Candid Scope
JF-Expert Member
- Nov 8, 2010
- 11,883
- 6,883
Mbunge wa Bariadi Magharibi Andrew Chenge
SAKATA la kumiliki dola 1.2 milioni za Kimarekani (zaidi ya Sh1.2bilioni) katika kisiwa cha Jersey, Uingereza, linalomkabili mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge, limeingia katika hatua mpya baada ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kutangaza kukamilisha uchunguzi na kukabidhi jalada kwa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), kwa hatua zaidi za kisheria. Chenge alikutwa na kiasi hicho cha fedha mwaka 2008, kufuatia uchunguzi wa kashfa ya ununuzi wa rada uliofanywa na Taasisi ya Makosa Makubwa ya Jinai ya Uingereza (SFO).
Chenge ambaye wakati wa ununuzi huo alikuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) anatuhumiwa kuwa kiungo muhimu katika ununuzi wa rada kati ya Serikali ya Tanzania na Kampuni ya BAE Systems. Hata hivyo, kufuatia Chenge kukutwa na kiasi hicho kikubwa cha fedha zenye utata ambacho alikiita vijisenti, kumekuwa na shinikizo kubwa kutoka kwa watu wa kada tofauti nchini wakitaka ashitakiwe, na jana Mkurugenzi wa Takukuru Dk Edward Hoseah, alitangaza hadharani mjini Arusha kwamba mtuhumiwa huyo wa ufisadi atashtakiwa chini ya kifungu cha 27 Sheria ya Takukuru ya mwaka 2007.
Sehemu yakifungu hicho cha sheria, kinaainisha kuwa mtu akiwa na mali ambazo hazilingani na kipato chake alichokipata akiwa madarakani au baada ya kuondoka, ni kosa kisheria. Mtu ambaye atafanya kosa akiwa au akishikilia madaraka ya umma, kwa kuishi kwa kipato ambacho hakilingani na kipato cha sasa au kile alichopata Au anayemiliki mali ambazo hazilingani na kipato chake kisheria, atakuwa akitenda kosa. Kifungu hicho kinaeleza.
Dk Hoseah alifafanua zaidi kwamba, kama DPP atalipitisha jalada hilo la Chenge, mbunge huyo atafikishwa mahakamani wakati wowote. Kashfa ya kuwa na fedha hizo katika akaunti ya nje, ndiyo ilimwondoa Chenge katika wadhifa wa Uwaziri wa Miundombinu mwaka 2008, baada ya gazeti la Guardian la Uingereza kufichua kuwa Mwanasheria Mkuu huyo wa Serikali wa zamani, alikuwa akimiliki kiasi hicho cha fedha. Hata hivyo, alipoulizwa na waandishi Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Julius Nyerere baada ya kuachana na msafara wa Rais Jakaya Kikwete, aliyekuwa akitoka naye ziarani nchini China, Chenge alikiri kumiliki akiba hiyo ya fedha, lakini akiziita ni vijisenti, jambo ambalo liliwashangaza watu wengi nchini na kuibua hasira zaidi.
Lakini, Dk Hoseah akifafanua zaidi mchakato huo mzito wa kisheria, alisema ni Watanzania wachache mno wanaoweza kuwa na akiba ya fedha kiasi kama hicho nje ya nchi au mahali kokote, jambo ambalo aliongeza kuwa ndilo lililowasukuma kufanya uchunguzi kuhusu fedha hizo za Chenge.
Asisitiza hana kesi ya rada
Kuhusu kuhusika kwa Chenge katika kashfa ya rada baada ya Mahakama Kuu Uingereza kuamuru BAE Systems kurejesha sehemu ya fedha kwa Tanzania kutokana na kubaini upotevu wa nyaraka muhimu za manunuzi halali, Dk Hoseah, alisema, mbunge huyo hahusiki na kwamba hakuna ushahidi wowote wa kumtia hatiani.
Kwa mujibu wa Dk Hoseah, waliohusika na kashfa hiyo tayari wameshatajwa na hata washiriki wao wanajulikana wakiwamo raia wa Uingereza. Nashangaa kuona Watanzania wakishikilia kuwa Chenge ashtakiwe kwa kitu ambacho hakina ushahidi, lakini wanasahau kuwaeleza Waingereza kuwa ndio wahusika, alifafanua Dk Hoseah, akirejea mchakato wa kesi hiyo ambayo Chenge alikuwa akiwakilishwa na mwanasheria wake wa Kimarekani, JJ Madorsky. Ingekuwa sio kweli, Waingereza hawangekaa kimya, wangesema, alisema Dk Hoseah.
Kuhusu Kagoda
Akizungumzia kashfa nyingine inayotikisa Kampuni ya Kagoda Agricultural Limited inayodaiwa kuchota Sh 40 bilioni kutoka Akaunti ya Madeni Nje (EPA) katika Benki Kuu Tanzania (BoT), alisema taasisi yake imeanzisha upya uchunguzi, licha ya kamati ya Rais Kikwete, kuwabana wahusika wakarudisha kitita hicho.
Dk Hoseah alisema kwa kutambua hilo, ndiyo maana amewaomba Watanzania wote wenye ushahidi wauwasilishe ofisini kwake ili kuwezesha kuendelea kwa mchakato huo wa kuwafikisha mahakamani wahusika wote. Mkuuu huyo wa Takukuru, alisema kwa sasa kumbukumbu katika jalada la usajili wa kampuni hiyo kwa Msajili wa Makampuni (Brela), zinaonyesha wamiliki wake wote wawili ni marehemu.
Kesi ya Mwakalebela
Wakati huo huo, Dk Hoseah amebainisha kwamba taasisi yake imekamilisha marekebisho ya mashtaka katika kesi inayomhusu, aliyewa katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Frederick Mwakalebela. Alisema Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoani Iringa ilikataa mashtaka ya awali ya Takukuru dhidi ya Mwakalebela kwa maelezo kuwa yafunguliwe kwa kutumia sheria mbili tofauti ambazo ni ile ya Gharama za Uchaguzi ya mwaka 2010 na ile ya Takukuru ya mwaka 2007.
Dk Hoseah alisema; Tumekamilisha marekebisho ya mashtaka dhidi ya Mwakalebela na tumeyafikisha mahakamani, ingawa tunasikia kuwa naye amefungua kesi Mahakama Kuu, tunasubiri, lakini kesi yake isingeweza kumalizika bila ya kusikilizwa.Aliongeza kesi hiyo inafanya idadi ya kesi zote za Uchaguzi Mkuu uliopita kufikia 18 hadi sasa na kwamba zote zitashughulikiwa na taasisi yake.
Kesi hiyo dhidi ya Chenge inatarajiwa kuwa moja ya kati ya kesi nzito nchini, kutokana na nafasi yake ya uongozi kama Mwanasheria Mkuu.
Mwananchi