Jirani yangu wa kule Goba hakuwa mtu wa kawaida

@
Jirani yangu wa kule Goba hakuwa mtu wa kawaida - 06

Sikupoteza muda, nilijiandaa upesi nikaongozana na jirani mmoja wa kiume mpaka hospitali Mwananyamala tulipoambiwa kuwa ndipo alipo bwana Tarimo. Tulipofika huko, tulipokelewa na mke wa bwana huyo akiwa na uso ulioparama kwa majonzi.

Mwanamke huyo hakuwa anaweza kuongea hata maneno mawili kwa usahihi, kila alipotoa neno moja ni kama vile alitoneshwa upya kidonda akaishia kunyamaza akiufunika uso wake, alikuwa anatia huruma kwelikweli na alinifanya niamini kuwa hali haikuwa shwari huko ndani. Mama huyo pembeni yake alikuwa akifarijiwa na mmoja wa ndugu yake Tarimo, ndugu ambaye mimi sikuwa namfahamu kwani alikuwa mgeni machoni pangu.

Ndugu huyo, kwasababu angalau yeye alikuwa anajiweza, basi ndo’ akawa anaongea na sisi kutupatia taarifa ya kinachoendelea hapo, kwa maelezo yake bwana Tarimo alikuwa amevunjika miguu yote miwili, mkono mmoja, kiuno na taya pia! Kwa namna hiyo bwana Tarimo alikuwa anangojea tu rufaa apelekwe Muhimbili.

Baada ya muda kidogo wa kungoja nilipata nafasi ya kumwona bwana huyo, kwakweli hakuwa anatamanika, ajali ilimchakaza sana, lilikuwa ni jambo la kheri sana kumwona bado yu hai, pale niliamini kweli kama siku yako ya kwenda haijafika basi hautaenda hata iweje.

Tulikaa hapo kwa muda wa lisaa limoja hivi kabla hatujageuza kurejea nyumbani. Tulipanga siku ya kuja kumwona tena bwana Tarimo huku tukisihi maombi mengi yanahitajika bwana huyo apate kusimama kwa mara nyingine. Kuja kufika nyumbani, majira ya saa nane hivi ya usiku, sikufanya kitu kingine nikaoga na kupumzika usiku wake nikiwaza kumhusu bwana Tarimo.

Yale yote aliyotaka kuniambia yaligeuka mawe … kweli hamna mtu anayeijua kesho yake, niliwaza nikijigeuza huku na kule pale kitandani. Sasa kitu pekee ambacho bwana Tarimo alikuwa ameniachia kikawa ni mawazo makubwa kumhusu bwana BIGI, kwanini bwana huyo aliniambia tufanye kila linalowezekana ili BIGI ahame pale? Ni nini aliona mpaka akafikia hitimisho kama hilo? Kwakweli nilitamani sana kujua kama kuna mtu ameyaona zaidi ya yale ambayo mimi nimeyaona.

Nikiwa naendelea kuwaza, akili yangu ikipiga mbizi katika dimbwi hilo la mawazo, mara usingizi ukanibeba msobemsobe nisijue nimepotelea humo saa ngapi, ni baadae ndo’ nilikuja kugutuka baada ya kusikia ndoo ikianguka chini huko nje puuuh, nikaamka upesi kuangaza dirishani. Bila shaka ndoo ile ilikuwapo kibarazani ndo’ maana kuanguka kwake kukawa na kishindo.

Niliitazama ndoo ile ikiwa inazungukazunguka pale chini mpaka ikatulia kabisa. Kimya. Sikuona mtu wala kitu cha kutilia shaka. Nilitazama lile geti dogo, geti jipya, nalo nikaliona limefungwa basi nikarejea kitandani nikiamini ndoo ile iliangushwa na upepo wa huko nje.

Nilitazama saa kwenye simu yangu, ilikuwa ni saa tisa, nikajilaza kuutafuta usingizi tena lakini kabla sijapotelea kwenye njozi nilisikia tena ndoo ikipigwa, nikashtuka. Mlio niliousikia ni kana kwamba mtu ameipiga teke ndoo ile, taratibu nikafungua pazia la dirisha kutazama.

