Hadithi: Sweet Pain(Mauvivu Matamu)

Hadithi: Sweet Pain(Mauvivu Matamu)

Kanungila Karim

JF-Expert Member
Joined
Apr 29, 2016
Posts
20,746
Reaction score
25,638
MTUNZI : ERIC SHIGONGO

MWANZO


HALI ya hewa ilikuwa ya baridi kali, kwa kipindi hicho cha mwezi Machi, ilikuwa ni hali ya kawaida kwa eneo hilo kuwa na baridi. Watu walikuwa wengi sokoni wakiendelea na shughuli zao kama kawaida.
Soko hilo lililopo eneo la Shokoni, Marangu, mkoani Kilimanjaro ni maarufu sana kwa uuzaji wa mazao mbalimbali.
Wilson Johnson, mzungu kutoka nchini Marekani akiwa na wenzake Joel Poulsen na David Robert walikuwa kijijini hapo kwa kazi moja tu; kumtafuta msichana mrembo ambaye wangesafiri naye hadi Marekani kwa ajili ya kwenda kwenye shindano la kumsaka msichana atakayecheza sinema iitwayo Sweet Pain. Ilikuwa ni kampeni ya Afrika nzima, walisambazwa mawakala mbalimbali kwa ajili ya kutafuta wasichana ambao wangeshindanishwa na mwisho mshindi angecheza sinema hiyo.
Ilikuwa ni kazi ngumu sana kumpata msichana mwenye sifa zilizohitajika. David Robert ambaye alikuwa ni Mtanzania aliyeishi nchini Marekani, ndiye alikuwa mwenyeji wa wageni wake hao maana wote walikuwa ndio mara ya kwanza kufika nchini Tanzania.
Walianzia jijini Tanga, Mwanza kisha baadaye wakaelekea mkoani Mbeya bila mafanikio yoyote. Wakiwa jijini Dar es Salaam tayari wamekata tamaa kabisa, David ndiye aliyetoa wazo la kwenda kijijini huko Marangu ili kujaribu bahati.
Wapo sokoni wakiangaza macho huku na huko na mara nyingi wale wazungu walikuwa wakiguna, wakisema kwamba hakuna uwezekano wa kumpata msichana mwenye vigezo kijijini hapo.
“Oh! Look, can't that girl be suitable for us?”
(Oh! Angalia, yule msichana hawezi kutufaa kweli?)
Wilson Johnson alisema akisonza kidole kuonesha mahali msichana aliyevaa nguo kuu-kuu akipita na kapu lake lenye bidhaa.
“My God! I can't believe my eyes, I do not remember when I can across a beautiful girl such as this one.
I think our mission has come to the end.
We have to talk to her right away!” (Mungu wangu! Siamini macho yangu, sikumbuki kama niliwahi kukutana na msichana mrembo kama huyu.
Nadhani safari yetu inaelekea ukingoni.
Ni lazima tuongee naye sasa hivi!)
Joel Poulsen akadakia. “David make sure you talk to the girl right now!”
(David hakikisha unaongea na yule msichana sasa hivi!) Wilson alimwambia David.
“Okay sir, I will do so.” (Sawa,nitafanya hivyo.)
Mara moja David akachepuka akimkimbilia yule msichana. Kwa kumtazama alionekana mrembo sana, lakini alikuwa amevaa nguo za hadhi ya chini kabisa.
David akachanganya miguu hadi alipomfikia sehemu aliyokuwa amesimama akinunua nyanya.
Alipofika alisimama nyuma yake, akimuacha amalize alichokuwa akikifanya kisha akamgusa bega na kumwambia: “Samahani, samahani sana!”
“Unasemaje?”
“Usinifikirie vibaya binti, mimi ni mtu mwema kwako na nina jambo zuri sana nataka kukushirikisha!”
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 02


Mawakala Wilson Johnson, Joel Poulsen na David Robert wameingia nchini Tanzania wakitokea Marekani kwa lengo la kumsaka msichana atakayeingia katika shindano la kumsaka msanii atakayeshiriki katika Filamu ya Sweet Pain, ambaye angecheza na mmoja wa wasanii maarufu kutoka Hollywood, Marekani.

Mshindi angepata dola za Kimarekeni milioni mia moja kama fedha za mkataba wa kucheza sinema hiyo. Mawakala hao walianzia Tanga, Mwanza, Mbeya na baadaye wakamalizia Dar es Salaam bila mafanikio yoyote.

Wakiwa wamekata tamaa kabisa, David Robert, Mtanzania anayeishi Marekani akawashauri wenzake wakajaribu kwenda katika kijiji cha Shokoni, Marangu mkoani Kilimanjaro. Wote kwa pamoja walikubaliana na kufunga safari hadi huko ambako dalili za kumpata msichana waliyekuwa wakimuhitaji zilikuwa ndogo.

Muda mwingi, wazungu Wilson Johnson na Joel Poulsen walikuwa wakilalamika kuwa wamepoteza muda wao bure kwa kuwa hawakuona wasichana wenye viwango kama yalivyokuwa matarajio yao.



Wakiwa katika soko maarufu la mazao la Shokoni, mtazamo wao ulibadilika baada ya kumuona msichana mwenye nguo zilizochoka lakini mwenye sura ya kuvutia kuliko kawaida, Manka. David ndiye aliyemfuata, akazungumza naye kisha baadaye akamkutanisha na wenzake na kukubaliana kwenda kwa mama yake.

Kila kitu kikawa sawa, ilikuwa ni huzuni kubwa sana kwa Martin, mchumba wa Manka lakini hakuwa na la kufanya zaidi ya kukubaliana naye, fedha ambazo angepata zilikuwa ni nyingi sana.

Siku ya safari ya kwenda Dar es Salaam ikafika, Martin akamsindikiza hadi kituoni, akapanda basi na kusafiri hadi Dar, aliposhuka katika Kituo cha Mabasi ya Mikoani cha Ubungo akachukua teksi na kuanza safari ya kwenda katika Hoteli ya Kempinski, walipofikia wenyeji wake.

Akiwa anapanga ngazi ili kuelekea mapokezi, taswira ya mpenzi wake Martin ikamjia. Aliumia sana kusafiri na kumuacha mwanaume ambaye anampenda kwa moyo wake wote.
Je, nini kitatokea? SONGA NAYO...

ALITAMANI sana kwenda Marekani, mwanga wa mafanikio ulionekana kuwemo nchini humo, lakini ndani ya moyo wake kulienea kijana fukara Martin. Tangu alipokutana na wale wageni kijijini kwao kwa mara ya kwanza na kuzungumza nao kuhusu kusafiri, alimsahau kabisa Martin.

Hakumkumbuka kwa lolote, macho yake yalikuwa Marekani. Alikuwa na hamu ya kupanda ndege kwa mara ya kwanza, maana siku zote aliishia kuziona zikipita angani.
Lakini ghafla moyo wake ukadunda, akihisi kumpoteza mtu muhimu sana katika maisha yake.

Alisimama pale kwenye ngazi akitafakari kwa muda mrefu sana. Alijitahidi kuzuia hisia zake, lakini ilikuwa vigumu sana. Mwisho, alitakiwa kufikiri zaidi juu ya maisha yake, maisha ambayo kama angefanikiwa kuyatengeneza basi hata Martini naye angefaidi kile alichokichuma.

“Lakini nakwenda kutafuta maisha. Mungu anaweza kunisaidia. Najua mimi siyo mzuri sana, si rahisi kushinda lakini hizo fedha nitakazopewa kwa ajili ya kushiriki ni nyingi na zitanisaidia katika maisha yangu mimi na Martin.

“Najua Martin unateseka lakini vumilia, muda si mrefu nitarejea mpenzi wako. Nakuahidi sitakusaliti hata mara moja,” alizungumza kwa sauti ya chini akiwa pale kwenye ngazi.
Baadaye akakata shauri kwenda mapokezi. Akapiga hatua za taratibu hadi alipofika na kukutana na sura ya msichana mrembo aliyekuwa amekaa kwenye kiti cha kuzunguka.

“Habari yako dada?”
“Salama, karibu.”
“Ahsante, pole na kazi.”
“Nimeshapoa, karibu sana. Naomba nikusaidie tafadhali.”

“Naitwa Manka, natokea Marangu, ni mgeni wa akina David Robert, wameniambia nije niwaulizie hapa mapokezi!”
“Ooooh! Wewe ndiye Manka kutoka Kilimanjaro?”
“Ndiyo!”
“Subiri...” yule dada akasema huku akinyanyua mkonga wa simu na kubonyeza vitufe vya namba.

Kimya cha muda mfupi kikapita, kisha akaanza kuzungumza na mtu aliyekuwa upande wa pili. Aliporudisha mkonga chini akamgeukia Manka na kuanza kuzungumza:
“Kaa pale, subiri anakuja!”
“Ahsante sana.”
Dakika mbili baadaye, David alitokea akiwa na tabasamu pana. Akamfuata Manka alipokuwa ameketi.

“Karibu sana, pole na safari!”
“Ahsante, shikamoo!”
“Marhaba Manka, habari za nyumbani?”
“Nzuri.”
“Mama hajambo?”

“Kabisa!”
“Basi karibu sana.”
“Nashukuru.”
Manka akasimama na kuongozana na David hadi kwenye lifti, David akabonyeza kitufe kilichokuwa mlangoni, ukafunguka! Manka akabaki anashangaa.

“Tuingie,” akasema David, Manka akaingia bila kuuliza, ingawa lilikuwa jambo geni kwake.
Walipoingia mlango ulijifunga, kisha David akabonyeza kifute kilichoandikwa namba tisa, lifti ikaanza kupanda juu taratibu. Manka alishtuka sana. Walipofika ghorofa ya tisa, lifti ilisimama na mlango ukafunga.

Wakatoka. Safari yao ikaishia kwenye chumba cha baa kilichokuwa katika ghorofa hiyo. Hapo Manka akakutana na wale wazungu wawili Wilson Johnson na Joel Poulsen.
Hakuwa akifahamu kuongea vizuri lugha ya Kiingereza, kwa hiyo aliwasalimia kwa Kiswahili kisha David akawa mkalimani wake. Tayari ilikuwa jioni, kilichofanyika ilikuwa ni kumuonesha chumba chake, kilichokuwa kimeshalipiwa kabla ya yeye kufika.

“Oga, halafu uje tule, najua utakuwa umechoka sana, kwa hiyo utapumzika hadi kesho tutakapokwenda mjini kwa ajili ya manunuzi ya nguo na kwenda salon tayari kwa matayarisho ya safari,” David alimwambia Manka.
“Sawa kaka David, ahsante sana.”
“Usijali.”

Manka akaingia katika chumba chake, moyoni alikiri hakuwahi kuingia katika chumba kizuri kama kile. Alihisi kama alikuwa peponi.
“Dah! Hivi watu wanaolala humu huwa wanawaza kama kuna kufa kweli?” alijiuliza akishangaa uzuri wa chumba kile.

Kila kitu kilikuwa kigeni kwake. Macho yake yalimeza uzuri wa chumba, akiwa haamini kama mwili wake ungelala juu ya kitanda kizuri kama kile alichokuwa akikiona.
Akasaula nguo zake kisha akaingia bafuni na kuoga huku akisngaa kila kitu. Alipokuwa tayari alitoka na kwenda alipowaacha akina David. Tayari walikuwa wameshaweka oda ya chakula kwa hiyo muda mfupi baadaye vyakula viliwekwa mezani, wakaanza kula kwa furaha.
Saa 4:00 za usiku, Manka aliaga kwenda kulala chumbani kwake.

