BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,789
- 288,015
Date::1/16/2009
Kwa masharti haya UDSM ni wabaguzi
Mwananchi
Kwa masharti haya UDSM ni wabaguzi
Mwananchi
MWISHONI mwa mwaka jana wanafunzi wa shahada ya kwanza kutoka vyuo vikuu saba vya umma nchini, walisimamishwa masomo kutokana na mgomo wao wa kupinga sera ya uchangiaji elimu ya juu.
Mgomo huo ulioanzia katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na baadaye kusambaa hadi katika vyuo vingine, ulilenga kuishinikiza serikali iwape mikopo wanafunzi wote kwa asilimia 100 bila kubagua.
Wanafunzi hao walikuwa wanapinga utaratibu wa sasa wa kuwatenga kwenye makundi, wengine kupewa mikopo kwa asilimia 100 na wengine hadi asilimia 20 tu.
Baada ya wanafunzi kusimamishwa, uongozi wa vyuo uliweka masharti magumu zaidi ya kurejea kwao kama vile kujaza fomu maalum.
Mathalani, mbali ya kulipa ada yote, uongozi wa UDSM umetangaza kufutwa kwa sheria zinazotambua kuwepo kwa Serikali ya Wanafunzi (Daruso) na kutoa vitambulisho vipya.
Kutokana na ugumu wa masharti hayo na kwa kuwa mkazo wa uongozi wa UDSM uko katika kupata pesa kwa asilimia ile ambayo kila mwanafunzi anapaswa kutoa, ni asilimia 33 tu ya wanafunzi wote wa shahada ya kwanza waliotekeleza na ambao kimsingi ndio wataruhusiwa kuingia darasani kuanzia Jumatatu.
Hii ina maana kuwa asilimia 67 watakuwa wamejifukuzisha chuo kwa kushindwa kutekeleza masharti yaliyowekwa na chuo.
Wadau mbalimbali wa elimu walikuwa wanadhani ya kuwa katika kipindi chote cha kuanzia Novemba 12, 2008 waliposimamishwa wanafunzi hao, mamlaka zinazohusika, yaani vyuo vikuu, Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu na serikali zingeyafanyia kazi kwa umakini madai ya wanafunzi.
Lakini badala yake wameyatupa kiasi kwamba asilimia 67 ya wanafunzi wengi wao kutoka familia masikini wanatarajiwa kukosa elimu ya juu kwa sababu ya umasikini wao.
Hapa tunaanza kushuhudia ubaguzi ukianza kujitokeza katika sekta ya elimu kwamba, watoto wa masikini hawana nafasi tena ya kupata elimu ya juu, ikimaanisha kuwa vyuo vya umma sasa ni sawa na vyuo binafsi ambako mwanafuzi asiyelipa ada hufukuzwa.
Na hapa ndipo tunajiuliza kwamba, UDSM wanafaidika vipi kwa wanafunzi wengi kiasi hicho kutimuliwa? Ni kwanini zinatolewa kauli kwamba, hakuna mwanafunzi atakayekosa masomo kwa sababu ya umasikini, lakini wengi wanafukuzwa? Tunarudia kutoa ushauri kwamba, sera ya uchangiaji wa elimu ya juu ipitiwe upya ili kutoa haki sawa kwa wanafuzi wote.