KATIBU Mkuu wa Wizara ya Fedha, Bw. Gray Mgonja, ametangaza rasmi kumburuta mahakamani Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dkt. Willbrod Slaa, kwa alichodai ni kuchafuliwa jina kwa tuhuma za ufisadi.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Dar es Salaam jana, Bw. Mgonja, alisema amefikia uamuzi huo kwa sababu tuhuma zilizotolewa dhidi yake katika mkutano wa hadhara uliofanyika Mwembeyanga hivi karibuni, si za kweli.
"Nitafungua kesi mapema iwezekanavyo, kwa sababu nimechafuliwa jina na tuhuma zimetolewa kwa nia mbaya ya kunipaka matope, hasa nikizingatia uadilifu wangu katika utumishi wa umma kwa miaka 33," alisema Bw. Mgonja.
Mbali ya Dkt. Slaa, alisema ataliburuza mahakamani gazeti la Mwanahalisi na kiwanda cha Printech kwa kusambaza taarifa alizodai kuwa za uongo.
Alisema tuhuma hizo haziwezi kumfanya ajiuzulu wadhifa wake kwa sababu si za kweli. Alisema kazi ya kumfikisha Dkt. Slaa mahakamani inafanywa na mawakili wake. Hata hivyo alikataa kutaja majina yao.
Alipoulizwa anatarajia kudai fidia kiasi gani, alisema suala hilo pia linashughulikiwa na mawakili wake. Alipotakiwa na waandishi wa habari aeleze ukweli kuhusiana na tuhuma zilizotolewa dhidi yake, Bw. Mgonja, alisema kwa sasa hawezi kuziongelea, kwa sababu huo ndio utakuwa utetezi wake mahakamani.
Alisema tuhuma alizotupiwa ni pigo kubwa kwake, hivyo hana njia nyingine ya kujitetea zaidi ya kumfikisha Dkt. Slaa mahakamani.
Bw. Mgonja alisema anamburuta mahakamani Dkt. Slaa yeye binafsi na si kwa kutumia wadhifa wake wa ukatibu Mkuu wa Hazina.
Alisema majibu ya tuhuma dhidi yake akiwa Katibu Mkuu Hazina, zitatolewa na Serikali. Alipoulizwa iweje atumie raslimali za Serikali kukanusha tuhuma zinazomkabili yeye binafsi, Bw. Mgonja alisema aliomba kutumia ukumbi wa mikutano wa ofisi yake ili kuzungumza na waandishi wa habari.
Ingawa Bw. Mgonja alisema anakanusha tuhuma dhidi yake binafsi, taarifa aliyoitoa kwa vyombo vya habari kuhusiana na nia yake ya kumfikisha Dkt. Slaa mahakamani ilikuwa imechapishwa kwenye karatasi zenye nembo ya Serikali.
Bw. Mgonja alipoulizwa kama tuhuma dhidi yake na viongozi wa Serikali zimeanza kuiathiri nchi kwa kunyimwa misaada, alisema hakuna kitu kama hicho.
"Kama tuhuma zingekuwa za kweli nchi ingeathirika, lakini kwa sasa hakuna kitu kama hicho."
Kuhusu kauli ambazo zimekuwa zikitolewa na mabalozi wakiitaka Serikali kuzitolea ufafanuzi, Bw. Mgonja alisema: "Hatufuati maneno ya mabalozi, wao wana vikomo vyao, sisi ni nchi."
Alipoulizwa ni kwa nini tuhuma hizo zitolewe dhidi yake na si kwa makatibu wakuu waliomtangulia, Bw. Mgonja alisema hali hiyo inaweza kuwa imechangiwa na upana wa demokrasia. Alisema tuhuma dhidi yake zina viashiria vya kisiasa.
Bw. Mgonja alipoulizwa anamiliki mali kiasi gani alizochuma katika kipindi chake cha utumishi wa Serikali, alijibu kuwa ni ndogo sana.
"Nina mali kidogo sana na mara kwa mara nimekuwa nikijaza fomu (za kuanisha mali ) na kuzipeleka Utumishi wa Umma, kuna taratibu zake, mnaweza mkaenda mkaomba mkapewa ili muone," alisema Bw. Mgonja.
Kuhusu tuhuma zilizotolewa dhidi ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Bw. Mgonja hakuwa tayari kuzungumzia suala hilo akisisitiza kuwa ni chombo kinachojitegemea. Hata hivyo alisema tuhuma hizo nazo zina majibu yake.
Bw. Mgonja anakuwa kiongozi wa pili kutangaza kufungua kesi mahakamani dhidi ya tuhuma hizo.
Juzi Waziri wa Nishati na Madini, Bw. Nazir Karamagi, alitangaza kumpeleka mahakamani, Dkt. Slaa na wenzake, kwa kile alichosema ni kumchafulia jina na kuonekana kuwa mtu asiyefaa mbele ya jamii.