Jirani yangu wa kule Goba hakuwa mtu wa kawaida

Jirani yangu wa kule Goba hakuwa mtu wa kawaida - 04

Kikao kilikwisha kwa pande zote mbili kuelewana, mwenye nyumba alisema baada ya siku tatu mafundi watakuja kwaajili ya kuanza ujenzi lakini pia hapohapo kabla kikao hakijaisha akasisitizia kuhusu kodi yake, hili nililijua tu litakuja, alisema na yeye atapata nguvu zaidi ya kuboresha miundombinu endapo sisi tutatoa pesa zake kwa wakati, baada ya kikao kuisha aliaga na kwenda zake na kila mtu akaendelea na shughuli zake, angalau sasa na mimi nikapumzika na macho ya yule shemeji, macho ambayo sikuelewa yanamaanisha nini zaidi ya kunitisha.

Zikapita siku mbili, mafundi hawakuja kama tulivyoambiwa, ikapita siku ya tatu na ya nne, hola, mpaka wiki nzima iliyoyoma si fundi wala mhandisi aliyekuja, mwenye nyumba anatupiga tu kalenda.

Siku moja nikiwa niko nyumbani, sikumbuki haswa zilipita siku ngapi tangu tufanye kile kikao, katika majira ya saa saba usiku nikasikia mtu anafungua mlango wake, sikujua ni nani maana mimi nilikuwa ndani sebuleni lakini ni bayana alikuwa ni jirani mmojawapo katika milango ile miwili, kidogo mlango wa grill ulifunguliwa kakaaa-kakaaaa kisha kukawa kimya, nami nikawa kimya nikiwaza huenda mtu anaenda maliwatoni hivyo nikaendelea na mambo yangu ya kutazama runinga.

Nilikaa kama nusu saa lakini sikusikia mlango ule wa grill ukifungwa, na kwa namna yoyote ile mlango ule usingeweza kufungwa bila kutoa sauti, hapo nikapata shaka. Nilitoka sebuleni nikaenda chumbani ili nipate kuchungulia nje kuna nini kinaendelea, nilipofungua pazia la dirisha kwanza nikatazama pikipiki yangu, nikaona kuna usalama, nikaangaza huku na kule lakini sikumwona mtu, nje kulikuwa kimya sana.

Nilitulia kusikiliza labda kuna mtu bafuni, napo sikusikia kitu, kila pembe ilikuwa kimya sana. Hapo nikapata wasiwasi. Niliufungua mlango nikaenda nje kutazama maana ule mlango wa grill kuwa wazi kwa muda wote huo haikuwa salama kabisa ukizingatia tulinusurika kupigwa tukio mara ya mwisho, huko nje nikatazama upande wa magharibi, hamna mtu, nikatazama upande wa mashariki nao hamna mtu, kabla ya kurudi ndani nikaenda kule bafuni, bafu zote zilikuwa zimezimwa taa hivyo nikahitimisha hamna mtu humo, basi nikarejea mlangoni na kuurejeshea ule mlango wa grill pasipo kuufunga na ufunguo ili kama kuna mtu huko nje basi ataingia na kuufunga mwenyewe, mimi nikareja sebuleni nikaendelea kutazama televisheni.

Nilitazama mpaka nilipohisi naelemewa na usingizi ndipo nikaenda zangu chumbani, huko nikajilaza na kuskilizia lakini muda wote huo sikusikia mlango wa grill ukifunguliwa, kulikuwa ni kimya tu kama hapo awali, nikajiuliza nini kinaendelea au ni mimi ndo' mwenye matatizo? Mpaka napitiwa na usingizi sikupata kusikia kitu, asubuhi palipokucha wakati naenda kuoga niende kazini, pale bombani, nilikutana na jirani yangu wa mlango mwingine ndani ya ile nyumba kubwa, mwanamke huyo alikuwa anafua nguo zake hapo nje, wanawake hawa huwa wana utaratibu wa kuamka mapema kufua kwaajili ya kuwahi kamba, baada ya kunisalimu aliniuliza,

"Shemeji, ni wewe ndo' uliacha mlango wa grill ukiwa wazi jana usiku?"

Nikamweleza namna mambo yalivyotokea kuwa mimi sikuuacha wazi bali niliurejeshea tu baada ya kusikia mtu alitoka, ajabu akaniambia kuwa mumewe asubuhi ya mapema sana alipotoka aliukuta mlango ukiwa wazi kabisa, umeachama kama mdomo! Nikastaajabu kusikia hayo, nilijiuliza ni muda gani mlango ulifunguliwa lakini sikupata majibu, nikaenda zangu kuoga nikilenga kuwa siku n'takayokutana na BIGI nimuulize kuhusu jambo hilo, sikuwa najua ni lini ila nilitumai ndani ya wiki hiyo basi nitambahatisha.

