Mama Amon
JF-Expert Member
- Mar 30, 2018
- 2,021
- 2,478
Hivi karibuni, wakati wa uzinduzi wa tamasha la machifu liitwalo BULABO, Raia Namba Moja anasikika akisema kwamba "wakina baba wenye uwezo wa kiuchumi ongezeni nyumba ya pili au ya tatu, sisi wanawake hatuna wivu, na hatukatai."
Kimantiki, hata wanawake wenye uwezo wa kiuchumi wanaweza kuongeza "nyumba ya pili au ya tatu" ilimradi wanaume husika wasiwe na wivu na wasikatae. Je, Katiba ya nchi inasema nini kuhusu mambo haya?
Napenda kujibu swali hili kwa uchache ili kumkumbusha yeye, na kila mtu, kila mahali, na kila wakati kuheshimu na kulinda Katiba ya nchi, ambayo inabeba tunu muhimu za Taifa letu, na hasa tunu ya "usawa wa binadamu" wanaume na binadamu wanawake:
1. Ibara ya 12(1) ya Katiba ya Tanzania (1977) inatambua kanuni ya usawa wa bindamu bila kujali dini, kabila, jinsi, wala eneo la kijiografia, kwa kutamka kwamba, "Binadamu wote ... ni sawa," katika vigezo vya akili, utashi na heshima ya utu.
2. Ndoa za mitala, yaani mwanamume mmoja aliyefunga ndoa na wanawake wengi (polygyny) au mwanamke mmoja aliyefunga ndoa na wanaume wengi (polyandry), zinakanusha kanuni ya usawa kati ya binadamu mwanamume na binadamu mwanamke.
Kulingana na profesa Immanuel Kant (1724–1804), kitendo cha mwanamume mmoja kuoa wake wengi au mwanamke mmoja kuolewa na wanaume wengi, ni kosa la kimaadili, kwa sababu ni kitedo kinachotoa haki zisizo sawa kwa wenza wa ndoa.
Kant (1997:388), katika kitabu chake kiitwacho, "Lectures on Ethics," kama kilivyotafsiriwa na Peter Heath na kuchapishwa huko Cambridge katika kampuni ya Cambridge University Press, anasisitiza jambo hili kwa maneno yafuatayo:
"Ikiwa mtu mmoja atakubali kuutoa kabisa mwili na roho yake yote kwa mtu mwingine, katika tabu na raha, bila kutofautisha hali hizi, ambapo mtu wa pili anakuwa amepata haki zote za kimapenzi juu ya mtu wa kwanza, lakini mtu wa kwanza asipate kipimo sawa cha haki za kimapenzi kutoka mtu wa pili, basi kuna ukosefu wa usawa hapa, kwa maana kwamba mahusiano haya yanavunja kanuni ya usawa wa binadamu."
3. Kwa hiyo ndoa za mitala zinavunja ibara ya 12(1) ya Katiba ya Tanzania, na hivyo, kifungu cha 10(2)(a) cha sheria ya ndoa ya mwaka 1971 kinachoruhusu ndoa hizo za mitala ni batili.
4. Ndoa isiyo ya mitala, yaani mwanamume mmoja aliyefunga ndoa na mwanamke mmoja (monogamy), haikanushi kanuni ya usawa kati ya binadamu mwanamume na binadamu mwanamke, kama ilivyotajwa katika ibara ya 12(1) ya Katiba ya Tanzania.
5. Kwa hiyo, ndoa isiyo ya mitala haivunji Katiba ya Tanzania.
6. Mfumo dume ni itikadi inayopinga kanuni ya usawa kati ya binadamu mwanamume na binadamu mwanamke.
7. Ndoa za mitala zinapinga kanuni ya usawa kati ya binadamu mwanamume na binadamu mwanamke.
8. Kwa hiyo, ndoa za mitala zinakuza mfumo dume.
9. Kila mwanamke anayeamini katika usawa wa binadamu mwanamume na binadamu mwanamke hawezi kukubali ndoa za mitala.
10. Kila mwanamke anayeamini katika usawa wa binadamu mwanamume na binadamu mwanamke, akifunga ndoa ya mitala atakuwa anaona wivu siku zote.
11. Kwa hiyo, inafuata kimantiki kwamba, mwanamke aliye katika ndoa ya mitala na haoni wivu anakuwa haamini katika usawa wa binadamu mwanamume na binadamu mwanamke.
Kwa kuhitimisha basi, napenda kusema yafuatayo: Huwa tunapima utiifu na ukiukaji wa kanuni za kisheria na kimaadili kwa kutumia chujio la kimantiki lifuatalo:
- Dokezo kuu: Kama kuna Kanuni X iliyovunjwa, basi, kuna ukaidi wa kanuni umefanyika.
