Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,476
- 39,995
GOLI NI GOLI HATA LA MPENDAZOE NALO GOLI!
Na. M. M. Mwanakijiji
Kwenye kandakanda kuna magoli yanaudhi sana na yanakera. Kuna magoli ambayo mtu unakubali tu kuwa goli hilo "halina utata" na mnajitahidi kurudisha majibu.
Lakini, wakati mwingine magoli mengine yanamfanya mtu usikie donge kooni, presha ipande na kushuka na hata kuna mengine yanaweza kufanya timu nzima muende kumzonga mwamuzi kwani goli lililokubaliwa linaonekana kama limependelewa.
Bahati mbaya goli ni goli liwe la kuudhi au kukera lakini alimradi limekubaliwa basi wakati wengine wanasikia machungu wajue kabisa ipo timu nyingine inashangilia hata kama na wao wanaona kwa kweli lile goli lilikuwa baya.
Mbunge wa Kishapu Mhe. Fred Mpendazoe kawafunga bao CCM tena bao la kuudhi, kukera, kupandisha hasira na kwa kila kipimo bao ambalo CCM ile ya zamani isingeweza kufungwa kijinga hivi. Bao alilowafunga naweza kulilinganisha na bao la "tobo" au linakaribiana na bao la kipa "kupigwa kanzu"! Mwingine anaweza kusema "kapigwa kanzu halafu akapigwa tobo".
Kujiondoa kwa Mpendazoe kutoka Chama cha Mapinduzi kwa sababu yeyote ile kwa namna aliyotoka kunatufanya tusubiri kwa hamu maelezo ya CCM ya kutufafanulia kwanini goli hili siyo goli.Chama cha Mapinduzi bila ya shaka ambacho kina wasomi na watu waliobobea katika propaganda ya uzugaji kwa maneno kinakaribiwa na wakati mgumu wa kuelezea kujiondoa kwa Mpendazoe na bila ya shaka wanachama wengine huko mbeleni.