Maige: Marufuku biashara ya nyamapori, magogo...................

Rutashubanyuma

JF-Expert Member
Sep 24, 2010
219,470
911,173
Maige: Marufuku biashara ya nyamapori, magogo

Thursday, 09 December 2010 14:22 newsroom




* Mikataba ya vitalu kupitiwa, wazalendo kupewa kipaumbele
Na Joseph Damas
WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige, amecharuka na kutoa maagizo mazito kwa viongozi waandamizi wa wizara yake, ikiwa sehemu ya mkakati wa utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM. Pia, ametangaza kupiga marufuku biashara ya nyamapori, ambayo imeshamiri maeneo mbalimbali na usafirishaji wa magogo nje ya nchi kwa kuwa ni kinyume cha sheria. Maige, ambaye alikuwa Naibu Waziri wa wizara hiyo katika miaka mitano iliyopita, alisema mazao ya misitu yanayoruhusiwa kusafirishwa nje ni mbao zenye upana wa inchi 4x4 na si zaidi ya hapo.
Kutokana na marufuku hiyo, ameziomba mamlaka husika, ikiwemo Jeshi la Polisi nchini na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuchukua hatua kwa atayekamatwa akijihusisha na biashara hizo. Aliyasema hayo mjini Dar es Salaam, jana alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari juu ya mikakati yake katika kuhakikisha rasilimali zilizopo chini ya wizara hiyo zinakuwa na tija kwa taifa.
“Kuuza nyamapori ni kosa, mlaji na muuzaji wote ni wahalifu na kuanzia sasa atakayekutwa anakula ama kuuza atakamatwa na kushitakiwa,” alisema Maige. Hata hivyo, alifafanua kuwa serikali inatoa vibali vya uwindaji wa wanyama, lakini inaweza kutolewa bure kwa jamii na sio kuuzwa. Kuhusu biashara ya magogo nje ya nchi, alisema imekuwa gumzo kwa muda mrefu na kwamba, kuanzia sasa sheria itachukua mkondo wake na wamedhamiria kulinda rasilimali za misitu.
Kuhusu safari za vigogo wa wizara hiyo nje, Maige ametaka kuangaliwa upya kwa misafara ya vigogo wa wizara hiyo wakiwemo viongozi waandamizi kwenda nje ya nchi kutangaza vivutio vya utalii.
Alisema hakuna sababu kwa viongozi hao kusafiri mara kwa mara kwenda nje ya nchi kwa kigezo cha kutangaza utalii na kuagiza kazi hiyo ifanywe na wahusika.
“Nimeagiza viongozi kuacha kuhodhi safari za nje ya nchi, waache wahusika wafanye kazi hiyo. Hilo lianze mara moja kama kuna ulazima kiongozi aende nje mara moja tu kwa mwaka,” alisema.
Pia, alisema viongozi waandamizi waende maeneo ya kazi na siyo kukaa ofisini ama kusubiri safari.
Alisema kuna baadhi ya maeneo ya mbuga za wanyama na vivutio vya utalii, viongozi hawajawahi kuonekana, hivyo wakati wa kukaa ofisini umekwisha.
“Safari za nje watu wanakwenda mno, lakini kutembelea maeneo ya kazi inakuwa vigumu, hilo sitaki kuliona tena,” alisema Maige.
Akizungumzia mapato ya serikali, Maige alisema katika kuhakikisha rasilimali za misitu na utalii zinakuwa na tija kwa taifa, ameagiza kupitiwa upya kwa mikataba ya zamani na kuiboresha.
Alisema mikataba itakayomalizika muda wake, itapitiwa upya na kufanyiwa marekebisho ili kukuza uchumi wa taifa.
Katika mikakati hiyo, Maige pia aliwaagiza viongozi wa wizara kuwabana wafanyabiashara wa mkaa ili kuhakikisha wanalipa kodi za serikali, ikiwemo ushuru wa misitu.
Alisema mabilioni ya shilingi yamekuwa yakipotea kila mwaka kutokana na wafanyabiashara wa mkaa kukwepa kulipa ushuru.
“Kwa Jiji la Dar es Salaam pekee mkaa unatakiwa kuingiza sh. bilioni tatu kwa mwezi, lakini kwa sasa tunakusanya sh. milioni 53 tu. Sasa nimeagiza tukusanye sh. milioni 500 kwa mwezi na utekelezaji wake uanze mara moja,” alisema Maige.
Hata hivyo, alikiri kuwa kuna udhaifu katika kusimamia sheria, na kwamba mamlaka husika hazina budi kusimamia hilo.
Kuhusu vitalu vya uwindaji, alisema moja ya eneo ambalo limekuwa likilalamikiwa kwa muda mrefu na Watanzania ni vitalu vya uwindaji, ambapo vingi vinadaiwa kumilikiwa na wageni.
Maige katika hili aliwatoa hofu Watanzani akisema kuwa vitali vya uwindaji sasa vitatolewa kwa kufuata sheria na taratibu.
Pia, alisema mikataba ya vitalu itakayokwisha muda wake itapitiwa upya na kutolewa kwa Watanzania wenye sifa, ikiwa ni mkakati wa kuboresha utendaji.
Akizungumzia changamoto zinazoikabili wizara yake, Maige alisema kwa sasa ni uhaba wa vitendea kazi katika kulinda usalama wa rasilimali.
Hata hivyo, alisema katika kupambana na majangili kwenye mbuga za wanyama, wana mpango wa kununua helikopta, ambayo itasaidia kurahisisha utendaji kazi.
Alisema maofisa wa wanyamapori wamekuwa wakikabiliana na majangili kwa kutumia magari, na kwamba wakati mwingine wanashindwa kuwahi eneo la tukio.
“Sasa tunataka kusaka majangili kwa helikopta, tupo kwenye mchakato na wadau ili kuangalia uwezekano wa kutekeleza mpango huu,” alisema Maige.
 
:I beg your pardon" haya ni kweli usemayo kijana Maige? Kwanza Hebu nenda huku hifadhi ya Ruaha karibu na Usangu unangalia hawa jamaa zako (wafanyakazi) na watu wa asili ya Kiarabu wanavyofagia wanayama pori katika Mbuga hii kama hawana akili timamu. Pili mbona hakuna publicity juu ya Mbugu za wanayama za kusimi sasa ni miaka 50 baadaya Uhuru?? Tafadhali we ni mzalendo linda maslahi ya taifa lako
 
Tatizo kubwa ni ugawaji holela wa vitalu vya kuwindia na kusafirisha nyamapori nnje ya nchi. Uwindaji wa ndani kwa ajili ya chakula unachohitaji ni usimamizi bora tu na siyo kuupiga marufuku. Ikumbukwe uwindaji ni moja ya nyenzo muhimu za kudhibiti idadi ya wanyama pori iendane na uwezo wa mazingira yao.
Waziri hakupaswa kuupepelea uchomaji mkaa kama chanzo kikubwa cha kodi bali kuhimiza upatikanaji wa nishati mbadala ili misitu isiangamizwe. Wrong shot!
 
Back
Top Bottom