Domo Kaya: Hukumu ni Kifo

Domo Kaya: Hukumu ni Kifo

Kudo

JF-Expert Member
Joined
Nov 2, 2017
Posts
1,821
Reaction score
6,122
RIWAYA; DOMOKAYA.
NA; BAHATI K MWAMBA.
SIMU; 0758573660/0658564341.

1.

Walishushwa kwenye basi la wafungwa na kuamriwa kuchuchumaa huku wakiwa wamefungwa pingu za miguu na mikono, afya zao hazikuwa imara sana, wengi walionekana dhoofu na wenye nyuso za kukata tamaa. Nyuma yao walisimama maofisa wa kikosi maalumu kutoka jeshi la Magereza, bunduki mikononi mwao na nyuso zenye shari zilikuwa nyuma ya migongo mahabusu na wafungwa waliokuwa wamechuchumaa.

Mahabusu na baadhi ya wafungwa ambao walikuwa wamerejea mahakamani baada ya rufaa zao kuanza kusikilizwa, waliinuliwa na kuongozwa kuingia kwenye sero maalumu ndani ya majengo ya mahakama kuu kanda ya Dar es laam, ulinzi ulikuwa mkali ndani na nje ya sero huku baadhi ya ndugu wa mahabusu na wafungwa wakizuiliwa kuwaona ndugu zao kama walivyozea siku za nyuma. Baadhi walijaribu kupenyeza rupia ili angalau wazisikie sauti za ndugu zao waliokuwa wakisota gerezani, lakini siku hiyo mambo hayakuwa kama walivyozoeshwa huko nyuma ambapo walitoa rushwa kwa maofisa wa magereza wanaokuwa kwenye mlango wa chumba cha watuhumiwa ndani ya mahakama, ili wazogoe na ndugu zao kwa uhuru zaidi kuliko wanavyokuwa wamekwenda kuwatembelea moja kwa moja gerezani.

Watu walijiuliza kuhusu kilichokuwa kikiendelea siku hiyo pale mahakamani, hawakupata jawabu na hakukuwa na kuwapa jawabu hilo kwa sababu itifaki ilizingatiwa, walitakiwa kukaa sehemu ya mapumziko na kungojea majina yao kuitwa ili wakasikilize uendeshwaji wa kesi za ndugu na jamaa zao. Viulizo hivyo kuhusu ulinzi mkali kwa mahabusu na wafungwa havikuwa kwa ndugu pekee, hata baadhi ya wafanyakazi wa mahakama walishangaa ijapokuwa walielewa ulinzi wa namna ile huwa ni kwa wafungwa hatari na wenye kesi kubwa, walishangaa kwa sababu hawakumbuki mara ya mwisho kuona tukio kama lile ilikuwa ni wakati gani tangu waajiriwe kama watumishi ndani ya mahakama kuu.

Mshangao huo haukuwa kwa wafanyakazi hao pekee, mshangao uliwakuta hadi wafungwa na mahabusu waliokuwa kwenye msafara ule wenye ulinzi mkali, hawakuwahi kuwa kwenye uangalizi mkubwa namna ile tena wengi wao wakiwa wamedhibitiwa kwa pingu za mikono na miguu.

Wengi wao licha ya kushangaa baadhi yao kufungwa namna ile lakini hawakuhofia sana kwa sababu asilimia kubwa, walikuwa wakifahamiana kwa maana ya kukaa mahabusu kwa muda mrefu, lakini kati ya wote hao, ni mtu mmoja tu ambae hakuwa akifahamika miongoni mwao na mtu yule alikuwa ni mahabusu kwa sababu alikuwa hana nguo maalumu za wafungwa.

Mtu yule alikuwa ni dhaifu ukimtizama, vidonda vibichi vilikuwa vimejenga himaya kwenye mwili wake kuonesha alipitia shuruba kabla ya kujumuishwa miongoni mwa mahabusu waliokuwa wamekwenda kusikiliza mienendo ya kesi zao. Wengi walijiuliza kuhusu mahabusu yule ambae alionekana kuwa mkimya wakati wote huku akiwa ni mwenye kukata tamaa.

Kukata tamaa au kuzama kwake mawazoni hakukuwa sababu kwa wenzake waliokuwa wameswekwa sero moja yenye hewa nzito ndani yake, walihisi pengine ni kwa sababu ya ugeni wake gerezani na tuhuma zilizomkabili, sababu kubwa iliyowafanya wajiulize ni namna ilivyotokea na wakajikuta wamepandishwa gari moja na yule bwana na kanuni ya usafirishwaji wao ikiwa imebadilika na kuwa yenye ulinzi mkali kuanzia gerezani hadi mahakamani.

Walishangaa kwa sababu ili uwe mahabusu ni lazima kesi yako iwe imewahi kutajwa mahakamani, lakini wao hawakuwahi kumuona yule bwana hapo kabla na hata kwenye kundi la mahabusu waliokuwa wakingojea tarehe za kesi zao, hakuwemo. Wao walimkuta ndani ya basi chini ya ulinzi mkali na walipotimia kwa idadi ikalazimu na wengine watendewe kama alivyokuwa ametendewa mtu yule, walifungwa pingu mikononi na miguuni huku idadi ya maofisa ikiwa ni kubwa tofauti na siku zingine. Maajabu kwao yalikuwa ni kuona msafara wao ukisindikizwa na gari nne, mbele mbili na nyuma mbili huku maofisa wengi wakiwa kwenye gari hizo na silaha mikononi mwao.

“Kwani leo kuna nini?” Mfungwa mmoja alisikika akimuuliza mwenzake kwa sauti ya chini sana.

“Kwa hiyo uliambiwa mimi ni mnajimu? Au uliambiwa nina ukoo na sheikh Shariff Majini nitabiri kinachoendelea?” Mfungwa aliyeulizwa alimtolea uvivu mwenzake kwa kuwa hata yeye alikuwa kwenye sintofahamu.

Ndani ya sero yule bwana mkimya alitengwa na wenzake, aliamriwa kukaa kwenye kona ya chumba huku ofisa mmoja akiwa kando yake na bunduki mkononi. Hakika ilikuwa ni ajabu ofisa wa magereza kukaa ndani ya chumba cha sero na watuhumiwa, chumba ambacho hakikufaa kwa lolote na ilionekana kipo maalumu kwa ajili ya watuhumiwa tu na si watu wengine, kilikuwa kichafu na chenye harufu nzito. Maswali mengi kwao kuhusu mtu yule hakukuwa na wa kuyajibu, walibaki watazamaji na kungojea hatima ya kesi zao.

Wakati wengine wakijiuliza maswali mengi kuhusu mahabusu huyo, mhusika mwenyewe nae alikuwa kwenye viulizo vingine ambavyo hakuwa akijua mwisho wake, wakati wenzake wakimuona akiwa kajiinamia, mwenzao alikuwa amezama kwenye tanuri kubwa la mawazo.

“Kwa nini kila kitu kinaonesha mimi ndiye niliyehusika na vifo vyao wote?” Alijiuliza huku akijaribu kukumbuka baadhi ya matukio yaliyomfanya afike pale.

“Hata jua lingeamua kugeuka kamwe nisingeinua kisu kumuua mke wangu wala yule hawala wake, nisingeweza.” Aliwaza huku akitikisa kichwa peke yake bila kujijua, kisha aliinua uso wake na kutizama juu, alihisi akitazamana na sura ya mke wake iliyojaa majonzi na uso wa majuto.

“Ulinitesa kwa maumivu ya mapenzi, nilikulilia wivu huku nikiwa na fukuto la maumivu moyoni mwangu lakini hukunielewa, bado umekufa kifo chako ila mimi naadhibiwa kwa ajili yako. Ni lipi kosa nililokutenda hadi uamue kunipitisha njia hii?” Alisema kwa sauti ndogo ambayo haikuwafikia watu wengine waliokuwa kwenye kile chumba maalumu kwa mahabusu.

“Ok, tuyaache hayo, ni kweli ulikuwa umeolewa mara ya pili? Je, ni mimi mume wa kwanza au nilikuwa ni wa pili nisiyetambuliwa?” Aliendelea kuongea huku chozi likichukua himaya kwenye mashavu yake kwa kutengeneza mchirizi kuelekea kidevuni.

