Daktari: Serikali inahusika ARV bandia

sir.JAPHET

JF-Expert Member
May 18, 2012
699
133
ATAKA IJIHOJI IJE NA MAJIBU, AELEZA ATHARI ZAKE, NAIBU WAZIRI ATAKA IPEWE MUDA ZAIDI KUCHUNGUZA TATIZO
Elias Msuya
WAKATI utata ukiendelea kugubika usambazwaji wa dawa bandia za kupunguza makali ya virusi vya Ukimwi (ARV), daktari katika Kitengo cha Ukimwi, Dar es Salaam ameitaka Serikali kujichunguza yenyewe, kwa kuwa dawa hizo hazisambazwi na watu binafsi.

Daktari huyo, Charles Lyimo ambaye ni Mkuu wa Idara ya Dawa katika Kitengo cha Ukimwi Hospitali ya Amana, alisema jana kuwa hakuna sababu ya kutafuta mchawi kwenye tatizo hilo; Serikali inahusika.

“Siyo rahisi kujua kwamba hii ni dawa halisi au bandia, lakini tuna uhakika na dawa tunazotumia kwa sababu zinaagizwa na Serikali peke yake. Hakuna mtu binafsi aliyepewa tenda (zabuni) ya kuziagiza,” alisema Dk Lyimo.
Dk Lyimo alisema awali, dawa hizo zilikuwa zikiagizwa kutoka Marekani, lakini baadaye utaratibu huo ukabadilishwa na zikaanza kuagizwa kutoka India.

“…(Serikali) inapeleka oda kiwandani na ndiyo inayozigawa dawa hizo na kuzisambaza kupitia Bohari Kuu ya Dawa (MSD). Lakini pia dawa hizi zinatengenezwa Arusha kwenye kiwanda kilichopewa kibali na Serikali,” alisema Lyimo na kuongeza:

“Kama kuna dawa bandia, basi Serikali ijihoji. Kwanza mimi ninaposikia habari hizo huwa nacheka tu kwa sababu tangu sakata hili limeanza, wizara inajigongagonga tu… hawatuhusishi wala kutuuliza… na sisi tunaendelea tu kugawa dawa…”

Alipotakiwa kueleza tofauti iliyopo kati ya ARV zinazotengenezwa India na zile za Tanzania, Dk Lyimo alisema: “Ni sawa na dawa za kutuliza maumivu za Panadol na Asprin. Kuna wagonjwa wenye vidonda vya tumbo hawawezi kutumia Asprin, hawa wanatumia Panadol. Vivyo hivyo kwenye Ukimwi kuna wagonjwa ambao wanapata madhara wanapotumia dawa za India. Hawa sasa tunawapa dawa za Tanzania.”

Dk Lyimo alisema mgonjwa anabadilishiwa ARV kulingana na jinsi zinavyompenda au kumdhuru na ikifikia hapo, mgonjwa huyo anahitaji uangalizi wa karibu wa daktari.

“Kuna dawa zinazonyonya damu, nyingine zinakula nyama na nyingine zinaleta maruweruwe na njozi mbaya. Kwa hiyo tukiona athari hizo tunambadilishia mgonjwa dawa hizo,” alisema Dk Lyimo.
Akizungumzia madai hayo, Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid alikiri kuwa ni Serikali pekee inayoagiza dawa hizo kwa ajili ya wananchi wake na akataka jamii ifahamu pia kuwa ni Serikali hiyohiyo iliyogundua tatizo hilo na kuanza kulifanyia kazi.

“Ni kweli Serikali pekee ndiyo inayoagiza dawa na Serikali hiyohiyo ndiyo iliyounda TFDA (Mamlaka ya Chakula na Dawa), ambayo kwa kazi nzuri imefanikiwa kugundua kuwapo kwa dawa bandia. Kwa hiyo tuwape muda wa uchunguzi,” alisema.

Hata hivyo, hakusema itaichukua TFDA muda gani kumaliza kazi hiyo akisema: “Hii ni kazi ya kitaalamu na inayohusisha mambo mengi. Siyo kwamba muda haujulikani, ripoti hiyo bado iko kwenye uchunguzi na uchunguzi unachukua muda mrefu… Tuwape muda wataalamu.”

Hata hivyo, mmiliki wa Kiwanda cha Tanzania Pharmaceutical Industries Ltd (TPIL) kinachotengeneza dawa hizo, Zarina Madabida alikaririwa na gazeti hili jana akisema kuwa ndicho kilichogundua kuwapo kwa dawa hizo na kutoa taarifa kwa TFDA kikiomba iingilie kati ili kuondoa dawa hizo bandia kwenye mzunguko.

Athari za ARV bandia
Kuhusu athari za dawa bandia, Dk Lyimo alisema mgonjwa anayezitumia hana tofauti na mtu anayekula unga ambao kimsingi hauwezi kutibu maradhi.

“Dawa bandia siyo lazima iwe na madhara kwa mgonjwa. Cha msingi hapo ni kwamba mgonjwa anayetumia ARV bandia anakuwa tu hajatumia dawa kwa muda unaotakiwa,” alisema na kuongeza:

“Mtu anaweza kutumia tu unga kutengeneza vidonge kisha akaweka nembo kwenye makopo na kuziuza kama ARV, hii ni kuwalaghai wagonjwa.”

“Mtu asipotumia dawa, kama CD4 zake zilikuwa zimeongezeka hadi kufikia 500, hushuka tena na wale wadudu hupata nguvu ya kushambulia vile virutubisho vya seli. Kwanza wadudu wale huwa wajanja zaidi na wanaweza kujibadilisha kama kinyonga. Hivyo mgonjwa hurudiwa na magonjwa nyemelezi… ni hatari mno.”

Dk Lyimo alisema kwa wastani hupokea kati ya wagonjwa 250 hadi 300 kwa siku hospitalini hapo na wote huja kuchukua dawa ili kuendelea na dozi zao. Alisema kutokana na usugu wa wadudu hao na tabia yao ya kubadilika badilika, dawa hizo ziko katika mchanganyiko wa makundi matatu yanayotosha kupambana nao.

“Kwa kawaida mwanadamu akiwa mzima ana CD4 1,500. Lakini akiathiriwa na Ukimwi zinapungua kwa sababu wale wadudu wanapoingia hushambulia virutubisho (membrane) na seli za kinga ndani ya damu.

“Hujipenyeza kwenye seli hizo na kujibadilisha na kufanana na seli hizo na huko ndiko wanakozaliana. Mtu anapotumia ARV, huvilewesha virusi na kuvifanya vishindwe kuzaliana, hivyo hula na vikishiba vinalala tu, lakini havifi,” alisema.

Alisema kutokana na gharama kubwa ya dawa hizo, wagonjwa hushauriwa kutumia ARV wakiwa na CD4 350, hata hivyo, wapo wanaoshindwa kuvumilia hasa kutokana na kuandamwa na magonjwa nyemelezi hata wanapokuwa na CD4 600.
 
Back
Top Bottom