Niliona ndoo ile ikiwa karibu na geti dogo, hapo inazungukazunguka kwenda kushoto na kulia, kulia na kushoto, alafu ikatulia tuli.

Nilitazama kando na kando lakini sikumwona mtu, kulikuwa kimya na kumetulia sana, nikajiuliza ni masikio na macho yangu ndiyo yananidanganya ama? Au ni usingizi na sijapata muda wa kutosha kupumzika? Sikupata majibu … niliendelea kutazama ile ndoo na pande zingine zote kwa muda wa dakika tano hivi, nilipoona hamna kitu niliachia pazia nikajilaza, sikusikia tena kitu mpaka jua linakucha na ndo’ mimi nikalala kwa amani.

Nilikuja kuamka baadae majira ya mchana baada ya kusikia sauti za watoto huko nje wakiwa wanacheza na kukimbizana. Nilitoka nikaenda kuoga kisha nikaketi sebuleni pamoja na tarakilishi yangu kufanya kazi za hapa na pale, muda si mwingi alikuja jirani mmoja aliyegonga mlango na kuniambia kuna zoezi la kuchangia pesa kwaajili ya kuifariji familia ya Tarimo na mkasa uliowapata.

Jirani huyo alikuwa ameshikilia daftari, peni, noti na sarafu lukuki mkono wake wa kushoto ambazo bila shaka alikuwa ameziokoteza kwa majirani wengine. Aliniambia Tarimo ameshahamishwa kwenda Muhimbili kwaajili ya matibabu zaidi na hizo pesa wanazozichanga si kwamba wameombwa na familia ya wahanga, lah, bali ni jitihada za kuonyesha umoja wetu nyakati za matatizo, nikaona vema.

Nilitoa pesa akanipatia peni kuandika jina langu pamoja na sahihi, sikuona haja ya lile jambo lakini kwasababu nililazimika basi nikafanya hivyo, niliandika jina langu na kiasi nilichotoa, katika karatasi lile nikapata kuona majina matano hivi ya majirani wengine waliokwisha kutoa, sikuyatilia maanani majina hayo wala kiasi walichotoa, ila kitu kilichonishangaza ni wingi wa sarafu zile alizokuwa amezishikilia bwana mchangaji, sarafu nyingi mno za hamsini hamsini, nikamuuliza kwa utani,

“Ndugu yangu, umekuwa kondakta?”

Bwana yule alitabasamu kwanza alafu akaniambia sarafu zingine anazo mfukoni, kweli nilipotazama nikaona mfuko wake umenenepa haswa. Nilistaajabu, yeye akaongezea kutabasamu kabla hajaniambia kuna jirani amempatia sarafu hizo na kwa ujumla wake zilikuwa yapata alfu ishirini! … baada ya hapo alienda zake kuendelea na zoezi la kuchanga pesa na mimi nikaendelea na shughuli zangu nilizokuwa nafanya.

Majira ya mchana, kwasababu ya kuboreka kukaa nyumbani tangu asubuhi, niliona ni vema nikanyoosha miguu kwa kutembea hapa na pale. Nilifikiria nielekee wapi, mwishowe nikakata shauri kwenda ‘bar’ fulani hivi ambayo ni mashuhuri kwa kuuza mbege kwani ilikuwa ni muda mrefu sijapata kinywaji hicho na nilihisi kiu chake. Nilichukua chupa ya lita moja na kiasi fulani cha pesa kisha nikashika njia kuelekea huko.

Ukiwa unatumia njia ya lami ya Goba kwenda mwelekeo wa Mbezi Mwisho, kuna kituo kinaitwa kwa Ndambi, kituo cha nyuma yake na cha Kontena ambacho ndipo kina sisi wa Goba Mashuka huteremkia. Ukishukia hapo kwa Ndambi kuna njia kubwa ya vumbi mkono wa kushoto, njia hiyo ukiifuata moja kwa moja, kwa kama dakika sita hivi, mkono wa kushoto utaiona bar hiyo niliyokuwa naiendea, hapo wanauza vinywaji vyote lakini pia wameandika kibao ‘Mbege Ipo’.