“Nijibu basi, au bado unanidharau? Bado hujafurahi na haya ninayopitia?” Alizidi kuongea huku wakati huu akiongeza sauti kidogo kiasi baadhi ya mahabusu waligeuka na kumtazama huku ofisa aliyekuwa akimlimda, akipiga hatua kumfuata.

“Yaani unataka kuchanganyikiwa kabla hata ya kumuona Jaji?” Ofisa alimwambia huku akimalizia kwa kucheka kicheko cha unafiki.

“Usiwe muoga, wewe ni mwanaume, jikaze.” Alimwambia kwa mara nyingine huku akiendelea kutabasamu kwa dhihaka.

Jamaa alikaa kimya bila kumjibu askari yule ambae hakuwa akijua kilichokuwa kikimsibu mahabusu wake, alichojali wakati huo ni kila mmoja ndani ya sero kufuata utaratibu ikiwa ni pamoja na kukaa kimya, mahakamani siyo sehemu ya kupiga kelele.

Wakati hayo yote yakitokea, mahabusu wengine walikuwa wakiendelea kuitwa kwenda kujitetea kwa tuhuma zilizokuwa zikiwakabili.

“Lakini sikuuwa mimi, nilimpenda mke wangu na nisingeliweza kufanya hivyo, tena nimuue na bwana'ake! Nisingeweza.” Aliendelea kuwa mawazoni huku akionekana kuumia kwa kilichokuwa kikitokea dhidi yake.

“Lakini ni nani aliua na kwa nini aliwaua? Kwa nini mimi ndiye nionekane nimeua?” Aliendelea kujiuliza huku dhahiri akionekana kuumia moyoni mwake.

“Dodi Danga!” Sauti nzito ya afande ilisikika kutokea mlangoni.
Mahabusu waligeuka nyuma na kumtazama jamaa aliyekuwa ametengwa peke yake, angalau walielewa aliitwa Dodi Danga kwa kuwa aliinuka baada ya jina kutajwa. Dodi alipita kando yao taratibu huku akivuta miguu yake ambayo ilibanwa vema na pingu za miguuni, nyuma yake alikuwepo ofisa wa magereza akiwa ameshika bunduki yake. Ukimya ulikuwa mkubwa na kilichosikika ni hatua zake, mlangoni alipokelewa na moafisa wengine ambao walimuongoza kuelekea kwenye chumba cha mahakama. Nje ya mlango wa mahakama kulikuwa na watu wengi wenye kamera na wengine simu za mkononi, alishangaa namna walivyochangamka baada ya kumuona, waligombea kupata nafasi ya kumpiga picha za kila aina, mnato na zile picha mjongeo. Dodi alishangaa na kuingiwa mfadhaiko, hakuwa amejiandaa kwa tukio kama lile na wala hakuwa amehisi kuna jambo litatokea la namna ile.

“Kwa nini napigwa picha na hawa waandishi? Au ni kawaida yao kuwapiga picha kila mahabusu wanaopita kuingia kwenye chumba cha mahakama?” Alijiuliza bila kupata jibu huku wakati huo maofisa waliokuwa nyuma yake wakimsukuma atembee haraka, lakini angeliwezaje kutembea haraka ikiwa amefungwa pingu miguuni? Angelitembea haraka wakati alikuwa amefungwa mikononi? Hakika aliona anaonewa kulazimishwa kufanya mambo ambayo waliomlazimisha walijua hataweza kuyafanya, lakini kikubwa aliona hawakuwa na utu ndani yao na walikiuka haki za binaadamu hadharani.

“Kwani huko nje kinaendelea nini?” Alijiuliza huku akiingia kwenye chumba chumba cha mahakama, aliongozwa kuingia kizimbani na askari wawili wakasimama pembeni ya kizimba. Kwa mara nyingine mshangao ulijenga himaya kichwani mwake, watu wengi sana walikuwa kwenye kile chumba cha mahakama na wengine walikosa nafasi ya kukaa na walibaki wakiwa wamesimama kwa utulivu mkubwa. Hakukuwa na taratibu za mwanzo za kimahakama kama vile; kuingia kwa Jaji na wazee wa baraza, askari wa mahakama kuamuru watu kusimama wakati wa kuingia kwa Jaji na taratibu nyinginezo. Yote hayo hayakufanyika kwa sababu tayari kesi kadhaa zilikuwa zimeshasikilizwa na yule Jaji na baraza lake, hayo hayakumshitua Dodi Danga, kilichomshitua ni namna kesi yake ilivyokuwa imeharakishwa kupelekwa mahakama kuu bila kupitia ngazi nyingine za kimahakama hadi kufikia hatua ya kupangiwa Jaji wa mahakama kuu kuisikiliza kesi yake.

Dodi Danga alishangaa kwa kuwa kesi ilikuwa imefika mahakama kuu na hakuwa amepewa nafasi ya kumpata wakili wake au serikali kumpa wakili kama angeshindwa kumudu gharama binafsi za mwanasheria anaemuamini.

“Tuhuma zangu ni kubwa sana na ninayo haki ya kuwa na mwanasheria atakae simamia kesi yangu, iweje hadi sasa kesi inasomwa ikiwa sina wakili? Au nitapewa fursa hiyo baada ya shitaka kusomwa kwa mara ya kwanza?” Alijiuliza huku akimtizama Jaji aliyekuwa amekaa kwenye meza yake akiendelea kupitia makabrasha yake, alizungusha macho na kumtizama karani wa mahakama namna alivyokuwa bize kukusanya karatasi zilizokuwa mezani kwake, mwisho alimalizia kwenye viti vitatu vilivyokuwa na mawakili watatu ambao hakujua walikuwa upande gani, wa mashitaka dhidi yake ama watetezi wake, alisubiri kuona kitakachofuata.
 
Taratibu za kimahakama zilifuatwa ikiwemo kusomwa kwa shitaka dhidi yake, alikuwa akituhumiwa kwa makosa mawili; kumiliki genge la uhalifu na kuua. Jaji alimsomea mashitaka yote mawili yaliyokuwa yakimkabili kisha akamsomea maelezo aliyoyaandika wakati akiwa mikononi mwa polisi.

“Mh!” Dodi aliguna kwa sauti ya chini huku akishindwa kuamini alichokuwa anakisikia, maelezo yote yaliyosomwa hakuyaandika yeye na hakuwahi kuandika maelezo wakati akiwa mikononi mwa watu waliokuwa wakijiita polisi, watu ambao tangu walipomkamata hawakuwahi kumpeleka kituo chochote cha polisi, zaidi walimlazimisha kuandika maelezo kwa namna walivyotaka wao na walimlazimisha kukiri kumuua mke wake Linatha Msuya na mtu mwingine aliyeitwa Ngurimi Mwangwa. Mateso aliyopitia kwa kiasi kikubwa yalichangiwa na yeye kutokukubaliana na walichomweleza, walimlazimisha lakini hakuwa tayari kukubali kufanya walichotaka, alikataa kuandika maelezo na alikataa kukiri kukubali kuwaua watu wawili ambao aliwatuhumu kuwa ni wapenzi.

Wakati akiendelea kuwaza mwenendo wa mambo pale mahakamani mara kikatokea kioja, hakikumshangaza yeye tu, bali na watu waliokuwa mle mahakamani ambao walielewa taratibu za sheria kwenye mashitaka ya aina ile. Jaji hakutoa nafasi kwa mtuhumiwa kukubali ama kuyakataa maelezo aliyoyasoma na badala yake, akaruhusu kesi iendelee kusikilizwa bila mtuhumiwa kupewa haki yake ya msingi ya kukubali ama kuyakataa maelezo yaliyowasilishwa mahakamani na upande wa mashitaka, maelezo ambayo kimsingi yangelichukuliwa kama ni miongoni mwa vielelezo muhimu kwenye mwenendo mzima wa kesi ile.

“Yakoje mambo haya?” Alijiuliza huku akimtizama Jaji kwa namna ya kumtuhumu kupokea maagizo namna ya kuendelesha kesi ile iliyokuwa mezani kwake.