- Dokezo dogo: Kwa mujibu wa seti ya ushahidi Y, Kanuni X imevunjwa.
- Hitimisho: Kwa hiyo kuna ukaidi dhidi ya Kanuni X umefanyika.
- Dokezo kuu: Kama ibara ya 12(1) ya Katiba ya Tanzania (1977) inayotetea usawa wa binadamu wote bila kujali tofauti za kijinsia imevunjwa, basi kuna ukaidi wa kikanuni unatokea.
- Dokezo dogo: Ni ukweli kwamba, kuna vitendo vya kuhamasisha , kutetea na kufungisha ndoa za mitala ambazo zinapingana na kanuni ya usawa kati ya wanaume na wanawake.
- Hitimisho: Kwa hiyo, kuna ukiukaji wa kikanuni unafanyika dhidi ya ibara ya 12(1) ya Katiba ya Tanzania (1977).
Lakini, kwa nini natoa wito huu?
Kati ya changamoto alizokumbana nazo Raia Namba Moja mara tu baada ya kukalia kiti chake, zifuatazo ni kubwa:
(1) Ubaguzi wa kijinsia kutoka na itikadi ya mfumo-dume;
(2) Ubaguzi wa kikanda (Ubara-na-Uzanzibara) kutokana na mfumo-tata wa Muungano;
(3) Ubaguzi wa kimbari kutokana na historia tata ya utumwa iliyojengeka juu ya tofauti zinazotukuzwa na mfumo-mbari; na
(4) Changamoto ya viatu vipana vya mtangulizi wake, na hasa ukiangalia kasi aliyokuwa nayo katika miradi mikubwa ya kitaifa.
Sisi watu tunaoamini katika kanuni ya "usawa wa binadamu" tulipambana kumsaidia Raia Namba Moja apate usingizi kwa kushambulia changamoto moja baada ya nyingine.
Ubaguzi unaotokana na mfumo-dume tuliupatia mwarobaini wa kisayansi, kifalsafa, kiteolojia na kisiasa. Lakini sasa, kuna kauli za Raia Namba moja zinatukuza mfumo-dume, ama kmoja kwa moja au kwa njia ya mzunguko. Zinafuta juhudi zetu.
Tatizo la Ubara-na-Uzanzibara limekuwa likififia kadiri kero za Muungano zinavyoshughulikiwa kisiasa na kisheria. Lakini, kuna maamuzi ya serikali ya Raia Namba Moja yanaleta fikra kwamba bado kanuni ya mwamba ngoma huvutia kwake inatumia mahali isipohitajika.
Ubaguzi unaotokana na mfumo-mbari tumepambana nao kihistoria, kifalsafa, kisayansi na kiteolojia, na tunaendelea.
Lakini, maudhui ya ajabu katika mkataba wa awali wa kampuni ya DP World unaonuka harufi ya utumwa kati ya Mwafrika wa Tanzania na Mwaraba wa Dubai, umejenga tena mazingira ambayo, ama moja kwa moja, au kwa njia ya mzunguko, yanaonekana kukumbatia itikadi ya mfumo-mbari (the racial superiority question), ambao ulikuwa msingi wa utumwa wa Mwafrika.
Mkataba huu umefuta juhudi zetu za kuwafanya watu waache kuwatilia shaka baadhi ya Watanzania wasio na asili ya kibantu. Sasa wau wanaanza kujiuliza swali: Hivi viongozi wa kitaifa wasio na asili ya KIbantu ni salama kiasi gani kwa taifa letu kisiasa, kiuchumi na kijamii? Kwa mujibu wa yaliyomo kwenye mkataba wa DP World hili ni swali halali.
Na changamoto ya viatu vikubwa vya mtangulizi wake anaishughulikia yeye kama anavyoona inafaa, lakini sisi baada ya kumtengenezea mazingira mazuri. Lakini, mara zote mapambano yetu yanaongozwa na maudhui ya ibara ya 12(1) ya Katiba ya nchi yetu. Huu ni moyo wa Taifa.
Kwa hiyo ningependa Raia Namba Moja, na washauri wake, waelewe kwamba, kila wanalofikiri, kusema na kufanya lisikwaruze ibara ya 12(1) ya Katiba ya Tanzania (1977). Na wanapoikwaruza kanuni hii, basi wafanye hima kukarabati mawazo, maneno na matendo yao. Vinginevyo wanabatilisha juhudi zetu.
Nawasilisha