Dawa za makalio, matiti, zauzwa kama njugu Dar...

Sinoni

JF-Expert Member
May 16, 2011
5,530
9,140
Dar es Salaam. Hakuna shaka kwamba sasa kuna ongezeko kubwa la matangazo ya dawa za kurekebisha maumbile, hasa za kuongeza ukubwa wa makalio, maziwa ya mwanamke na nyonga.
Mitandao ya kijamii imekuwa kinara katika kutoa matangazo ya bidhaa hizo zinazodaiwa na wauzaji kuwa zinaboresha mvuto wa mwanamke.
Matangazo hayo hujumuisha picha zinazoonyesha wanawake wasio na makalio, matiti au hips kubwa kabla ya kutumia na picha zinazoonyesha wamebadilika baada ya kuzitumia.
Watu maarufu, hasa kwenye tasnia ya sanaa ndiyo wamekuwa madalali wakubwa wa bidhaa hizo, wakitumia kurasa zao za mitandaoni kuzitangaza kwa mbinu tofauti. Wingi wa matangazo hayo unakupa picha kuwa bidhaa hizo, ambazo Serikali imekuwa ikijitahidi kuelimisha watu madhara yake, zinapatikana kirahisi na kwenye maduka au ofisi ambazo mhitaji anaweza kufika bila wasiwasi.
Lakini si hivyo. Biashara hizo sasa zinauzwa kama vipisi vya bangi; zinauzwa kwa ujanja na kwa siri kubwa, Mwananchi imefuatilia na ina habari kamili.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa wateja wakubwa wa bidhaa hizo ni wasichana ambao wameridhishwa na jinsi biashara hiyo inavyofanya kazi. Eneo la Kariakoo, ambalo lina biashara za kila aina, ni moja ya vituo vikuu vya wauzaji wa dawa hizo ambao ni rahisi kwao kukufuata ulipo wakupe dawa hizo, lakini hawaruhusu uende kwenye ofisi zao kwa maelezo kuwa kazi yao ina changamoto nyingi.
Katika mawasiliano baina ya waandishi wa gazeti na wauzaji wa dawa hizo maeneo ya Kariakoo, ilibainika kuwa biashara hiyo si ya wazi.
Mwandishi aliyepata namba ya simu ya muuzaji dawa hizo kwenye moja ya matangazo na kumpigia, alijaribu kumshawishi mfanyabiashara huyo amueleza zilipo ofisi zao, lakini alikataa katukatu.
Mazungumzo yalionyesha wazi kwamba hakutaka mwandishi afike dukani kwake kwa kuhofia kuwa anaweza kuwa mbaya kwake na mazungumzo na mtu huyo aliyejitambulisha kwa jina la Dk James yalikuwa hivi:
Mwandishi: Habari ninahitaji huduma katika duka lako nipo hapa Msimbazi Polisi
Dk James: Unahitaji dawa gani? Nitajie bei yake halisi?
Mwandishi: Hapana nahitaji kufika eneo ulipo ili niangalie na bidhaa nyingine.