“Hivi ni kweli inaweza kuwa ni tuhuma za mauaji pekee zilizonyuma ya hili jambo? Au kuna kitu kinasukuma hili jambo kuwa namna hii?” Dodi aliwaza huku akisikia sauti ya Jaji ikimruhusu wakili wa upande wa mashitaka, aanze kumuuliza maswali. Kuruhusiwa kwa wakili wa upande wa mashitaka kumuuliza maswali mtuhumiwa, kulikuwa kunadhihirisha kuna kipengele kingine kilikuwa kimerukwa na Jaji na Dodi hakujua kama kilirukwa babati mbaya ama ni makusudi yalifanyika. Kwa utaratibu ili kuweka haki baina ya upande wa mashitaka na mshitakiwa, Jaji alipaswa kumuuliza mtuhumiwa kama yupo tayari kesi isikilizwe bila wakili wa upande wa utetezi au apewe nafasi ya kumpata wakili wa kumtetea na kama mtuhumiwa asingelikuwa na uwezo wa kumpata mwanasheria wake binafsi, milango ingelikuwa wazi kwa wakili kutoka serikalini kusimama upande wa utetezi. Lakini Jaji hakutoa nafasi hiyo kwa mtuhumiwa na badala yake akaruhusu kusikilizwa kwa kesi.

Dodi alizidi kukata tamaa na kwa matukio hayo madogo tayari alishaona hakuwa na pa kutokea, ingelihitajika miujiza pekee ili kumtoa kwenye shimo alilokuwa anazidi kuzama, aliwaza zaidi baada ya kujua hata huko nje hakukuwa na mtu wa kumsaidia, maisha yake yalikuwa ni yake peke yake na mara chache alikuwa akishirikiana na mtu wake wa karibu ambae alikuwa ni zaidi ya ndugu kwake, mtu yule ndiye aliyekuwa amemtoa kwenye ufukara na kumfanya angalau aweze kuyamudu maisha yake, alimfunza mengi na kumsaidia vingi lakini bahati mbaya ni kwamba, mtu yule hakuwa nchini kwa zaidi ya miaka mitano japo biashara zake zilikuwa bado zinaendelea.

Dodi Danga aliona matumaini ya kupata utetezi yakipotea hasa baada ya kujijua hakuwa na ndugu hata mmoja kwenye maisha yake, alikulia mtaani na maisha yake yaliishia mtaani. Hakuwahi kumjua baba yake wala kumjua mama yake, kiufupi alikuwa ni yatima tena yatima ambae hakuwa na ndugu hata mmoja hapa Duniani, ndugu yake pekee alikuwa ni huyo mtu aliyemsaidia ukubwani na wakati mtu huyo alipoondoka kwenye maisha yake, ndipo akajitokeza mwanamke Linatha. Linatha aliingia kwenye maisha yake na kuwa mke na ndugu yake, hakuona kama yupo mtu mwingine wa kumuamini zaidi ya mke wake Linatha. Akafunga nae ndoa mbele ya ndugu za mke huku yeye akiwaalika marafiki zake wachache wa kibiashara baada ya kushindwa kuyapata mawasiliano ya rafiki yake ambae wakati huo alikuwa nje ya nchi, nchi gani alipokuwa, hakujua.
Dodi chozi la uchungu lilimtoka huku akiyakumbuka maneno ya Jaji wakati alipokuwa akimsomea shitaka dhidi yake.

Jaji: “ Dodi Danga umri miaka 35, unatuhumiwa kwa mashitaka mawili, mosi; tarehe 12/3/2019 maeneo ya Mbezi mwisho majira ya saa tatu na nusu usiku, ulimuua bwana Ngurimi Mwangwa na kisha tarehe 13/3/2019 majira ya saa moja ahsubuhi unatuhumiwa kufanikisha mauaji ya Bi. Linatha Msuya akiwa kwenye chumba cha hoteli Afrikana iliyoko maeneo ya Kimara Temboni. Wahanga wa matukio hayo ni wanandoa. Shitaka la pili tuhuma za kumiliki genge uhalifu ambalo kwa kushirikiana mlifanikiwa kutenda makosa hayo katika tarehe tajwa hapo juu lengo….”

Machozi yalizidi kumbubujika baada ya kukumbuka kauli hiyo kutoka kwa Jaji, kilichomuuma zaidi ni kusikia ya kuwa alimuua mke wa mtu na si mke wake Linatha.

“Ina maana ni kweli Linatha alikuwa ni mke wa mtu mwingine? Mbona ndugu zake wako wapi wathibitishe hili mbele yangu?” Alijiuliza huku akizungusha macho yake kwenye kile chumba cha mahakama kuona kama angeliweza kumuona hata ndugu wa Linatha, lakini hakumuona wala kuona mtu yeyote aliyekuwa akimfahamu, hata rafiki wa mke wake hakuwaona.

“Nakuuliza wewe bwana Dodi!” Sauti ya wakili ilimshitua kutoka mawazoni, akarejesha uso wake kumtizama wakili aliyekuwa hatua chache mbele yake akiwa ameshika karatasi mikononi mwake.

“Rudia…!” Dodi alimwambia na wakili akamtizama kwa sekunde chache na kurudia swali alilokuwa amemuuliza.

Wakili: Unaitwa Dodi Danga na umri wako ni miaka 35?.

Dodi: Ndiyo.

Wakili: Umewahi kuugua magonjwa ya akili au ndugu yako yeyote umewahi kumshuhudia akiumwa?

Dodi: Hapana.

Wakili: Unahakika hujawahi kuugua?

Dodi: Ndiyo.

Wakili: Hiki ni nini?

Dodi: Karatasi.

Wakili: Mbona mimi naona ni vidole vilivyoshika karatasi?

Dodi: Kimya.

Wakili: Huoni kama akili zako hazifanyi kazi sawasawa?

Dodi: Basi mmoja kati yangu na wewe, hana akili.

Wakili: Kwenu mlizaliwa wangapi?

Dodi: Kimya.

Wakili: Jibu swali.(kwa ukali)

Dodi: Kimya.

Wakili anamgeukia Jaji..

Wakili: Mheshimiwa Jaji, hajibu maswali yangu inanikwamisha kutekeleza majukumu yangu.

Jaji: Bwana Dodi Danga, unatakiwa kujibu maswali unayoulizwa.

Dodi alimtizama Jaji kwa jicho kali lenye kumsuta kwa kukiuka vipengele muhimu kwenye kuendesha kesi ile, badala yake anamtaka ajibu kila anachoulizwa, hapana, Dodi aliona hahitaji kuendeelea kuwa mnyonge hata kama isingelimsaidia, lakini angalau watu waliokuwa ndani ya mahakama watajua kulikuwa na baadhi ya vitu muhimu vilikiukwa siku ile.
 
“Mheshimiwa Jaji na mahakama tukufu, nachelea kusema siko tayari kuendelea kujibu maswali bila mwanasheria wangu, pia nakana mashitaka yote uliyonisomea na muhimu zaidi, naomba niandike maelezo yangu mwenyewe hapa mahakamani kwa kuwa maelezo uliyopewa na kuyasoma, sikuyaandika na sikuwahi kuyaandika popote. Hivyo maelezo hayo ni batili na kudhibitisha hilo, maofisa walionihoji naomba wajitokeze hapa na kuthibitisha maelezo hayo yananihusu na niliyaandika mbele ya nani kama shahidi, wathibitishe kituo kipi cha polisi nilishikiliwa na kuandika maelezo hayo.” Dodi alisema kwa kujiamini kabisa tofauti na alivyoingia ndani ya mahakama, Jaji na wakili aliyekuwa kasimama walitazamana, wakili akataka kusema neno, lakini Jaji akamzuia na kuruhusu mahitaji ya mtuhumiwa yazingatiwe na aliahirisha kesi hadi tarehe nyingine na upande wa mashitaka ukamilishe baadhi ya matakwa ya msingi, pia aliruhusu Dodi aandike maelezo ndani ya mahakama kwa kuwa alikuwa na haki ya kufanya hivyo.

Lakini swali kwa raia waliokuwa wakisikiliza kesi ile pamoja na Dodi mwenyewe lilikuwa ni, ‘Jaji alikuwa wapi wakati wote hadi akumbushwe?’ Ni kweli hakuwa amejua mtuhumiwa alikuwa anahitaji kupata haki zake za msingi kabla ya kuruhusu kesi kusikilizwa? Ina maana mtuhumiwa angelikuwa hana ufahamu wa sheria kesi ingeendelea kusikilizwa na kutolewa hukumu? Jaji alijisahau au kuna kitu kilikuwa nyuma yake? Alifanya vile kumfurahisha nani?

