UONGOZI wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) umewafukuza kazi madaktari 229 walioko katika mafunzo kwa njia ya vitendo kutokana na mgomo wa siku nne wakishinikiza kulipwa posho zao za mwezi mmoja.
Hatua ya kuwafukuza madaktari hao, imesababisha huduma za afya kudorora na kuna madai kwamba baadhi ya wagonjwa walikosa huduma kwa siku nzima ya jana kutokana na kutokuwepo kwa madaktari.
Mkurugenzi wa hospitali hiyo, Dk. Marina Njelekela, tangu juzi alikataa kuzungumza na waandishi wa habari, na kutwa nzima ya jana simu yake ya kiganjani ilikuwa ikiita bila kupokelewa.
Madaktari hao walifukuzwa kupitia tangazo la barua iliyosainiwa na Dk. Marina Njelekela kisha kubandikwa katika kila wodi za hospitali hiyo likibeba kichwa cha habari: Kuhusu kurudishwa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii.
Kwa mujibu wa tangazo, uongozi wa Muhimbili umewataka madaktari hao kuchukua barua zao ili waende Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kupangiwa kazi katika vituo vingine, kwa vile hawatakiwi tena pia.
Mara upatapo barua hii unatakiwa kujeresha vifaa vyote ulivyopewa na hospitali vikiwemo funguo za chumba na kitambulisho na kuripoti Wizara ya afya mara moja, ilisema sehemu ya barua hiyo ambayo nakala yake pia imepelekwa kwa Katibu Mkuu Wizara ya Afya na Ustawi Jamii, Blandina Nyoni.
Kwa mujibu wa barua hiyo madaktari hao wamekiuka makubaliano ya kifungu namba 1(b)(d) (e) (f) (g) kama ilivyoelekezwa na Katibu Mkuu katika barua yake ya kuwapangia mafunzo katika Hospitali ya Muhimbili.
Habari kutoka ndani ya hospitali hiyo zinaeleza kwamba madaktari hao walirejea kazini jana majira ya saa 11.00 alfajiri wakiwa wamevalia nguo zao za kazi na kabla hawajaingia wodini walizuiwa na walinzi wakitakiwa kuangalia matangazo yaliyoeleza kusimamishwa kwao kazi.
Akizungumza na waandishi wa habari hospitalini hapo kiongozi wa madaktari hao wanafunzi, Dk. Deogratius Mally, alisema wanashangazwa na hatua ya uongozi huo kuwasimamisha kazi wakati mkataba wao unatambuliwa na Wizara ya Afya.
Alisema wakati wanadai haki yao hawakuitisha mgomo, hivyo wanashangazwa na hatua ya uongozi huo kuingilia suala ambalo lilitakiwa kufanywa na wizara kwani hata mkataba wao wa ajira hausemi hivyo.
Barua ya madai yetu tuliandika kwa Katibu Mkuu Wizara ya Afya na si Mkurugenzi wa Muhimbili, alisema Dk. Mally.
Alisema kutokana na hali hiyo jana walijipanga kumtafuta mwanasheria na kukaa naye ili watafakari walipokosea ili baada ya kikao na mwanasheria huyo Jumatatu ijayo waende wizarani.
Mgomo huo wa madaktari ulianza mwanzoni mwa wiki hii kwa madaktari hao kushinikiza kulipwa jumla ya sh milioni 176 ambazo ni posho zao za kujikimu za mwezi Desemba mwaka jana.
Kwa maelezo yao walidai hawatamaliza mgomo huo hadi hapo watakapolipwa fedha hizo.
Hata hivyo juzi jioni walianza kulipwa baada ya serikali kusalimu amri.
Hali yazidi kuwa tete Dodoma
Huko Dodoma, madaktari wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma wameendelea na msimamo wa kutofanya kazi hadi watakapolipwa fedha zao huku utoaji wa huduma kwa wagonjwa ukiendelea kudorora.
Mgomo huo wa madaktari ambao ulianza juzi asubuhi umesababisha wagonjwa wengi waliolazwa na wale wanaofika hospitalini hapo kukosa huduma zinazostahili.
Madaktari hao wamegoma wakishinikiza Wizara ya Afya iwalipe fedha zao za miezi miwili wanazodai.
Zaidi ya madaktari 33 wanaidai wizara hiyo malipo ya fedha kuanzia mwezi Novemba na Desemba mwaka jana ambazo hawajalipwa hadi leo.
Hata hivyo, kaimu mganga mkuu wa hospitali ya mkoa, Dk. Nassoro Mzee, alisema malipo ya madaktari hao yanashughulikiwa baada ya fedha kufikishwa Hazina ndogo ya Dodoma.
Fedha zimeshafika na zipo kwenye utaratibu wa malipo, naamini hadi Jumatatu madaktari wote watakuwa wamelipwa fedha zao, alisema.
Hata hivyo, katibu wa hospitali hiyo, Isaack Kaneno, alisema madaktari hao wamekataa kuingia kazini hadi wapate fedha mkononi, licha ya kuambiwa kuwa ziko Hazina na zinashughulikiwa.
Inasikitisha kwamba wenyewe wanadai mwezi mmoja na hapohapo kuna watumishi wengine wa serikali wanadai miezi mingi, mbona hawajagoma? alisema.
Hata hivyo, katibu mkuu alisema kwa mujibu wa taratibbu za kazi, mfanyakazi akigoma kwa siku tatu mfululizo atakuwa amejifuta kazi mwenyewe.
Tanzania Daima ilipomtafuta Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Blandina Nyoni, kuzungumzia suala hilo simu yake iliita mara zote alipopigiwa bila majibu.
My Take: Ukitaka ubaya na mtu dai haki yako!
|