Kampuni ya kigeni ya Security Group inavyokwepa kodi Tanzania
Kampuni ya ulinzi ya kimataifa ya Security Group, ambayo inatoa huduma ya ulinzi kwa Umoja wa Mataifa (U.N.), mabalozi, mabenki na ofisi nyingine kubwa nchini Tanzania, inahusika na kashfa kubwa ya kukwepa kodi, utapeli, kuwakosesha ajira Watanzania na kuvunja sheria za nchi.
Kampuni hiyo inafanya utapeli mkubwa kwa kuajiri wafanyakazi wachache wake wenyewe na badala yake kuwavalisha sare (uniform za Security Group) wafanyakazi wa kampuni za ulinzi za Kitanzania ili kukwepa kodi na gharama za uendeshaji.
Security Group Tanzania ina wafanyakazi wa kwake wenyewe takriban 300 tu, lakini inatumia zaidi ya wafanyakazi 1,000 wa kampuni za ulinzi za Kitanzania kwa kuwavalisha sare zake na kuwaweka walinde ofisi za Umoja wa Mataifa na nyinginezo.
Kampuni hiyo ya Security Group inalipwa mabilioni ya shilingi kwa kutoa huduma kwa kuwachaji wateja wake kama kampuni ya kimataifa kumbe inatumia walinzi wa kampuni za Kitanzania wanaolipwa mishahara midogo wafanye kazi hizo.
Kuna mtandao wa raia wa Kenya ambao unatumika kufanikisha wizi huu mkubwa na unyonyaji wa wafanyakazi wa Tanzania.
Security Group Tanzania inaongozwa na Mkenya ambaye anashirikiana na kampuni ya ulinzi iliyosajiliwa Tanzania, Iron Side, lakini inayoongozwa na Mkenya ili kuhakikisha ukwepaji kodi huu.
Kampuni ya Iron Side ina wafanyakazi zaidi ya 700 ambao wanalipwa mshahara mdogo kama wafanyakazi wa kampuni ya kiTanzania. Hata hivyo, Security Group inawavalisha sare zake wafanyakazi hawa na kuwafanyikisha kazi kama wafanyakazi wa kampuni ya kimataifa ya ulinzi lakini inawapunja mshahara.
Kampuni hii ya Security Group pia inaitumia kampuni nyingine ya ulinzi ya Kitanzania, Insight Security, kufanya ukwepaji huu mkubwa wa kodi.
Kwa mujibu wa sheria za nchi, makampuni ya ulinzi ya kimataifa yanatakiwa yawalipe wafanyakazi wao mshahara wa juu kuliko makampuni ya ulinzi ya Kitanzania.
Wadau wa sekta ya ulinzi wanasema kuwa makampuni ya kimataifa ya ulinzi yanatakiwa yawalipe wafanyakazi wake kima cha chini cha mshara (net salary) cha shilingi 154,000.
Makampuni ya Kitanzania yanatakiwa kuwalipa wafanyakazi wake mshahara usiopungua 117,440.
Kampuni hii ya Security Group inawatapeli wateja wake wakubwa Tanzania, ikiwemo ofisi za Umoja wa Mataifa na mabenki, kuwa inawawekea walinzi waliopata mafunzo ya kimataifa kumbe inatumia wafanyakazi wa kampuni ndogo ambao hawajapata mafunzo ya kutosha na kuwavalisha sare zake ili kukwepa kodi.
Pia kampuni hii inawanyima haki ya ajira na mishahara Watanzania na kukwepa kodi za serikali.
Taarifa hizi zimetolewa na wafanyakazi wa kampuni hiyo ya Ulinzi (anonymous) ambao wamechoshwa na kunyonywa na kampuni hii ya kigeni ya Security Group inayowatumia kwa kuwavalisha sare za kampuni hiyo ili ipate tenda kubwa za ulinzi, lakini inawapunja mishahara na kukwepa kodi za serikali.