“Sawa usiku mwema dada Manka.”
“Nanyi pia, naomba uniagie na hao!”
“Bila shaka.”
Manka alipoingia chumbani kwake, hakuwa na kitu kingine cha kufanya zaidi ya kujitupa kitandani na kulala. Alilala fofofo, akihisi kupata starehe ya ajabu ambayo hakuwahi kuipata katika maisha yake. Hata hivyo, ndoto juu ya mpenzi wake Martin, zilimtawala usiku mzima.

***
Kitu cha kwanza kufanyika asubuhi walipotoka hotelini, ilikuwa ni kwenda saluni. Manka aliingizwa katika saluni maarufu ya kiume iliyokuwa Posta iitwayo The Ball Barber Shop, David akataka nywele za Manka zikatwe na ziwe fupi kabisa na ziwekwe dawa aina ya Wave pamoja na Super Black. Baada ya kutoa maagizo hayo yeye na wenzake wakaondoka na kwenda Uhamiaji, kushughulikia hati ya kusafiria ya Manka. Fedha ikaongea, ikapatikana siku hiyo hiyo!

Saa moja baadaye waliporudi saluni, walimkuta Manka akiwa mpya kabisa. Alikuwa amependeza kuliko kawaida.
“Siamini macho yangu, huyu mtoto uzuri wake unazidi kuongezeka, sidhani kama hatashinda...lazima ashinde,” Wilson alimwambia Joel.
“Mh!” David akaguna.

“Mbona umeguna David?” Joel akauliza.
“Kama tungeondoka bila kwenda Kilimanjaro, tulikuwa tumemuacha msichana mzuri sana,” David akasema.
Walikuwa wakizungumza kwa lugha ya Kiingereza, kwa hiyo Manka hakuelewa kitu. David akalipa kisha wakaanza kutembea katika maduka ya nguo, wakamnunulia kila aina ya nguo za thamani, viatu na mapambo mengine.
Walipomaliza kufanya manunuzi, walirudi hotelini, wakiwa wanasubiri kwa hamu kubwa siku ya safari.

***
Ilikuwa kama ndoto, Manka alikuwa amekaa kwenye siti akiwa amefunga mkanda, ndani ya ndege ikiwa angani. Alitamani sana kukanyaga ardhi ya Marekani.
Ndege ilipokuwa ikichana mawimbi, Manka akashangaa anaanza kumkumbuka tena mpenzi wake Martin. Ghafla akaanza kulia. Alijihisi hakuwa tayari kwa safari.

“Mbona unalia?” David alimwuliza baada ya kuona machozi mashavuni mwa Manka.
“Mmh! Mmh!” Manka akajibu akitingisha kichwa kukataa.
“Hebu niambie, nini kimekupata?”
“Martin!” akasema Manka akizidi kulia.

Je, manka ataghairisha safari???

Tukutane katika sehemu ya tatu.
 
Tutupie dongo la 3

Sent using Jamii Forums mobile app
SEHEMU YA 03



David Robert, Mtanzania anayeishi Marekani anaingia Marangu, mkoani Kilimanjaro akiwa na wenzake Wilson Johnson na Joel Poulsen ambao ni wazungu, kwa pamoja wanamsaka msichana mrembo ambaye angeweza kuingia kwenye shindano la kumsaka msanii atakayepewa mkataba wa dola milioni mia moja kwa ajili ya kucheza Sinema ya Sweet Pain huko Marekani.

Muda mwingi, wazungu Wilson Johnson na mwenzake Joel Poulsen walikuwa wakilalamika kuwa wamepoteza muda wao bure kwa kuwa hawakuona wasichana wenye viwango walivyohitaji. Wakiwa katika soko maarufu la mazao la Shokoni, mtazamo wao ulibadilika baada ya kumuona msichana mwenye nguo zilizochoka lakini mwenye sura ya kuvutia kuliko kawaida, Manka.

David ndiye aliyemfuata, akazungumza naye kisha baadaye akamkutanisha na wenzake na kukubaliana kwenda kwa mama yake kwanza. Kila kitu kikawa sawa. Matayarisho ya safari yakafanyika, Manka akaondoka kuelekea Dar es Salaam kuwafuata akina David, lakini nyuma akimuacha mpenzi wake Martin ambaye alikuwa anampenda kuliko kawaida.

Dar es Salaam alikutana na akina David ambao walimpeleka madukani kwa ajili ya kununua nguo na baadaye wakampeleka saluni. Akatengenezwa nywele zake na kubadilika. Manka akawa mpya kabisa.

Wakiwa kwenye ndege, safarini kuelekea Los Angeles, Marekani, Manka alimkumbuka mpenzi wake Martin. Alijitahidi sana kujikaza na kuficha hisia zake, lakini akazidiwa, ghafla machozi yakaanza kuchuruzika machoni mwake.

David pekee ndiye aliyegundua kwamba Manka alikuwa akilia. Alipomuuliza, akamjibu kwa kifupi; Martin!
Je, nini kitatokea? SONGA NAYO...

HISIA kali juu ya mpenzi wake Martin ndizo zilizomjia na kumtesa moyoni. Alitamani sana kwenda Marekani na ni kweli tayari alikuwa angani kwenye ndege akielekea huko, lakini alishindwa kuelewa ni kwa namna gani angeweza kukaa mbali na mpenzi wake.

Haikuwa hiyari yake machozi kumwagika machoni mwake, bali mapenzi mazito ambayo yalishindwa kujificha na kutoka hadharani! Alimpenda sana Martin wake.

David hakuelewa kilichompata Manka, lakini hata alipomtajia jina la Martin alibaki na mshangao, hakuelewa maana yake. Akamwangalia Manka machoni, alipogundua hilo, akazidi kulia.
“Manka tafadhali, acha kulia. Enhee huyo Martin ni nani?”
“Martin?”

“Ndiyo ni nani?”
“Mchumba’angu!”
“Amefanyaje sasa? Ndiye anayekusababisha ulie?”
“Ndiyo...nampenda sana. Sijui ni kwa nini nashindwa kuamini kuwa hatachukua mwanamke mwingine! Naona kama anaweza kunisaliti.”

“Hapana Manka, huna sababu ya kuwaza hivyo, kama anakupenda hawezi kufanya hivyo.”
“Najikuta nimepoteza matumaini kabisa, nahisi kama nimefanya uamuzi mbaya kwenda Marekani.”

“Kwani umesahau kwamba unakwenda kwa ajili ya kutengeneza maisha yako? Kumbuka kwamba iwapo utashinda, utapata dola milioni mia moja, ni fedha nyingi sana ambazo zinaweza kubadilisha kabisa maisha yako.

“Hilo ndilo jambo la msingi zaidi unalopaswa kufikiria kwa sasa, mengine yote achana nayo. Kwa nini usimwamini mwenzako? Halafu hutakiwi kuwa na mawazo, maana unakwenda kushindana, lazima akili yako iwe imetulia kabisa!”
“Sawa kaka David, nimekuelewa vizuri!”

“Kama ndivyo, naomba ufute machozi.”
Manka hakubisha, akafuta machozi na kujitahidi kutulia. Machoni hakuwa na machozi kabisa lakini ndani ya moyo wake alikuwa katika wakati mgumu sana wa mawazo dhidi ya Martin wake.

Hata hivyo, hakukuwa na jinsi, aliutuliza moyo wake, akajitahidi kukubaliana na hali halisi. Safari ikaendelea, ilikuwa ni mara yake ya kwanza kusafiri na ndege, lakini furaha yake ilizimwa na Martin.

***
Walipotua katika uwanja wa ndege, David na wenzake wakaongozana na Manka hadi nje ya uwanja ambapo waliwakuta watu waliofika kuwapokea wanawasubiri wao. Walikuwa ni wanaume wawili, Moses na Jackson.

Walipokutanisha macho yao tu na Manka wote wakaonekana kupagawa. Manka alikuwa mwanamke mrembo kuliko kawaida. Haikuwa rahisi kuamini kwamba alitokea kijijini Shokoni akiwa hana hili wala lile.
Siri iliyokuwa nyuma ya mwonekano wake hawakuijua, waliojua yote hayo ni David na wenzake.

“Sijapata kuona msichana mzuri kama huyu, bila shaka ndiye atakayeshinda!” Jackson akamwambia Moses.
“Ni kweli, kule kuna wasichana wengi wazuri, lakini huyu amewazidi wote. Kwa hakika ni mwanamke mrembo sana!”

Walikuwa wakizungumza wakati akina David na Manka wakiwa wanawakaribia kabisa.
“Poleni sana na safari,” akasema Moses akiwaangalia akina David.
“Ahsante sana!”
“Naona mmekuja na malkia?”

“Ndiyo hivyo, tuna imani anaweza kubahatika!”
“Hongereni sana kwa kazi nzuri!”
“Tunashukuru sana, vipi huku wameshakuja wote?”
“Wengi waliokuwa bado, wameingia juzi, jana na leo, mpaka sasa hivi bado nchi tatu tu; Ghana, Zimbabwe na Malawi, wengine wote tayari.”
“Ok! Basi twendeni hotelini.”

“Karibuni sana...Tanzania ndiyo ina warembo kiasi hicho? Kuna haja ya kwenda kutembea huko siku moja, unaweza kujikuta unaoa Mtanzania...” Moses akatania.
Bila kupoteza muda, wakaingia kwenye magari, safari ya kwenda hotelini ilipo kambi ya warembo hao ikaanza. Njia nzima Manka alikuwa akishangaa jinsi Los Angeles lilivyo katika mpangilio mzuri wa kuvutia.

Kila kitu kilikuwa kipya kwake, hakutegemea kama kuna siku angefika kwenye jimbo kubwa na la kupendeza kiasi kile. Kuna wakati alikuwa akidhani yupo ndotoni, lakini fikra hizo zilikatishwa na matukio yote kufanyika kwa uhalisia.
Isingekuwa rahisi kuwa amelala kwa siku zote hizo, hivyo akaamini kwamba ni kweli alikuwa amekanyaga nchi ya Marekani bila kutegemea.

“Mh! Pazuri sana huku kaka David.”
“Ni kweli, huku wenzetu wameendelea sana, kila kitu ni mipango, kama nasi tukiweka mipango ya muda mrefu, tunaweza kuibadilisha Tanzania yetu!”
“Ni kweli kabisa!”

Safari iliendelea, gari walilopanda David na Manka likiwa limetangulia na lingine lililowabeba Wilson na Joel likiwafuata kwa nyuma. Ni kama Manka alikuwa ameingia kwenye dunia mpya kabisa. Mazingira ya Los Angeles yalimtamanisha sana.
“Belair Hotel!” Manka alisoma maandishi hayo juu ya bango lililokuwa katika lango kubwa la kuingilia katika hoteli hiyo.

Dereva akaendesha taratibu hadi kwenye maegesho, akaegesha. Wote wakashuka, nyuma yao gari lingine likaingia na kuegesha, wakashuka na kuungana na wenzao, kisha wakaongozana kuingia mapokezi.

Manka akafanyiwa usajili kisha akaoneshwa chumba chake ndani ya hoteli hiyo. Alitakiwa kupumzika kwanza, hadi jioni ambapo angekutanishwa na washiriki wengine. Ndivyo ilivyokuwa jioni walikutana kwenye chumba cha mkutano kwa ajili ya kufahamiana.
Kulikuwa na wasichana wengi warembo kutoka nchi mbalimbali za Bara la Afrika, ambao kila mmoja alikuwa anatamani kushinda mkataba huo ambao ungebadilisha kabisa maisha yao.