Ili kuifikia Bar hiyo kwa sisi ambao tunatokea Goba kwa Mashuka unalazimika kutembea umbali mrefu kukwea kilima mpaka kituo cha Kontena alafu urudi kituo cha nyuma cha Kwa Ndambi, vinginevyo, kwa njia fupi zaidi ya miguu, unakatiza kwenye lile korongo kubwa kuibukia ng’ambo ambako huko ndo’ kwa Ndambi, yaani kwa Ndambi na hapo Mashuka pametenganishwa tu na korongo hilo, korongo ambalo si njia rasmi bali watu hulitumia tu kwaajili ya kupunguza umbali wa safari.

Korongo hilo majira ya usiku huwa na kiza totoro, bila ya kutembea na kurunzi huwezi kuona unapokanyaga na kwasababu hiyo watu hawapendi kutumia njia hiyo, hata majira hayo ya mchana ni watu wachache wachache wangependa kupita hapo.

Nilikatiza korongoni nikipiga mahesabu ya kwenda na kuwahi kurudi kabla ya giza halijawa kubwa kwani sikutaka kutumia njia ndefu zaidi ya ile. Nilipomaliza korongo hilo, nilitumia kama dakika sita tu kufika katika ile bar, hapo nilikuta mziki mtamu na laini ukipiga kuburudisha wateja, tena ule muziki usiokuwa na fujo wala purukushani, nikaona ni vema sana nikipumzika hapo. Watu wachache na muziki usiokuwa na fujo ni moja ya mandhari zangu pendwa kabisa.

Nilitafuta sehemu palipokuwa pweke, nikakaa hapo, muda mchache tu mhudumu akaja kunikirimu. Mhudumu huyo ndiye aliyekuwa mmiliki wa ile biashara hivyo alikuwa anafanya kazi kwa moyo wake wote.

“Karibu, kaka.”

“Ahsante,” nilimwitikia nikampatia chupa yangu na kumwambia: “nahitaji mbege lita moja.”

Mara akaufinyanga uso wake kwa kuhuzunika.

“Daah pole, mbege imeisha muda si mrefu. Hapa ni mpaka kesho tena!”

Basi kwasababu hiyo nililazimika kuagiza bia mbili za baridi ili safari yangu yote isiwe bure, nikawa nakunywa taratibu huku naperuzi simu yangu nikiingia hapa na kutokea pale, nikiingia pale na kutokea hapa, kwa mbali muziki ukiniburudisha vilivyo.

Niliagiza bia tena na tena, kwa namna nilivyokuwa ‘busy’ na simu sikuwa natambua hata bia zile zilikua zinaenda wapi, nilijikuta nakunywa chupa na chupa hata nisijali. Baadae nilipata ‘kampani’ ya bwana mmoja ambaye naye alikuwa mpenzi wa nyimbo zile zilizokuwa zinapigwa basi nikajikuta nazidi kulowea hapo, tunaongea hiki na kile, kuja kupata ufahamu ni saa mbili usiku, kinyume kabisa na muda niliopanga kuondoka!

Nilinyanyuka upesi nikalipia bili yangu kisha nikaanza kiguu na njia, mwelekeo ni uleule wa korongoni kwani sikuwa radhi kuzunguka na njia ndefu ya kule barabarani, baada ya dakika chache nikafika korongoni, nilipotazama humo nikahamaki kwa kiza chake, aisee, kulikuwa ni kweusi tiii! Ile miti ambayo inapeperuka kwa upepo nyakati za mchana iligeuka kuwa mavitu meusi marefu ambayo yanatisha kwelikweli, ilitaka moyo sana kupita humo.

Niliwaza kurudi nyuma lakini nilipofikiria umbali wa safari ile, mmmh, nikajipa moyo, nitapita humohumo, siwezi kurudi nyuma wakati mataa ya nyumbani nayaona yalee kwa macho yangu, basi nikaingia korongoni huku nikitumia mwanga wa tochi ya simu yangu.