Ikapita siku mbili, sikumwona BIGI wala mkewe, siku ya tatu yake nikiwa sebuleni majira yangu ya usiku mtulivu, siku hiyo sikuwa natazama televisheni bali namalizia kazi fulani kwenye laptop, nikasikia mtu akiufungua mlango na kisha akaufungua mlango wa grill kakakaaa-kaaakaa, nikakaa tenge, mara hiyo sikutaka kupuuzia nilinyanyuka upesi nikaenda chumbani kutazama, ile kufungua tu pazia nikamwona mtu akiishia kwa kulifunga geti dogo, sikumjua mtu huyo ni nani kwani nilichoambulia kukiona ni mkono tu tena kwa muda mchache mno, basi nikabaki hapo nikiendelea kutazama pengine nitaona kitu.

Ngoja lakini wapi! Nilitumia kama nusu saa hapo lakini sikuona kitu nami nilikuwa nina hamu sana ya kumwona mtu huyo kwani niliamini yeye ndiye yule aliyeacha geti wazi siku ile, nilitamani kujua anafanya nini muda huo na kwanini anaacha geti wazi?

Nilikaa hapo dirishani kwa muda mrefu pasipo kuona kitu nikakata shauri kwenda nje, nilipoufungua mlango wangu kudaka korido nilisikia sauti ya watu wakizungumza, nikasita nikiskiliza. Sauti hiyo ilikuwa inatokea kwenye chumba cha BIGI na nilipoisikiliza kwa kitambo kidogo tu nilibaini sauti hiyo haikuwa ngeni masikioni mwangu, nilishawahi kuisikia mahali, ila ni wapi?

Kidogo kuwaza nikaikumbuka, sauti hii ilikuwa ni ileile niliyoisikia siku ile kwenye mlango huuhuu nikajua ni ya televisheni, ina maana imejirudia au ni masikio yangu? Nilistaajabu, lakini kadiri nilivyoisikia sauti hiyo tena na tena, tena kwa umakini, nikaamini kabisa haikuwa sauti ya televisheni, sauti hiyo ilikuwa ya watu wanaozoza na kunong'ona kitu ambacho sikuwasikia vema nikaelewa.

Nikiwa naendelea kuskiza hapo, mara nikasikia kishindo cha hatua za mtu kibarazani alafu mlango wa grill ukafunguliwa kakaaa kaakaaa! Nikashtuka kweli kweli, ni kama vile moyo wangu uliruka pigo moja kwa fujo!

Upesi nilirejea karibu na mlango wangu nikayatupa macho kule langoni, punde nikamshuhudia BIGI akiingia ndani huku amebebelea kiroba kitupu mkononi, huku juu amevalia 'vest' yake ileile aliyokuja nayo wakati mke wake anaumwa, aliponiona alisimama akan'tazama, nahisi na yeye alishtushwa na uwepo wangu pale, alinitazama pasipo kusema kitu chochote ila mimi nikamsalimu, hakujibu, alisimama tu akiendelea kun'tazama, sijui alikuwa anawaza kitu gani, mapigo yangu ya moyo yalikuwa yanapiga kwa kasi sana, niliona ni busara kuingia ndani kwangu upesi nikaufunga mlango kwa funguo kisha nikasimama hapo kusikiliza, kimya, nlidhani nitasikia vishindo vya miguu vikijongea lakini sikusikia chochote zaidi ya sauti ya mlango ukifungwa kisha kukawa kimya tena.

Nilizima kila kitu changu nikaenda chumbani moja kwa moja mpaka dirishani. Nilitazama pale kibarazani nikaona mlango wa grill ukiwa wazi. Nilitamani kwenda kuufunga lakini nikawaza vipi kama bwana yule akawa bado hajamaliza shughuli zake? Nikaona ni stara nikitulia lakini niendelee kungoja kama atatoka tena.

Nilingoja hapo kitandani kwangu mpaka usingizi ukanibeba, sikusikia kitu abadani. Kesho yake niliporejea tu kazini nikaelezwa kulitokea mjadala mkubwa hapo nyumbani juu ya swala la mlango wa grill kuachwa wazi kwa mara nyingine tena usiku ulopita, siku hiyo majira ya saa tatu hivi usiku kama sijakosea, nilikutana na jirani yangu yule wa dukani tukaongea mambo kadhaa kuhusu hapo nyumbani, moja kuhusu swala la ujenzi wa uzio na namna ambavyo mwenye nyumba haeleweki, na pili kuhusu swala la mlango wa grill kuachwa wazi nyakati za usiku. Bwana huyo alikuwa ndo' mtu wa kwanza kutoka asubuhi hivyo yeye ndiye aliyekuwa anaukuta mlango huo ukiwa wazi.

Kwa upande wangu nilimweleza yale niliyoyajua ya kuwa bwana BIGI ndiye anayeacha mlango huo wazi na basi kwa pamoja tukaazimia kumwambia endapo yeyote akipata nafasi hiyo. Siku zikapita, sijui kama yeye alifanikiwa kuonana na jamaa lakini mimi sikufanikiwa na uzuri mlango haukuachwa wazi tena.

