Hip Hop haiuzi; Wimbo unaoongoza kwa kujibiwa Bongo

Feb 6, 2024
40
50
HIP HOP HAIUZI - MADEE
WIMBO UNAOONGOZA KWA KUJIBIWA BONGO

HAMADI ALLY ndilo jina lake halisi lakini alipoingia kwenye uga wa michano akaona atafute jina ambalo litakaa kisanii lakini halitatoka nje sana ya jina lake la asili.

Historia yake kwa urefu itakuja kwenye andiko lijalo, kwa leo tubaki kwenye mada ya wimbo ambao ulileta sintofahamu kubwa kwa wapenzi wa Rap/ Hip Hop na WENGINE wamekuwa wakiujibu wimbo huu mpaka leo.

Kwanza naanza na wasanii ambao Madee aliwapitia humo; alimpaka Mangwea, Mr Blue, Langa, na Joti

"Uvumilivu ulimshinda mpaka Albert Mangwea
Akachenji She got a gwan, kidogo akasogea."

"usipofanya hivyo, hupati promo kama Langa"

" Huwezi fananisha alipo Joti, Mr Bean"
Hii ilikaziwa na Mike T kwenye ngoma ya BISHOO iliyofanywa na Ras Lion na John Walker anaposema, kamchek J Lo halafu urudi Bongo ndipo utaona game ni soo. Hizi ni zile zama za BONGO KAMA NEW YORK, kila kitu cha Bongo kilifananishwa na kile cha Mtoni.

Akawasifia watu waliokuwa wakibadilika kama Inspector Haroun na akasisitiza kuwa kama angeshindwa RnB angeimba Zouk au Taarab! Ndipo aliposema ama angebadilika kama Inspector Babu. Cha ajabu, sijawahi kusikia Madee akifanya yote haya aliyojinadi kwenye wimbo huu.

Mambo mengine ambayo Madee aliyakanyagia kwenye ngoma yake ni kwamba wana HIP HOP walivaa kama wezi, muziki wenyewe wa kishamba, huimbi mpaka ushike panga! Jukwaani hawawezi, sokoni nd'o wamelowa,

" Kwanza Hip Hop ni uhuni, kila siku kupigana." Halafu mbele anajisifia kwamba yeye ni mtoto wa Manzese kama fujo ashazoea!! Sasa mgomvi hataki wenzake wagombane! Madee bana!

Mko wachache hamvumi, bado mnaleta uhasama." Kwa kipindi kile, Bongo Fleva ilihusishwa na ulaini, hivyo kila aliyeingia kwenye game alikuwa anarap. Hapa Hamadi alilazimisha vina.

"Kwanza hamna MISINGI, nd'o maana mnayumbayumba." Hapa kama ameongea kitu cha ukweli hivi, kusingekuwa na ukweli, wasingetokea wana wanaojiita WATUNZA MISINGI, Ina maana kweli MCs na Rappers wengi wameisusa MISINGI.

"Hamjafika shule ya msingi, HAKI ELIMU ka Kayumba" Sugu alimjibu kuwa wenye elimu hawategemei game, wanauza lecture na Cv.

Hip Hop ndiyo genre yenye wasomi wengi Bongo na duniani kwa ujumla

Ukitoa George Weah, mwanasoka, bado Hip Hop ndiyo imetoa wabunge na mawaziri wengi.

Na Hawa wote ni VIDATO SITA WALIVYOPITIA NDIVYO VILIVYOWASAIDIA ( Kwa sauti ya Solo) Sasa nani anafahamu kiwango cha elimu cha Hamadi??

"Hip Hop ina NGUZO, wengi hamziwezi
Kwanza mavazi yenu mtaani mnaonekana wezi"
Huu mstari unanitafakarisha Sana. Watoto WALIANZA na skinny jeans, sasa wapo bize kuvaa magauni na sketi, je Madee anaona uvaaji huu ndiyo unaofaa kwa watoto wa kiume?

Kwamba yale mabuga, yale matisheti maovasaizi, mzee Hamadi aliona yalifanana na nguo za wezi!!!

Who inspired him to grab the mic?? How did he wear? Hapa kama hakulazimisha vina basi alipania kuwaudhi wana.

"Najua kuna wengine WATAVIZIA KUNIPIGA
ILA HAMNIWEZI, NINA SHERIA ZA KIKWETE, MKINIZINGUA SANA NITAWAFANYA VIWETE"

Line ya kuviziwa inaonesha Madee aliona wengi hawakuwa wakijiamini ila mpaka wavizie watu.