Nilitembea taratibu nikiwa naangaza ninapokanyaga, ndani ya korongo hilo kupo kimya, cha zaidi unachosikia ni matawi ya miti pale upepo unapopuliza. Nikiwa katikati ya korongo hilo, mara nilisikia sauti ya kitu kinachotembea … kabla sijafanya jambo lolote, mara nikasikia kitu hicho kikimbia! Niligeuka kuangaza kwa macho na tochi ya simu yangu nikamwona paka mmoja akiwa anakimbia kama mwehu, ni kana kwamba paka huyo alishambuliwa na mtu ama aliona kitu cha hatari.

Nilimtazama namna anavyokimbia nikajikuta napatwa na hofu nisijue ni ya kitu gani. Paka yule alipoishia katika macho yangu, upande uleule alokuwa anakimbilia, nikapata kuona viroba vitatu vikiwa vimepangana … sikujua ni nini lakini viroba hivyo vilinikumbusha taswira ya bwana BIGI upesi mno!

Vipi kama vile viroba ndo’ vile anavyovibeba nyakati za usiku wa manane? Nilijiuliza.

Nilivitazama kwa sekunde kadhaa, nafsi yangu ikawa inanituma niende nikavitazame viroba hivyo vina nini ndani yake. Baada ya muda mchache wa kujiuliza nilikata shauri kwenda kutazama, nikakwea kingo ya korongo na kuvuta kiroba kimojawapo mpaka chini miguuni mwangu. Kiroba hicho kilikuwa cheupe na kimefungwa mdomo kwa kamba ya katani, niliposogeza uso wangu karibu na kiroba hicho nilihisi harufu kali ya kuoza, na harufu hiyo ikawa inaongezeka kadiri nilivyokuwa najaribu kufungua kamba ile kuona kilichomo ndani.

***

Muendelezo soma Jirani yangu wa Kule Goba hakuwa mtu wa kawaida
Nourhan pita hapa kuna madini mazuriiii
 
Yule Jirani yangu wa Goba, hakuwa mtu wa kawaida - MWISHO.



Siku mbili baada ya kumwona Bembela akiwa na shangazi yake usiku ule wamebebela mfuko nisijue wapi walipotokea na nini walibebelea, nilipigiwa simu na Mwenye nyumba majira ya mchana nikiwa kazini.

Bwana huyo baada ya kunisalimu na kuniuliza mambo ya nyumbani, aliniuliza kama kuna watu wamefika pale nyumbani kumuulizia bwana BIGI, nikamwambia sifahamu, binafsi sikuona mtu labda wapangaji wengine, baada ya hapo nikamuuliza hali za wale wagonjwa, akanieleza hali zao ni bora ya jana yake, siku hiyo alipitia asubuhi hospitali kabla ya kwenda kwenye shughuli zake akakutana na hali mbaya sana ya bwana BIGI.

Alinambia, "yule bwana sijui sasa kama kuna kupona. Amepooza mwili wake mzima, ni wa kugeuza na kumfuta tu, sasa wanataka kumpatia rufaa!"

Aliniambia hofu yake endapo bwana huyo akifa maana hamjui mtu wake hata mmoja na wala hana mawasiliano nao, achilia mbali hata mkataba naye hana, sijui ataeleza kitu gani akaeleweka mbele ya vyombo vya usalama, lakini pia hata mkewe ambaye alikuwa anategemea atapoa ili amhudumie mumewe na kutoa taarifa kwa watu wao wa karibu naye hali yake haikuwa inaeleweka, tangu amefikishwa hapo hospitali hajapata kuonekana akifungua macho wala kutoa ishara yoyote ya mawasiliano, amepimwa kila kitu, hamna kinachosoma na hitilafu ila fahamu hazimo, ajabu gani?

Aliniaga akiniambia alimwacha yule bwana, mpangaji aloongozana naye siku ile kwenda naye hospitali, baadae atampigia kumuuliza maendeleo, baada ya hapo akakata simu nikaendelea na shughuli zangu.

Kesho yake majira ya jioni nikiwa natoka kazini, nikakutana na huyo mpangaji mwenzangu kwenye geti dogo akiwa anarejea nyumbani, bwana huyo alikuwa ametoka kwenye mihangaiko yake ya hapa na pale, tulisalimiana kisha akanieleza ya kule hospitali.