Nakumbuka siku ambayo mafundi walikuja kwaajili ya ujenzi ndo siku ambayo nilipata kumwona bwana BIGI. Siku hiyo ilikuwa ni usiku kama wa saa nane hivi kama niko sawa, nilikuwa sebuleni kama kawaida yangu kabla ya kwenda kulala, televisheni inaongea lakini akili yangu yote ipo kwenye simu naperuzi mitandaoni, naingia instagram, whatsapp na JamiiForums.

Nilisikia mlango unafunguliwa na kisha mlango wa grill, nikanyanyuka kwenda kutazama dirishani. Hapo nilimwona BIGI akiwa amebebelea kiroba begani mwake anatoka kwenda geti dogo.

Kwasababu za ujenzi, geti hilo lilikuwa wazi tena limeegeshwa pembeni kabisa hivyo unaweza kuona mpaka nje. Nikamwona mtu huyo akitokomea huko mpaka kiza kikammeza!

Niliendelea kukaa hapo kwa muda kidogo lakini sikumwona akirudi, nikajua ni kama kawaida sitamshuhudia mpaka nitakapolala, lakini siku hiyo hali ilikuwa tofauti, baada ya kurudi kule sebuleni na kukaa kwa dakika kadhaa nilisikia kishindo cha mtu akikatiza koridoni alafu sauti ya mlango ikaita, nikawaza moja kwa moja atakuwa BIGI ndo amerejea lakini kwanini haufungi mlango wa grill? Nikaazimia ningoje kidogo hapo na nikiona kimya basi nitatoka nikaufunge mlango huo mwenyewe.

Kweli nilikaa hapo kwa kama nusu saa hivi, kimya, nilienda chumbani kutazama dirishani, hali ilikuwa shwari, nikauendea mlango wangu kuufungua lakini nilipotekenya tu funguo nikasikia mlango mwingine unafunguliwa, nikatulia kuskiza.

Vishindo vilipita koridoni nikahisi na kuamini kabisa alikuwa ni BIGI, vishindo hivyo vilipofifia nikaufungua mlango na kuchungulia nje, kweli alikuwa BIGI, nilimwona anatoka nje ya uzio akiwa na kiroba chake begani. Sikujua alikuwa anabebelea kitu gani humo lakini kilichonitatiza zaidi ni kwanini alikuwa anafanya zoezi hilo usiku wa manane?

Nilitoka nikatembea kwa upesi lakini pia kwa uangalifu mpaka kwenye geti dogo. Hapo nilirusha macho yangu kule kutazama, kwa mbali kwa msaada wa mataa mengine ya kule nje, nikamwona BIGI akiwa anayoyomea kuelekea kule korongoni, kule ambapo ndiyo wezi wanapokimbilia. Mwendo wake ulikuwa wa haraka sana na kwasababu ya uweusi wake basi kiroba ndo kilikuwa kinaonekana kikikata upepo, kile kinapepea, kilee kinapepea!

Niliijikuta nina hamu ya kwenda zaidi kutazama.


***
 
Jioni nikitoka kazi, tunaendelea.
Jioni ya nchi gani mkuu? wengine huku tumelala bado
Screenshot_20230206-124757.png
 
Jirani yangu wa kule Goba hakuwa mtu wa kawaida - 03

Haikukaa muda mtoto akanyamaza kisha kukawa kimya sana, kimya cha usiku, nami nikakaa kitandani kubembeleza usingizi ambao baada ya muda ukanichukua.

Usiku huo, sikukumbuka ni nini ila nilikuja kushtuka majira ya saa kumi na moja ya alfajiri nisijue kilichonikurupusha ni kitu gani. Kidogo nikasikia sauti iliyonishtua sana, pengine kwasababu nilikua katika hali ile ya taharuki, ilikuwa ni sauti ya maji yakiichapa ndoo kwa presha kubwa, nilipotazama nikaona moja wa majirani akiwa anachota maji, baada ya hapo sikuupata usingizi tena mpaka majira yangu ya kwenda kazini yalipowadia.

Siku hiyo nilihangaika mno kazini, usingizi ulikuwa unanikaba narembua macho kama mjinga, kila nilipopata nafasi ya kuegemea kitu, hata kama sikudhamiria, nikawa napitiwa na usingizi. Nilikuwa mithili ya teja mwenye arosto.

Nilipochomoka kazini na kufika nyumbani majira ya jioni, sikuchukua muda nikajilaza kwa uchovu. Nililala majira ya saa kumi na mbili, kwasababu hiyo nilijikuta naamka majira ya usiku mnene usingizi umekata, nikatoka kwenda kuoga maana joto nalo lilikuwa jingi na tokea nilivyorudi nyumbani sikupata kuoga, nilijilaza tu kama ng'ombe.

