Kuuwa bila ya haki

Mandago

JF-Expert Member
Feb 8, 2008
238
99
KUUWA BILA YA HAKI.

Kuuwa bila ya haki ni katika madhambi makubwa sana. Mwenyezi Mungu S.W.T. ameharamisha kuuwa nafsi ya mtu mwingine bila haki. Kwa sababu kajaalia uhai wa maisha ya mtu na kuwepo kwake hapa duniani ni kitu kitukufu sana. Kwa hali hiyo kumuuwa mtu kwa makusudi ni kumdhulumu uhai kiumbe wa Mwenyezi Mungu. Na adhabu ya kuuwa kwa makusudi ni ya duniani na Akhera. Ama adhabu ya duniani ni kulipiziwa kisasi kwa kuuliwa na adhabu ya Akhera ni Moto wa Jahannam na ghadhabu ya Mwenyezi Mungu Mtukufu ikiwa pamoja na laana Yake. Aya nyingi ndani ya Qur-ani pamoja na Hadithi za Mtume S.A.W. zimeelezea haya. Na zimetuhadharisha kwa jambo hili ovu. Kwanza Mwenyezi Mungu S.W.T. kasema katika Suratil Israa (Bani Israil) aya ya 33, "

"Wala msiuwe nafsi ambayo Mwenyezi Mungu ameiharamisha (kuiua) isipokuwa kwa haki. Na aliyeuliwa kwa kudhulumiwa basi tumempa madaraka mrithi wake. Lakini asipite mpaka katika kuuwa. Hakika yeye atasaidiwa (na sheria maadam anayo haki) "

Kisha kasema katika Suratin Nisaa aya ya 93, "

"Na mwenye kumwuwa Muumini kwa makusudi, basi malipo yake ni Jahannam, humo atakaa milele; na Mwenyezi Mungu amemghadhibikia na amemlaani na amemwandalia adhabu kubwa."

Pia kasema katika Suratil Maaida aya ya 32, "

"Kwa sababu ya hayo tukawaandikia wana wa Israil ya kwamba atakaemwuwa mtu bila ya yeye kuuwa mtu, au bila ya kufanya fisadi katika nchi, basi ni kama amewauwa watu wote; na mwenye kumwacha mtu hai (kumsaidia kuishi) ni kama amewaacha hai watu wote…"

Tena kasema katika Suratil Takwyr aya ya 8 na ya 9, "

"Na mtoto mwanamke aliyezikwa hali ya kuwa yu hai atakapoulizwa. Kwa makosa gani aliuawa?"

Na katika Hadithi ya Ibn Masoud R.A.A. iliyotolewa na L-Bukhari na Muslim, mtu mmoja alimuuliza Mtume S.A.W., "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Jee, ipi dhambi kubwa kabisa mbele ya Mwenyezi Mungu?" Mtume S.A.W. akajibu akasema:

"Usijaalie (usikifananishe) kitu chochote sawa na Mwenyezi Mungu, na hali Yeye kakuumba wewe." Akauliza kitu gani kingine? Akamjibu, "Usimwue mtoto wako kwa khofu atakula na wewe." Akauliza kitu gani kingine?"

Akamjibu, "Usimzini mke wa jirani yako."

Ndipo Mwenyezi Mungu alipoteremsha Suratil Furqaan aya ya 68 na ya 70 kusadikisha ukweli wa maneno ya Mtume Wake S.A.W., "

"Na wale wasiomuomba mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu, wala hawaui nafsi aliyoiharimisha Mwenyezi Mungu isipokuwa kwa haki, wala hawazini; na atakaefanya hayo atapata madhara (papa hapa ulimwenguni kabla ya Akhera). Na atazidishiwa adhabu siku ya Kiyama na atakaa humo kwa kufedheheka (muda mrefu kabisa) milele. Ila yule atakaetubia na kuamini na kufanya vitendo vizuri…"

Pia imeharamishwa kuuwana baina ya Mwislamu na Mwislamu bila ya haki au sheria inayoruhusu. Na ikiwa watauwana bila ya udhuru wowote ule basi wajue kwamba malipo yao ni Moto, kwa uthibitisho wa Hadithi iliyotolewa na L-Bukhari, Muslim na Ahmad, Mtume S.A.W. kasema, "

"Wanapokutana Waislamu wawili kwa panga zao atakayeuwa na atakayeuliwa katika Moto." Aliulizwa ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Huyo ni muuaji. Lakini jee, aliyeuliwa ana makosa gani?" Akajibu, "Kwani alikuwa akingoja kwa hamu kumuuwa mwenziwe."

Makusudio ya Hadithi hii ni kwamba ikiwa Waislamu wawili watapigana bila ya haki yoyote ile au sababu; labda pengine kwa sababu ya mali au cheo au sifa basi jazaa yao ni Moto. Lakini anayepigania haki yake au kujitetea kwa sababu kadhulumiwa au jambo litakalomfanya kuwa lazima apigane, huyu haingii katika Hadithi hii. Na Mwenyezi Mungu anajua zaidi.

Pia imetajwa katika Hadithi sahihi kwamba kitu cha kwanza atakachohukumiwa mja katika haki za watu ni kumwaga damu bila ya haki. Kama alivyosema Mtume S.A.W. katika Hadithi iliyotolewa na Nnasaai, L-Bukhari na Muslim, "

"Kitu cha kwanza kuhukumiwa baina ya watu siku ya Kiyama ni umwagaji wa damu."

 
sawawia kabisa. wako wapi wale wanaojiita watetezi wa haki za Bin,Adam anaopinga adhabu ya kunyongwa mpaka kufa
 
Asante shekhe!
Bwana Mungu akubariki sana, uendelee na `daawa` yako juu ya wanajamii!
 
Back
Top Bottom