Dk James: Ukielekezwa dukani ukafika hapa na ukakuta bei tofauti? Si tatizo, nimekuomba unitumie meseji ili unachokitaka nikuambie ni kiasi gani cha fedha. Kila sehemu kuna utaratibu wake, jaribu kuwa mwelewa huwezi kujua nakuuliza hivi kwa sababu gani. Sisi tunakutana na changamoto nyingi katika biashara yetu.
Mwandishi: Ninataka dawa ya kuongeza unene wa miguu.
Dk James: Sawa hiyo inauzwa Sh100,000 kwa dawa ya mafuta na ile ya vidonge ni Sh200,000. Hii unaitumia kupaka miguuni lakini hata kwenye hips na makalio pia unaweza kuitumia ukawa na shepu nzuri kwa hiyo kama unahitaji sema uletewe ulipo.
Mwandishi: Nipo hapa Msimbazi nielekeze dukani. Pia, nataka kuonana na daktari anipe maelekezo zaidi na anisaidie kujibu maswali yangu.
Dk James: Sawa kama unahitaji kuongea na mimi itakubidi usubiri kama dakika 15 nitakuwa nimefika hapo tuweze kuzungumza.
Baada ya dakika 15 kupita niliwasiliana naye kwa mara nyingine na safari hii alinifahamisha kwamba vijana wawili wamfuate ili wampeleke dukani, lakini mwandishi aliondoka kabla ya kufika.
Katika mazungumzo ya awali, Dk James alisema pia anazo dawa za kupaka za kutengeza nyonga na makalio kwa Sh100,000 na vidonge ni Sh200,000. Kuongeza hamu ya kula ni Sh120,000.
Alisema pia anayo dawa ya kuongeza unene na uzito wa mwili ambazo ni Sh120,000 kwa dawa ya maji na vidonge Sh100,000, huku dawa ya kupunguza unene ikiuzwa kwa Sh1,500,000.
“Ninazo dawa za kuondoa kitambi na nyama za kiunoni, kuondoa mvi zisirudi tena, kuongeza maumbile ya kiume na nguvu kwa njia ya kupaka mafuta na vidonge maalum vya kulainisha ngozi na kuondoa michirizi na mipasuko mwilini,” alisema ‘daktari’ huyo. Mfanyabiashara huyo alisema pia anazo zenye uwezo wa kupunguza au kuongeza maziwa na kuyasimamisha, kurefusha nywele na kuzuia kukatika ovyo na kuondoa makunyanzi yani ngozi ya uzee.

Mmoja kati ya wateja wa Dk James ambaye hakutaka kutajwa jina lake alisema ametumia bidhaa zake na amefanikiwa, huku akiweka bayana kuwa daktari huyo hupendelea kukutana na wateja wake barabarani na si katika kituo chake cha Kariakoo.
“Nilinunua dawa kwa ajili ya kuongeza ukubwa wa matiti, nimefanikiwa. Kiasi ambacho yamefikia, nimeniridhika na hapo nimeacha kutumia dawa hiyo,” anashuhudia msichana mmoja ambaye picha yake iko kwenye mtandao wa Dk James. “Kwa sasa nina mpango wa kurudi tena kwake ili nipate dawa ya kuongeza makalio na kunenepesha miguu ili nivae vimini.”

Dawa nyingine ambayo wengi wamekuwa wakiitumia inaitwa Buchi Rash, ambayo kwa mujibu wa Dk James inapunguza kitambi na uzito. Akizungumza na Mwananchim muuzaji anayefahamika kwa jina la Nahydah Allaraqya, Buchi Rash, alisema inatengenezwa hapa nchini kwa kutumia mitishamba na inauzwa Sh45,000 kwa dawa ya kupunguza kitambi na Sh55,000 kwa dawa ya kupunguza mwili.
“Matumizi yake ni wiki moja au siku 10 na inatagemea na unene wa mtu kama wewe. Kama ni mnene sana unaweza kutumia dozi mbili na kuendelea, Inategemea unataka kupungua kilo ngapi na ukifikisha zile unaacha unaanza mazoezi na diet,” alisema Nahdah ambaye duka lake lipo Msasani Samaki jijini Dar es Salaam.
“Dawa zetu zimedhititishwa na Mkemia Mkuu wa Serikali kwa kutupa namba 565.”

Mwigizaji wa filamu, Salma Jabu, ambaye ni maarufu kwa jina la Nisha, anauza dawa za kupunguza unene na vitambi pia, lakini dawa zake hajazipa jina na wala haijaeleweka sehemu maalum anayouzia zaidi ya mtandaoni.
Nisha alisema bidhaa hizo zinazotengenezwa kwa mitishamba zinatoka China na huja kutokana na maombi maalum.

Alisema hajazipa jina kwa kuwa anahofia watu wengine wanaweza kuiga mawazo yake na kuharibu biashara.
“Tunauza Sh180,000 tunakuletea ulipo,” alisema akiongeza kuwa mabadiliko yanaonekana ndani ya wiki moja. “Kuna vidonge na majani. Unachemsha maji unachukua jani moja unaweka kwenye kikombe na baada ya dakika tatu unachukua vidonge viwili unakunywa pamoja na yale maji, jioni pia unakunywa.”

Mamlaka husika zinasemaje
Pamoja na wauza dawa hizo kudai kuwa Mkemia Mkuu wa Serikali ameziidhinisha baada ya kuzipima, ofisi hiyo imekanusha vikali.
Mkemi Mkuu wa Serikali, Profesa Samwel Manyele alisema ofisi yake haifanyi kazi ya kuidhinisha dawa zozote, bali kuthibitisha usalama wake kwa mtumiaji baada ya kupelekewa na Mamlaka ya Chakula na dawa (TFDA) ambayo hutaka zichunguzwe kabla ya kuruhusu zianze kutumika nchini.
“Mkemia Mkuu hathibitishi dawa wala kipodozi tunachofanya ni kuangalia kama dawa zina madhara kwa matumizi ya binadamu. Walio na jukumu la kuruhusu itumike au ni TFDA ambao wao ndiyo mara nyingi hutuletea sampuli kwa ajili ya uchunguzi,” alisema.

Hata TFDA ilikanusha kuruhusu kutumika kwa dawa hizo au kuzithibitisha, na badala yake ikaeleza kuwa ni hatari kwa watumiaji.
Ofisa uhusiano wa TFDA, Gaudensia Simwanza alisema hakuna hata kipodozi kimoja au dawa inayotajwa kuongeza makalio wala matiti ambayo kimekaguliwa na kuthibitishwa kuwa ni salama kwa matumizi ya binadamu.
Alisema bidhaa hizo zimekuwa zikiuzwa kwa magendo na mara kadhaa mamlaka hiyo imekuwa ikijaribu kuwasaka wauzaji bila mafanikio.

“Matangazo hayo tunayaona kwenye mitandao na tulichoabini vipodozi hivi vinauzwa kwa siri mno. Tunajaribu kuwafuatilia lakini mwisho wa siku hatupati vyanzo vyake halisi. Zinaingizwa hapa nchini kwa njia za panya,” alisema. Kwa mujibu wa Simwanza, vipodozi hivyo vina madhara makubwa kwa watumiaji ikiwamo kusababisha ugonjwa wa saratani na wakati mwingine kuharibu maumbile tofauti na matarajio ya mtumiaji.

“Kuna wakati mtu anaweza kutumia kwa lengo la kuongeza makalio, halafu matokeo yasiwe mazuri. Upande mmoja wa makalio unaweza ukaongezeka, mwingine ukabaki kama lilivyo na zaidi ya hapo anaweza pia kupata saratani. Hizi dawa si nzuri.”
Alifafanua kuwa TFDA inaendelea kutoa elimu kwa jamii, hususan makundi ya vijana ambayo ndiyo waathirika wakubwa wa vipodozi hivyo, kwa kuwaeleza athari zake.
Awali, biashara hiyo haikuwa ikifanywa kisiri na dawa za kuongeza makalio zilipata umaarufu, huku wasichana walioonekana wana nyonga isiyo ya kawaida wakielezewa kuwa wana “makalio ya kichina”.
Hata hivyo, TFDA ilianza kampeni kali ya kupambana na wauzaji na kusababisha biashara ya dawa hizo ipotee kabla ya wauzaji kugundua mbinu hiyo mpya ya kuuza kwa kumfuata mteja.
 
Kucha bandia, kope bandia, matiti bandia, nywele bandia, mapaja bandia, makalio bandia, rangi bandia dah! Hata ukikutana nao unapulizwa na mchanganyiko wa harufu za madawa mbalimbali waliyopaka, namna hii niliwahi kumsahau Mwanaidi wangu
 
Kucha bandia, kope bandia, matiti bandia, nywele bandia, mapaja bandia, makalio bandia, rangi bandia dah! Hata ukikutana nao unapulizwa na mchanganyiko wa harufu za madawa mbalimbali waliyopaka, namna hii niliwahi kumsahau Mwanaidi wangu
Its because people are being loved when they are fake and being hated when they are real.
 
Kucha bandia, kope bandia, matiti bandia, nywele bandia, mapaja bandia, makalio bandia, rangi bandia dah! Hata ukikutana nao unapulizwa na mchanganyiko wa harufu za madawa mbalimbali waliyopaka, namna hii niliwahi kumsahau Mwanaidi wangu
tunautaka utandawazi, ila utandawazi haututaki ...
 
Back
Top Bottom