Maswali yalikuwa mengi na hakukuwa na wa kuyajibu, kila aliyejiuliza aliishia kuzua walakini kichwani mwake bila majibu sahihi.
Wakati watu wakizidi kujiuliza, Dodi Danga alishushwa kizimbani na kuongozwa nje ya chumba cha mahakama akiwa chini ulinzi mkali kama ilivyokuwa wakati akiingia. Kama kawaida, nje alikutana na kundi kubwa la waandishi wa habari ambao walihakikisha wanapata picha nzuri za kuuzia vichwa vya habari kwenye magazeti yao na kuuzia habari mtandaoni.
Dodi aliongozwa hadi nje ya jengo la mahakama na kupelekwa moja kwa moja gari la wafungwa, hakupitishwa kwenye chumba cha mahabusu kwa kuwa tayari kesi yake ilikuwa imeshasikilizwa. Ndani ya gari aliwakuta baadhi ya watuhumiwa wengine wakiwa wameshaingia na kukaa, askari wenye silaha na wao walikuwa ni miongoni mwa watu waliowakuta ndani ya gari. Ulinzi uliimarishwa zaidi baada ya yeye kuingia, askari wenye silaha waliongezeka nje na ndani ya gari. Hali hiyo ilisababisha baadhi ya watu waliokuwa wakijiuliza kuhusu hali ya ulinzi siku ile, angalau walipunguza shauku baada ya kuhisi sababu ilikuwa ni yule bwana mpole ambae hakuonekana kuwa mkorofi wala mwenye mambo mengi.

*******

Majira ya saa tisa alasiri gari la wafungwa liliingia kwenye milango ya gereza na kuongozwa sehemu maalumu ya kusimama, baada ya gari hilo kusimama, wafungwa na mahabusu waliokuwemo waliamriwa kushuka chini ya ulinzi mkali. Wale mahabusu na wafungwa wazoefu ndani ya lile gereza, waliruhusiwa kuendelea na majukumu yao baada ya kupitia utaratibu fulani wa kawaida kwao, wafungwa na mahabusu wapya waliongozwa sehemu nyingine iliyokuwa na uwazi finyu, walipangwa msatari mmoja mnyoofu na kisha majina yao yalianza kuitwa. Jina la kwanza lilikuwa ni la Dodi Danga, aliitika kwa sauti ya kivivu huku akianza kupiga hatua kuelekea kwenye mlango wa ofisi iliyokuwa hatua chache kutoka pale walipokuwa wamepanga mstari. Alipiga hatua chache na kabla hajaufikia mlango, ofisa mmoja alipiga hatua ndefu na kwenda kusimama mbele yake kibabe, mkononi akiwa ameshika funguo nyingi zilizokuwa zimeungwanishwa na waya mwembamba. Ofisa yule bila kumsemesha, alichagua funguo moja na kuanza kumfungua pingu za mikono na miguu na alipomaliza, alimruhusu aeingie kwenye ile ofisi.

Dodi alikaribishwa kwa tabasamu la kinafiki na maofisa wawili waliokuwa ndani ya kile chumba walichokiita ofisi, hakikuwa chumba chenye hadhi ya ofisi, hakukuwa na kitu chochote ndani zaidi ya kiti kimoja alichokuwa amekalia ofisa mmoja aliyekuwa ameshika kalamu na daftari huku mguu mmoja akiwa ameuweka juu ya mwingine.

“Vua nguo haraka.” Ofisa mmoja ambae alikuwa amesimama alimuamuru Dodi huku lile tabasamu la kejeli likiwa mbali na uso wake.

Dodi alisita kwa kuwa hakuwa anaelewa walichotaka kukifanya wale mabwana.

“Hatuna muda wa kukubembeleza fala wewe!” Afande alifoka huku akisindikiza na kofi zito lililotua mgongoni kwa Dodi na kumwacha akiugulia maumivu yaliyokuwa yakisambaa mwilini mwake kwa kasi.
Dodi hakutaka kuzua mgogoro na wale jamaa ambao walionekana kupenda ukorofi kwa wafungwa na mahabusu bila kujali utu, alivua nguo zake na kubaki uchi mbele ya wanaume wenzake ambao wao walikuwa wamevaa nguo zao. Ofisa mmoja alizichukua nguo zake na kuzikagua na aliporidhika alizirusha chini na kumgeukia.

“Tupe mavi yetu.” Ofisa aliongea kwa sauti ya mamlaka. Dodi hakuelewa alichosema alibaki akimtizama bila kumsemesha.

“Ina maana huelewi kitu gani? Jikamue kinyesi tuhakikishe hujaficha kitu huko.” Jamaa alifoka huku akijiandaa kunyanyua mkono wake kwa nia ya kumwadhibu.
Ala! Dodi alishangaa, ilikuwa ni zaidi ya fedheha kwake, kitendo cha kulazimishwa kujisaidia mbele za watu wengine ilikuwa ni zaidi ya dharau na kudhalilishwa na hakuww tayari kwa hilo. Alikataa kufanya walichotaka, alibaki akiwa amesimama huku akiwatizama, hakuwa na cha zaidi mbele ya wale maafande ambao hakuona kama walikuwa wanastahili kuwafanyia kitendo kama kile binaadamu wenzao.

“Unatupotezea muda kishundu wewe.” Askari mmoja aliunguruma huku akimchota mtama safi uliyombwaga sakafuni mithili ya kifurushi cha bangi.

“Wakati mwingine jifunze kuheshimu kazi za watu.” Jamaa aliongea huku akimtandika teke zito lilitua sawia mbavuni mwake, aligugumia kwa maumivu huku akijaribu kujizoazoa chini.

“Achana nae mtu mwenyewe anaonekana kuwa nusu mfu nusu hai.” Ofisa aliyekuwa amekaa alimshauri mwenzake ambae alikuwa akijiandaa kushusha pigo lingine mwilini mwa Dodi Danga.

“Unadhani sisi huwa tunakuja kutafuta wafungwa mtaani? Si mnajileta wenyewe? Sasa unaogopa nini kukuchuchumaa mbele ya wenzako?” Jamaa aliendelea kumsimanga huku akimsukumia nguo zake kwa mguu, Dodi alizipokea na kujikokota hadi alipofanikiwa kusimama, akazivaa na kutoka ndani ya kile chumba. Nje alipokelewa na maofisa waliokuwa nje kisha akaongozwa kuelekea kwenye moja ya sero maalumu kwa watu maalumu ndani ya gereza. Aliingingizwa kwenye sero hiyo ambayo ilikuwa ni mahususi kwa wafungwa ambao ni hatarishi ama wanaotumikia adhabu. Ndani yake hakukuwa na mwanga, wala hakukuwa na sehemu ya kupitisha mwanga kutoka nje, kiufupi kilikuwa ni chumba yai, hakukuwa na dirisha na hata mlango ulionekana wakati wa kufunguliwa ama kufungwa, baada ya hapo sehemu ya mlango ilikuwa ni sawa na ukuta.

Dodi Danga alisimama katikati ya kile chumba huku akijaribu kupambana na harufu kali iliyokuwa mle chumbani, alisimama ili angalau aruhusu akili yake iweze kuzoea mazingira ya kile chumba. Zilipita dakika kumi akiwa amesimama, alipohisi angalau pua zake zilishaanza kuzoea harufu ya kile chumba, alinyoosha mikono yake na kuanza kupapasa hapa na pale hadi alipofanikiwa kugusa kitanda kidogo cha chuma kilichokuwa na godoro chakavu juu yake, hakujali, alijitupa juu yake na kufumba macho yake ili angalau aweze kupata lau lepe la usingizi baada ya kuwa ameukosa kwa zaidi ya wiki mbili, wakati wote huo alikuwa akibadilishiwa aina za mateso ili mradi akubali tuhuma walizompa. Alipojilaza alihisi kila sehemu ya mwili wake ilikuwa chungu, maumivu yalikuwa ni makali kila alipojaribu kujigeuza. Licha ya maumivu hayo lakini hakuwa tayari kuukosa usingizi ili angalau apumzishe akili yake iliyokuwa ikiandamwa na wingu kubwa la mawazo. Dodi alifumba macho na kuuruhusu ubongo wake ulale huku ukiacha mwili wake ukishambuliwa kwa shangwe na kunguni waliokuwa na njaa kali.