Siku hiyo waliingia wasichana wawili tu kambini hapo, Manka aliyetokea Kilimanjaro, Tanzania na Wambui aliyetokea Nairobi, Kenya. Kwa kawaida, huanza kuingia wenyeji kwanza kisha wageni kuingia mwishoni.

Wa kwanza kuingia alikuwa ni Wambui ambaye alishangiliwa lakini si kwa kiwango kikubwa. Hatimaye zamu ya Manka ikafika, alipoingia tu kwenye chumba cha mkutano, watu wote wakamtolea macho!

Manka akaogopa sana. Akasita kutembea, akasimama na kujiangalia kama alikuwa amevaa vizuri, aliamini walikuwa wakimshangaa kutokana na kukosea kitu fulani katika mpangilio wa mavazi yake.

Hakujua kwamba, alikuwa kivutio kikubwa kwao! Bila kuelewa kilichotokea, Manka alikuwa akikaribia kunyakua kitita cha dola milioni mia moja!

Je, manka atafanikish ndto ya kuish maisha ya kifahari na martin???
 
SEHEMU YA 04


Walipokutana naye kwa mara ya kwanza kijijini Shokoni, Marangu mkoani Kilimanjaro hawakutegemea kama Manka angekuwa mrembo kama alivyoonekana baada ya kumtengeza jijini Dar es Salaam tayari kwa maandalizi ya kwenda nchini Marekani kwa shindano la kumsaka msichana mwenye mvuto wa kuigiza filamu ya Sweet Pain.

Wote kwa pamoja, Wilson, Joel na David wakiwa na Manka wakapanda ndege kwa safari ya kwenda Los Angeles, Marekani. Wakiwa angani Manka alimkumbuka mpenzi wake Martin. Alijitahidi sana kujikaza na kuficha hisia zake, lakini akazidiwa, ghafla machozi yakaanza kuchuruzika machoni mwake.

David akawa na kazi ya kumtuliza, ambapo alifanikiwa na Manka kunyamaza kabisa. Waliendelea na safari hadi walipotua jijini Los Angeles, Marekani Manka akiwa mgeni kwa kila kitu.

Walipotua uwanja wa ndege, tayari kulikuwa na watu maalum wa kuwapokea waliokuwa na magari wakiwasubiri, wakaingia kwenye magari na safari ya kwenda hotelini ikaanza.
Baada ya mwendo wa muda mfupi, waliingia kwenye Hoteli ya Belair iliyokuwa katikati ya Jiji la Los Angeles ambapo kambi ya washiriki wa filamu hiyo ilikuwepo. Manka akaoneshwa chumba alichotakiwa kulala na kuingia humo alipopumzika hado jioni ambapo alitakiwa kukutanishwa na washiriki wenzake.

Siku hiyo walikuwa wameingia washiri kutoka nchi mbili; yeye na Wambui kutoka Kenya. Wa kwanza kuingia katika chumba cha mkutano alikuwa ni Wambui wa Kenya, ambaye hakushangiliwa sana, alipoingia Manka kelele zikasikika ukumbi mzima!

Manka akaogopa na kushindwa kutembea, alichoamini yeye ni kwamba washiriki wenzake walikuwa wanamzomea, akasimama na kujiangalia kama kuna kitu alikuwa amekosea katika mwili wake. Hakujua kwamba uzuri wake uliwashangaza wengi na hawakuwa wakimzomea bali wanamshangilia.
Je, nini kitatokea? SONGA NAYO...

SHANGWE ziliendelea kusikika ukumbini, warembo wakimshangilia sana Manka. Kwake ilikuwa ni makelele, alihisi kama anazomewa. Tangu siku ya kwanza warembo walipoanza kuingia katika kambi ile, kila walipoingia wageni ilikuwa lazima watambulishwe.

Mara zote wale walioonekana kuvutia zaidi kuliko wengine walikuwa wakishangiliwa sana. Pamoja na kwamba walishaingia warembo wengi, Manka alionekana kuvunja rekodi. Alikuwa mzuri kuliko Martha wa Rwanda ambaye alivunja rekodi kwa kuonekana kuwa ndiye msichana mrembo kuliko wote, lakini baada ya ujio wake alionekana kumzidi!
“Manka karibu, tembea usiogope,” David akamwambia Manka ambaye alionekana kupigwa na butwaa.

Katika maisha yake alijua yeye ni msichana wa chini ambaye isingekuwa rahisi kukubalika mahali popote, mtu pekee ambaye alionekana kumkubali katika maisha yake naye akamkubali alikuwa ni Martin tu, mpenzi wa moyo wake.
“Sijaelewa,” akasema Manka akionekana kuogopa sana.
“Hujaelewa nini?”

“Yaani sijaelewa kama wananishangilia au wananizomea!”
“Mh! Manka, siku zote wanaoshangilia huonekana usoni na hata wanaozomea pia sura zao hudhihirisha hilo.”
“Haya ngoja nijitahidi,” Manka akasema akionekana kuona haya.
Akaanza kupiga hatua za taratibu kuelekea mbele. Shangwe zikazidi. Manka alikuwa tishio katika kambi ile. Uzuri wake ulikuwa wa kutisha.

“Hawa ndiyo wageni wetu ambao wameingia hapa kambini leo. Huyu ni Wambui Steven kutoka Nairobi Kenya, naye atakuwa miongoni mwenu hadi siku ya shindano,” Paul Lewis, ambaye alikuwa mkufunzi wa washiriki hao alisema.

Watu wote ndani ya ukumbi wakaanza kushangilia. Aliwaacha mpaka waliponyamaza kabisa, akamshika mkono Manka, kabla hajatamka chochote, tayari kelele zilishaanza kupigwa.
“Anaitwa Manka Matias, yeye anatokea Kilimanjaro, Tanzania. Hawa ndiyo wageni walioingia leo hii kujiunga nasi. Tafadhali tuwape ushirikiano wa kila namna,” alisema Paul.

Kelele za makofi zikaendelea, alionekana kukubalika kwa kasi sana. Kilichofuata baada ya hapo ilikuwa ni kuelekea katika ukumbi maalum wa chakula, wakapata chakula cha usiku pamoja kisha wote wakaingia vyumbani mwao.

***
Baada ya chai ya pamoja, asubuhi ya siku iliyofuata, Manka aliitwa na David aliyeongozana naye hadi ofisini kwa Moses Chrissant ambaye alikuwa ndiye Msimamizi Mkuu wa Kambi kwa mazungumzo zaidi.

“Kama unavyomuona ni mrembo sana, anaonekana kuwa na nafasi kubwa ya kushinda, lakini ana mapungufu kadhaa ambayo tunatakiwa kumsaidia ili awe bora,” David alimwambia Moses kwa Kiingereza.

“Ndiyo David, hata mimi naona anafaa sana, mpaka hapa tulipofikia, sijui kama kuna ambaye anaweza kushindana naye!”
“Ni kweli kabisa.”
“Mlimchoropoa wapi?”

“Acha ndugu yangu, yaani tulikuwa tumeshakata tamaa kabisa, tukaamua kwenda kijijini kabisa, huwezi kuamini kabisa, tukakutana naye.
“Tena alikuwa mchafu kabisa, lakini tulipomfikisha mjini, tukamwingiza saluni na kumnunulia nguo mpya, matokeo ndiyo haya unayoyaona hapa!”
“Dah! Nyie wakali sana. Mimi sioni kama ana tatizo, kwani umeona ana tatizo gani?”
“Si kubwa sana, ni dogo tu!”

“Ni nini?”
“Lugha.”
“Anaongea lugha gani?”
“Umesahau mara hii lugha ya Watanzania?”
“Kiswahili?”

“Ndiyo, tena huyu ametokea kule lugha hiyo ilipozaliwa kabisa. Hafahamu Kiingereza na ni lugha ambayo itatumia katika sinema hiyo, lazima apate kozi.”
“Sina pingamizi aanze mara moja, maana hayupo peke yake.”
“Sawa.”

Baada ya hayo, Manka akatambulishwa kwa Moses kisha akaelezwa mpango mzima uliokuwepo, akakubaliana nao. Wiki moja baadaye akaanza rasmi kujifunza Kiingereza.
Manka alimshangaza mwalimu wake, alikuwa na kichwa chepesi kuliko kawaida, ndani ya wiki mbili tayari alikuwa ameshajua vizuri elimu ya mwanzo ya lugha hiyo.
Angalau alikuwa akiweza kuwasiliana na wenzake, ambao wengi walikuwa wakitumia lugha hiyo vizuri.

Siku ya shindano ikazidi kukaribia, naye akizidi kukazana kuongeza bidii zaidi katika kujifunza lugha hiyo.
Baada ya mwezi mmoja alikuwa anajua kuzungumza na kuandika lugha hiyo vizuri. Matumaini ya kuibuka mshindi yakazidi kuongezeka.

Kwa muda aliokaa kambini hapo aligundua kwamba washiriki wengi walikuwa wakimwogopa kutokana na uwezo wake mkubwa wa kuonesha kipaji chake hadharani, alishazoeana na wenzake na wakati wa mashindano madogo madogo alikuwa akishinda.

Ilifika wakati, hata yeye mwenyewe alianza kujiamini kuwa alikuwa na mvuto na uwezekano wa kushinda ulikuwa mkubwa. Hata hivyo, hakujipa asilimia mia moja, kwani miongoni mwa washiriki wenzake, kuna wengine aliamini walikuwa na uwezo kumzidi yeye.
Akaisubiria kwa hamu sana siku ya shindano hilo.

***
Ukumbi ulikuwa umejaa watu wengi sana wakifuatilia shindano la kumtafuta msichana mwenye mvuto ambaye angeshiriki katika filamu ya Sweet Pain, tayari washiriki walishapita raundi moja na kilichokuwa kikisubiriwa ni kutajwa majina ya washiriki waliongia Kumi Bora.

MC akatangaza majina ya waliongia Kumi Bora, ambapo Manka alikuwa mmoja wao. Alifurahi sana kuingia hatua hiyo, hakuamini kama amefanikiwa kuendelea kuwepo kwenye shindano, maana zawadi kwa washiriki waliofika katika hatua hiyo ilikuwa kubwa sana!

Mchujo ukaendelea, wakatajwa Tano Bora, naye akawepo, kila kitu kiliendelea kuwa kama miujiza katika maisha yake. Hatimaye ikafikia hatua ya kuwataja washiriki walioingia Tatu Bora, hapo kitete kikamjaa akiwa hajui kitakachotokea.

“Walioingia Tatu Bora ni Martha Lucas kutoka Rwanda, Mariam Enziku wa Nigeria na Manka Matias wa Tanzania...” jina la Manka lilipotajwa, ukumbi mzima ukalipuka kwa kelele za kumshangilia.

Ni kama walikuwa wakisubiri yeye tu atajwe. Manka hakuamini kabisa. Moyo ukamdunda sana, ukamuingia kitu kama cha ubaridi mkali, jasho jembamba likimtoka mwili mzima! Kitendawili kikabaki kwa atakayekuwa mshindi.
 
SEHEMU YA 05



Watafutaji wa watu wenye vipaji duniani (Talents Scouts) wanaingia nchini Tanzania kwa lengo la kumtafuta msichana mwenye sifa za kushiriki kucheza filamu iitwayo The Sweet Pain, inayomwonesha msichana wa Kiafrika aliyechukuliwa kwenda Ulaya ambako aligeuzwa mtumwa wa ngono na kuteseka vibaya.