Sheria za Kikwete sasa! Sizijui mpaka leo au nd'o ile aliyosema: UKITAKA KULA, SHARTI NA WEWE ULIWE??

"SI ULIMGEZA BUSTER, MWENZIO SASA ANAIMBA, FALA BADILIKA FASTA, TUA MZIGO WA UJINGA"
Wafuatiliaji wa mambo, naomba mnisaidie kunitajia nyimbo ambazo Buster ameimba.

HIP HOP HAIUZI, MUULIZE HATA MAMU
KUNA TAPE ZA FULANI, DUKANI KAMA SANAMU.

Lord Eyes aliijibu hii, "SIYO LAZIMA NIUZE KARIAKOO."

BONGE ALININYANYASA ILA MI NI MBISHI TU"
Alinyanyaswa na nini? Au mabosi waliwekeza pesa lakini ikawa hairudi??

"MIMI MTOTO WA MANZESE KAMA FUJO NSHAZOEA"
Niweke wazi kuwa ngoma hii naipenda, mbali na mapungufu mengi niliyoyaainisha hapo juu.

Niliipenda kwa sababu tu aliifanya Madee, kwa Nini? Madee ni miongoni mwa wasanii wa kiume nilioona kwamba walikuwa WANYONGE, sasa ulivyotoka mgoma huu, akanipruvu wrong vibaya sana!

Ila kunipruvu wrong kungenoga kama angewachana Dudu na Pina. Sidhani kama angefikisha hata siku bila kulazwa!!

"HIP HOP HAIFAI, BONGO HAINA MASLAHI
NAIFANANISHA NA MKE MZURI LAKINI BADO HAZAI."
Mstari unaonikera kuliko yote!! Kuudhihaki ulemavu wa watu, ambao wengi wao hawakuutaka! Haikuwa sanaa!

" WACHACHE WALIONISALITI NAWAPOKONYA MIC NA WOTE WALIOBAKIA NAWAFANYA MARAFIKI"
Hapa sikumwelewa, anawasema wanaoendelea kurap au wale walioamua kuimba??

"TANZANIA BONGO FLEVA FIT'NA, FIT'NA"
Nimeongelea hapo juu kuwa maneno Rap/ Bongo Fleva/ Hip Hop yalitumiwa kama neno moja kwa baadhi ya watu, akiwemo Madee mwenyewe maana ngoma nzima kaitaja HIP HOP lakini kwenye outro anaitaja Bongo Fleva.

"Mimi ndo mkaanga sumu, shati langu halilambwi
Hip Hop - Bongo Fleva sema zipi hazibambi???"
Hapa tena kazigawanya kama genres mbili zenye ukianzani mkubwa!!

Kitu alichosema ukweli bwana Hamadi ni pale aliposema, " THAT'S WHY MPAKA LEO, MI' SIJUI NAIMBA NINI" Nitalirudia neno hili.

Ukiachana na kutojua anaimba nini, bwana Hamadi akasema ukweli, " TALE ALINIKATAZA NISIIMBE KAMA NYINYI." Kumbe haukuwa utashi wake ila wa mbunge wa sasa, meneja wa "Tiiaipii Tiioopii"

Ndiyo maana Farid Kubanda akawatolea uvivu wote wawili, kwenye ngoma ya MIMI kwa kusema, " WATOTO WANAPENDA KURAP, MABOSI WANAWAFOSI WAIMBE"

Ila naona badala ya kumpiga mawe Madee aliyechoma moto kijiji chetu, ingekuwa busara kuanza na wale waliouwasha moto. Madee anasema:

" Hip Hop siyo Bongo, Chegge kasema Amerika.
Mwendo wa Bongo Fleva kama Ragga na Jamaica."

Ni kweli Said Chegge Chigunda, kwenye goma lake la rege, DUDE LA KIMATAIFA alisema:
" Ukienda Congo, utakata mauno oyooo!
Hip Hop ya kweli ipo America."

Chegge aliwasha moto, sikusikia akimaindiwa, labda kwa sababu kilikuwa kijimstari tu.

Lakini pia wazo la Madee lilitoka kwa Msafiri Kondo, Mwanazuoni aliyekomaa ambaye baada ya kukosa gari la Shigongo akasikika akisema;
" Nilianza kuimba Hardcore, wadosi wakachomoa
Bana, HIYO HAIUZI, HAIPENDWI TENA INABOA."

Ambapo mstari huu umerudiwa na Madee, kama ulivyo, ambapo yeye anasema;
" Jukwaani hawawezi, sokoni nd'o wamelowa,
Hip Hop HAIUZI, HAIPENDWI, TENA INABOA."