Wakati Dodi Danga akilala gerezani, upande mwingine kulikuwa na jambo lililokuwa likiendelea, jambo lililozua mambo ndani ya jiji la Dar es laam.
 
Wakati Dodi Danga akilala gerezani, upande mwingine kulikuwa na jambo lililokuwa likiendelea, jambo lililozua mambo ndani ya jiji la Dar es laam.

*******

2.

Ndege kubwa ya shirika la ndege la Tanzania ilitua salama kwenye uwanja wa kimataifa wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, abiria wengi walifurahi na kumshukuru Mungu kwa kuwafikisha salama baada ya safari ndefu ya zaidi ya saa kumi. Miongoni mwa abiria hao alikuwemo mwanaume mmoja mwembamba na mrefu, mwenye sura isiyovutia wala isiyochukiza,macho yake makubwa hakuona umuhimu wa kuyaficha kwa miwani. Mwanaume yule aliongozana na abiria wengine kutoka nje ya ndege akiwa na begi lake dogo mkononi, hakuonekana kuwa ni mwenye haraka bali alionekana kuwa na ujanjaujanja wa kuzungusha macho yake kila kona ya uwanja.

“Hatimae nimerejea nchini kwangu kwenye ardhi iliyobarikiwa.” Aliwaza huku mguu wake wa kulia ukitua chini kutoka kwenye ngazi maalumu za kushushia abiria. Alisimama kwa sekunde thelathini huku macho yake yakizunguka kila pande ya uwanja, alipoona kupo shwari alianza kupiga hatua zake taratibu kuelekea sehemu ya kukaguliwa ili aweze kutoka nje ya uwanja.
Dakika tatu baadae alikuwa akitokeza kwenye lango nje ya mipaka ya uwanja na kulakiwa na madereva taxi wengi waliokuwa hapo, alinyoosha mkono wake wa kulia na kuwapa ishara ya kukataa huduma yao, aliwapita na kuongoza kuelekea barabarani. Alifanya vile kwa kuwa hakuwa akitarajia kupokelewa na mtu yeyote pale uwanjani, hata mtu ambae alikuwa na taarifa ya ujio wake alitambua asingeliweza kwenda kumpokea kwa sababu alielewa utaratibu wake, hakupenda kupokelewa wala hakuwa muumini wa kutumia usafiri binafsi, siku zote alijihisi salama zaidi endapo angelitumia usafiri wa umma. Alitembea kwa hatua zake ndefu hadi alipofika barabarani, alitazama kushoto na kulia kisha akapiga hatua na kuvuka barabara baada ya kuhakikisha hakukuwa na gari pande zote mbili. Hatua zake za mwisho ziliishia kwenye kituo cha abiria wanaousubiri daladala za kuelekea katikati ya mji na nyingine pembezoni mwa mji. Dakika chache alizokuwa akingojea daladala ya kuelekea alipohitaji, alishuhudia namna watu walivyokuwa wakisukumana kuwahi kwenye milango ya daladala huku wengine wakitumia nafasi hiyo kuwaibia wenzao.

“Hii ndiyo Dar es Laam!” Aliwaza huku akitabasamu baada ya kushuhudia mwanamama mmoja akiingia ndani ya daladala kwa kupitia dirishani. Wakati akiwa bado anautafakari ujasiri wa yule mwaanamke, masikio yake yalisikia sauti ya konda akitangaza vituo vya sehemu gari lake lilielekea, moja ya kituo kilichotajwa ni kile alichokuwa akitarajia kushukia. Aligeuza shingo upande wake wa kulia na kuliona gari likitafuta nafasi ya kuingia kituoni huku konda aliyekuwa akitangaza vituo, akiwa amening'inia mlangoni. Gari ilisimama na yeye akawa miongoni mwa abiria waliowahi kupanda, licha ya msongamano wa abiria ndani ya daladala lakini alipata nafasi na kusimama huku akihakikisha begi lake likiwa haliko mbali na mikono yake. Safari ilianza huku baadhi ya abiria wakisikika wakilalama kwa sababu ya mbanano ndani ya gari, konda hakuonekana kuwajali na bado alikuwa akitangaza vituo kwa watu aliowaona njiani kumaanisha, bado alihitaji watu wengine kulipanda gari lake.

Kwa kuwa yeye alikuwa amepata nafasi ya kusimama licha ya kuzongwa hapa na pale, lakini hakuwa na ulalamishi kwa sababu hiyo ndiyo ilikuwa hali halisi ya jiji la Dar es laam na hakukuwa na mbadala wa kukwamua adha ile licha ya barabara ya gari za mwendo kasi kuendelea kujengwa kwa kasi ili angalau kupunguza kero ile, lakini hata hiyo aliamini haikuwa tiba ya ugonjwa ule maana hata sehemu ujenzi ulipomalizika na gari za mwendokasi kuanza kazi, bado adha ya mbanano ilikuwa vilevile na hiyo ni kwa sababu baadhi ya maeneo zilipopita gari zile, daladala hazikuruhusiwa kupeleka au kuchukua abiria maeneo hayo na kusababisha mwendokasi iwe ni tegemezi na matokeo yake mzigo ukawa mkubwa mara dufu na kero ikaongezeka.

Bwana yule aliachana na mawazo hayo ya usafiri ndani ya jiji, alizama kuwaza kilichokuwa kimemfanya arejee nchini licha ya kwamba alikuwa ameamua kuhamisha makazi yake kwa muda nje ya nchi, alilazimika kuhama kwa sababu ya kazi yake aliyokuwa akiifanya kuingiliwa na kundi ambalo hakuwa akihitaji kujihusisha nalo. Aliamua kuhamisha makazi kwa sababu watu wa serikali walianza kumtumia kwenye kazi zao na matokeo yake akajikuta akitumika kama mwanausalama bila hiyari yake, hiyo ilikuwa ni sababu kubwa kwa sababu hakupenda kabisa kuzoeana na watu wa serikalini ambao hakuwahi kuwaamini kwenye maisha yake, hakutaka pia wamzoee na kumfahamu kiundani kitu ambacho aliamini kingelikuja kumpa taabu mbele ya safari, kuzoena huko na wakati mwingine kulazimika kufanya kazi chafu kwa niaba ya serikali, alikufananisha na urafiki wa swala na Simba ambao daima ni urafiki wa mashaka na haudumu. Kujiepusha na urafiki huo aliona ni vema akae mbali na nchi hii na alifunga mianya yote ya mawasiliano ambayo ingetumika kuwasiliana nae. Aligawa baadhi ya mali zake kwa marafiki zake na mali nyingine aliziacha mikononi mwa taasisi za misaada alizokuwa amezianzisha. Miongoni mwa watu waliofaidika na mali hizo ni rafiki yake wa karibu, Dodi Danga. Kabla ya kumgawia alihakikisha amemfundisha mambo mengi sana ikiwemo, kumuondoa kwenye uraibu wa utumizi wa sigara na pombe, kumfundisha mbinu za mapigano na kujihami, kujitolea kwa jamii na baadhi ya mambo ya msingi ambayo binaadamu wa kawaida hutakiwa kuwa nayo. Kitu pekee ambacho hakumfunza na hakutaka kumfunza ni aina ya kazi aliyokuwa akiifanya, kazi ya umamluki wa kuua watu na kuiba mali kulingana na hitaji la mteja wake. Watu wa aina yake kwa lugha ya watu weupe kutoka bara ulaya huwaita Hitman.

Licha ya kumgawia mali nyingi lakini hakuwahi kumwambia nchi atakayokwenda kuishi, wala hakuwahi kumpa mawasiliano yake ijapokuwa yeye alikuwa akifuatilia kila kilichokuwa kikiendelea nchini. Mtu pekee aliyekuwa akifahamu alipo ni rafiki yake wa tangu utoto, rafiki ambae walipitia mengi wakiwa pamoja, rafiki ambae walikuwa wakifanya kazi ya aina moja japo zenye utofauti mdogo kiutekelezaji, ila wote walikuwa ni Hitman. Rafiki huyo walikuwa wakiwasiliana kila mara ndiye aliyempa taarifa iliyomfanya afunge safari hadi jijini Dar es laam, safari ambayo hakuwahi kudhani ingeliweza kumkutanisha na mambo makubwa na mazito ambayo hakuwa akijua ni sawa na maji ya kina kirefu.

