Stephano Mgendanyi
JF-Expert Member
- May 16, 2020
- 3,119
- 1,429
KIWANJA CHA NDEGE CHA KISASA KUJENGWA NJOMBE KARIBUNI
Naibu Waziri wa Uchukuzi David Kihenzile amesema kwa mwaka wa fedha 2025/2026 Serikali inatarajia kutenga fedha kwa ajili ya kukamilisha upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa kiwanja cha ndege cha kisasa cha Njombe, na tayari Serikali imeidhinisha taarifa za awali za upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ambapo zaidi ya shilingi milioni 800 zilitengwa kwa mwaka 2024/2025.
Akijibu swali la Mbunge wa Njombe Mjini, Deodatus Mwanyika bungeni Dodoma Aprili 10, 2025, Kihenzile amesema mara baada ya taratibu hizo kukamilika, ujenzi utaanza kulingana na upatikanaji wa fedha.
Akielezea umuhimu wa Kiwanja cha Ndege cha Njombe, Kihenzile amesema ni muhimu kimkakati hususani kwenye kukuza uchukuzi katika usafiri wa anga kijamii, kiuchumi na kibiashara ikiwemo biashara ya mazao ya misitu, mbogamboga, matunda (maparachichi) ambayo yote hayo huzalishwa na kusafirishwa nje ya nchi.
Aidha, kufuatia uboreshwaji wa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) uliopelekea manunuzi ya ndege kubwa ya mizigo aina ya Boeing 767-300 F, Serikali kupitia Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) kwa kushirikiana na Mkoa wa Njombe imekamilisha uchambuzi wa eneo jipya la TANWAT kwa ajili ya ujenzi wa kiwanja kipya cha ndege, na sasa Serikali inaendelea na taratibu za utwaaji wa ardhi.