Wamezunguka Tanzania nzima hatimaye wakafika mkoani Kilimanjaro kwenye Kijiji cha Shokoni, Marangu, ambako walikutana na msichana aitwaye Manka! Walipomwona tu kwa uzuri na sifa zake za mwanamke halisi wa Kiafrika, akiwa na ngozi nyeusi, nyororo ya kuvutia, wafuatiliaji hao David na Joel walitetemeka na kuamini msichana waliyekuwa wakimtafuta ndiye aliyekuwa mbele yao.

Baada ya kuwaona wazazi wake na kuongea nao, hatimaye walikubaliana na taratibu za safari zikafanywa, Manka akiwa na maumivu makali moyoni mwake sababu alikuwa anamwacha mvulana aliyempenda, Martin. Hakuwa na jinsi, wakaagana kwa huzuni kubwa na kusafiri hadi Dar es Salaam ambako siku chache baadaye waliunganisha hadi Los Angeles, Marekani, kichwani mwake Manka akimfikiria Martin na kulia.

Hakuwa Manka peke yake aliyekuwa amepatikana, wasichana kutoka pande mbalimbali za dunia walikuwa wamekusanywa katika jiji hilo kwa ajili ya kushiriki shindano liitwalo Who is the next movie star? ambalo lingemtoa msichana mmoja tu wa kushiriki katika filamu hiyo.

Wasichana waliokusanywa ni wazuri na wana sifa zote, wanamtetemesha Manka hasa kwa sababu lugha ya Kiingereza kwake ilikuwa ni tatizo. Hata hivyo akajipa moyo na kujifunza Kiingereza kwa muda kabla ya shindano ili awe na uwezo wa kuwasiliana.

Siku yenyewe ilipofika hakuamini alipoibuka miongoni mwa wasichana watatu bora, wakiwemo Martina Lucas kutoka Rwanda na Mariam Enziku kutoka Nigeria. Swali ni kwamba nani ataibuka mshindi mkuu wa mkataba wa dola za Kimarekani milioni mia moja? Nini kitaendelea katika maisha ya Manka na Martin? Ndiyo mwisho? SONGA NAYO…

Ukumbi wa The Ball Room uliopo Hollywood ulikuwa umejaa idadi kubwa ya watu maarufu. Hakuna mcheza sinema maarufu duniani ambaye hakuwepo. Wote wakitaka kufahamu ni nani angeibuka mshindi usiku huo. Watu walikuwa ni kama wameunganishwa kwenye umeme kwa jinsi walivyokuwa wamechangamka na kushangilia.

Jina la Manka lilitajwa kwa sauti ya juu kwamba ndiye aliyestahili kuwa mshindi kati ya watatu waliokuwa wamebaki, ingawa alikuwa mgeni nchini Marekani alijipatia idadi kubwa sana ya mashabiki kuliko washiriki wenzake, nyuma ya pazia alishindwa kujizuia, machozi yalikuwa yakimtoka kama yuko kwenye msiba, yalikuwa ya furaha si huzuni.

“You are going to win!” (Utashinda!) Mariam, mshiriki kutoka Nigeria alimwambia akionesha kukata tamaa.
“Me? Win you? Me can’t win you, because you good kuliko me!” (Mimi? Mimi siwezi kuwashinda nyinyi, kwa sababu nyie ni wazuri kuliko mimi) Manka aliongea kwa Kiingereza chake cha kuunganisha.

“Yeah, you have all the qualities of an African woman! With your low hair cut, you beat us all.” (Ndiyo, una sifa zote za mwanamke wa Kiafrika, kwa mtindo wa nywele fupi uliokata, unatushinda wote.)
“Okay! We wait and see!” (Sawa! Tusubiri tuone!) Manka alijibu kwa alivyoweza lakini walimwelewa.

Sauti ya mwongozaji wa sherehe ilisikika kupitia kipaza sauti, akimkaribisha Mkurugenzi wa Kampuni ya Centurion Films ambayo ilitarajiwa kuitengeneza Filamu ya The Sweet Pain, Bw. Jon Curtis, ambaye usiku huo ndiye alikuwa jaji mkuu ili apande jukwaani kwenda kufanya kazi moja tu; kumtangaza mshindi ambaye angejinyakulia mkataba mnono wa kutengeneza filamu na kampuni hiyo wenye gharama ya dola milioni mia moja, sawasawa na shilingi za Kitanzania bilioni mia moja na hamsini.

Watu wote ukumbini walishangilia, nyuma ya pazia ni Manka na wenzake wakiwa wamekumbatiana, huku wakilia na kutetemeka, kilikuwa ni kipindi kigumu sana katika maisha ya mwanadamu ambacho kingebadilisha maisha ya mmoja wao milele. Hawakujua ni nani angeshinda, miili ilikuwa imekufa ganzi, hawakuwa na hisia sehemu nyingine yoyote ya mwili isipokuwa masikio peke yake ambaye yalisubiri kusikia jina.

“Mungu wangu nisaidie nishinde! Cha kwanza nitakachofanya ni kumchukua Martin pamoja na wazazi wangu kuwahamishia hapa Marekani, pia nitatoa zaka kanisani ili kazi yako iweze kwenda mbele, nisaidie Mungu wangu.” Manka alijisemea moyoni mwake huku machoni yakimtoka.
***

Tanzania nzima watu walikuwa nyuma ya runinga zao wakifuatilia ambacho kingetokea. Nchi nzima ilikuwa imetulia, kulikuwa na ukimya wa ajabu. Martin alikuwa kwenye ukumbi wa CCM kijijini kwao Shokoni ambako watu walikusanyika kufuatilia mafanikio ya mtoto wao, moyoni alikuwa na maumivu badala ya furaha, akijua kabisa ushindi wa Manka ungewatenganisha na wasingeweza kuwa kitu kimoja tena, ahadi waliyowekeana ya kuoana ingekuwa mashakani.

“Hawezi tena kuwa mke wangu, tazama watu walioko hapo ukumbini, wote ni matajiri na ambao siku zote tulizoea kuwaona kwenye sinema, wanamshangilia yeye, kweli Manka atarejea na kuwa na mtu kama mimi tena?” Hayo ndiyo mawazo yaliyokuwa yakiendelea kichwani kwa Martin wakati wote wa shindano hilo.

“….And the winner of next movie star competition, who goes home with a contract worth one hundred million US dollars is …..” (….Na mshindi wa shindano la nyota ajaye wa filamu ambaye atajipatia mkataba wa dola milioni mia moja za Kimarekani ni….”) mwendesha sherehe aliongea kisha kukaa kimya watu wote ukumbini wakatulia, mapigo ya moyo vifuani mwao yakawa yanakwenda kwa kasi, wengine wakahisi mioyo yao imesimama wakisubiri jina litajwe.

Hivyo ndivyo ilivyokuwa nchini Tanzania na kijijini Shokoni, watu wote walikuwa wakisubiri jina la Manka litajwe isipokuwa Martin peke yake, kiukweli hakutaka kabisa Manka ashinde ili arejee waendelee na uhusiano wao. Mwendesha sherehe alipotaja jina la Manka dakika tatu baadaye ukumbi wote ulilipuka kwa shangwe.

Kila kona ya Tanzania watu walishangilia, mama yake Manka alianguka chini na kuzimia lakini Martin aliondoka ukumbini kwa huzuni na kwenda kujificha katikati ya migomba na kuanza kulia akiamini moyoni mwake huo ndiyo ulikuwa mwisho wa yeye na msichana aliyempenda, jambo ambalo hakutaka kabisa litokee.

Manka alibebwa juu juu na mashabiki wake huku televisheni dunia nzima zikionesha tukio hilo, alikuwa akilia kwa furaha, kumbukumbu zake zikimrejesha nyumbani. Alijua kabisa Watanzania wote walikuwa wamefurahi, hasa Martin ambaye kwa vyovyote ilikuwa ni lazima afurahie ushindi wake.

Dakika kumi na tano baadaye alishushwa chini na watu ukumbini wakatulia, bodi nzima ya shindano la The next movie star, viongozi wa Kampuni ya Centurion Films wakaja mbele na mfano wa hundi ulioandikwa ‘USD One Hundred Million’ na akakabidhiwa mbele ya watu wote.

Katika maisha yake Manka hakuwahi hata kumiliki laki moja ya kwake binafsi lakini sasa alikuwa amekabidhiwa kitita cha dola milioni mia moja. Huu ulikuwa ni muujiza, hakuelewa hata maana ya utajiri huo ingawa alijua ni fedha nyingi.

Maisha yake yalikuwa yamebadilika kufumba na kufumbua, hatima ya umaskini ulioitesa familia yake kwa muda mrefu ilikuwa imewadia. Akaongozwa kuelekea kwenye kipaza sauti ili atoe maneno yake ya shukrani, bahati nzuri alikuwa ameandaa karatasi yenye maneno hayo kwa ajili ya kuyasoma kama angeshinda, akaingiza mkono wake kwenye suruali aliyovaa na kuitoa karatasi hiyo kisha kuiweka juu ya meza yenye kipaza sauti na kuanza kusoma huku akibubujikwa na machozi.

“Praise God!” (Bwana asifiwe!)
“Amen!” Watu wote ukumbini wakaitikia.
“This is a miracle, God is good all the time!
First and foremost, I want to thank God for what he has done for me, without him, I wouldn’t be standing here today. All my life, I knew I didn’t have what it takes to be a star, but God himself knew it and made it possible. Secondly my parents for good upbringing and the love they gave me, asante baba, asante mama kwa kila kitu, ushindi huu ni wenu. And third, I thank the love of my heart, Martin, I love you till eternity! And lastly my fellow Tanzanians and you my fans, I promise never to let you down…” (Huu ni muujiza, Mungu ni mwema wakati wote! Kwanza kabisa napenda kumshukuru Mungu kwa aliyonitendea, sababu bila yeye, nisingekuwa nimesimama hapa leo.

Maisha yangu yote nilijua sina sifa za kuwa nyota, lakini Mungu mwenyewe alijua na amelifanya hili kutokea. Pili, napenda kuwashukuru wazazi wangu kwa kunilea vyema na kwa upendo walionipa, asante baba, asante mama kwa kila kitu, ushindi huu ni wenu.

Tatu, namshukuru mpenzi wa moyo wangu, Martin, nitakupenda milele! Na mwisho Watanzania wenzangu na nyinyi mashabiki wangu, naahidi sitawaangusha…) Manka alimaliza na kuendelea kulia, moyoni mwake alijua kabisa hata Martin alikuwa akiangalia, lakini haikuwa hivyo kijana huyo alikuwa migombani akibubujikwa na machozi kwa hisia kwamba ushindi huo ndiyo ulikuwa mwisho wa kuwa na Manka.
 
SEHEMU YA 06


Binti aishie kijiji cha Shokoni, Marangu Mkoani Kilimanjaro (Manka) anapata bahati adimu kabisa duniani baada ya kugunduliwa na watafutaji wa watu wenye vipaji (Talent Scouts) waliokuwa wakizunguka dunia nzima kumtafuta msichana ambaye angeweza kushiriki katika sinema iitwayo Sweet Pain na kupelekwa moja kwa moja hadi jijini Los Angeles, California kupambanishwa na wasichana wengine na kuibuka katika tatu bora na hatimaye kushinda nafasi hiyo.

Akiwa haamini kilichotokea, Manka amesimama jukwaani kutoa shukrani zake huku dunia nzima ikimtazama kupitia runinga, Tanzania watu wanashangilia kwa ushindi kwa huo, ameiletea sifa kubwa na kuitangaza nchi yake akiwa mtu ambaye hakujulikana na mtu yeyote.