Mawazo yake yalikoma baada ya dereva kushika breki ghafla na kusababisha watu waliokuwa wamesimama kugongana kwa kukosa mhilimi, hata wale waliokuwa wamekaa nao walikutana na adha ya kuyumbishwa miili yao. Wapo waliosikika wakilalamikia kitendo kile na wapo waliokaa kimya bila kusema neno, miongoni mwa abiria ambao hawakusema neno alikuwa ni yeye ijapokuwa moyoni mwake alilaani kitendo kile huku akihisi dereva ni mzembe na hakuwa makini barabarani. Wakati watu wakiwa hawaelewi kilichokuwa kikiendelea, walishangaa dereva akifungua mlango na kuanza kutimuwa mbio kurejea walikotokea, lakini hakufika mbali, alirushwa juu na kitu ambacho abiria waliokuwa wakimshuhudia walishindwa kuelewa, lakini walishuhudia akianguka chini huku masikio yao yakisikia mlio mkali wa mlipuko mwembamba, baadhi ya abiria waliokuwa ndani ya ile daladala walielewa ulikuwa ni mlio wa bunduki ya kivita na hapo ndipo kikazuka kizaazaa ndani ya gari, kila mmoja akitaka kuwahi kujirusha nje na wale waliokuwa wamesimama walianza kusukumana ili watokee mlamgoni, kina mama walisikika wakilia hovyo na baadhi ya vijana walisikika wakilalamika kukosa nafasi ya kuwahi kutoka nje.

Wakati abiria wengine wakihangaika kupata nafasi ya kutoka nje, yule abiria mrefu hakuwaza kama wao na hakuwa mgeni na milio ya risasi hivyo alielewa ni nini maana ya utulivu wakati wa tukio la ghafla kama hilo. Kwanza alihitaji kujua waliorusha risasi walilenga nini, ujambazi ama majibizano ya risasi baina makundi mawili. Pili alitambua jambo la muhimu zaidi ilikuwa ni kujua mahali alipo ili kujua namna ya kujiokoa endapo ingelihitajika. Wakati akiwaza hayo, viwiko vya mikono yake vilikuwa na kazi ya kuwagonga watu waliokuwa wakimkaribia, hakutaka kuzongwa, akajichagulia sehemu aliokuwa amesimama na kuimiliki kwa kuweka udhibiti madhubuti kuhakikisha hatetereshwi na watu waliotaharuki baada ya kusikia mlio wa risasi. Watu waliendelea kugongana kuwahi mlangoni na wengine wakifanikiwa kuruka madirishani, wakati huohuo mlio wa risasi nyingine ulisikika karibu kabisa na lile gari na ikafuatiwa na sauti kali ya amri, watu waliokuwa wamefanikiwa kutoka nje waliamriwa kujisalimisha na walitishiwa kuchakazwa risasi kwa yeyote ambae angelikaidi. Yule bwana akiwa na wasiwasi mkubwa, aliiinama kidogo na kutizama nje, macho yake yaliona kundi la watu zaidi ya sita wakilizunguka lile gari huku wakiwa na silaha zao mikononi, watu wengine wawili walianza kuwakusanya wale waliokuwa wakijaribu kukimbia. Wavamizi wote walikuwa wamevaa mizula iliyokuwa imefunika kuanzia kichwani hadi shingoni na kuacha pua na macho pekee, hawakuwa tofauti na ninja kwa namna walivyokuwa wamevaa.

Ndani ya dakika moja gari lilikuwa limezingirwa huku wale waliokuwa wakijaribu kukimbia na wao walikusanywa pamoja na kuombwa kutulia bila kuleta pingamizi. Yote haya yalifanyika njia ya juu kwenye daraja kubwa lililojengwa maeneo ya Tazara na, fujo za watekaji zilisababisha tafrani kubwa kwa watu waliokuwa wakitumia njia zile za juu, wengine walifanikiwa kugeuza magari yao na kurejea walikotoka, wengine walishuka kwenye magari yao na kuamua kutimua mbio kunusuru roho zao. Yaliyokuwa yakiendelea upande wa juu wa daraja yalizua tafrani nyingine kwa watu waliokuwa upande wa chini, kila mmoja alikimbia kunusuru uhai wake huku waliowengi wakiogopa mazingaombwe ya risasi kupigwa juu na kukata kona kufuata watu, hakuna mtu ambae alikuwa tayari kutolewa mfano wa aina ile ya mizangaombwe kutoka kwenye vinywa vya maofisa wa jeshi la polisi.

Kizungumkuti kilichokuwa kikiendelea hakikumfanya mgeni aliyekuwa kwenye daladala apoteze umakini, alitulia na kuwahesabu watu waliokuwa na silaha kisha akajaribu kuwaza lengo lao na kwa nini walionekana kuilenga daladala aliyokuwemo, hisia mbaya zikapita kichwani mwake na alijikuta akihema kwa nguvu pa-si na kuwa na uhakika wa mawazo yake.

“Kama walinilenga mimi, walijuaje nipo kwenye hii gari?” Alijiuliza huku akijaribu kuthaminisha mazingira ya kutorokea endapo angelipata mwanya wa kufanya hivyo.

“Tatizo hili ni daraja refu sana na lina upana mkubwa, jamaa hawatachelewa kunichakaza kwa risasi….”, Aliwaza, wakati huo masikio yake yalisikia sauti ya mamlaka ikiwaamuru waliokuwa ndani ya daladala waanze kushuka mmoja na kwa utulivu.

“Kuna nini?” Alijuliza huku akivaa begi lake mgongoni na kuungana na watu waliokuwa wameanza kushuka, wengi wao wakionekana kutetemeka na mmoja aliyekuwa amemtangulia alikuwa amelowesha nguo zake kwa mkojo, alijikojolea.

Watu wote walishuka na kupigishwa magoti chini wakiwa chini ya ulinzi mkali, baadhi yao walikuwa wakitizamwa kwa makini sana jambo lilizua maswali kwa yule jamaa, miongoni mwa waliotizamwa sana na mmoja wa wavamizi ambae alionekana kuwa kiongozi, alikuwa ni yeye.

“Mbona hawa watu wanajiamini sana wala hawaonekani kuwa na haraka kwa hiki wanachokifanya.” Aliwaza huku akiwa makini kumtizama kiongozi wa watekaji aliyekuwa ameshika kiswaswadu mkononi mwake, alionekana kutizama picha au ujumbe fulani.

“Lengo ni nini?” Alijiuliza huku macho yake yakigongana na macho ya kiongozi wa watekaji ambae alikuwa akivuta hatua zake kumfuata.

“Simama.” Jamaa alimwambia baada ya kumfikia.

Mgeni alisita kusimama, akazungusha shingo yake kutizama upande wake wa kushoto kisha upande wake wa kulia, alikuwa ni kama hana uhakika na aliyeambiwa asimame, alifanya kusudi.

“Zuki Gadu…!” Jamaa aliita kwa hasira huku akikodoa jicho la ghadhabu. Mgeni aliinua uso wake na kutizamana na kiongozi wa watekaji ambao wakati huo walikuwa wameliweka chini ya ulinzi daraja la Tazara.

“Usitake nirudie kulitaja jina lako.” Kiongozi alimfokea.

Zuki Gadu ambae alikuwa amekutana na kitu ambacho hakukitarajia, aliinuka taratibu huku akiwa ameweka mikono yake kichwani, utulivu ukiwa mkubwa.
 
Mgeni alisita kusimama, akazungusha shingo yake kutizama upande wake wa kushoto kisha upande wake wa kulia, alikuwa ni kama hana uhakika na aliyeambiwa asimame, alifanya kusudi.

“Zuki Gadu…!” Jamaa aliita kwa hasira huku akikodoa jicho la ghadhabu. Mgeni aliinua uso wake na kutizamana na kiongozi wa watekaji ambao wakati huo walikuwa wameliweka chini ya ulinzi daraja la Tazara.

“Usitake nirudie kulitaja jina lako.” Kiongozi alimfokea.

Zuki Gadu ambae alikuwa amekutana na kitu ambacho hakukitarajia, aliinuka taratibu huku akiwa ameweka mikono yake kichwani, utulivu ukiwa mkubwa.

“Nifuate!” Yule kiongozi alisema na kuanza kupiga hatua kuelekea zilipokuwa Van mbili nyeusi.

