tonicimmobility
JF-Expert Member
- Jun 17, 2025
- 493
- 1,038
Soma pia: Kimbunga Ragasa chafika China baada ya kuua watu 17 Taiwan
Kimbunga kikali kilichopewa jina la “Melissa” kinaripotiwa kuikaribia Jamaica kikiwa na kasi kubwa ya upepo na mvua nyingi. Wataalamu wa hali ya hewa wanasema kuwa kimbunga hicho ni dhoruba kali zaidi duniani mwaka huu, na huenda kikawa kimbunga kibaya zaidi kuwahi kuikumba Jamaica.
Kwa mujibu wa Kituo cha Habari Kimataifa cha #AlJazeera, leo Oktoba 28, 2025, Kituo cha Kitaifa cha Vimbunga cha Marekani (National Hurricane Center - NHC) kimesema kimbunga hicho ni dhoruba ya kiwango cha juu kabisa cha hatari, kikiwa na kasi ya upepo wa hadi kilomita 282 kwa saa.
Wataalamu wa kituo hicho wamesema kuwa kimbunga hicho kimeendelea kuongezeka nguvu kutokana na joto la juu la bahari katika eneo la Karibea, jambo lililochangia kuipa nguvu zaidi dhoruba hiyo.
kimbunga hicho kinaripotiwa kujongea kwa mwendo wa taratibu chini ya kilomita tano kwa saa, hali inayoashiria kuwa maeneo yatakayopitiwa yatakumbwa na mvua kubwa kwa muda mrefu, na hivyo kuongeza hatari ya mafuriko makubwa pamoja na maporomoko ya ardhi.
Mamlaka nchini Jamaica zimefunga viwanja vya ndege, shule, na huduma nyingine za umma. Vituo vya dharura na makazi ya muda vimefunguliwa kwa ajili ya kuwahifadhi wakazi waliolazimika kuondoka makwao. Inaelezwa kuwa serikali pia imetenga bajeti ya dharura kusaidia juhudi za uokoaji na utoaji wa misaada.
Kituo cha Kitaifa cha Vimbunga Marekani pia kimeonya kuwa mawimbi makubwa na hatari ya baharini yanaweza kufikia hadi futi 13 katika maeneo ya pwani ya kusini mwa Jamaica, hali inayotishia maisha ya wakazi wa maeneo ya karibu na bahari.
Ripoti zinaeleza kuwa watu wengi nchini Jamaica tayari wamehamishwa kutoka maeneo hatarishi, huku wengi wakiwa na wasiwasi kwa siku kadhaa wakisubiri kuona nini kitatokea baada ya dhoruba hiyo.
Hadi sasa, watu watatu wameripotiwa kupoteza maisha nchini Jamaica kutokana na kimbunga hicho, huku wengine wanne wakifariki dunia huko Haiti na Jamhuri ya Dominika.