Kashfa polisi Morogoro kuwalinda wauza mihadarati

engmtolera

JF-Expert Member
Oct 21, 2010
5,150
1,437
KASHFA POLISI MOROGORO KUWALINDA WAUZA MIHADARATI17/11/2011
0 Comments


Siku chache baada ya Kikosi Maalumu cha Kupambana na Ujambazi mkoani Morogoro 'Anti-Robery', kutuhumiwa kujihusisha na mtandao wa majambazi, kashfa nyingine imelikumba jeshi hilo ambapo safari hii linadaiwa kuwalinda wafanyabiashara wakubwa wa dawa za kulevya mkoani humo.

Kashfa hiyo imetolewa juzi na mzazi wa mwanafunzi Elizaphan Shadrack (16) anayesoma kidato cha pili katika Shule ya Sekondari Morogoro, Bw. Shadrack Gando, ambaye analituhumu jeshi hilo kushindwa kuwakamata wafanyabiashara sita wa dawa ya kulevya mkoani humo ambao wamekuwa wakimtumia mtoto wake kusafirisha na kuuza dawa hizo.

Bw. Gando, ambaye pia ni mtumishi katika shule hiyo, alitoa tuhuma hizo kwa waandishi wa habari na kudai kuwa, madai hayo ameyafikisha katika vyombo mbalimbali vya usalama likiwemo Jeshi la Polisi mkoani humo, Ofisi ya Usalama wa Taifa, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), pamoja na Kitengo cha Kupambana na Dawa za Kulevya nchini.

Alisema pamoja na kupeleka taarifa za wafanyabiashara hao katika ofisi hizo, hadi sasa hakuna hatua zozote zilizochukuliwa.

Akizungumzia mazingira ya mtoto wake kushirikishwa katika biashara hiyo, Bw. Gando alisema hali hiyo ilianza kujionesha Aprili mwaka huu baada ya kutoweka nyumbani kwake wiki mbili na nusu, “Tukiwa nyumbani, tulishtuka kuona teksi ikisimama na kumshusha Shadrack ambaye alikuwa amelewa hali ambayo ilitupa wasiwasi mkubwa, tulijaribu kumuhoji dereva kujua ni wapi amemtoa mtoto na kutuambia yeye alimuokota katikati ya mji, eneo la Masika akiwa hajitambui, tulimchukua na kumpeleka hospitali kwa ajili ya matibabu,” alisema Bw. Gando.

Alisema wiki tatu baadae, Shadrack alitoweka tena katika mazingira ya kutatanisha na kuonekana mkoani Arusha akiwa na watu wanaodhaniwa kujihusisha na biashara hiyo.

Aliongeza kuwa, baada ya kupata taarifa hizo, alimpigia simu ndugu yake wa karibu ambaye ni mtumishi katika Kitengo cha Kupambana na Dawa za Kulevya mkoani humo ili afuatilie nyendo za mtoto huyo lakini wakati akiendelea na kazi hiyo, Shadrack alirudi nyumbani kwao Morogoro.

“Baada ya kurejea nyumbani, tuliamua kumpeleka Kituo Kikuu cha Polisi mkoani hapa ili aweze kuhojiwa na kutaja majina ya watu ambao wanamtumia katika biashara ya dawa za kulevya mkoani hapa na Arusha mbele ya askari na Mkuu wa Polisi wa Wilaya, “Orodha ya wafanyabiashara waliotajwa, inahusisha watoto wa wafanyabiashara wakubwa mkoani hapa na mmoja ni ndugu wa kigogo mstaafu wa Jeshi la Polisi,” alisema Bw. Gando.

Alisema jambo la kushangaza, jeshi hilo halijachukua hatua zozote kwa wahusika waliotajwa katika orodha ambapo hivi sasa, mtoto wake ametoweka tena nyumbani kwake, “Nimekuwa nikipokea simu za vitisho kutoka kwa wahusika waliotajwa polisi, suala hili pia nimelifikisha katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa ambaye alimpa maelekezo Kamanda wa Polisi Mkoa ili aweze kulishughulikia, binafsi naamini kuna harufu ya rushwa kwa sababu wahusika wa biashara hii wanafahamika. “Wafanyabiashara wa dawa za kulevya mkoani hapa wanafahamika na wamekuwa wakijiita vigogo wa kuuza unga,” alisema.

Akizungumzia tuhuma hizo, Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani humo, Joseph Rugila, alikiri jeshi hilo kufanya mahojiano na Shadrack pamoja na kupokea majina ya watu wanaodaiwa kujihusisha na biashara hiyo mkoani humo, “Kimsingi tunaendelea na upepelezi, tuhuma hizi ni nzito hivyo tunahitaji kufanya uchunguzi makini ili tujiridhishe na madai haya vinginevyo unaweza kumtuhumu mtu lakini ukakosa ushahidi,” alisema Kamanda Rugila.

Kamanda wa TAKUKURU mkoani humo, Bi. Stella Mpanju, naye alikiri kupokea tuhuma hizo kwa mzazi wa mwanafunzi huyo na kudai kuwa, maofisa wake wanaendelea kuzifanyia kazi ili kubaini kama kuna mazingira ya rushwa ambayo yanachangia watuhumiwa washindwe kukamatwa.

Wiki iliyopita, Kamanda wa Polisi mkoani humo, Adolfina Chialo, aliamuru kukamatwa na kuwekwa mahabusu askari wake Bw. Donald Mathew, kupisha uchunguzi wa tuhuma alizotoa kwa askari wenzake na maofisa wa jeshi hilo.

Askari huyo mwenye cheo cha DC namba F 3276, anadaiwa kutoa tuhuma hizo kupitia gazeti moja linalotoka kila wiki kuwa baadhi ya askari wenzake, wanahusika kuwafanyia matendo maovu raia wasio na hatia madai ambayo yalipingwa na Kamanda Chialo.




source: Kashfa Polisi Morogoro kuwalinda wauza mihadarati - Wavuti
 
mambo ya kenya hayooooooooooo,hii ni kawaida sana kwa Nchi za Kiafrica
 
Back
Top Bottom