Kwa jeshi la polisi nchini kuzuia wapenzi na wafuasi wa vyama vya siasa kuwasindikiza wateule wao wagombea wa kiti cha urais na kuzuiwa kwa msafara wa Lowassa kwenda kuhani msiba wa mzee Peter Kisumo leo ni ishara kwamba Rais Jakaya Kikwete anahofia uwepo wa Lowassa msibani hapo. Kwa maoni yangu kama ningekua Rais wa nchi basi kujumuika na wananchi na familia na jamii nzima ya Watanzania kwa wingi wao na tofauti zao za kidini, rangi, kipato, itikadi na hata asili zao ndio jambo ambalo ningelenga kulionyesha leo kwa kutumia msiba huu kuukuza umoja wetu wa kitaifa na kuchochea amani inayoweza kustahimili tofauti zetu kwa kuuimarisha U-Tanzania wetu.
Hapa pangekua mahali ambapo utamaduni wa Kitanzania kujumuika pamoja kushiriki "sherehe" ya mwisho ya mwanadamu, Mtanzania mwenzetu, tena aliyeishi kwa kulihudumia Taifa, hakika uwingi wowote hata milioni zote takribani 45 za Watanzania wangepaswa kuruhusiwa kuhani msiba wa Mtanzania mwenzao wakiwemo wapinzani na wafuasi wa Lowassa, pia na Lowassa mwenyewe.
Busara ndio itatamalaki siku zote, mabavu, hofu na ujinga hazijawahi kuwa silaha za kutawala umma, hata siku moja. Hapa leo tena Rais amepoteza alama moja zaidi katika kushawishi Watanzania si tu kuchagua chama chake cha CCM katika uchaguzi mkuu utakaofanyika wiki chache zijazo bali kuukumbuka utawala wake kama utawala uliojumuisha, wenye mamlaka na wasionayo, wakubwa kwa wadogo, wapinzani na wana CCM.