Godbless J Lema
Arusha MP
- Sep 28, 2013
- 92
- 2,205
Kamanda Mawazo ameuawa na Mfumo wa Jeshi la Polisi
Alikuwa kijana aliyeamini katika Mabadiliko, alitembea Nchi nzima kwa shida kujenga ufahamu kuhusu Ukweli, Haki na Usawa. Ameuwawa akiwa akitoka kwenye kazi za Chama chake, akavamiwa, akapigwa na baadae kufariki. Ni nani amefanya kitendo hiki?
Watu wengi mnalaumu Wanachama wa CCM kwani ndio waliofanya kazi hiyo, hapana, mnakosea. Mawazo ameuwawa na mfumo wa Serikali na Jeshi la polisi unaojali ukatili na uovu. Mauaji yataendelea sana, kwani wengi wamekishauwawa na kuumizwa bila Serikali kuchukua hatua.
Polisi wanaowajibika kwa utawala unaojali ukatili, ubaya, na uovu ni lazima watamsaidia Shetani kufanya kazi. Polisi wanaoshindwa kukamata wahalifu na na kuwajibisha wahalifu, wao ndio wanaosaidia Taifa hili kuingia Vitani, Matukio ya Green guard kuvamia na kujeruhi na hata kuua ni mengi katika Taifa hili, Wahalifu wanalindwa na sasa wana ujasiri wa kufanya wanavyotaka. Sioni siku nyingi za Amani Tanzania, magari ya kuwasha na silaha za moto zitashindwa kupambana na Umma uliojawa hasira na Uchungu, propaganda pia zitashidwa kutengeneza hali ya usalama, masikitiko yangu ni kuwa hali hii itamkuta kila Mtu aidha ni mwenye haki au ni asiye na haki. Usalama wa Nchi haujengwi na wingi wa silaha wala wingi wa Askari, Isipokuwa utawala unaojali Haki na Usawa.
Uhalifu wa namna hii katika Taifa hili unajengwa na Polisi walioshindwa kazi zao kwa kuzingatia Uadilifu na Sheria za kazi, Kamati za Siasa za Chama Tawala ndio zinatoa maelekezo ya utendaji wa Jeshi la Polisi. Kwa mfano hapa Arusha RPC ni mdau namba moja wa CCM na hivi karibuni katika vikao vyake vya kampeni ya kumsaidia mgombea Ubunge wa CCM alichokaa na Viongozi wa bodaboda alitoa maelekezo mabaya na ya uharibifu dhidi yangu, unafikiri nini? Ni lazima Vijana hawa kama watakosa Utu, wanaweza kufanya uhalifu mbaya sana kwangu, kwani anayepaswa kulinda amani ndiye anayesimamia Mipango mibaya ya uhalifu.
Mambo haya ni lazima yafike mwisho. Polisi mnapaswa kuwa na hekima sasa na mtambue kuwa hali ya Usalama Nchini haiko salama, Watoto wenu, Wazazi wenu, Wake zenu na familia zenu ziko Mitaani, Ukatili na Uonevu unapoongezeka kwa Watu wanyonge, ndivyo hivyo Watu hawa wanaanza kufikiria njia mbadala ya kujitetea, naona Binadamu wa Tanzania anaanza kuelekea huko.
Ni nani anafuata baada ya Mawazo? Ni vita ya kujilinda au kukubali kuwa Maiti kwa njia ya mapanga na vipigo? Tulitafakari jambo hili wote, kwani Utulivu huu tulionao hauna muda mrefu kutoweka na ndipo Nchi yetu itakuwa Nchi ya Ukiwa.
Moyo wangu umeumia na kuchoka sana nahitaji msaada zaidi, Ni Kijana rafiki mzuri niliyemuingiza kwenye Siasa, nilimpa Suruali, Mkanda, na Koti wakati ninampleka kumtambulisha kwa ajili ya kura za maoni kwenye Chama cha Tlp wakati huo, tuliishi wote na familia zetu zikapendana sana, hakuwahi kuwa mnafiki juu ya anachokipigania.
Mawazo umeuwawa? Kosa lako ni kuwa CHADEMA na kufanya Siasa? Mkuu wa Wilaya ya Geita atafurahi sasa, kwani alishawahi kutamani kuona maiti yako na leo ameshuhudia, Rafiki zako tunatafakari kwa kina na Uchungu mkubwa.
Ni heri Vita inayotafuta Haki na Usawa kuliko Amani inayopumbaza na kudhalilisha Utu wa Binadamu.
Nilikuwa nakupenda sana Mawazo.
Godbless Jonathan Lema