Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,315
- 33,109
Ziara ya Rais Jakaya Kikwete kwenye kata ambayo haijawahi kutembelewa na rais yeyote tangu Tanzania ijitawale, juzi ilikuwa ngumu baada ya baadhi ya magari kukwama kwa muda likiwamo na la Mama Salma.
Hali hiyo iliyotokea juzi ilitokana na ubovu wa barabara ambayo ililazimu trekta kutumika kuyakwamua.
Adha hiyo iliyapata magari hayo ambayo yanatumiwa na watu waliopo kwenye ziara ya Rais Kikwete mkoani Tabora.
Rais alikuwa akiendelea na ziara yake akitokea Tabora Mjini kwenda kata ya Kitunda ambayo haijawahi kutembelewa na rais yeyote tangu Tanzania ipate uhuru mwaka 1961.
Kutokana na ubovu wa barabara, helikopta ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) ililazimika kuitwa kutoka Tabora mjini kwa ajili ya kwenda kumchukua rais kumpeleka Wilaya ya Sikonge.
Baada ya Rais kumaliza kuhutubia wananchi katika kata hiyo, helikopta hiyo ilitua na kumchukua tena kumrudisha Sikonge.
Aidha, baadhi ya magari yaliyokuwa katika msafara huo nayo yalizama katika madimbwi na kulazimika kuvutwa na trekta.
Akizungumza na wananchi wa kata hiyo ya Kitunda, Rais alifurahishwa na maendeleo ya elimu na kisha akatoa Sh. milioni sita kwa ajili ya ujenzi wa shule katika kata tatu za tarafa ya Kiwelu wilayani Sikonge.
Alisema elimu ndiyo njia pekee ya kuwakomboa wananchi hivyo lazima waikazanie.
Aidha, Rais aliagiza ijengwe barabara inayopitika muda wote kwa mwaka badala ya ilivyo sasa. Kuhusu maji, pia aliagiza yapelekwe kabla ya Julai ili atakaporudi akute kuna huduma hiyo.
Aliwataka wananchi kubadilika na kuachana na tabia ya kuishi kwa kuhamahama kufuata malisho ya mifugo.
Hii tabia imepitwa na wakati, lazima mbadilike na kuanza kufuga kwa njia za kisasa ikiwemo kupanda nyasi za malisho badala ya kuhamahama kufuata malisho, alisema. Kwa upande wao wananchi katika eneo hilo walifurahi kutokana na kutembelewa na rais ikiwa ni mara ya kwanza tangu wapate uhuru.
Wakati huo huo, Rais Kikwete amewaonya Watanzania kuachana na tabia ya kutegemea wafadhili wawafanyie kila kitu, badala yake amewataka wajitahidi kujiletea maendeleo kwa kutumia raslimali chache walizonazo.
Alitoa onyo hilo jana wilayani Uyui, Mkoa wa Tabora alipokuwa akizungumza na wakazi wa kijiji cha Mbola katika kata ya Ilolangula alipotembelea mradi wa Millennium Village (Kijiji cha Mileniamu).
Alisema wafadhili bado wanahitajika kuwasaidia wananchi kujikwamua kiuchumi, lakini sio kazi yao kuwafanyia wananchi kila kitu. Sisi wananchi tatizo letu tunataka hawa wafadhili watusaidie kila kitu, jambo ambalo haliwezekani, alisema.
Rais Kikwete alitembelea mradi huo ambao unawasaidia wakazi wa vijijini 15 katika Wilaya ya Uyui ambao unafadhiliwa na nchi mbalimbali zikiwemo Japan na Marekani na kusimamiwa na Shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP). Aliwaambia wananchi hao kuwa waone misaada wanayopewa sasa ni kama changamoto ili waweze kujitahidi kujikwamua wenyewe kimaisha.
Mradi huo unalenga kuwajengea uwezo wananchi wa vijiji 15 kwa kuwasaidia katika nyanja za kilimo, afya, huduma za jamii, kuondoa umasikini na kuwapatia pembejeo ikiwemo mbolea ya ruzuku na kuwapatia elimu. Aliongeza kuwa kama wananchi wataendeleza dhana ya kuisubiri serikali kuwaletea maendeleo, watachelewa na kuachwa nyuma na watu wengine duniani.
Alifafanua kuwa Tanzania na nchi nyingine za Kusini mwa Jangwa la Sahara ni maskini na kwamba wananchi wakiendelea kutegemea kuletewa maendeleo watakuwa wanajidanganya.
Akisisitiza umuhimu wa kujitegemea, Rais Kikwete alitoa mfano wa mji wa Osaka nchini Japan ambao pato lake linazidi nchi za Afrika zilizopo Kusini mwa Jangwa la Sahara.
Aliwasisitiza wananchi kuanza angalau na walichonacho ili wakiwaita wafadhili wawe wamesogea kidogo.
Meneja wa mradi huo, Dk. Gilson Nyadzi, alisema umepata mwitikio mkubwa kutoka kwa wananchi.
Alisema wameanza vizuri katika sekta ya maji ambapo wamechimba visima, kujenga zahanati, shule na kuhimiza kilimo bora katika vijiji husika. Aidha, alisema wanatarajia kutumia zaidi Sh. milioni 350 kujenga barabara.
Katika hatua nyingine, Rais Kikwete aliwatahadharisha wakazi wa kata hiyo kuacha kutumia mbolea ya ruzuku wanayopewa na wafadhili kulimia tumbaku.
Alifafanua kuwa tumbaku ni kitu hatari ambacho wafadhili hawawezi kukubali kukifadhili hivyo wananchi wasithubutu kuwachokoza.
Akitoa taarifa kwa Rais, Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Abeid Mwinyimusa, alisema hivi sasa watoto wanapenda kwenda shule kwa kuwa wanapatiwa chakula shuleni.
Mheshimiwa mahudhurio yameongezeka, baada ya wazazi kuchangia mahindi ili watoto wao waweze kupata chakula, alisema.
Rais Kikwete jana aliweka jiwe la msingi katika ujenzi wa Chuo cha Jamii ambacho kitakuwa kinatoa mafunzo mbalimbali, kuzindua miradi ya visima iliyofadhiliwa na UNDP.
CHANZO: NIPASHE