Wakati mama yake Manka amezimia kwa furaha, watu wote kijijini kwao wanashangilia na kuimba nyimbo za sifa, mtu mmoja hajafurahia kabisa tukio hilo, huyu si mwingine bali Martin, mpenzi wa Manka kwa muda mrefu waliyeishi pamoja kijijini wakiamini siku moja wangefunga ndoa na kuzaa watoto.

Martin amejificha migombani ambako analia kwa uchungu kwa kuamini kabisa huo ndiyo ulikuwa mwisho wa yeye kuwa na Manka, msichana aliyempenda kuliko mwingine yeyote na hakutarajia kabisa maishani mwake kumpenda msichana tena. Akaendelea kulia kwa uchungu akiomba muujiza utokee ili kila kitu alichokishuhudia kiwe ndoto.
Je, nini kinaendelea? SONGA NAYO…

Haikuwa hivyo, kila kitu kilibaki kuwa halisi, Manka alikuwa ameibuka mshindi wa shindano la The Next Movie Star, ushindi ulioambatana na kitita cha dola milioni mia moja, fedha ambazo hata matajiri wengi nchini mwake, aliowaogopa na kuwahofia hawakuwa nacho. Hakika alikuwa miongoni mwa watu matajiri nchini Tanzania na duniani, ndani ya sekunde kadhaa.

“Haitawezekana tena, sioni umuhimu wa kuendelea kuishi.” Martin alitamka maneno hayo baada ya kusikia watu wakizidi kushangilia na kuliimba jina la Manka, taratibu akanyanyuka kutoka mahali alipokuwa ameketi na kuanza kutembea akipita katikati ya migomba kwa msaada wa mbalamwezi mpaka akafika nyumbani kwao.

Aliushika mlango wa matete uliokuwepo mlangoni na kuuweka kando, kisha akaingia ndani na kuurudisha mahali pake, akawa amefunga. Kilichofuata hapo ni kuuchukua mpini uliounganishwa kwa kamba na mlango akauzungusha na kuuweka kama kizuizi cha mlango usifunguke, hivyo ndivyo walivyofunga, hicho ndicho kilikuwa kitasa chao, hakika waliishi katika umaskini uliokithiri.

“Nani?” Mama yake aliuliza.
“Mimi mama.”
“Mbona umechelewa?”

Martin hakujibu kitu, akaingia chumbani kwake na kujitupa juu ya mkeka uliokuwa sakafuni kisha akaendelea kulia kwa uchungu. Moyo wake ulikuwa na maumivu makali ambayo hayakuwa na mtu wa kuyatuliza isipokuwa Manka peke yake, hakupata usingizi mpaka saa kumi na mbili asubuhi mama yake alipomwamsha ili waongozane kwenda shambani walikokuwa na kibarua cha kuvuna kahawa.

“Mama naumwa.”
“Basi pumzika.” Mama yake alijibu bila kuelewa kilichokuwa kikimsumbua mwanaye, akaondoka peke yake kwenda kibaruani ambako aliwajibika mpaka saa nane mchana ndipo aliporudi nyumbani na kumkuta Martin akiwa bado amelala jambo ambalo halikuwa la kawaida kabisa.

“Vipi bado umelala?”
“Ndiyo mama sijisikii vizuri.”
“Nikupeleke hospitali?”
“Hapana mama.”

“Nikupe habari njema labda utajisikia nafuu?”
“Nipatie mama.” Martin alijibu akijua kabisa lazima mama yake angekuwa amesikia habari za Manka mitaani wakati akitoka shambani.

“Nasikia Manka amepata bahati ya mabilioni.”
Badala ya kujibu chochote, Martin aliangua kilio mbele ya mama yake jambo lililomfanya mzazi wake ashangae, kwani yeye ndiye alitakuwa kuwa mtu wa kwanza kufurahi sababu Manka alikuwa rafiki yake mkubwa. Ikabidi mama aketi kando na kumuuliza sababu ya kulia kwake, ndipo Martin akamsimulia mama yake kila kitu na ni kwa nini alikuwa ameumia kiasi hicho.

“Mwanangu.”
“Naam mama.”
“Huhitaji kuumia, kama Mungu amepanga Manka awe wako atakuwa, kama si hivyo hata ungefanya nini haiwezekani.”
“Nimekusikia mama lakini imeniuma.”
“Usijali.”

Pamoja na kufarijiwa na mama yake, Martin alibaki ndani kwa siku nne akilia, hakula chochote zaidi ya kunywa maji, juhudi za mama yake kumbembeleza hazikuzaa matunda, hofu kwamba angekufa kwa njaa ikaanza kumuingia. Akalazimika kutafuta ushauri kwa mchungaji wa kanisani ambaye alikuja na kufanya maombi na Martin, hapo ndipo akakubali kula baada ya kupewa matumaini.

***
Habari za Manka kushinda ushiriki katika filamu ya The Sweet Pain, zilikuwa katika kila chombo cha habari duniani kote, picha yake ikionyeshwa katika magazeti na vituo vya televisheni, kuanzia CNN mpaka SkyNews, kama jinsi radi ipigavyo, ndivyo binti huyo alivyokuwa ameingia katika orodha ya watu maarufu duniani.

Tayari alishapewa muda wa kuishi maeneo ya Bel-Air ambako waliishi watu maarufu na matajiri nchini Marekani, ndani ya nyumba yake kulikuwa na kila kitu na idadi ya wafanyakazi wasiopungua watano. Pamoja na yote hayo, kichwani mwake Manka alifikiria familia yake na mtu mwingine mmoja muhimu sana, Martin.

“Natamani Martin angekuwa hapa, lazima siku moja nimlete kuishi nami kwenye hii nyumba.” Aliwaza Manka akiendelea kushangazwa na kila kitu kilichokuwa kikimtokea.
Mfululizo wa tafrija uliendelea kumpongeza, maisha yake sasa yalikuwa yamezungukwa na watu maarufu kuanzia kina Sharon Stone mpaka kina Bruce Wills na Denzel Washington, alishindwa kuamini kama kweli alikuwa kwenye maisha hayo.

Wote wakimpongeza na kumsifia huku wakimtaka ajifunze kwa moyo wake wote uigizaji atakapokuwa kwenye chuo cha Hollywood Film Academy ambako angesoma kwa miezi sita kabla upigaji wa picha wa sinema haujaanza.

“Nitafanya kila kinachowezekana, sitawaangusha.” Ndivyo alivyosema, maneno hayo hayakutoka tu mdomoni, bali moyoni, Manka alikuwa amedhamiria, hakutaka tena kurudi kijijini Shokoni ambako alihisi alikuwa amekombolewa na sasa alikuwa na wajibu wa kufanya kila kilichowezekana ili awakomboe wengine; hasa wazazi wake pamoja na Martin.

Wiki moja baadaye aliandikishwa katika chuo hicho kwa masomo ya uigizaji, hapo alikutana na wanafunzi wengine wengi, wote walifurahi kumuona na kuwa naye darasa moja kwani taarifa zake walishazisoma kupitia vyombo vya habari. Mtu aliyempeleka chuoni asubuhi na kumrudisha nyumbani hakuwa mwingine bali mkurugenzi wa kampuni ya Centurion, Jon Curtis.

“Masomo yakoje?”
“Yanaendelea vizuri.”
“Chukua hii ni zawadi yako.” Jon Curtis alimkabidhi Manka kikasha kidogo cha rangi nyekundu.

“Ni nini?”
“Fungua utaona ndani.”
“Sasa hivi?”
“Fungua tu.”

Manka alipofungua kikasha hicho alishangaa macho yake yalipogongana na vitu vilivyong’ara sana, ulikuwa ni mkufu pamoja na hereni. Hakuelewa zilitengenezwa kwa kitu gani ndipo akamuuliza Jon Curtis ambaye alijibu bila kusita kwamba zilitengenezwa kwa almasi.
“Mungu wangu almasi?”
“Ndiyo.”

“Zangu?”
“Ndiyo, zawadi yako kwa kufanya vizuri.”
“Asante Curtis.”
“Hakuna shida.”
“Naweza kujua ni kwa nini umeninunulia kitu cha thamani kiasi hiki?”
“Zawadi tu.”

“Basi asante.”
Ukaribu wao ulizidi kuongezeka, kadiri siku zilivyozidi kusonga, Jon Curtis akawa ndiye mtu wa karibu na Manka. Mara nyingi jioni alimchukua kwenda kumtembeza sehemu mbalimbali za Los Angeles ili apate kuzoea, wakipendelea sana kwenda kula chakula cha jioni kwenye hoteli ya Beverly Hills.

Kila kitu walichokiona Manka kilimshangaza na hakukoma kumshukuru Mungu pamoja na Jon Curtis kwa wema aliokuwa akimfanyia lakini kichwani mwake jina la mtu mmoja aitwaye Martin halikufutika, kila mara alimjia na akatamani awepo Los Angeles wakati huo.
“Una umri gani Curtis?”
“Sabini na mbili. Kwa nini umeuliza?”

“Nataka tu kufahamu, wewe si ni rafiki yangu?”
“Ndiyo.”
“Nisamehe kama nimekukosea.”
“Hapana, leo ningependa ufike nyumbani kwangu.”
“Ni wapi?”

“Hapa hapa Beverly Hills, mwendo wa kama dakika tatu kutoka hapa hotelini.”
“Hakuna shida.”
Walipomaliza kula chakula cha usiku waliingia ndani ya gari la Curtis aina ya Ferari na kuongoza moja kwa moja hadi nyumbani kwake, lango likafunguka na wote wakaingia ndani. Kulia kwake Manka baada ya kushuka garini alishangaa kuona twiga wawili wakitembea, jambo ambalo hakutarajia kabisa kukutana nalo nchini Marekani.

“Twiga?”
“Ndiyo, niliwatoa huko huko kwenu.”
“Sijawahi kuona twiga, hii ni mara ya kwanza.”
“Usijali, utaona mengi.”

Curtis alianza kumtembeza Manka kwenye nyumba yake, hakuwahi hata mara moja kufikiri kama kuna watu walioishi katika nyumba za kifahari kiasi hicho, kwake Manka hiyo ilikuwa kama mbingu duniani. Kulikuwa na kila kitu ndani hata jumba la sinema, mabwawa mawili ya kuogelea. Alibaki kushangaa kila kitu ambacho macho yalitua juu yake.

Walipotoka nje alikutana na zizi la magari ya kila aina na baadaye wakaelekea kwenye uwanja wa ndege kulikokuwa na ndege mbili kubwa na helikopta moja, zote zilikuwa mali ya Jon Curtis. Baada ya zoezi hilo ndipo wakarejea ndani na kuketi kando ya bwawa la kuogelea ambako mfanyakazi alifika haraka kuwahudumia.

“Mke wako yuko wapi?” Manka aliuliza baada ya kuagiza soda.
“Alifariki miaka kumi iliyopita pamoja na watoto wangu wawili katika ajali ya ndege.”
“Aah! Pole sana.”
 
SEHEMU YA 07


Maisha ya Manka yamebadilika ghafla, ule msemo wa kulala maskini kuamka tajiri unamhusu yeye. Si jambo rahisi kutoka kijijini Shokoni, hadi Hollywood na kujishindia kitita cha dola milioni mia moja (sawa na shilingi za Kitanzania bilioni mia moja na hamsini) katika shindano la kumsaka msichana ambaye angeigiza katika filamu iitwayo Sweet Pain inayoandaliwa na kampuni iitwayo Centurion Films.

