DC wa Mbinga ahojiwa matumizi ya bilioni 1.5/-

NGULI

JF-Expert Member
Mar 31, 2008
4,803
637
Na Mwandishi wetu

WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amemwagiza Mkuu wa Wilaya ya Mbinga, Kanali Mstaafu Edmund Mjengwa afuatilie na kuhakiki (value for money) matumizi ya Sh bilioni 1.5 za ujenzi wa mabanio na mifereji ya umwagiliaji katika miradi 19 lakini matokeo ya miradi hiyo ni hafifu.

Akizungumza mara baada ya kupokea taarifa ya kilimo ya wilaya hiyo juzi, Waziri Mkuu alisema haridhishwi na maelezo yaliyotolewa kwenye taarifa hiyo kuhusu kazi ya kukamilisha ujenzi wa miradi hiyo ikilinganishwa na hali halisi ya eneo linalotumika kwa umwagiliaji maji.

“Nimeona ripoti yenu kuwa mmetumia Sh bilioni 1.469 kati ya mwaka 2005 na sasa, fedha iliyowekezwa ni nyingi lakini eneo linalotumika kwa kilimo cha umwagiliaji ni dogo sana, ni kwa nini hakuna mabadiliko? DC nataka ufuatilie hizo skimu za umwagiliaji na ujiridhishe juu ya matumizi ya fedha hizi,’’ alisema Waziri Mkuu.

Waziri Mkuu alihoji iweje eneo la wilaya linalofaa kwa umwagiliaji ni hekta 15,224 lakini linalotumika ni hekta 418 tu ambalo ni sawa na asilimia 2.7 ya eneo lote linalofaa kwa kilimo hicho.

“Kama mmewekeza na kazi imekamilika ni kwa nini hali haibadiliki au ni miundombinu hewa?,’’ alihoji Waziri Mkuu.

Akizungumzia kuhusu matumizi ya zana bora za kilimo, waziri mkuu alimtaka mkuu huyo wa wilaya na watendaji wengine wa wilaya kukaa pamoja na kuongeza idadi ya matrekta makubwa kwa sababu moja waliloliagiza katika mwaka huu wa fedha halitoshi.

“Mmesema hali ya Mbinga ni milima mingi kwa hiyo matrekta madogo hayafai lakini hata hilo trekta moja mliloagiza kwa wilaya nzima litafaa nini? Wasaidieni wananchi kuibua miradi katika DADPS kwani hatuwezi kwenda kwa hiyo kasi ya kinyonga... Huu ni wakati wa kuongeza maeneo ya kilimo kwa kufuata kanuni bora na kutumia zana za kisasa,’’ alisisitiza.

Alisema: “Si kila mkulima mdogo anaweza kumudu bei ya trekta kubwa kwa hiyo inabidi katika programu zenu za kuweka vituo vya taaluma vya kata muongeze idadi kutoka vinne mlivyopanga katika mwaka ujao wa fedha, ili walau kila kata iwe na trekta moja,’’ aliongeza.

Wilaya ya Mbinga ina kata 37, tarafa sita na vijiji 207.

Pinda alionya kuwa kwenye maeneo ambayo yanaweza kulimwa sesa, bado wanaweza kuagiza matrekta madogo (Power Tillers) ili muwasaidie wananchi kulima eneo kubwa kwa muda mfupi. “Hizo tatu mlizopanga kununua ni chache sana kwani najua watu wa Mbinga ni wachapa kazi, wanachohitaji wao ni usimamizi mzuri tu.’’

Waziri Mkuu pia amekagua shamba la mahindi la majaribio ya matumizi ya mbolea mbalimbali katika kurutubisha ardhi katika kijiji cha Mtama, kukagua mtambo wa kukoboa kahawa katika Kijiji cha Utiri na kutembelea kituo cha utafiti wa Kahawa cha TACRI katika kijiji cha Myangayanga.

Ziara ya Waziri Mkuu katika mikoa ya Ruvuma, Kigoma na Rukwa ni mfululizo wa ziara zake za kufuatilia maagizo ya kilimo yaliyofikiwa katika mkutano alioutisha Oktoba mwaka jana kuweka malengo ya kuinua kilimo katika mikoa sita ya Morogoro, Iringa, Mbeya, Ruvuma, Kigoma na Rukwa.
 
Mh. Pinda zinakushtua LEO Tsh. 1.5 billion zilizopigwa toka mwaka 2005 mpaka sasa! Kwa nini hukufuatilia kipindi chote hicho tangu ukiwa waziri - TAMISEMI (2005 mpaka Feb 2008)??? Au ndo mmejenga ukuta badala ya madaraja mbele ya nyuso zenu??
 
Back
Top Bottom