Dar es Salaam. Aliyekuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Omar Mahita amesema baadhi ya askari polisi wanashindwa kuwachukulia hatua za kisheria viongozi wanaovunja sheria za nchi wakihofia kupoteza nafasi zao za kazi.
Akizungumza hayo wakati maadhimisho ya miaka 10 ya Mtandao wa Polisi Wanawake Tanzania (TPFN), leo Novemba 8 amesema askari wanatakiwa kuwa na ujasiri.
“Askari wanatakiwa wakiwa kazini wasisite kumchukulia hatua kiongozi yeyote watakayemkuta na makosa’’amesema
Mahita amesema askari polisi wanakuwa waoga hawataki kuthubutu hivyo wanatakiwa kuwa jasiri hata kama lolote litatokea.
“Kwa nini askari wengi hawataki kuthubutu wanataka kulinda kazi zao hivyo wanatakiwa wapambane na wawe jasiri na wasipofanya hivyo ipo siku itawarudia,”amesema Mahita.
Naye Kamishna wa Polisi Jamii nchini,Musa Ali Musa ameutaka Mtandao wa Polisi Wanawake Tanzania (TPFN) kufuata maadili ya kazi na kuendelea kufanya kazi kwa ujasiri kwa mujibu wa sheria za nchi.
Musa amesema maadhimisho hayo yataleta mafanikio kwa Jeshi la Polisi na nchi kwa ujumla hivyo wataweza kufanya tathimini ya kutambua mafanikio na mapungufu yaliyojitokeza.
Mwananchi