Bwana yule akaniambia mambo ambayo Mwenye Nyumba hakupata kusema au pengine hakuwa anayajua.

Alisema: "Baada ya leo asubuhi kutoka kule, mimi sitokaa nirudi tena kule hospitali hata mwenye nyumba akiniomba na kunilamba miguu."

Nikastaajabu kweli na maamuzi hayo ambayo niliyaona ya ghafla, kabla sijamuuliza kulikoni, akaniambia mwanamke yule alokuwapo hospitali hakuwa mgonjwa, mwanamke yule ni mzima kila ifikapo usiku, maneno hayo yakanifanya nimuulize: "ushawahi kuwa kule hospitali majira ya usiku?"

Akanijibu "lah!" na kusema kamwe hajawahi lakini alionana, asubuhi ya siku hiyo, na nesi alokuwa anaingia zamu usiku, nesi huyo alimwita kando akamuuliza mwanaume yule yaani BIGI ni ndugu yake? Akamwambia ndio na yule mwanamke ni shemeji yake, basi akamwambia mwanamke yule huenda ndo' amemuadhiri ndugu yake mpaka kufikia vile.

Bwana yule alisema: "nilimuuliza nesi kwanini anawaza hivyo akaniambia yeye ana uzoefu na hayo mambo ya hospitali, anajua mambo ya kutibiwa hospitali na mambo ya kutafuta njia zingine mbadala, na hili la kwetu ni la njia mbadala, tena tufanye upesi kabla hatujampoteza ndugu yetu."

Bwana yule akaniambia nesi huyo alishawahi kumshuhudia mwanamke yule,kama kivuli, akiwa anatembea wodi ya watoto na wazazi nyakati za usiku, na anaamini ni kweli alichoona sio mauzauza ama kiini macho, lakini alipoenda kutazama kitanda chake bado akamkuta mwanamke huyo hapo, mwili wake umetulia kitandani, na jambo hilo si mara moja bali mara mbili.

Ajabu kule kote mwanamke huyo alikokatiza, kesho yake paliongokea msiba ya watoto kwenye vitanda viwiliviwili, kwa siku mbili wakapoteza watoto wachanga wanne!

"Ndugu yangu," bwana yule aliita kisha akasema, "kuanzia leo mimi sitahusika kwa namna yoyote na wale mabwana, hata iweje, yote nimewaachia wale ndugu zao walokuja hapa kuhani msiba."

Nikahamaki,

"Ndugu hao uliwaona?"

Akanambia hapana ila kama walikuja wakati wa msiba basi waje pia na kuwatazama huko hospitali, nikabaini bwana huyo amepandwa na jazba, niliagana naye akaondoka zake, kesho yake asubuhi ya mapema nikiwa najiandaa kwenda kazini mwenye nyumba akanipigia simu, akaniambia amepitia hospitali asubuhi ya siku hiyo akapata taarifa bwana BIGI amefariki dunia!

Alisema: "Kifo chake kimetokea usiku wa kuamkia leo kwahiyo hapa tunapoongea, mwili wake umehifadhiwa."

Kuhusu mkewe, alinambia bado hali yake iko vilevile, hamna afueni wala ahueni, namna alivyoletwa ndo' namna alivyo, lakini kabla hatujamaliza maongezi akaniomba ningoje mara moja atanirejea, akakata simu.

Yakapita masaa kama mawili, hakunipigia, nishafika kazini na ninaendelea na mambo yangu lakini kule nyumbani kabla sijaondoka nilishaacha taarifa ya msiba, baada ya masaa hayo nlosema, mwenye nyumba alinipigia akaniambia muda ule alokata simu, kuna watu walikuja hapo hospitali wakisema wao ni ndugu zake na BIGI, akaniuliza kuna mtu niliyempa taarifa kuwa BIGI yuko hospitalini hapo? Nikamjibu hapana, akasema;

"Basi itakuwa Muddy, nampigia hapokei simu yangu, sijui yuko wapi?"

Muddy ni yule jamaa jirani aloongozana na mwenye nyumba kwenda naye kule hospitali, mwenye nyumba aliponieleza anampigia bwana huyo hampati nikakumbuka moja kwa moja maneno alosema yule bwana jana yake usiku nilipokutana naye, pengine alihisi mwenye nyumba anamtafuta ili aende hospitali, kitu ambacho yeye hakukitaka tena abadani.

Lakini kama ndiye Muddy alisema kuhusu BIGI kuwa kule hospitali, je alikutana na hao majaa lini? Mimi sikuamini kabisa hilo jambo. Na kama kweli hao majamaa wamemjuaje mwenye nyumba ukizingatia mwenye nyumba hata kwenye msiba hakuwapo?

Sikukaa nikayajua.

Baadae jioni niliporejea nyumbani, nilimkuta baba mwenye nyumba akiwa pamoja na Mjumbe, vijana wawili wa ulinzi shirikishi na mabwana wawili ambao sikuwatambua. Tulisalimiana kisha mwenye nyumba akanieleza kinachoendelea hapo ya kwamba mabwana wale wawili ni ndugu zake na BIGI na wamekuja hapo kubeba vitu vyao.

Alinieleza mabwana wale ndo' waliofika kule hospitali kujumuika naye, kama haitoshi, walisimamia kila kitu kuhusu gharama za matibabu na kitanda alicholalia BIGI muda wote ule wa kuuguzwa.

Lakini mimi nikabaki na maswali, sawa mabwana hao wameibuka na kubeba majukumu, lakini tuna uhakika gani kama wao ni ndugu halisi wa BIGI? Nilijiulizia moyoni...

Vitu vyote vya BIGI vilitolewa nje, kweli hakukuwa na cha maana, yaani ungeweza kubeba vitu hivyo kichwani ukaondoka navyo kwa miguu, kulikuwa ni mifuko mifuko, viroba, nguo na mavitu mengine kadhaa ambayo kwakweli sikuona kama yana tija, ajabu ni kwamba mabwana wale hawakubakiza hata kitu, kila kilichochao walibeba, hata yale ambayo unaweza dhania ni taka, yote hayo walikuwa wanakusanyia katika kiroba chao kikubwa walichokuja nacho.

Wakiwa wanafanya hivyo mimi nikaona moja ya 'toy' la mwanangu, nikawaambia hiki ni changu hamna kwenda nacho, hapo ukaibuka mzozo, mabwana wale hawakuwa tayari kuacha kitu, nami kuona vile nikapata mashaka juu ya kwanini wanang'ang'ania vile vitu kiasi hiko, mpango wao ni nini?

Nikapambana mpaka nilipohakikisha 'toy' ile haiendi kokote, swala hilo likawafanya majirani wengine nao wasogee kuziangatia vitu vile vinavyobebwa, hamaki majirani watatu wakapata nguo zao humo, tena wawili kati yao walipata nguo zao za ndani!

Hamna aliyejua ni namna gani nguo hizo zilifika humo, lakini kila mtu alikiri zilipotea kambani baada ya kuanikwa juani. Baada ya kila kitu kuwa sawa, mabwana wale walifunga kiroba chao kisha mmoja wao akasema, tena kwa sauti kuu:

"Kama kuna mtu yeyote mwenye kitu cha (akataja jina halisi la bwana BIGI) basi naomba akirejeshe hapa ... Kama vile mlivyodai vyenu, basi na vya kwake vyote virejeshwe, kama sivyo basi mwenye nacho atakuja kupata matatizo hapo baadae na sisi hatutabeba lawama."

Kimya,

Hakuna kilichorejeshwa, Bwana huyo akarudia tena maneno yake, kama kuna yeyote alowahi kubeba mali yoyote ya bwana BIGI basi airejeshe, la sivyo atakuja kujilaumu.

Kimya.

Mabwana wale walipoona kila kitu ni sawa, wakampatia mwenye nyumba mkono wa kheri na kisha Mjumbe, alafu wakasema msiba wa bwana BIGI utakuwapo maeneo ya Chanika eneo ambalo sikumbuki linaitwaje, baada ya hapo wakaenda zao na kile kiroba chao kikubwa, huo ukawa ndo' mwisho wa BIGI na mambo yake pale Goba. Baada ya hapo sikuwahi kumsikia wala kumwona tena bwana huyo. Sikumbuki kama kuna jirani yoyote aloenda kuhani msiba huo huko Chanika, laiti ingelikuwa hivyo basi ningelipata taarifa fulani.

Ikapita siku moja, siku ya pili, bila ya bwana BIGI, kila kitu kikiwa shwari, wiki moja na wiki ya pili, kila kitu kimetulia, hamna maisha ya usiku wala vimbwanga vyake, baada ya mwezi kukoma Bembela alihama pale nyumbani nisijue wapi alipoelekea, lakini sehemu yake ya biashara ilibakia kuwa ni ileile, nyuma ya kituo cha Goba Kontena.

Hapo mara kadhaa nilikuwa namkuta akiwa anahudumia watu, hata ameajiri wadada wawili wa kumsaidia maana wateja walikuwa wengi sana. Siku moja, nadhani ni baada ya kama mwezi kupita tangu amehama pale nyumbani, nilipita pale katika eneo lake la biashara kumsalimu, siku hiyo nilikuwa mwenyewe nyumbani maana mke wangu alikuwa ameenda huko Ugweno, Kilimanjaro, kwao kusalimu pamoja na mtoto, hivyo nilivyokuwa nikirejea nyumbani nilikuwa napitia hapo kupata chakula cha usiku kabla ya kwenda kulaza mazima ninaposhuka kule Mashuka.

Nilifanya hivyo mara kadhaa, kama majuma matatu hivi, nikikutana na Bembela kila siku na kila mara tukiongea naye mambo ya hapa na pale. Nilishawahi kumuuliza shangazi yuko wapi, akaniambia ameshakwenda zake Tanga lakini anashukuru kwani maisha si haba, kila kitu kinaenda sawa, sasa alikuwa anatazamia kumalizia nyumba yake aliyokuwa anajenga maeneo ya Kimara, Temboni.

Bembela, kwakweli, hakuwa yule Bembela wa zamani, kitendo cha kuajiri wasichana wawili na yeye akiwa wa tatu katika shughuli ile ya mama n'tilie ilionyesha namna gani alivyokua amepiga hatua kubwa kiuchumi.

Ilikuja kufikia pahali hata mimi nilokuwa naenda pale kupata chakula, zamani nikihudumiwa kama mfalme, sasa nikawa napanga foleni tena mpaka niwe nasisitiza mara mbili au tatu ndo' sahani ipate kuja mezani!

Nikatambua kweli maisha yanabadilika, na mengine, kama bahati, yanabadilika mbele ya macho yetu ya nyama, yaani tunapata kuyashuhudia yakiwa yanatokea tangu mwanzo wake mpaka mwisho wake.

Lakini mpaka leo, mimi binafsi, sijawahi kujua ni nini haswa kilichokuja kutokea katikati ya majuma na miezi kadhaa baina ya Bembela na yule shoga yake ... lakini mwanamke yule, yaani shoga yake na Bembela, ambaye tulikuwa tunaendelea kuishi naye pale nyumbani, ndiye baadae alikuja kugeuka kuwa mdomo wa kusema kuwa Bembela anamtumia yule mtoto na mke wa BIGI kwenye mafanikio ya biashara yake.

Sasa amepata mali na pesa, hakuna anayemjali na kumkumbuka, hata yeye alokuwa naye karibu katika yale yote alopitia ....


***
Mkuu Tunashukuru Sana KWA kushare na sisi kipande story hii muhimu......tumejifunza na kuelimika katika viingi juu ya mienendo ya maisha ya mwanadamu
 
Hicho kisa mbona sijawahi kiona, nime maliza soma hichi kisa cha jirani wa goba hakuwa mtu wa kawaida.
Natamani sana nisome na hicho cha steve tukibaki hai.
Naomba nitag kwenye hiyo story mkuu.
 
Hicho kisa mbona sijawahi kiona, nime maliza soma hichi kisa cha jirani wa goba hakuwa mtu wa kawaida.
Natamani sana nisome na hicho cha steve tukibaki hai.
Naomba nitag kwenye hiyo story mkuu.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom