"Waingereza wana msemo: "Nature abhors a vacuum", "hulka huchukia ombwe". Hata siasa huchukia ombwe. Kama uongozi ni mbovu, upo kama haupo, au upo kwa maslahi ya wenyewe, watatokea watu waujaze uwazi uliopo; hauwezi kuachwa wazi hivi hivi. Lakini uongozi mbovu ni kama mzoga, una tabia ya kukaribisha mafisi na mainzi. Tusidhani kuwa hulka ya siasa yetu ni tofauti na hulka ya siasa ya watu wengine; kwamba sisi tunaweza kuvumilia uongozi mbovu na tusivune matunda ya hulka ya uongozi mbovu" (Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania, Zimbabwe Publishing House 1993:52)
Ati, CCM imeshajirekebisha na kuziba ombwe hilo la uongozi chamani na serikalini mwake? Kama bado, wapinzani wana nafasi yo yote ya kuliziba katika uchaguzi wa mwaka kesho? Wapinzani wenyewe, wanao uwezo wa kuweka uongozi imara usiotetereka na wenye kuweka maslahi ya wananchi mbele? Kwa maneno mengine, kuna chama cha upinzani makini ambacho kinaweza kuchukua nafasi ya CCM, na kuleta mabadiliko yatakayolinufaisha taifa?