Zuki Gadu maarufu kwa jina la Miguu ya kuku alifuata nyuma taratibu huku akiwa haelewi kilichokuwa kikiendelea, watekaji wengine aliwaona walivyokuwa wakimtizama kwa umakini mkubwa.

“Lengo ni mimi, lakini walijuaje nitafika leo? Wananitakia nini?” Alijiuliza huku akiongozwa kuingia upande wa nyuma wa gari aina ya Van, alipokelewa na watu wawili waliokuwa na silaha mikononi mwao na hawakuonekana kuwa na sura za masihara, macho yao yalitangaza hatari wakati wote.
Baada ya kuingia ndani ya Van watu wengine watatu waliingia na kufanya idadi yao kuwa watano, kiongozi wao alisalia nje na mlango ukafungwa huku watu wawili wakimweka katikati yao, mwingine alimsogelea na kumwamuru anyooshe mikono yake mbele, akanyoosha na kufungwa pingu kisha akafungwa kitambaa usoni na wale jamaa hawakusema kitu, alichosikia ni gari kuwashwa na safari kuanza. Hakujua alipokuwa akipelekwa na aliamua kutulia kwa sababu hakuwa ameona nafasi ambayo ingeliweza kumuondoa kwenye mikono ya wale watu ambao hakujua walikuwa na lengo gani nae.

“Ni kwa wema au ni kwa ubaya?” Alijiuliza na hakukuwa na wa kumjibu.

“Mnanipeleka wapi?” Hatimae alipaza sauti yake na kuwauliza wale mabwana ambao wakati huo hakuwa akiwaona kwa sababu ya kufungwa kitambaa usoni.

“Usiwe na haraka mwanampotevu.” Jamaa mmoja alimjibu kwa sauti ya kebehi.

“Kwani ni dhambi mkinishirikisha tunakoenda?” Zuki alihoji kwa mara nyingine.

“Hata tukikwambia utafanya nini?” Jamaa alimuuliza.

“Nitafanya nini ikiwa nipo kwenye himaya yenu? Nahitaji kufahamu tu.” Zuki alijibu.

“Basi kuwa mpole na usubiri kuona utakapofika.”, Jamaa alimwambia huku akisikika kusogeza miguu yake.

Zuki aliamua kukaa kimya kwa kuwa hakuona kama atapewa ushirikiano aliouhitaji kutoka kwa wale mabwana. Kwa kuwa walikuwa wamemfunga uso wake ili asiweze kuona walipokuwa wakielekea, aliamua kuruhusu masikio yake yasikie kila walipokuwa wakipunguza ama kuongeza mwendo, alitumia njia ya kikomando kukariri kila kona walipokuwa wakipita bila macho yake kuwa wazi. Alijifunza njia hiyo kutoka kwa mmoja wa makomando wa jeshi la nchi fulani ambae alikuwa ni rafiki yake mkubwa, komando huyo alimwambia, wao makomando ni heri uwazibe masikio na uwaachie macho kuliko kuwafunga macho na kuwaachia masikio. Masikio yao yamebeba hisia zote na hushirikiana na ubongo kupima umbali, sauti ama mwendo wa kitu chochote kinachokuwa karibu. Zuki aliamua kutumia mbinu hiyo kupima umbali watakaokuwa wamesafiri njiani, aliinamisha kichwa chake na kuzivuta pumzi zake kisha alizishusha taratibu na kuruhusu ubongo wake ushirikiane na masikio yake.

Alikadiria umbali wa kilomita mbili tangu walipoliacha daraja lililopo Tazara hadi aliposikia gari ikipunguza mwendo na kukunja kushoto na kusimama huku ikiunguruma. Gari ilisimama kwa nusu dakika kisha ikaendelea na safari kwa mwendo wa taratibu sana, haikutembea zaidi ya mita sabini, ikasimama. Hapo masikio yake yakapata uhai, alisikia mlango wa nyuma ukifunguliwa na watu waliokuwa karibu yake wakiharakisha kushuka. Sekunde chache baadae alihisi mkono wa mtu ukimshika na kumuinua, akainuka bila kuambiwa na akaongozwa kushuka ndani ya gari. Alipoweka miguu yake chini, hazikupita sekunde sita alijikuta kapiga magoti bila kupenda baada ya kupigwa kiufundi nyuma ya magoti yake. Miguu yake ilifungwa harakaharaka na kitambaa kikatolewa usoni,mbele yake kulikuwa na watu zaidi ya kumi wakiwa wamesimama na silaha zao na wakati huu wengi wao walikuwa wamefunua nyuso zao, huku baadhi yao wakiwa wamezifunika kama walivyokuwa wakati wanamchukua mateka.

Kwa utulivu mkubwa bila kuhamaki, alizungusha kichwa chake taratibu kuyakagua mazingira aliyokuwepo, aligundua alikuwa kwenye moja ya sehemu zenye idadi kubwa ya makontena mithili ya bandari kavu, lakini ukuta uliokuwa umezunguka eneo lile ulimfanya ajue hakuwa bandarini. Akazihakikisha hisia zake kwa namna gari ilivyokuwa imetembea umbali mfupi hadi kufika pale walipokuwa.

“Hatupo mbali na Tazara.” Aliwaza huku akimtizama jamaa mmoja akimfuata pale alipokuwa.

“Bwana Zuki Gadu, tumekuleta hapa mahojiano mafupi kisha tutakuachia uendelee na shughuli zako.” Yule jamaa alimwambia huku akimvua begi lake ambalo lilikuwa mgongoni hadi wakati huo.

“Ninyi ni kina nani?” Zuki aliwauliza.

“Sisi ni jeshi la polisi na hapa upo sehemu salama kabisa.” Jamaa alimjibu huku akifungua zipu za begi lake na kuanza kukagua vilivyokuwemo.

“Polisi gani mnateka raia? Kama ni makosa nimefanya au maelezo fulani kutoka kwangu, kwa nini msingetumia njia za kawaida?” Zuki alihoji tena, yule bwana aligeuza shingo yake na kumtizama kisha akatabasamu kifedhuli.

“Njia za kawaida? Njia gani zingelifaa kwako Zuki?” Aliuliza huku akilitupa begi chini na kumsogelea.

“Unadhani ni nani asiyekufahamu? Nani asiyefahamu ujanja ulionao kuwakwepa maofisa wa jeshi la polisi?” Jamaa alimuuliza huku lile tabasamu likiwa halipo usoni mwake.

“Mimi ni raia kama raia wengine, sidhani kama ningelihitajika ningelishindwa kufika kituoni.” Zuki alimwambia.

“Wapo wa kufika ila siyo wewe. Wewe ni sawa na Njorowe, hukamatiki hata kwa pumba.”

“Kwa nini mmeamua kunikamata kwa kutumia njia hii? Kwa nini mmediriki kumuua hadi yule dereva kisa mnipate mimi?”

“Yule dereva alitumika kama sababu ya kuwatuliza watu ili upatikane kirahisi.”

“Bila kumuua mnahisi nisingelipatikana?”

“Una aakili nyingi sana, huo ungelikuwa mwanya wako wa kutorokea endapo tungeliacha watu wakimbie kwenye ile flyover.”

“Kwa hiyo mnataka nini kwangu?”

“Usiwe na haraka utaulizwa maswali unayotaka kusikia, kikubwa tunaomba ushirikiano wako.” Jamaa alimwambia huku akianza kuondoka. Sekunde chache baadae Zuki Gadu alikuwa akiinua na kukotwa kuelekea kwenye moja ya myumba zilizokuwa pale. Mlango ulifunguliwa na alibwagwa chini kama mzigo wa mihogo mibichi, vumbi lilitimka kuonesha hakukuwa na sakafu wala usafi ukiokuwa ukifanyika kwenye ile nyumba ambayo, ndani hakukuwa na kitu chochote zaidi ya kiti chakavu ambacho kisingeliweza kuhimili kubeba angalau kilo tano. Wakati Zuki akiajiandaa kuinuka, alishangaa akiinuliwa kwa nguvu na watu wawili kisha nanga ikapitishwa kwenye mnyororo mfupi unaounganisha pete mbili zilizokuwa zimeshika mikono yake, nanga ilikuwa imeungaunishwa na mnyororo mrefu ambao ulikuwa umepita kwenye kenchi za nyumba na kuangukia upande mwingine. Mtu mmoja alikimbia haraka na kwenda upande mwingine na kuanza kuvuta mnyororo ambao ikuwa ukijizungusha kwenye kenchi, nanga ikavutwa juu na kuivuta mikono ya Zuki kuelekea juu hadi aliponing'inia. Jamaa aliyekuwa akivuta mnyororo alizuia na kigingi ili mnyororo usifyatuke na kumrejesha mateka wao chini.