Amefundishwa Kiingereza na kuwa na uwezo wa kukiongea vizuri, baadaye anaandikishwa katika chuo cha uigizaji mambo ya filamu kiitwacho Hollywood Film Academy ambako anajifunza uigizaji. Amepewa nyumba ya kifahari ya kuishi na kila siku Mkurugenzi wa kampuni ya Centurion, Jon Curtis humpeleka chuoni na kumrejesha nyumbani kwake.
Kitendo hiki kinasababisha ukaribu mkubwa sana wa watu hawa wawili, pamoja na hayo yote, Martin, mpenzi wa Manka aliyeko nchini Tanzania hajaondoka kichwani mwake.

Kila siku humfikiria na kuamini iko siku wangeishi pamoja kama mke na mume, mpango wake ni kuwahamisha wazazi wake pamoja na Martin nchini Marekani. Jon Curtis anamkaribisha Manka nyumbani kwake, katika maeneo ya watu matajiri huko Beverly Hills.
Anashangazwa na utajiri wa ajabu alionao, ikiwa ni pamoja na ndege binafsi, magari mengi ya kifahari na twiga aliowafuga kwenye bustani yake. Katika maisha yake Manka hakuwahi kufikiria kama kuna siku moja angefika sehemu kama hiyo au kukutana na watu wa aina ya Jon Curtis.

“Mke wako yuko wapi?” ndilo swali ambalo Manka aliuliza walipoketi kando ya bwawa la kuogelea, yaliyofuata hapo ni maelezo ya Jon Curtis juu ya huzuni aliyokuwa nayo pamoja na utajiri wote uliomzunguka, baada ya kufiwa na mke na watoto wake wawili katika ajali ya ndege.
Je, nini kinaendelea leo? SONGA NAYO…

“Pole sana!” Manka alisema kwa mara ya pili baada ya kuona Jon amebaki kimya akiwa ameinamisha kichwa chake chini. Alionyesha huzuni kubwa ambayo Manka aliishuhudia kwa macho yake, isingewezekana mzee mwenye umri kama wake aigize huzuni kama hakuwa nayo.

“Inaniuma sana, kila siku nawakumbuka na sijui kama nitakuja kuwasahau, kila kitu ndani ya nyumba hii kinanikumbusha familia yangu, kwa kweli ni kama nimechanganyikiwa tangu wakati huo.” Jon aliongea, Manka alipomwangalia vizuri machoni aligundua machozi yalikuwa yakimlengalenga akamsogelea na kumkumbatia katika kuonyesha upendo, bila kupoteza nafasi Jon Curtis naye akazungusha mikono yake mabegani kwa Manka, kitu ambacho wote wawili hawakukitarajia kikatokea..

“I think I love you…” (Nafikiri ninakupenda…) Jon aliongea huku midomo ikimtetemeka.
“You think? Only thinking? Do you trust your mind?” (Unafikiri? Kufikiri tu? Unaiamini akili yako?) Manka aliuliza kwa mshangao.

“Sorry if you have taken it badly, I meant I love you with the whole of my heart, soul and mind, please fill the empty place in my heart left by my dear wife.” (Samahani kama umeelewa vibaya, nilimaanisha nakupenda kwa moyo, roho na akili yangu yote, tafadhali jaza nafasi tupu iliyoachwa moyoni mwangu na mpendwa mke wangu.) Aliongea Jon akimuangalia Manka usoni.

Mwili wa Manka ukatetemeka, hakuwahi kutarajia maishani mwake mwanamume mwenye utajiri na umaarufu kama aliokuwa nao Jon angeweza kuwa amesimama mbele yake akimtaka awe mke wake, kwa kasi ya ajabu, taswira ya Martin ikaonekana akilini mwake akimkumbusha kuhusu kuwa mwaminifu kwa penzi lao. Huzuni ikamuingia moyoni mwake, akamuonea Martin huruma kwani alihitaji kuwa jasiri kupita kiasi kupambana na jaribu lililokuwa limesimama mbele ya uso wake; machozi yakamtoka.

“Do not cry, I am not forcing you to say yes, you can still say no and nothing will change in your contract! This is not by force, you have to be willing to do it. Do you understand?” (Usilie, sikulazimishi kukubali, unaweza kukataa na hakuna kitakachobadilika kwenye mkataba wako! Hii siyo lazima, unapaswa ukubali kwa hiari yako kushiriki. Umenielewa?) Jon aliongea uso wake ukiwa umefungulia tabasamu.

“Yes I understand, I am a virgin Jon! I have never had sex, and I planned to keep myself pure until I get married.” (Ndiyo naelewa, Jon mimi ni bikira! Sijawahi kufanya tendo la ndoa, nilipanga kujitunza niwe safi mpaka siku nitakapoolewa.)
“We are going to get married.” (Tutaoana.)

“Oh! My God, I have a fiancé already and we love each other so much!” (Oh! Mungu wangu, nina mchumba tayari na tunapendana sana.)
“Where is he?” (Yuko wapi?)

“He is in Tanzania, East Africa!” (Yuko Tanzania, Afrika Mashariki.) Manka aliongea, taswira ya Martin ikiwa imefunika kabisa akili yake.
“Stop being ridiculous!” (Acha kuwa kichekesho.)
“Why?” (Kwa nini?)

“You are in Hollywood Manka! Everybody will be shocked to get the news that you are still dating a dirty boy from Africa, take me seriously, we don’t do that in Hollywood, superstars date fellow superstars!” (Upo Hollywood Manka! Kila mtu atashtuka akipata habari unatoka na mvulana mchafu kutoka Afrika, nichukulie kwa umakini, hatufanyi hivyo hapa Hollywood, huu ni ulimwengu tofauti, nyota kwa nyota hutoka pamoja) Jon aliongea huku akimuangalia Manka aliyeinamisha kichwa chini, maneno yote aliyoambiwa yalimuingia moja kwa moja hadi moyoni na kumfanya aanze kujiona mshamba na kuamini kweli pengine hakutakiwa kwa mafanikio aliyoyapata kuwa na mvulana kama Martin tena.

“He will be hurt!” (Ataumia.)
“You don’t have to give a damn about that, he will be find someone of his type!” (Usijali kuhusu hilo, naye atapata mwenzake wa aina yake.)
Siku hiyo badala ya kurejea nyumbani kwake, Manka alilala chumbani kwa Jon Curtis, akijisikia msaliti na moyo wake ukishitakiwa, yote aliyoyafanya usiku huo alimuona Martin akiyashuhudia. Hiyo ilimfanya alie usiku mzima, kiasi kwamba Jon Curtis alishindwa kumfanya chochote mpaka asubuhi alipompeleka nyumbani kwake kujiandaa kisha kumpeleka shuleni kuendelea na masomo.

Mpaka anamaliza masomo yake na kujipatia diploma ya kuigiza akiwa mwanafunzi bora katika darasa lake, kilichokuwa mbele yake kikiwa ni kuigiza filamu ya Sweet Pain, Manka alishalala nyumbani kwa Jon Curtis mara ambazo hakuwa na uwezo wa kuzikumbuka na tayari alishapoteza kitu cha muhimu kabisa ambacho aliahidi tangu utotoni mwake kumtunzia mumewe; bikira.

Akilini mwake Martin alikuwemo nusu, hakumfikiria sana kama zamani. Kuna wakati ilipita wiki nzima bila hata kumkumbuka ingawa bado barua ziliendelea kumiminika kutoka Afrika, Martin akisisitiza kwamba bado alimpenda na alimuombea kwa Mungu abaki na msimamo ule ule ili siku moja waje kuishi pamoja.

Hakuna hata moja iliyojibiwa, akili ya Manka ilishahamia kwa Jon Curtis, kilichokuwa kikisubiriwa sasa ni ndoa kati yao ambayo ilipangwa kufanyika baada ya kumaliza kupiga picha ya sinema ya Sweet Pain barani Afrika katika nchi ya Tanzania na Uarabuni kabla ya kurejea Marekani na kumalizia sehemu ya mwisho.

Bado jina la Manka ambaye sasa badala ya kuliandika kama ambavyo siku zote liliandikwa, alibadilisha na kuondoa “a” mwisho akaweka “er” ili lifanane na la Kimarekani zaidi, badala ya kumuita au kuandika Manka kwenye vyombo vya habari sasa likawa linaandikwa Manker. Kila gazeti bado lilimuongelea, televisheni zote zilimtangaza na kwenye tafrija zote za Hollywood kamera zilimwelekea yeye na alifanya mahojiano mengi katika televisheni, kifupi alishakuwa nyota kabla hata hajashiriki kwenye sinema ya Sweet Pain.

Mwezi mmoja baadaye ndege aina ya Boeing 737 iliondoka Los Angeles kuelekea Dar es Salaam Tanzania ikiwa na timu nzima ya kurekodi sinema ya Sweet Pain, Manka akiwa miongoni mwao, Jon Curtis akiwa kando tena wakiwa kwenye kiti kimoja cha ndege.

Haikuwa siri tena miongoni mwa timu nzima, kwamba walikuwa ni mtu na mpenzi wake.
Ilikuwa ni safari ya raha mno, tayari Manka alishawasiliana na wazazi wake na kuwaomba wawepo Dar es Salaam watakapoingia ili apate nafasi ya kuongea nao kabla kazi haijaanza.

Taarifa hizo zilitangazwa na vyombo vyote vya habari nchini Tanzania, maelfu ya watu walifurika uwanja wa ndege bila kujali ndege ilikuwa inatua saa tatu usiku, ili wapate kumuona Manka kwa macho. Hakuwa mtu wa kawaida nchini mwake, alikuwa nyota na shujaa wa taifa la Tanzania.

Waziri wa Habari na Michezo, Mheshimiwa Renatus Kajuna, alikuwepo uwanja wa ndege kumpokea Manka ambaye sasa aliitwa mtoto wa Tanzania, kama kawaida alipewa sifa zote ambazo hakuna aliyempa wala kumsaidia alipokuwa akiishi kijijini. Baada ya kupata umaarufu na mafanikio sasa alikuwa ni kama kito cha thamani, kiasi cha waziri kujitokeza uwanja wa ndege kumpokea.

Watu alioongozana nao hawakuamini waliposhuhudia umati wa watu waliokuwa wakimshangilia Manka kwa nguvu zao zote, waandishi wa habari walikuwepo kupiga picha wakati Manka akikumbatiana na wazazi wake na kulia machozi, kisha viongozi mbalimbali na baadaye kuingia ndani ya gari lililoandaliwa yeye pamoja na Jon Curtis na baadhi ya wanachama wa timu wakaondoka mpaka hoteli ya Atriums iliyopo Sinza jijini Dar es Salaam ambako ulinzi ulikuwa umetandazwa kuhakikisha hakuna baya lolote linampata Manka na timu aliyoongozana nayo.

Ilikuwa ni furaha mno kwa Manka kuwaona tena wazazi wake pamoja na mapokezi aliyopewa, hakika alijisikia vizuri kufika nyumbani na alimtambulisha Jon Curtis kwa wazazi wake kama rafiki na mtu aliyemsaidia maishani. Hakutaka kusema chochote juu ya uhusiano wao.
***

Saa kumi na mbili jioni siku iliyofuata basi liitwalo Kilimanjaro lilikuwa limesimama kwenye msururu maeneo ya Ubungo kwenye mataa, abiria wote waliokuwemo walikuwa wamechoshwa na safari ndefu kutoka Moshi kuja Dar es Salaam. Walichotaka sasa ni kufika stendi ili washuke na kuelekea makwao.

Kwenye kiti cha nyuma kabisa cha basi, aliketi kijana aliyevaa shati ambalo halikuwa rahisi kuelewaka kama rangi yake ilikuwa nyeupe au kahawia sababu ya uchafu, suruali aliyovaa ilikuwa na viraka vingi na miguuni hakuwa na viatu. Macho yake yote mawili yalikuwa yameelekezwa kwenye runinga iliyokuwa ndani ya basi ikionyesha mapokezi ya Manka Ikulu ambako siku hiyo alialikwa na rais kwa ajili ya chakula cha usiku, uso wake ukajawa na tasabamu.

“Siamini kama ni Manka, bila shaka matatizo yangu yatakuwa yamefika mwisho baada ya kumuona, atakuwa bado ananipenda kweli? Hawezi kunichukia!” aliwaza kijana huyo basi likikata kona kuingia stendi ya Ubungo na hakujua mahali pa kwenda kushuka, hii ilikuwa ni mara yake ya kwanza kuingia jijini Dar es Salaam na kusafiri nje ya Mkoa wa Kilimanjaro na alikuwa ameuza mbuzi bila idhini ya mama yake ili apate nauli ya kumleta Dar es Salaam kukutana na Manka.

Jina pekee alilokuwa akilikumbuka katika akili yake ni Atriums Hotel, Sinza.
 
SEHEMU YA 08

Ni kama ndoto kwa Manka, kutoka kijijini Shokoni hadi Hollywood na kujishindia kitita cha dola milioni mia moja (sawa na shilingi za Kitanzania bilioni mia moja na hamsini)! Hakuwahi kuota maishani mwake. Ndani ya muda mfupi anafundishwa Kiingereza na kuwa na uwezo wa kukiongea vizuri. Baadaye anaandikishwa katika Chuo cha Uigizaji cha Hollywood Film Academy ambako anajifunza uigizaji.

Anabadilika kabisa na uzuri wake unajionesha dhahiri kama waridi linaloanza kuchanua.

Baada ya mipango yote kukamilika juu ya maandalizi ya Filamu ya Sweet Pain, hatimaye safari ya kuanza upigaji picha za filamu hiyo kwenye nchi za Tanzania, Uarabuni na Marekani unaanza. Timu nzima inasafiri mpaka Dar es Salaam, Manka naye yumo huku Jon Curtis akiwa kando yake. Uhusiano wao siyo siri tena, kila mtu Hollywood anajua.

Mapokezi makubwa yaliyoongozwa na Waziri wa Habari na Michezo, Mheshimiwa Renatus Kajuna yanamshangaza mno Manka kwani ni kitu ambacho hakukitegemea. Baada ya mapokezi hayo, msafara unaelekea kwenye Hoteli ya The Atriums, Sinza na ulinzi unaimarishwa kuzunguka hoteli hiyo.

Upande wa pili, kijana Martin yuko ndani ya Basi la Kilimanjaro na tayari amewasili Ubungo, akitokea Moshi. Kilichomleta si kingine bali ni kukutana na mpenzi wake wa siku nyingi, Manka.
Je, nini kinafuatia? Martin atakutana na Manka?
SONGA NAYO…

“Kaka’angu samahani naomba kukuuliza!”
“Unasemaje dogo? Huna nauli nini?”
“Hapana kaka’angu, mimi ni mgeni hapa Bongo, naomba kuulizia eti Hoteli ya Atriums iko maeneo gani?”

“The Atriums? Unazungumzia ile hoteli ya kitalii ya Sinza?”
“Itakuwa ndiyo hiyohiyo! Yesuuu!”
“Unaenda kufanya nini The Atriums wewe Mangi? Mbona hufanani na hadhi ya hoteli yenyewe?”
“Kuna mtu namfuata kaka’angu, amenielekeza kuwa nikifika Bongo niulize Atriums Hoteli.”

“Ok, panda daladala zinazoenda Kariakoo, mwambie konda akushushe Shekilango. Ukishuka tembea mpaka kwenye stendi nyingine ya daladala ziendazo Mwenge, mkono wako wa kushoto. Ukipanda magari ya Mwenge mwambie konda akushushe Afrikasana, pale utamuuliza mtu yeyote atakuonesha kwani iko barabarani tu. Kwani umetokea wapi?”
“Shokoni, Moshi!” ”Hivyo ulivyo umesafiri kutoka Moshi?”
“Ndiyo! Kwani nikoje braza?”

Martin alikuwa akizungumza na mwanamume aliyemsimamisha nje ya Kituo cha Mabasi yaendayo mikoani cha Ubungo, muda mfupi baada ya kuteremka kwenye Basi la Kilimanjaro lililomsafirisha kutoka kijijini kwao.
“Akambe!”
“Ndiyo nini?”
“Maana yake ni asante kwa Kichaga, unajua kule kwetu kila mtu anaelewa lugha ya asili, nikajua na huku,” aliongea Martin huku akitaka kupiga magoti kumshukuru yule mwanamume ambaye alimuwahi na kumzuia.
“Una nauli?”

“Eeh! Fedha niliyouza mbuzi bado ninayo! Itanitosha,” alijibu Martin na kuachana na yule mtu, akawa anatembea kuelekea kilipo kituo cha daladala, Ubungo.
Kilichomleta Martin jijini Dar es Salaam siyo kingine bali kukutana na mpenzi wake, Manka baada ya kupata taarifa kupitia vyombo mbalimbali vya habari kuwa mwanadada huyo aliwasili kutokea Hollywood, Marekani.

Hakuwahi kufika jijini Dar es Salaam, ile ilikuwa ni mara yake ya kwanza kabisa. Ramani pekee aliyoona itamsaidia kukutana na Manka ni jina la hoteli aliyofikia, The Atriums. Aliamini akifika hotelini hapo, basi lazima ataonana naye ingawa hakuwa na uhakika kama kweli atamkubali kwani kwa kipindi kirefu sasa hakuwa akijibu barua alizokuwa anamtumia.

“Potelea mbali? Nitaenda kujua hukohuko! Lakini wakati anaondoka aliniahidi kuwa hatabadili uamuzi wake wa kuoana na mimi hata iweje.”
Alipofika kituoni alipanda daladala ya kwenda Kariakoo, akafuata maelekezo ya yule mtu, akashuka Shekilango. Alitembea hatua kadhaa, akatokea kwenye barabara ya Shekilango, akasubiri daladala za kwenda Mwenge.

Muda mfupi baadaye akawa ndani ya daladala. Hakuwa na mzigo wowote zaidi ya mfuko wa plastiki (Malboro) ambao ndani yake kulikuwa na suruali mbili kuukuu na shati moja.
Daladala aliyopanda ilipofika Afrikasana, Martin alishuka na kuanza kushangaa huku na kule, akiwa hajui aelekee wapi. Alipouliza kwa wapiga debe waliokuwa pale kituoni, walitazama kisha wakapeana ishara.

“Twende tukupeleke!” vijana wawili waliotopea kwenye matumizi ya madawa ya kulevya (mateja) walimvusha barabara na kwenda naye upande wa pili. Hawakuwa wakimpeleka The Atriums kama alivyoomba bali walitaka kwenda kumkaba na kumpora kila alichokuwa nacho.
“Hatufiki tu? Mbona nimeambiwa siyo mbali na barabara?”
“We tufuate sisi, kama unakujua si uende mwenyewe?”

Martin alikuwa mpole, akawa anawafuata kama kondoo anayepelekwa machinjioni. Walipoingia kwenye uchochoro, walimgeuzia kibao na kumkaba. Mmoja akamshika kwa nguvu huku yule mwenzake akimpekua mwili mzima.

Walifanikiwa kuziona fedha zake alizokuwa amezificha kwenye nguo yake ya ndani.
Wakamsukumia ukutani kisha wakatimua na kumuacha anapiga kelele za kuomba msaada. Licha ya kulia sana, hakuna aliyejitokeza kumsaidia. Wale vibaka wakatokomea kusikojulikana.

Kwa masikitiko aliinuka kutoka pale chini alipokuwa ameanguka, akajipukuta vumbi na kuanza kuondoka huku akichechemea mguu mmoja. Licha ya tukio lile la kuporwa na vibaka, bado hakukata tamaa. Alijiapiza kuwa lazima akutane na Manka.
***
“Bosi kuna mtu anatusumbua huku getini!” aliongea kiongozi wa kundi la walinzi binafsi la Simba Ultimate Guards waliokuwa wanalinda Hoteli ya The Atriums mbele ya Mkurugenzi wa Kampuni ya Centurion, Jon Curtis. Ujio wa Manka na wenzake ndani ya hoteli ile, uliwafanya walinzi kuongezwa mara dufu huku wakiwa na silaha nzito ili kukabiliana na yeyote ambaye angeleta fujo kwa wageni.
“Anataka nini?”
“Amesema anataka kuonana na Manka!”
“Mwambie tumepumzika, kama ana shida aje kesho jioni tukishamaliza kazi.”
Yule mlinzi aliyapokea maagizo na kuondoka haraka eneo lile, akimuacha Jon akiwa anacheza kwenye ‘swimming pool’ na Manka.
“Jon my love!” (Jon mpenzi)

“Yes baby!” (Naam mpenzi)
“Would you marry me?” (Utanioa?)
“Why not Manka! As soon as we finish the shooting of Sweet Pain, I will do it!” (Kwa nini nisikuoe Manka? Tukishamaliza tu kupiga picha za Sweet Pain, nitatekeleza)
“Sure?” (Kweli)
“Yeah!” (Ndiyo)

Manka na Jon walikumbatiana kimahaba, wakagusisha ndimi zao na kuanza kuelea kwenye ulimwengu tofauti. Waliendelea kufanyiana michezo ya kimahaba mpaka walipokolea kisawasawa, wakaanza kukokotana kuelekea kwenye chumba walichofikia.
Hakuna aliyewashangaa kwani kwenye kitabu cha wageni waliandikisha kuwa ni mume na mke. Walipoingia ndani, Jon alimbeba Manka juu juu na kumtupa juu ya kitanda kikubwa cha kifahari, akavua nguo za kuogelea alizokuwa amezivaa. Alipomaliza akamsogelea Manka pale kitandani na kumfanyia vilevile. Sekunde chache baadaye wakawa kama walivyozaliwa.

“Jon! Unajua niliamua kuvunja ahadi niliyowekeana na mpenzi wangu wa zamani kwa ajili yako? Sikuwahi kumjua mwanaume, wewe ndiyo uliyenionesha njia, tafadhali naomba usije kunitenda,” aliongea Manka kwa uchungu huku akitokwa na machozi.

“Najua Manka! Heshima uliyonipa ya kuwa mwanaume wa kwanza kulifaidi penzi lako imenifanya nisahau machungu yote ya kufiwa na mke wangu na watoto. Siwezi kukutenda. Nitakupa kila unachotaka ili mradi ufurahi siku zote za maisha yako.”

“Hivi ikitokea mpenzi wangu wa zamani amekuja na anataka kunioa, utafanya nini?”
“Niko tayari hata kutuma watu wampige risasi, ili mradi nisikupoteze!”
“Nini? Uko tayari kuua kwa ajili yangu? Kumbe wewe ni mkatili kiasi hicho?”
“Hapana siyo ukatili, penzi lako limenichanganya na siko tayari kukukosa,” aliongea Jon na kumkumbatia Manka kwa nguvu, wakazama kwenye dimbwi la mahaba.

Walikuja kushtuliwa na mtu aliyekuwa anagonga mlango wa chumba walichokuwa wamelala ndani yake.

Jon aliamka na kujifunga taulo kisha kwenda kufungua, akakutana na yule mkuu wa walinzi akiwa amesimama wima.

“Vipi tena? Nikiwa nimepumzika na mke wangu huwa sipendi usumbufu!”
“Samahani bosi, yule mtu bado anatusumbua, hataki kuelewa chochote. Analia kama mtoto akishinikiza kuwa lazima amuone Manka.”
“Amesema anaitwa nani?”

“Martin!”
Sauti ile ya mlinzi ilipenya mpaka kwenye ngoma za masikio ya Manka aliyekuwa amelala kutokana na uchovu wa kushiriki mchezo wa kikubwa na Jon. Akajifunga taulo na kumfuata Jon pale mlangoni.

“Anaitwa nani?”
“Martin!” yule mlinzi akarudia kulitaja jina lile. Manka na Jon wakatazamana usoni, mapigo ya moyo ya Manka yakaongezeka kwa kasi, kijasho chembamba kikawa kinamtoka.
 
SEHEMU YA 09



Msichana mrembo aishiye kijijini (Manka) pamoja na mpenzi wake Martin ambao wana ndoto ya kuoana baadaye maishani mwao, anapata bahati ya kukutana na watu waliokuwa wakizunguka duniani kumtafuta msichana ambaye angeshiriki kucheza sinema iitwayo Sweet Pain inayomwongelea msichana wa Kiafrika aliyechukuliwa kutoka katika bara hili na kupelekwa Marekani ambako alifanywa mtumwa wa ngono.

Manka anashinda nafasi hiyo kwenye mchuano uliofanyika katika Jiji la Los Angeles na kujishindia mkataba mnono wa dola milioni mia moja, maisha ya Manka yanabadilika ghafla, anakuwa miongoni mwa watu matajiri duniani na hapo hapo ulimwengu wake unabadilika, sasa anakuwa mtu wa kukutana na watu maarufu huko Hollywood ambao siku zote aliwaona kwenye sinema.

Ingawa wakati anaondoka Tanzania alimuahidi Martin kwamba asingemwacha, jambo hilo lilishindikana kwani bila kutarajia anajikuta katika mapenzi mazito na Jon Curtis, ambaye ni Mkurugenzi wa Kampuni inayotengeneza filamu hiyo. Uhusiano huu unamfanya Manka taratibu aanze kumfuta Martin kichwani mwake, ingawa kijana huyo bado anaendelea kuteseka kwa mapenzi kijijini kwao Shokoni, Marangu Kilimanjaro.

Wakati wa kupiga picha za filamu ya Sweet Pain, Manka akiongozana na Jon Curtis pamoja na timu nzima ya wapiga picha waliruka kwa ndege kutoka Marekani na kutua Tanzania ambako walipokelewa kishujaa na kufikia kwenye Hoteli ya Atriums iliyopo Sinza jijini Dar es Salaam.

Vyombo vyote vya habari vikamtangaza Manka na baadaye akakaribishwa Ikulu kula chakula na rais wa nchi, huo ndio ulikuwa utamaduni wa Tanzania, kumheshimu mtu pale tu anapofanya vizuri bila mchango wowote katika mafanikio yake.
Martin alipoyaona matangazo ya Manka kwenye vyombo vya habari, furaha ilimjaa moyoni na kujikuta akichukua mbuzi wawili wa mama yake na kuwauza ili apate nauli ya kusafiria hadi jijini Dar es Salaam ambako hakuwahi kufika hata mara moja.

Aliingia jijini Dar es Salaam jioni na kuulizia mahali hoteli hiyo ilipokuwa. Wasamaria wema wakamwelekeza mpaka akafika na kuanza kung’ang’ania akutanishwe na Manka jambo ambalo walinzi hawakulikubali, mwisho mmoja wao akaamua kwenda hadi kwenye chumba chao na kugonga.
Je, nini kitaendelea? SONGA NAYO…

“Samahani bosi yule mtu bado anatusumbua, hataki kuelewa chochote. Analia kama mtoto akishinikiza kuwa lazima amuone Manka,” mlinzi aliongea mbele ya Jon Curtis kwa Kiingereza cha kuunganisha.
“Amesema anaitwa nani?”

“Martin,” yule mlinzi akarudia kulitaja jina lile, Manka na Jon wakatazamana usoni, mapigo ya moyo wa Manka yakaongezeka kwa kasi, kijasho chembamba kikawa kinamtoka.
“Kwa nini unatoka jasho kiasi hicho?” Jon alimuuliza Manka mlinzi alipoondoka.
“Njoo ndani.”
“Kuna nini? Huyo Martin ni nani? Mbona umeshtuka sana?”
“Unamfahamu, nimewahi kukueleza habari zake.”
“Lini? Mbona sikumbuki?”

“Keti chini nikueleze,” Manka aliongea akimkalisha Curtis kitini, kwa kasi ya ajabu alinyanyuka na kuchukua ufunguo kisha kutoka na kukimbia na kuufunga mlango wa chumba chake, akimuacha Curtis katika mshangao. Haraka alitembea hadi kwenye lango kuu la kuingilia huku akihema kwa nguvu sababu ya hasira kali aliyokuwa nayo, wa kwanza kukutana naye alikuwa ni mlinzi aliyekuja kuwagongea.
“Nani amekuambia uje kugonga?”

“Hakuna aliyeniambia ila nimemuonea tu huruma anavyolia, nikawapa taarifa watu wa mapokezi lakini walipojaribu kuwapigia simu yenu ikawa haiingii nafikiri mlikuwa mmeweka mkono wa simu pembeni.”
“Yuko wapi huyo anayenitafuta?”
“Yuko hapo nje, njoo nikuonyeshe na samahani sana kwa usumbufu.” Mlinzi aliongea akiwa ameingiwa na hofu nyingi.

Mlango mdogo ukafunguliwa na Manka akawa wa kwanza kutoka na kusimama nje akimuangalia kijana aliyeketi kwenye msingi wa nyumba, ambaye alipomuona tu alinyanyuka na kutanua mikono yake tayari kwa kumkumbatia huku akimwita kwa jina na kuonyesha furaha yake.
“Don’t touch me!” (Usiniguse.) Aliongea Manka akimuangalia Martin kwa jicho la dharau.
“Sijakuelewa, ongea Kiswahili Manka.” Martin aliongea akishusha mikono yake yote miwili chini.

Ingawa hakuelewa kilichosemwa sura ya Manka ambaye kila mara alitema mate chini kama ishara ya dharau huku akifoka kwa Kiingereza, ilitosha kabisa kumuonyesha Martin kwamba hakutakiwa mahali pale, Manka hakuwa wake tena, walikuwa watu wawili kwenye madaraja tofauti, moyo ukamuuma na machozi kumbubujika.
“Get him out of here!” (Mwondoeni hapa!) Aliendelea kufoka Manka akiongea na walinzi wake, ndani ya sekunde chache tu Martin alikuwa amebebwa juu juu na wanaume warefu wenye miili yenye misuli mikubwa huku akilia na kwenda kutupwa kwenye mtaro uliokuwa na maji machafu.

“Manka! Manka! Kumbuka tulikotoka, umenifanyia udhalilishaji wa hali ya juu sana, moyo umeniuma sababu nimemwibia mama yake mbuzi wake nikaenda kuwauza ili nipate nauli ya kuja kukuona wewe. Kumbuka mimi ni maskini ninayekupenda kwa dhati hata kama wewe ni tajiri. Narudi nyumbani Moshi, nitafanya biashara yoyote ili nipate fedha na kumrudishia mama yangu mbuzi wake, wewe endelea na maisha yako ya utajiri, wakati wowote katika maisha yako ukikwama au mwanaume yeyote akikunyanyasa naomba ukumbuke kuna mwanaume mmoja aliyekupenda kwa dhati, anaitwa Martin, nitakuwepo nikiwa nakusubiri, sitaoa mwanamke mwingine kama si wewe…” Martin akaongea akipitisha kidole chake shingoni kama ishara ya kuapa, mashavu yote yalikuwa yamelowa machozi.

“Toka hapa! Kwenda zako Kilimanjaro ukanywe mbege.” Aliongea Manka kwa dharau kisha kutokomea ndani bila huruma.
Martin alibaki hapo akilia kwa muda wa kama saa nzima, ikabidi anyanyuke na kuvuka barabara hadi upande wa pili ambako alianza kutembea taratibu huku akiendelea kububujikwa na machozi mpaka akafika stendi ya mabasi ya Ubungo na kuingia ndani akaenda kujificha kwenye moja ya kona ya jumba la wasafiri.

Usiku mzima hakulala akifikiria alichokiona, mawazoni mwake akidhani pengine ilikuwa ni ndoto ndefu ambayo angezinduka na kujikuta amelala kitandani, Manka akiwa bado yuko Marekani na wakiendelea kuwasiliana. Haikuwa hivyo, ukweli uliendelea kuwa ukweli.
Majira ya kama saa kumi na moja asubuhi alianza kusikia kelele za wapiga debe wakiita abiria, yeye akatembea kumfuata mmoja aliyekuwa akisema: “Moshi, Arusha! Moshi, Arusha!” na kuanza kuongea naye akiuliza kama angeweza kupewa msaada wa kufika Kilimanjaro kwa fedha aliyokuwa nayo. Mfukoni alikuwa amebakiza shilingi elfu saba tu wakati nauli ilikuwa ni shilingi elfu kumi na tano.

“Labda utasimama.”
“Niko tayari ilimradi nifike nyumbani.”
“Mbona macho mekundu?” mpiga debe alimuuliza Martin baada ya kumuangalia vizuri kwa msaada wa taa.
“Nimefiwa.”
“Pole sana.”

“Asante.”
“Haya ngoja nikuombee kwa kondakta.”
Saa kumi na mbili kamili asubuhi basi liliondoka likiwa limejaa, Martin peke yake ndiye abiria aliyekuwa amesimama. Kichwa chake kilikuwa kimejawa na mawazo ya Manka na kitu gani angemuambia mama yake juu ya mbuzi aliowauza.
Mawazo hayo na hofu ya mama ilimfanya ateremke Segera, moyoni mwake akiwa ameamua kuelekea Tanga kutafuta maisha mpaka atakapopata fedha ya kutosha kununua mbuzi wa mama yake. Hakuwa hata na senti moja mfukoni mwake, alichofanya ni kuomba msaada kwenye lori lililobeba machungwa ambalo mwisho wa safari yake ulikuwa ni Tanga mjini, dereva wa lori hilo alimuonea huruma na kuamua kumsaidia.

Waliingia Tanga akiwa na njaa ya kutosha na kushushwa karibu kabisa na jengo la Majestic Cinema, macho yake kibao kilichoandikwa Rusha Roho Restaurant, watu wakiwa wameketi kwenye viti wakiendelea kula. Akatamani kuwa mmoja wao lakini umaskini ndio uliomfanya ashindwe kuingia ndani ya mgahawa huo, badala yake akaendelea kutembea kwenda mbele na kukata kulia.

“Akaro Advocates & Co.” Akafanikiwa kuyasoma maandishi hayo kwenye kibao kimoja kilichoning’inia wakati akipita kwenye veranda ambalo mbele yake kulikuwa na meza kubwa ya kuuzia magazeti.
“Akaro? Huyu lazima atakuwa ni Mchaga, bila shaka naweza kupata msaada.” Aliwaza kichwani mwake na kuusogelea mlango, akabisha hodi na kuingia ndani, mama mmoja wa makamu akiwa amejitanda ushungi mweupe alikuwa nyuma ya kompyuta akichapa.

“Karibu kijana.”
“Asante shikamoo mama.”Je, nini kitaendelea?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom