Wabunge wetu waachane na fikra mgando zilizozoeleka ambazo ni potofu za kuzani kwamba mwarobaini wa matatizo yetu ni kupandisha bei ya petroli, mafuta ya taa, bia na soda.
Kuongeza bei za petroli kwa shilingi 100 kwa lita kama baadhi ya wabunge walivyoshupalia itaongeza ugumu wa maisha kwa wananchi wote na wala haitasaidia cho chote kwenye upatikanaji wa maji. Bado fedha zitakazopelekwa kwenye miradi ya maji zitakuwa asilimia ndogo tu ya bajeti. Mwaka jana ni asilimia 25% tu ya bajeti hiyo ndiyo iliweza kupatikana.
Wabunge wanatakiwa kujikita kwenye chanzo na sababu hasa ya serikali kushindwa kutekeleza bajeti kwa kiwango cha kuridhisha, na kupendekeza ufumbuzi wake. Sababu kuu ni misaada/ mikopo kutoka nje kutopatikana (budget support) kama ilivyopangwa. Vyama vya upinzani vimekuwa mbele kukwamisha misaada hii. Vimekuwa hadi vinazunguka nchi mbali mbali duniani kuzitaka nchi hizo ziiwekee vikwazo vya kiuchumi nchi yetu kwa sababu mbali mbali za kipuuzi. Tulishuhudia Maalim Seif alichofanya kwenye ziara zake huko Amerika na Ulaya baada ya kuukosa urais. Tulishuhudia ziara ya Mbowe na timu yake huko Ulaya baada ya Lowassa kukosa uraisi. Tulishuhudia furaha waliyopata upinzani baada ya Millennium Challenge kutunyima matrillion ya pesa.
Sasa kama serikali ikikosa hizo source za nje, lazima miradi mingi ya kimaendeleo hususani ya maji itaathirika. Maana fedha za uendeshaji wa serikali kama kulipa mishahara na baadhi ya madeni (ya wakandrasi, waalimu nk) lazima ifanyike. Gharama hizi za uendeshaji wa serikali zinakomba karibia asilimia 90% au zaidi ya makusanyo yetu yote ya pesa za ndani na hivyo kusababisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo kuwa asilimia 0% hadi 25% tu; tena ni baada ya kubana matumizi kweli kweli (ufisadi, watumishi hewa/ feki nk). Kuongeza bei ya petroli, bia na soda haitasaidia cho chote.
Sasa nani wa kulaamiwa hapa? Halafu unakuta watu hawa wanaotusababishia haya ndiyo wanaoshupaa kuibana serikali kwa nini haitoi pesa zote zilizopangwa kwenye bajeti. Watu hawa ni wa kupuuzwa. Kamwe serikali isikubali mawazo yao ya kuongeza bei ya petroli na mafuta ya taa. Lengo lao ni kutaka wananchi wasiipende serikali yao kwa kuwaongezea ugumu wa maisha ili ndoto zao za urais zipate kutimia.