Maumivu makali yalipita kwenye mbavu zake huku mikono ikianza kumuuma kuliko kawaida. Dakika chache baadae yule kiongozi aliingia pale huku akiwa amekunja sura yake tofauti na mwanzo.

“Swali langu la kwanza kwako ni, Kwa nini umerejea Tanzania?”

Zuki akimtizama kwa mshangao, hakuwa ametarajia kuulizwa swali kama lile wakati kama ule.

“Yaani unaniuliza nimefuata nini nchini kwangu?” Zuki nae aliulimuuliza huku akikunja uso wake kuonesha anapitia maumivu makali.

“Jibu swali na usikulize swali.” Jamaa aliunguruma.

Zuki alitabasamu kivivu na kusema…

“Nimerejea nyumbani kwa kuwa hapa ndipo Nyumbani.”

“Kama ni nyumbani, kwa nini uliuliza mali zako na kuondoka? Ulitgemea kutokurudi, sasa kilichokurejesha ni nini?”

“Kwani siruhusiwi kuuza mali yangu? Siruhusiwi kusafiri?”

“Lakini ipo sababu iliyokurejesha, tunaomba hiyo sababu.”

“Ok, nimerudi kuendeleza biashara zangu.”

“Siyo kweli..”

“Ooh kumbe jibu mnalo? Kwa nini mwaniuliza?”

“Tunahisi ila tunahitaji utupe ukweli wako.”

“Sina ukweli wowote zaidi ya kurejea kwenye nchi yangu kuendeleza biashara zangu.”

“Biashara!...mmh! Biashara gani? Zile ulizommilikisha Dodi Danga?”

“Kwani biashara hizo ni haramu? Hazilipiwi kodi?”

“Siyo haramu..”

“Hizo ndizo zimenirejesha.”

“Kwa nini uzirudie, huko ulikoenda kumetokea nini? Umeua kama kawaida yako?”

“Huko maisha yamenishinda, nimeamua kurejea nchini kwangu.”

“Mh! Kwa nini usiseme umeua, au umeiba?”

“Inaonekana unafahamu vingi kutoka kwangu… Kwenye orodha yako uliwahi kuona jina la mtu niliyeumuua? Kati ya hao niliowaua, yupo ambae ni muungwana, raia mwema?”

“Ila bado haikuondolei ukweli kwamba, wewe ni muuaji.”

“Ni kweli na hata nikipewa tenda ya kukuua nitaanya hivyo bure kabisa.”

“Kwa nini? Nami ni dhalimu kama hao uliowauwa?”

“Good, kumbe unajua hao niwauawao ni dhalimu eeh! Basi sioni kama unatoafautiana nao na kama unatenda ya kuniua, fanya hivyo sasa ila ukiniacha, tambua utaiona pepo shetani usoni mwako.” Zuki Gadu alimpiga mkwara mzito yule bwana ambae alibaki akiwa anamtizama bila kusema neno, bila shaka alikuwa akipima uzito wa kauli alizoambiwa na macho ya msemaji hayakuonesha chembe ya utani.

“Waoh! Unaonekana u mtaalamu wa kupiga watu mikwara, ila nataka nikwambie kitu…” Jamaa alinyamaza na kuwatizama wenzake kisha akarudi kwa Zuki..

“Kwa mchezo huu, hutoboi.” Alisema huku akimtemea mate usoni na kutoa tabasamu la kukera.

“Bado naihitaji sababu ya wewe kurejea hapa mjini na wakati huu utaisema kwa zawadi ya bolibo.” Jamaa alisema na kuwageukia vijana wake, aliwapa ishara fulani na kusogea nyuma. Watatu kati yao walipiga hatua na kumfikia Zuki ambae bado alikuwa amening'nia huku miguu yake ikiwa mbali na ardhi. Wale mabwana hawakuwa na la kusema kwake bali waliamua kusema kwa vitendo, walimshushia makonde mazito kila sehemu ya mwili wake na walipochoka, walitumia vitako vya bunduki kumuadhibu bila kujali maumivu aliyokuwa akipitia. Walimpiga zaidi ya dakika saba, waliporidhika na kipigo walichompa, wakajisogeza pembeni na kumwacha akitweta kwa maumivu na hasira.

“Bado haupo tayari kusema kilichokuleta hapa mjini?” Jamaa alimuuliza baada ya kumsogelea.

“Hivi ulisema ninyi ni maofisa wa jeshi la polisi?” Zuki alimuuliza huku akipuuza kujibu alichoulizwa.

“Huamini?”

“Kwa nini mnaniumiza kwa swali lisilo na kichwa wala miguu?”

“Swali hilo lina umuhimu mkubwa sana kwetu.”

“Nani aliyewatuma kunifanyia haya?”

“Ukimjua, utakufa!”

“Nitafurahi nikifa nikiwa namjua kuliko kufa nikiwa simjui.” Zuki alisema huku akipata jibu la baadhi ya maswali aliyokuwa akijiuliza, alitaka kujua wale watu walikuwa wamemfikisha pale kwa upelelezi wao au walitumwa na mtu. Jibu alilipata baada ya kuuliza swali ambalo aliyeulizwa hakutambua mtego wake, alijibu bila kuelewa amejibu swali ambalo pengine hakutakiwa kulijibu wakati kama ule, ila kwa kuwa ninge huja yakishatokea, hakujua umuhimu wa jibu lake kwa mateka wake.

“Wanaume wanaadhibiana kwa kupimana ubavu, mbona mnanifunga? Mnajiamini nifungueni niwape majibu ya maswali yenu.” Zuki aliamua kumkera yule jamaa, alifanya vile ili kujiweka mbali na swali alilokuwa akiulizwa.

“Unahisi unaogopwa? Kwa kipi?” Jamaa alijitutumua kuuliza huku dhahiri akionekana kuchukizwa na lugha ya kebehi kutoka kwa Zuki.

“Kama hamniogopi, kwa nini mnanifunga ingali mpo wengi na silaha mikononi?”

“Unahisi tukikufungua utaweza kupambana?”

“Jaribu kunifungua..” Zuki alimjibu, jamaa akawapa ishara vijana wake, mmoja akakimbia na kwenda kufyatua mnyororo na ukaserereka kwa kasi kitendo kilichomfanya abwagike chini mithili ya chatu aliyeteleza mtini. Vumbi zito lilitimka huku wale watekaji wakisikika wakitoa vicheko vya kebehi na ujivuni.

“Nyanyuka upambane bwana Miguu ya kuku.” Kiongozi wa watekaji waliojinasibu kuwa ni maofisa wa jeshi la polisi, alimwambia huku akimwinua na kumpigisha magoti. Wengine walitengeneza duara na kumzunguka.

"*********

Tukutane baadae
 
Mie sijasoma mpaka mwisho ndugu.
Ila nimejikuta nacomment tu.
Punguza mhaho boss! Tunashauriwa kuchangia kile tukionacho, kukifahamu... Ila kukurupuka na kuandika vitu ambavyo huna hakika navyo, jukwaa lilisilohusiana na uandikacho, ni kuzua taharuki tu kwa wenye uvivu wa kusoma, ambao watakimbilia komenti yako na kujaji Uzi mzima ambao hauhusiani...
 
Punguza mhaho boss! Tunashauriwa kuchangia kile tukionacho, kukifahamu... Ila kukurupuka na kuandika vitu ambavyo huna hakika navyo, jukwaa lilisilohusiana na uandikacho, ni kuzua taharuki tu kwa wenye uvivu wa kusoma, ambao watakimbilia komenti yako na kujaji Uzi mzima ambao hauhusiani...
Mambo yasiwe mengi mkuu.
 
Hii hadithi inaonekana tamu sana,endelea kutupia sura nyingine
 
Kudo mpaka mwisho hii au ipo sokoni?kama ipo sokoni funguka tukuchangie mzee,vya bure vinaumiza!
 
Back
Top Bottom