Solo Thang alipiga dongo hili indirectly, hakushughulikiwa, lakini Madee akakipata cha moto.

Lakini nikirudi nyuma tena, kwenye ngoma ya Fid Q iitwayo NI HAYO TU, kuna sauti ya Madee mle, baada ya Fid Q kujinadi, yeye anasema:
" AH! FID Q KITU GANI!! ACHANA NAYE ASIKUZINGUENI, BONGO FLEVA KITU GANI!!"

Kuna mawili hapa, ima Madee alisema Bongo Fleva akiwa na maana ya genre nzima ikihusisha hadi Rap, ambapo kwa kipindi kile, ilichukuliwa hivyo

Au aliidiss Bongo Fleva, ambayo ilikuja kuchukuliwa kama muziki wa kuimba peke yake, mbali na Rap, na alipoona wadau na wana waliokuwa wakifanya na kupenda Bongo Fleva hawakushughulika naye, akaona abadili upande wa pili wa sarafu, wa HIP HOP ( RAP) na kukutana na moto wa wale aliowaona wezi.

Ishu nyingine aliyoiibua bwana Madee kwenye ngoma yake ni kwamba;

"NYIE WA MIKOANI ND'O MNALETA MUZIKI HUO,
SIYE KIBONGOBONGO, TUNAUONA MIZINGUO"

Wakati Karama Masudi, Mkuu wa Kikosi, Kamanda Mulla Omari, Kala Pina kwenye WABISHI WA DASLAM anasema;

" Mbishi toka Zamani, zama za KWANZA
TOKA GAME INAANZA, KATIKA ARDHI YA TANZA
DAR ND'O ILIPOANZIA, MIKOANI MKAFUATIA"

Sasa Wakongwe, na watoto wa Dar, naomba mnisaidie kwenye ukinzani huu wa hoja ulioletwa na watoto wa Dar wenzenu, nani alikuwa sahihi na nani alitupeleka chaka kuhusu evolution ya Rap Bongo??

Mara muziki unauza, mara muziki ule hauuzi, huu ni UPUUZI- CP(waa)

Na ni UPUUZI kusema GAME HALIUZI
WAKATI WE UNANGOJA KUUZA TAPE NA CD
SI' TUNAUZA MPAKA LECTURE KWA SABABU TUNA CV
- SUGU FT STARA - MCHAKAMCHAKA

MBONA HAIUZI? KIVIPI USINIUDHI, MI NAKAZA NYUZI, WE' KAMA HAIKULIPI NI MPUUZI" - NGWEA FT BABUU - WA KITAA

Watatu wote hawa waliongelea hoja ya UPUUZI WA MADEE.

Ngwea alimjibu, Langa pia alimjibu kwenye ngoma yake ya HIP HOP kwa kusema kwenye outro:
HIP HOP ND'O MAISHA, ASIJE MTU KUBABAISHA.

Mr Blue alikuwa bize kulilia penzi la Wema aliyeibwa na Kigogo Myama Waryoba TID huku Joti akiwa bize na wenzake kuisimamisha ZE COMEDY.

HIP HOP MZUKA, HIP HOP INAUZA,
HATA KWA WAJINGA PIA HUPATA MAARIFA - SISTER P - NANI MKALI?

Itakulipa vipi wakati unaimba matusi?- KINGDOM- AFANDE SELE FT MANGUSTINO

KUNA MAHUSTLER AMBAO HAIWALIPI KA' MADEE WA TIP TOP- FID Q FT SIR NATURE- UTAUA GAME.

Fid bana, hakujua amwite Madee, Mc au Rapper akaona amwite HUSTLER.

ETI HIP HOP HAIUZI, AAH! WAPI, YOU ARE LIAR- ROMA FT JOS MTAMBO- KIDOLE CHA MWISHO

ROMA akadai type za akina Madee ndo ambao wakishiba ugali wanaanza kubishana NANI ALIANZISHA VIDUKU??

Hardcore redioni wanasema haiwezi chezwa - NINAKOTOKA- Geez Mabovu ft Joh Makini

Mara Hip Hop HAIUZI- Young Killer - Sinaga swagga

S'kia wewe, ndo umesema HIP HOP hai...??? Ungekuwa na sauti kama Chid Benz ungesema hivyo wewe? HIP HOP IMESHANOGA- OMMY G FT SLAUGHTER

... Ni Kama nambite Masihi
Kwa HESHIMA, namnyang'anya Mic, Madee - DIZASTA

DIZASTA anamnyang'anya mic Madee wakati Madee naye alijinadi kuwapokonya mic, wasaliti.

