Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,295
- 33,079
Maoni ya katuni
Tunaambiwa na tumeshuhudia kwamba ile mipaka ya nchi moja moja duniani kwa sasa haifanyi tena kazi. Hii ni kwa sababu maendeleo ya sayansi na tekinolojia ambayo yanasukumwa zaidi na nguvu za mawasiliano ya kompyuta yamevunja kabisa mipaka ya mataifa. Mipaka hii imebakia kuwa ni utambulisho wa kisiasa tu, lakini kimsingi watu wameungana katika jumuiko moja kubwa duniani, kijiji cha dunia.
Tunapokuwa katika muingiliano wa namna hii kwa hakika wanaonufaika nao ni wale walioko tayari kujifunza mbinu mpya, kutumia fursa zilizopo kuongeza tija na kwa ujumla kuungana katika jumuiko hilo kama wadau wanaonufaika kadri iwezekanavyo.
Leo hii yapo mataifa yaliyokuwa nyuma sana kama sisi miaka tuliyopata uhuru, lakini yamepaa katika kupiga hatua za kimaendeleo, iwe kwenye
kujenga uwezo wa rasilimali watu wake, kujenga miundombinu ya aina zote; barabara, reli, bandari na mawasiliano ya simu; kwa kasi ambayo inawapa fursa na uwezo wa kunufaika na muingiliano wa mataifa kama kijiji kimoja cha dunia.
Aina ya mataifa haya ni kama zile nchi za Malaysia, Singapore, Taiwan, Korea Kusini na Hong Kong, hakuna ubishi kwamba mataifa haya
yalipiga hatua kubwa sana za maendeleo katika kipindi cha miaka ya 1960 hadi 1990, ni kipindi ambacho nasi kama taifa tulikuwa tumekwisha kupata uhuru.
Wakati mataifa mengine yakisonga mbele kwa kasi hiyo na yakiwa ndiyo wadau wakuu wanaonufaika na mageuzi ya dunia kugeuka kuwa kijiji
kimoja, sisi bado tumefungwa ndani ya boksi tukielekeza nguvu zetu katika dhana potofu mno, hususani ushirikina.
Tangu mwaka jana taifa hili limeingiliwa na janga la kuuawa kwa watu wenye ulemavu wa ngozi (albino). Watu hawa wanauawa au kukatwa sehemu za miili yako kwa kile kinachoaminika kuwa ni kusaidia watu kuwa matajiri. Yaani mikakati, fikra na kila mbinu ya baadhi ya watu wetu
katika baadhi ya jamii zetu imerahisishwa na kuporomoka na kuamini kwamba viungo vya watu wenye ulamavu wa ngozi ni njia ya kufikia utajiri!
Wimbi hili lilipamba moto sana mwaka jana, lakini baadaye lilipungua baada ya kuwako kwa juhudi za vyombo vya usalama vya ndani ya nchi, vikishirikiana na raia kuwasaka watu waliokuwa wanafanya biashara ya viungo vya walemavu wa ngozi. Kuna kesi kadhaa zilifunguliwa
mahakamani hasa maeneo ya Kanda ya Ziwa, nyingine zimekwisha kuhukumiwa, hata hivyo bado hofu kwa walemavu hawa bado iko juu.
Wakati imani ya wananchi ikiwa inaanza kurejea kwamba vitendo hivi vya kishenzi na kishirikiana vilikuwa vinatoweka nchini, mwishoni mwa wiki tukio la kusikitisha limeibuka wilayani Geita, Mwanza ambako mtoto mwenye ulemavu wa ngozi mwenye umri wa miaka 13 amekatwa vidole viwili na mtu mmoja kisha kukimbia navyo. Uhalifu huu unaakisi imani za kishirikiana ambazo zimekuwako ndani ya jamii yetu kwa muda mrefu.
Tunasikitika na kumpa pole Adamu Robert (13) ambaye amekumbwa na masahibu haya kwa kuwa tu ni mlemavu wa ngozi, tunamwombea kwa mola wake amjalie apate nafuu na kupona kabisa, lakini tukijua fika kwamba ameachiwa kilema cha maisha.
Kwa muda mrefu tumejiuliza swali gumu, kwamba inakuwaje watu wanadangayika kwamba unaweza tu kuwa na kiungo cha albino na hivyo
kufanikiwa katika biashara au shughuli yoyote unayofanya? Mbona hizi imani ni dhaifu sana hasa katika ulimwengu wa leo ambao umefunuliwa dhahiri kwa kila mmoja kutokana na maendeleo ya mawasiliano ya kompyuta?
Tunajua vyombo vya usalama, hususan Jeshi la Polisi, wamesema kuwa uhalifu kama huu wa kukata binadamu wengine viungo vyao vya mwili
au hata kuwaua kabisa kwa kisingizo cha kutafuta dawa ya utajiri, haukubaliki. Polisi wametoa dau nono kwa yeyote atalayetoa taarifa za kufanikisha kukamatwa kwa muhalifu aliyemjeruhi Adamu, tunapongeza pia juhudi hizi.
Mwisho, tungependa kulaani vitendo vyote vya ukatili dhidi ya albino kwa kisingizio cha imani za kishirikina kwamba viungo vyao ni bahati ya
utajiri, kadhalika tunaichagiza jamii kushirikiana kutokomeza vitendo hivi vinavyotuchafua kama taifa mbele ya jumuiya kimataifa.
Ni ujinga wa hali ya juu kuelekeza mawazo yetu katika imani za kishirikina za kukata viungo vya albino wakati maendeleo ya sayansi, tekinolojia na mawasiliano ya kompyuta ni ushirikiana wa wazi wa kimataifa ambao hatuna njia ila kuwa sehemu yake kama kweli tunataka utajiri na maendeleo ya kweli.
CHANZO: NIPASHE