Nje kulikuwa kumetulia sana, kelele zangu za kuchota maji ndo ziliharibu utulivu, bomba lilikuwa na presha kubwa sana kama ugomvi, nilipomaliza nikaingia bafuni lakini nikiwa navua taulo langu mara nikasika kaaa-kaaa-kaaa, sauti ya grill la nyumba kubwa, nikatulia kimya kuskiza, sikusikia kitu, nikahofu anaweza akawa mwizi anaingia ndani hivyo nikachungulia kwa mwanya wa mlango, sikuona kitu, nikafungua mlango ili nione vema, taulo langu kiunoni, nikarusha macho kule kibarazani, sikuona kitu.

Nikatoka bafuni kusogelea nyumba kubwa, hamaki nikasikia kelele za mwizi mwizi, kufumba na kufumbua nikamwona mtu akitoka ndani ya nyumba kubwa kwa kasi kubwa, lengo lake lilikuwa ni kuufuata ukuta akwee lakini aliponiona nipo upande huu wa magharibi ya nyumba akabadili mwelekeo kukimbilia mashariki, kule kwenye geti kubwa, nami nikaongeza mwendo kumkimbiza, mkono wangu wa kuume umeshikilia fundo la taulo iliyomo kiunoni mwangu, kukata kona nikamwona mwizi yule akikwea ukuta, sikumuwahi akawa amesharukia huko nje, na mimi sikujaribu kuhangaika maana niko nusu uchi nisije nikaacha mazaga hadharani, kidogo akatokea jirani mmoja na kisha mwingine akiwa ameongozana na mkewe, mwanamke huyo akasema alimkuta mwizi akiwa anapekua viatu ambavyo vipo mwishoni kabisa wa korido wakati anatoka aende maliwatoni ndipo akapiga kelele za mwizi.

Basi kama ilivyo ada mjadala ukaanza tena wa mambo ya wezi, wakaongezeka na majirani wengine kadhaa haswa wa vile vyumba vya nje, nao wakasimuliwa yaliyotokea na wakatoa maoni yao, tukakubaliana kwa dhati kuwa mwenye nyumba anapaswa kuitwa kikao kuhusu hili maana akipigiwa tu simu na kuelezwa haitatosha, inabidi aje tumsihi atuongezee urefu wa ukuta na pia atuboreshee miundombinu ya usalama mathalani geti, kwani kodi si tunalipa bwana?

Tukiwa tunajadiliana hayo, nilitazama dirisha la chumba anamoishi BIGI maana dirisha hilo limetazama upande huu na halipo mbali sana na geti kubwa, bila shaka hata hapo tulipokuwa tusimama kuongea alikuwa anatusikia vema maana tupo karibu na dirisha hilo. Nilipotazama nikaona dirisha lenye kiza maana ndani hakukuwa kumewashwa taa lakini nilipotia umakini hapo nikabaini pazia la dirisha lilikuwa limefunguliwa kidogo, nikahisi kabisa kuna mtu yumo pale anachungulia nje.

Kitu kilichonifanya nikaamini hivyo ni pale nilipoendelea kulitazama lile dirisha, pazia liliachiwa likafunga, baada ya muda kidogo pazia likafunguliwa tena na nilipotazama nikaona limefungwa upesi. Sikujua ni nani alikuwa dirishani hapo sababu ya giza la chumbani lakini nilipatwa na maswali kama sio kustaajabu na watu wale.

Baada ya muda kidogo, kila mtu alirejea kwenye kiota chake na mimi nikarejea bafuni kuoga. Nilichokifanya sasa niliufunga ule mlango wa grill kwa ufunguo alafu nikaenda nao bafuni kwaajili ya usalama zaidi, lakini kabla sijamaliza kuoga nikasikia mtu akigonga mlango, mlango ule wa grill, hakika nikashtuka, nikasema na nafsi yangu pengine kuna mtu anataka kutoka kwenda maliwato na funguo ninayo mimi, basi nikajifunga taulo upesi pasipo kujikausha mwili ili nipate kutoka haraka, mara nikasikia tena mlango unagongwa, mara hii unagongwa kwanguvu sana bam-bam-bam-bam!

Nikatoka na kuyarusha macho yangu upesi kule kibarazani, nikamwona mtu mkubwa amesimama mlangoni. Mwanga wa kibarazani haukua ang'avu lakini nilimtambua mtu yule alikuwa ni BIGI, mkononi ameshikilia mkoba. Nilimsalimu na kumwambia ufunguo ninao mimi kisha nikamfungulia mlango akaingia ndani, nami nikaingia ndani kumfuatia, mkononi nina ndoo yangu ya kuogea, lakini nilipopiga hatua kadhaa kuufuata mlango wangu nikabaini nimeacha sabuni ya kuogea bafuni kwasababu ya ile haraka yangu, basi sikuwa na budi kurudi nje.

Nilipotoka nikasikia sauti ya pikipiki nje ya uzio, alikuwa ni yule jamaa bodaboda, yale yalikuwa ni moja ya majira yake ya kurejea nyumbani. Alifungua geti dogo akaingia ndani, kabla hajaenda kuegesha chombo chake alinisalimu na kuniuliza kama kuna mtu ameingia hapo nyumbani muda si mrefu, nikamjibu BIGI ndiye ameingia, akaniuliza;

"Yule jamaa mgeni enh?"

Nikamjibu ndio na kumuuliza, "kwani unamjua?" Akaniambia alishawahi mwona siku moja hapo nyumbani, mke wake akamwambia kuwa ni mpangaji mpya na amekuwa akikutana naye mara chache chache huko barabarani usiku mkubwa.

Alisema,

"Basi nilidhani nimemfananisha, nimemwona hapo kilimani akiwa anashuka na mdada fulani hivi, nadhani ni mkewe, nikajaribu kuwashtua ili nije nao lakini sikufanikiwa, nikasema nimeona vibaya nini?"

Pale nyumbani jografia yake ilikuwa hivi, kwa mtu anayetumia usafiri, aidha gari au pikipiki, kuna mahali fulani akifika hatoweza kutumia njia fupi zaidi (shortcut) ya kufika nyumbani kwasababu njia hiyo ni mbovu na nyembamba sana, hivyo atalazimika kuendelea kunyoosha na barabara mpaka mbele kabisa ambapo atakata kona na kuanza kurudi nyuma kwendea nyumbani, kwasababu hiyo ni kawaida kwa mtembea kwa miguu akafika mapema nyumbani kabla ya mwenye usafiri endapo wakiachania hapo.

Tukiachana na hilo, maelezo ya jamaa huyu kwamba alimwona BIGI na mwanamke aliyemdhania kwamba ni mkewe wakiwa wanatembea kuja nyumbani yalinitatiza kiasi kwasababu mimi nilimpokea BIGI akiwa peke yake mlangoni na mkoba wake mkononi, huyo mwanamke sikumwona machoni pangu.

Nikamuuliza kama kweli aliona vema, akasema ana uhakika na alichosema, nami sikutaka kusema zaidi mengine yakabaki ndani yangu, yeye akaenda kupaki chombo chake na kuingia zake ndani, na mimi pia nikaingia ndani na kujilaza kitandani ...

Nikawaza.

Nikajigeuza kitandani nikiwaza.

Hamna nilichoelewa.

Kama BIGI na mkewe hawakuwamo ndani, yule aliyekuwa anachungulia dirishani muda ule ni nani? Ni mtoto wao au? Na huyo mwanamke ambaye alikuwa na BIGI njiani lakini hakufika naye nyumbani, ni mkewe kweli? Kama ndiye mbona sasa ..... Aaagh ... Sikuelewa kitu! Hamna kilichokuwa kinaeleweka, nilikaa hapo mpaka kunakucha maana sikuwa na usingizi kabisa, ajabu wakati jua linawaka ndipo nikaanza kuona macho mazito, nashukuru ilikuwa ni weekend na siku hizo sikuwa naenda kazini basi nikajilalia zangu.

Kesho yake, siku ya jumapili, mwenye nyumba alifika pale nyumbani majira ya mchana kwaajili ya kuitikia wito wetu wa kikao. Kama kawaida yake alipofika alipita kila mlango akigonga na kusalimu na baada ya muda mchache karibia kila mtu akasogea kibarazani kwaajili ya kikao kile cha dharura, watu waliokosekana walikuwa wachache sana; yule jamaa bodaboda pamoja na BIGI ila wengine wote walikuwapo ikiwemo mke wa BIGI pia.

Mwanamke huyo alikuwa ameketi kwenye kona, amejitanda mtandio kichwani, ametulia tuli tofauti kabisa na wenzake, hata kikao kilipoanza karibia kila mtu alisema ya kwake lakini kwake hali ilikuwa tofauti, hakushiriki kwenye chochote, pengine sababu ni bubu hata angesema asingeeleweka, nikajiwazia mwenyewe moyoni, lakini cha ajabu ni kwamba kila niliporusha macho yangu kumtazama, aidha kiwiziwizi ama moja kwa moja, nilikutana na macho yake akinitazama.

Haikujalisha niliupoteza muda kiasi gani baada ya kumtazama ila kila nilipoyarejesha tena macho yangu kwake, nilimkuta mwanamke yule ananitazama. Macho yake hayakuwa ya urafiki.




**
Duuh...!. Hii kali
 
Nimejiuliza Mambo mengi Sana
1. Kwann yule Bibi alikuambia vile? Mazingira ya hiyo zahanati hapana nyumba ya karibu kiasi kwamba ushindwe kumkuta njiani kwa muda mchache uliyopishana nae baada ya wewe kuruhusiwa kurudi nyumbani na Big
Kimazingira ya kawaida huwezi kwenda hospitali private bila pesa na endapo ukiwa mgonjwa Sana unahudumiwa baadae unalipia na kwa umri wake usiku ule kwenda hospitali peke yake ni changamoto

2. Kwanini mke wa big akukate jicho kiasi kile? Kwenye kikao

3. Mwili wa mke wa big kuwa wabaridi Sana mithili ya maiti

4. Ulijificha chooni big akahisi Kuna mtu means machale yalimcheza


Haya tupo twasubiri muendelezo
Sorry, ni story ya kwel??
 
Jirani yangu wa kule Goba hakuwa mtu wa kawaida - 06




Sikupoteza muda, nilijiandaa upesi nikaongozana na jirani mmoja wa kiume mpaka hospitali Mwananyamala tulipoambiwa kuwa ndipo alipo bwana Tarimo. Tulipofika huko, tulipokelewa na mke wa bwana huyo akiwa na uso ulioparama kwa majonzi.

Mwanamke huyo hakuwa anaweza kuongea hata maneno mawili kwa usahihi, kila alipotoa neno moja ni kama vile alitoneshwa upya kidonda akaishia kunyamaza akiufunika uso wake, alikuwa anatia huruma kwelikweli na alinifanya niamini kuwa hali haikuwa shwari huko ndani. Mama huyo pembeni yake alikuwa akifarijiwa na mmoja wa ndugu yake Tarimo, ndugu ambaye mimi sikuwa namfahamu kwani alikuwa mgeni machoni pangu.

Ndugu huyo, kwasababu angalau yeye alikuwa anajiweza, basi ndo’ akawa anaongea na sisi kutupatia taarifa ya kinachoendelea hapo, kwa maelezo yake bwana Tarimo alikuwa amevunjika miguu yote miwili, mkono mmoja, kiuno na taya pia! Kwa namna hiyo bwana Tarimo alikuwa anangojea tu rufaa apelekwe Muhimbili.

Baada ya muda kidogo wa kungoja nilipata nafasi ya kumwona bwana huyo, kwakweli hakuwa anatamanika, ajali ilimchakaza sana, lilikuwa ni jambo la kheri sana kumwona bado yu hai, pale niliamini kweli kama siku yako ya kwenda haijafika basi hautaenda hata iweje.

Tulikaa hapo kwa muda wa lisaa limoja hivi kabla hatujageuza kurejea nyumbani. Tulipanga siku ya kuja kumwona tena bwana Tarimo huku tukisihi maombi mengi yanahitajika bwana huyo apate kusimama kwa mara nyingine. Kuja kufika nyumbani, majira ya saa nane hivi ya usiku, sikufanya kitu kingine nikaoga na kupumzika usiku wake nikiwaza kumhusu bwana Tarimo.

Yale yote aliyotaka kuniambia yaligeuka mawe … kweli hamna mtu anayeijua kesho yake, niliwaza nikijigeuza huku na kule pale kitandani. Sasa kitu pekee ambacho bwana Tarimo alikuwa ameniachia kikawa ni mawazo makubwa kumhusu bwana BIGI, kwanini bwana huyo aliniambia tufanye kila linalowezekana ili BIGI ahame pale? Ni nini aliona mpaka akafikia hitimisho kama hilo? Kwakweli nilitamani sana kujua kama kuna mtu ameyaona zaidi ya yale ambayo mimi nimeyaona.

Nikiwa naendelea kuwaza, akili yangu ikipiga mbizi katika dimbwi hilo la mawazo, mara usingizi ukanibeba msobemsobe nisijue nimepotelea humo saa ngapi, ni baadae ndo’ nilikuja kugutuka baada ya kusikia ndoo ikianguka chini huko nje puuuh, nikaamka upesi kuangaza dirishani. Bila shaka ndoo ile ilikuwapo kibarazani ndo’ maana kuanguka kwake kukawa na kishindo.

Niliitazama ndoo ile ikiwa inazungukazunguka pale chini mpaka ikatulia kabisa. Kimya. Sikuona mtu wala kitu cha kutilia shaka. Nilitazama lile geti dogo, geti jipya, nalo nikaliona limefungwa basi nikarejea kitandani nikiamini ndoo ile iliangushwa na upepo wa huko nje.

Nilitazama saa kwenye simu yangu, ilikuwa ni saa tisa, nikajilaza kuutafuta usingizi tena lakini kabla sijapotelea kwenye njozi nilisikia tena ndoo ikipigwa, nikashtuka. Mlio niliousikia ni kana kwamba mtu ameipiga teke ndoo ile, taratibu nikafungua pazia la dirisha kutazama.

Niliona ndoo ile ikiwa karibu na geti dogo, hapo inazungukazunguka kwenda kushoto na kulia, kulia na kushoto, alafu ikatulia tuli.

Nilitazama kando na kando lakini sikumwona mtu, kulikuwa kimya na kumetulia sana, nikajiuliza ni masikio na macho yangu ndiyo yananidanganya ama? Au ni usingizi na sijapata muda wa kutosha kupumzika? Sikupata majibu … niliendelea kutazama ile ndoo na pande zingine zote kwa muda wa dakika tano hivi, nilipoona hamna kitu niliachia pazia nikajilaza, sikusikia tena kitu mpaka jua linakucha na ndo’ mimi nikalala kwa amani.

Nilikuja kuamka baadae majira ya mchana baada ya kusikia sauti za watoto huko nje wakiwa wanacheza na kukimbizana. Nilitoka nikaenda kuoga kisha nikaketi sebuleni pamoja na tarakilishi yangu kufanya kazi za hapa na pale, muda si mwingi alikuja jirani mmoja aliyegonga mlango na kuniambia kuna zoezi la kuchangia pesa kwaajili ya kuifariji familia ya Tarimo na mkasa uliowapata.

Jirani huyo alikuwa ameshikilia daftari, peni, noti na sarafu lukuki mkono wake wa kushoto ambazo bila shaka alikuwa ameziokoteza kwa majirani wengine. Aliniambia Tarimo ameshahamishwa kwenda Muhimbili kwaajili ya matibabu zaidi na hizo pesa wanazozichanga si kwamba wameombwa na familia ya wahanga, lah, bali ni jitihada za kuonyesha umoja wetu nyakati za matatizo, nikaona vema.

Nilitoa pesa akanipatia peni kuandika jina langu pamoja na sahihi, sikuona haja ya lile jambo lakini kwasababu nililazimika basi nikafanya hivyo, niliandika jina langu na kiasi nilichotoa, katika karatasi lile nikapata kuona majina matano hivi ya majirani wengine waliokwisha kutoa, sikuyatilia maanani majina hayo wala kiasi walichotoa, ila kitu kilichonishangaza ni wingi wa sarafu zile alizokuwa amezishikilia bwana mchangaji, sarafu nyingi mno za hamsini hamsini, nikamuuliza kwa utani,

“Ndugu yangu, umekuwa kondakta?”

Bwana yule alitabasamu kwanza alafu akaniambia sarafu zingine anazo mfukoni, kweli nilipotazama nikaona mfuko wake umenenepa haswa. Nilistaajabu, yeye akaongezea kutabasamu kabla hajaniambia kuna jirani amempatia sarafu hizo na kwa ujumla wake zilikuwa yapata alfu ishirini! … baada ya hapo alienda zake kuendelea na zoezi la kuchanga pesa na mimi nikaendelea na shughuli zangu nilizokuwa nafanya.

Majira ya mchana, kwasababu ya kuboreka kukaa nyumbani tangu asubuhi, niliona ni vema nikanyoosha miguu kwa kutembea hapa na pale. Nilifikiria nielekee wapi, mwishowe nikakata shauri kwenda ‘bar’ fulani hivi ambayo ni mashuhuri kwa kuuza mbege kwani ilikuwa ni muda mrefu sijapata kinywaji hicho na nilihisi kiu chake. Nilichukua chupa ya lita moja na kiasi fulani cha pesa kisha nikashika njia kuelekea huko.

Ukiwa unatumia njia ya lami ya Goba kwenda mwelekeo wa Mbezi Mwisho, kuna kituo kinaitwa kwa Ndambi, kituo cha nyuma yake na cha Kontena ambacho ndipo kina sisi wa Goba Mashuka huteremkia. Ukishukia hapo kwa Ndambi kuna njia kubwa ya vumbi mkono wa kushoto, njia hiyo ukiifuata moja kwa moja, kwa kama dakika sita hivi, mkono wa kushoto utaiona bar hiyo niliyokuwa naiendea, hapo wanauza vinywaji vyote lakini pia wameandika kibao ‘Mbege Ipo’.

Ili kuifikia Bar hiyo kwa sisi ambao tunatokea Goba kwa Mashuka unalazimika kutembea umbali mrefu kukwea kilima mpaka kituo cha Kontena alafu urudi kituo cha nyuma cha Kwa Ndambi, vinginevyo, kwa njia fupi zaidi ya miguu, unakatiza kwenye lile korongo kubwa kuibukia ng’ambo ambako huko ndo’ kwa Ndambi, yaani kwa Ndambi na hapo Mashuka pametenganishwa tu na korongo hilo, korongo ambalo si njia rasmi bali watu hulitumia tu kwaajili ya kupunguza umbali wa safari.

Korongo hilo majira ya usiku huwa na kiza totoro, bila ya kutembea na kurunzi huwezi kuona unapokanyaga na kwasababu hiyo watu hawapendi kutumia njia hiyo, hata majira hayo ya mchana ni watu wachache wachache wangependa kupita hapo.

Nilikatiza korongoni nikipiga mahesabu ya kwenda na kuwahi kurudi kabla ya giza halijawa kubwa kwani sikutaka kutumia njia ndefu zaidi ya ile. Nilipomaliza korongo hilo, nilitumia kama dakika sita tu kufika katika ile bar, hapo nilikuta mziki mtamu na laini ukipiga kuburudisha wateja, tena ule muziki usiokuwa na fujo wala purukushani, nikaona ni vema sana nikipumzika hapo. Watu wachache na muziki usiokuwa na fujo ni moja ya mandhari zangu pendwa kabisa.

Nilitafuta sehemu palipokuwa pweke, nikakaa hapo, muda mchache tu mhudumu akaja kunikirimu. Mhudumu huyo ndiye aliyekuwa mmiliki wa ile biashara hivyo alikuwa anafanya kazi kwa moyo wake wote.

“Karibu, kaka.”

“Ahsante,” nilimwitikia nikampatia chupa yangu na kumwambia: “nahitaji mbege lita moja.”

Mara akaufinyanga uso wake kwa kuhuzunika.

“Daah pole, mbege imeisha muda si mrefu. Hapa ni mpaka kesho tena!”

Basi kwasababu hiyo nililazimika kuagiza bia mbili za baridi ili safari yangu yote isiwe bure, nikawa nakunywa taratibu huku naperuzi simu yangu nikiingia hapa na kutokea pale, nikiingia pale na kutokea hapa, kwa mbali muziki ukiniburudisha vilivyo.

Niliagiza bia tena na tena, kwa namna nilivyokuwa ‘busy’ na simu sikuwa natambua hata bia zile zilikua zinaenda wapi, nilijikuta nakunywa chupa na chupa hata nisijali. Baadae nilipata ‘kampani’ ya bwana mmoja ambaye naye alikuwa mpenzi wa nyimbo zile zilizokuwa zinapigwa basi nikajikuta nazidi kulowea hapo, tunaongea hiki na kile, kuja kupata ufahamu ni saa mbili usiku, kinyume kabisa na muda niliopanga kuondoka!

Nilinyanyuka upesi nikalipia bili yangu kisha nikaanza kiguu na njia, mwelekeo ni uleule wa korongoni kwani sikuwa radhi kuzunguka na njia ndefu ya kule barabarani, baada ya dakika chache nikafika korongoni, nilipotazama humo nikahamaki kwa kiza chake, aisee, kulikuwa ni kweusi tiii! Ile miti ambayo inapeperuka kwa upepo nyakati za mchana iligeuka kuwa mavitu meusi marefu ambayo yanatisha kwelikweli, ilitaka moyo sana kupita humo.

Niliwaza kurudi nyuma lakini nilipofikiria umbali wa safari ile, mmmh, nikajipa moyo, nitapita humohumo, siwezi kurudi nyuma wakati mataa ya nyumbani nayaona yalee kwa macho yangu, basi nikaingia korongoni huku nikitumia mwanga wa tochi ya simu yangu.

Nilitembea taratibu nikiwa naangaza ninapokanyaga, ndani ya korongo hilo kupo kimya, cha zaidi unachosikia ni matawi ya miti pale upepo unapopuliza. Nikiwa katikati ya korongo hilo, mara nilisikia sauti ya kitu kinachotembea … kabla sijafanya jambo lolote, mara nikasikia kitu hicho kikimbia! Niligeuka kuangaza kwa macho na tochi ya simu yangu nikamwona paka mmoja akiwa anakimbia kama mwehu, ni kana kwamba paka huyo alishambuliwa na mtu ama aliona kitu cha hatari.

Nilimtazama namna anavyokimbia nikajikuta napatwa na hofu nisijue ni ya kitu gani. Paka yule alipoishia katika macho yangu, upande uleule alokuwa anakimbilia, nikapata kuona viroba vitatu vikiwa vimepangana … sikujua ni nini lakini viroba hivyo vilinikumbusha taswira ya bwana BIGI upesi mno!

Vipi kama vile viroba ndo’ vile anavyovibeba nyakati za usiku wa manane? Nilijiuliza.

Nilivitazama kwa sekunde kadhaa, nafsi yangu ikawa inanituma niende nikavitazame viroba hivyo vina nini ndani yake. Baada ya muda mchache wa kujiuliza nilikata shauri kwenda kutazama, nikakwea kingo ya korongo na kuvuta kiroba kimojawapo mpaka chini miguuni mwangu. Kiroba hicho kilikuwa cheupe na kimefungwa mdomo kwa kamba ya katani, niliposogeza uso wangu karibu na kiroba hicho nilihisi harufu kali ya kuoza, na harufu hiyo ikawa inaongezeka kadiri nilivyokuwa najaribu kufungua kamba ile kuona kilichomo ndani.



***
Big anafanya nini !!!! Inatisha
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom