa katika nchi maskini na zile zinazoendelea, dhuluma zinazofanywa na baadhi ya watawala wake.
Katika kipindi cha takribani miaka miwili na miezi minne hivi, Watanzania na Walimwengu kwa ujumla, wameshuhudia viongozi wa juu wa serikali ya awamu ya nne wanavyoachia nyadhifa zao.
Hatua hiyo ya viongozi kuachia nyadhifa zao haimaanishi wamehusika na tuhuma zinazoenezwa juu yao, bali ni ishara ya heshima na uwajibikaji.
Hatuwezi kuwahukumu viongozi hao kuwa `walivaa ngozi ya kondoo`, huku wakijijua ni `mbwa mwitu` bali walionyesha mfano mzuri wa kuwajibika ingawa wapo wengi wa aina hiyo wanaotakiwa kufuata nyayo zao.
Kuwajibika si dhambi, wala kuwajibika si aibu bali kama kiongozi, anazidi kujijengea heshima.
Mhadhiri wa Sayansi ya Siasa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Mwesiga Baregu, anatanabaisha kwamba baada ya Tanzania kupata Uhuru, uongozi wa wakati huo ulikuwa ukitegemea Rais zaidi.
Hata hivyo, alikiri kuwa viongozi wa wakati huo walikuwa na maadili makubwa ikilinganishwa na wa sasa.
Alisema mtu mbadhirifu au aliyepatikana na rushwa, alikuwa hana nafasi wala sifa ya kuendelea kuwa kiongozi, kwani Rais, wakati huo hayati Mwalimu Julius Nyerere, hakusita kumchukulia hatua kali ikiwa ni pamoja na kumfukuza kazi moja kwa moja.
``Wakati huo ilikuwa amri moja tu kwa kiongozi asiye na maadili. Zamani kiongozi akiitwa Ikulu anatetemeka, anajua akirudi hana kazi, ni kiama kwake, lakini sasa hivi mambo tofauti.`` alisema.
Alisema kipindi cha awamu ya kwanza, kulikuwa na matukio mengi ya viongozi kujiuzulu, kufukuzwa na kustaafishwa kazi.
Miongoni mwa tukio la kujiuzulu kwa kuwajibika ni la aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi, kutokana na makosa yaliyotokea katika wizara yake.
Katika serikali ya sasa viongozi wengine walioachia ngazi zao kwa uwajibikaji mapema mwaka huu ni aliyekuwa Waziri Mkuu Bw. Edward Lowassa, aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Bw. Nazir Karamagi, aliyekuwa Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk. Ibrahim Msabaha na hivi karibuni aliyekuwa Waziri wa Miundombinu, Bw. Andrew Chenge.
Hata hivyo, aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Daud Balali, alifukuzwa kazi ingawa ni baada ya kumuandikia Rais kuwa ameamua kujiuzulu.
Uwajibikaji ni sehemu ya uadilifu, nidhamu na kujijengea heshima ndani ya familia ya anayewajibika, lakini zaidi nje ya familia yake na nje ya mipaka ya nchi, kwani kiongozi anaonyesha kujutia kilichotokea akiwa kiongozi katika eneo lake, lakini kujiuzulu kwa shinikizo la umma, hilo halimletei heshima kiongozi.
Kwa mujibu wa Profesa Baregu, kumekuwa na matukio mengi ya ubadhirifu, hali ambayo imewaudhi wananchi hadi kufikia umma huo kuchukia kudanganywa huku mali zao wakishuhudia zikiporwa.
Profesa Baregu alisema shinikizo la nguvu ya umma limechangia kuibuka kwa mambo mengi maovu.
Pia alivipongeza vyama vya upinzani hasa ushirika wa vyama vinne vya CHADEMA, CUF, TLP na NCCR-Mageuzi.
Alisema vyama hivyo kwa kushirikiana na umma wa Watanzania, waliweza kufanikiwa kuufikisha ujumbe, kilio chao cha kuporwa mali zao, na matokeo yalijidhihirisha na kwa upande mwingine serikali imeonyesha nia ya kushughulikia malalamiko hayo.
Hatua iliyofikiwa na serikali ya kuanika uozo uliojitokeza, ni hatua muhimu sana na ya kuungwa mkono na wananchi wengi, hicho ndicho kilichokuwa kikisubiriwa na umma wa Watanzania.
Aidha, hatua hiyo itairejesha heshima na imani ya Watanzania kwa uongozi wa Taifa na mihimili yote ya nchi.
Naye Askofu Mkuu Msaidizi wa Kanisa Katholiki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mhashamu Methedius Kilaini, ameonyesha kukerwa na watu wanaohusika na ufisadi.
``Mimi simjui fisadi, lakini ninachukia sana hali hiyo. lakini nimeridhika jinsi suala hili lilivyoibuliwa, kwani haya mambo yalikuwepo tangu enzi za mababu, lakini, nani awe wa kwanza kumfunga paka kengele,`` alisema.
Aliwashauri Wabunge, kutokana na ujasiri wao kuliibua suala hili na kulizungumzia kwa kina, waendeleze jitihada hizo hadi mafisadi watakapojulikana na kufikishwa mahakamani, kwani huko wananchi watakapowajua na kupata haki yao.
Askofu Kilaini alikuwa akimaanisha, huwezi kumnyooshea mtu kidole kuwa ni fisadi, kwani wengi wanaamini viongozi wote waliojiuzulu ni mafisadi, la hasha, hao walifanya hivyo kama sehemu ya uwajibikaji, kwani tuhuma hizo zimeibuka wakati wao wakiwa ni viongozi wa maeneo yanayotuhumiwa.
Kwa maana hiyo, uchunguzi unaofanywa na serikali katika maeneo hayo wananchi wanaamini utawaibua mafisadi, pengine ni wale waliojiuzulu kwa heshima au wengine.
Inawezekana kabisa, Rais Kikwete ana dhamira ya kweli ya kuwaondolea umaskini na kero zote zinazowakabili wananchi, lakini wapo wanaokwenda kinyume na dhamira hiyo.
Hata hivyo kuna dalili yawezekana Rais Kikwete ameonyesha kukerwa na ufisadi pamoja na rushwa, ndiyo maana alishindwa kulitolea maamuzi suala hilo na badala yake ameviachia vyombo vya dola kulishughulikia, na Watanzania wanasubiri kwa hamu sana matokeo ya uchunguzi huo.
Kumekuwa na maoni mbalimbali yaliyokuwa yakitolewa na wananchi na viongozi wa dini, juu ya nini kifanyike kwa wale wote watakaobainika kuhusika na kupora mali za Watanzania.
Pia yapo maoni yaliyotolewa na Kamati Teule ya Bunge iliyokuwa ikiongozwa na Mbunge wa Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe, kuchunguza tuhuma za Richmond.
Baadhi ya maoni ya wananchi na viongozi wa dini ni serikali kuwachukulia hatua haraka wale wote wanaodhani ni mafisadi ikiwa ni pamoja na kufilisi mali zao.
Maoni hayo ni ya haraka sana, tunaamini hakuna mtu anayemfahamu fisadi, cha msingi ni wananchi kuwa na subira, kusubiri uchunguzi unaoendelea wa vyombo vya dola.
Cha msingi ni vyombo hivyo kufanyakazi yake kwa umakini na ukweli na uwazi ili Watanzania waendelee kujenga heshima kwa serikali yao ya awamu ya nne na hata Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Ili suala hili lisiendelee kuwa mjadala, tena mjadala wa kutoaminiani, dhamana ya ukweli wa mambo yenyewe iko mikononi mwa vyombo vilivyoteuliwa na serikali katika kuchunguza masuala hayo.
Vyombo hivyo visipofanyakazi yake kwa makini na ukweli, viongozi waliojiuzulu nyadhifa zao hawatakwepa hasira za wananchi, na maisha yao yatakuwa juu ya mikono ya Watanzania.
Watanzania kama kawaida yao ni wapole, hivyo upole wao usichukuliwe kama ni mazuzu.
Tanzania ni yetu, hakuna mgeni atakayetutengenezea amani na utulivu, kwani suala hili likichukuliwa kwa jazba, urithi wa amani yetu utabakia kama historia, Mungu ibariki Afrika, Mungu ibariki Tanzania