Kala Pina, nabii koko
Tukija kwenye vina, ni wazi, Madee ch*ko- Nikki Mbishi

Bongo inauza Gospel, Madee mkumbusheni- Stereo

Watatu wa mwisho kwenye orodha hii walitoka familia ya Tamaduni.

Ngoma hii ilileta maneno na nakumbuka DJs wa RFA walikuwa wanaogopa kuipiga ngoma nzima.

Nilikuwa natoroka skuli ili niisikilize ngoma nzima lakini nikaishia kuambulia kipande cha beat Kisha zikawa zinagongwa ngoma nyingine!!

Vipi umemsamehe Madee kwa hili au bado una hasira naye??

Je, una kumbukumbu gani nyingine inayohusiana na wimbo huu?


MWANDISHI WA AINA YAKE.


Karibu whatsApp KWA Habari zaidi karibuni wanaaaa.


Screenshot_20240308-101335.png
 
Uandishi mzuri sana

Sent using Jamii Forums mobile app
Naunga mkono hoja.
Lakini Madee ni mtunzi mzuri, lines zake zipo fresh, ukiona kitu kimejibiwa kimegusa mfupa au aliyesema ni mtu anayeshika attention yao, maana wangeeimba wakina S-Kide Sijui watoto wa mbwa,wangepuuzwa tu.

Those times wasanii wa hiphop ni wengi lakin wachache kati yao ndio walikuwa wanalijua game la biashara. Walikuwa wanatumia Sanaaa kupata U-Spoon , madem. But game ilikuwa tamu.

Ukicheki Hiphop ya sasa ipo diluted kidog, sio ngumu kama Zamani. Zamani content ziilikuw ni Storytelling, huyu atahadithia kisa cha mtoto Iddi, yule Mpenzi Jini, huyu ataimbia mambo mambo. So ilikuwa ni uwezo wa kuweka story, yenye vina na vibes. Plus vibes la kujisifu, ila kwa sasa wana tengeneza zaid Club bangers..

So Madee alikuwa sahihi tu, vijana wali mpinga lakn wame msikiliza.
 
Sina uhakika kama Ngoma ya Langa "hiphop " na ya Madee "hip-hop haiuzi" ipi ilianza kutoka ila nahisi ya Langa ndo ya Kwanza...

Lakini nikirudi kwenye mada ni kweli Ngoma ya Hiphop haiuzi inawezekana ndo Ngoma iliyojibiwa sana na wana hip-hop wengi wa bongo.. wengine walitamani hata wamkamate wamkwide lakini ndo hivo tena alishawatisha ye n mtoto wa manzese kama ni fujo ameshazizoea...

Madee alipiga kwenye mshono hasa maana ukiisikiliza Ngoma Kwa Makini utaelewa wasanii wengi wa hip-hop hapa bongo ni kama wanafanya Tu kuburudisha washikaji lakini sio kupata dooo...

Mfano kwenye Ngoma ya Fid Q Siri ya mtungi anasema hivi "ustar anaotinga/ majumba mandinga/ ya bwana Almasi (diamond platinum) je hizi "track za harakati" ni ujinga?? Hapo alihoji wasanii wa Kubana pua kama diamond platinum kupata mafanikio makubwa kiuchumi kutokana na muziki wa kulia lia je, hawa wanaofanya hip-hop wanapoteza muda maana hapo alikiri kua "HIPHOP HAIUZI WALA HAILIPI" ...

Lakini pia Songa aliwahi kusema "Hatuuzi sokoni tunauza juu Kwa juu" kumaanisha Hiphop haina soko ndo maana wanauza Ngoma zao directly... Rejea wanachofanya Nikki mbishi na Nash MC hua wakitoa album wanaitambulisha Tu kisha ili uipate lazima wakuuzie wao kama nguo dukani...

Anyway nimechoka kutype lakini Madee alikua na lengo la kuwaamsha Wana hiphop watafute njia sahihi ya kupata hela kulingana na kazi zao kubwa but wengi wakimchukulia negative... Walau Stamina alimwelewa ndo maana aliwahi kuimba "hakuna Muziki wa biashara ila kuna biashara ya muziki .."

Alichokifanya Madee enzi ya Jakaya kikwete ndo hiki alichokifanya Khaligraph Jones enzi za Samia Saluhu kwenye Ngoma yake ya "Bongo fevor" lakini Wana hip-hop wameishia kuwatukana na kuwajibu vibaya "manabii" badala ya kusikiliza "neno" lao...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom