Kanungila Karim
JF-Expert Member
- Apr 29, 2016
- 20,746
- 25,638
CHRIS hakuweza kuvumilia zaidi, akatembea kwa haraka akitetemeka miguu. Alipowafikia akasimama na kuwaangalia kwa kuwakazia macho. Si Davis wala Pamela walioshtuka.
Ni kama hawakuona chochote wala yeyote. Wakaendelea na shughuli zao. Muda huohuo, kwa ghafla sana, Chris akasikia kibao cha nguvu mgongoni mwake...
“Nani?” akasema akipaza sauti.
“Cut...” Director Mushi akasema akiwaamrisha wasitishe kuigiza.
Chris akiwa amefura akageuza uso wake. Hamad! Alikutana na uso wa baba yake mzazi ukiwa umekunjamana!
Mzee Joseph Shila.
“Kweli unaweza kuzaa watoto lakini si wote watakuwa watoto bora. Daktari mzima, tena niliyepoteza mamilioni yangu kukusomesha nje ya nchi, unakaa na hawa wajinga wamevaa vichupi mnaigiza?
“Hivi Christopher mwanangu utakua lini wewe? Lini utakuwa mtu mzima na kuelewa ninayokuambia? Pumbaaf, endelea na ujinga wako,” akasema mzee Shila kisha akaondoka zake.
Chris akabaki ameduwaa.
Mushi alibaki anashangaa tu asijue cha kufanya. Neno moja likamponyoka kwa haraka: “What is going on Chris?”
Chris hakujibu.
“Kwa nini tunaharibiana kazi? Hivi kweli scene moja inaweza kutuchukulia siku nzima? Jana ulisema unaumwa kichwa, leo umechelewa location ukasema ulikuwa kwenye upasuaji, baadaye tena sijui unamwita mtu aje kutuharibia kazi ili iweje?
“Kama unaona hutaki kufanya hii sinema si uache kaka? Unadhani wewe ni staa sana siyo? Ni bora kufanya kazi na chipukizi wenye nidhamu kuliko kuhangaika na nyie mastaa mnaotusumbua vichwa kila siku,” akasema Mushi kwa hasira.
Scene hiyo ilimsumbua sana kutokana na ugumu wake...tena siku hiyo walipatia kwa kiasi kikubwa sana kuvaa uhalisia katika kiwango cha juu. Kosa la mzee Shila lilimuumiza sana, maana liliwatoa wasanii katika mwendelezo mzuri wa kuvutia.
“Samahani kaka, unanifikiria vibaya. Yule ni baba yangu.”
“Baba yako?” akauliza Mushi kwa sauti ya upole.
“Ndiyo...ni baba yangu.”
“Imekuwaje?”
“Ni habari ndefu.”
“Samahani sana kaka.”
“Usijali.”
“Upo kwenye mood nzuri na tunaweza kuendelea?” akauliza Mushi.
“Bila shaka.”
“Kweli?”
“Nitajitahidi...”
“Sawa...usijali, tutaendelea palepale...kaeni tayari...kamera upo sawa? Boom please...light...Ok! Action...” akasema Mushi.
“Pamela!!!” neno hilo likamtoka Chris huku machozi yakimiminika kwa kasi sana.
Ilikuwa sauti iliyojaa huzuni na kitetemeshi cha hali ya juu. Kweli alivaa uhusika sawasawa. Ni kweli, tukio lile alitakiwa kutoa machozi, alipaswa kuonyesha huzuni kama alivyofanya.
Hakuna aliyejua ila ukweli ni kwamba alifanikiwa zaidi kutokana na machungu ya kero za mzee wake na si kwa sababu ya tukio lililokuwa ndani ya scene ile.
***
Mzigo mzito ulimjaa Chris kichwani. Mwanamke yule mrembo aliuteka mtima wake. Alikuwa mweusi, mrefu wa wastani mwenye umbo namba nane. Alisuka nywele zake katika mtindo wa rasta nene.
Alivaa sketi fupi ya khaki, iliyofanya miguu yake ya bia ionekane vizuri zaidi. Chris akasahau mawazo yote, akatembea hadi kwenye mlango wa kuingilia chooni na kusimama hapo.
Dakika mbili baadaye yule mrembo alitoka msalani na kumpita Chris pale alipokuwa amesimama. Yule msichana alimwangalia Chris ambaye alijitahidi kutabasamu lakini hakuonyesha kama alimuona! Akapita na hamsini zake. Chris akakasirika!
Na umaarufu wote huo?
Tanzania nzima ilimfahamu kutokana na umaarufu wake kwenye filamu za Kibongo. Mara zote amekuwa mstaarabu na kamwe huwa hatumii umaarufu wake kuwapata wasichana lakini safari hii alitamani sana kutumia silaha hiyo.
Jambo la kusikitisha ni kwamba, silaha hiyo ni kama ilikuwa butu au haiwezi kabisa kutumika. Pengine ingeweza kutumika na ilikuwa na nguvu mujarabu lakini siyo kwa msichana yule!
Itaendelea.