CCM yaingiwa hofu Arumeru Mashariki

EasyFit

JF-Expert Member
Jul 4, 2011
1,269
1,082
Yaomba NGOs zisitoe elimu ya uraia

Kisa? Zinaegemea vyama vya upinzani


Chama cha Mapinduzi (CCM) kimeanza kuonyesha hofu juu ya uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Arumeru Mashariki, baada ya Katibu wake wa Halmashauri Kuu (NEC), Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, kuitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).

Kudhibiti tabia ya baadhi ya asasi za kiraia ambazo amedai badala ya kufanya kazi ya kutoa elimu ya mpigakura zimekuwa zikitumia mwanya huo kufanya kampeni.

Nape alisema hayo wakati akichangia mada kuhusu maandalizi ya uchaguzi mdogo wa jimbo hilo na udiwani katika kata nane, iliyowasilishwa na Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, katika mkutano kati ya Tume hiyo na viongozi wa vyama vya siasa uliongozwa na Mwenyekiti wa NEC, Jaji Mstaafu, Damian Lubuva.

Nape alisema kuna baadhi ya asasi ambazo zimekuwa zikitumia jina la kutoa elimu ya mpigakura, lakini badala yake zimekuwa zikitumia mwanya huo kufanya kampeni.

"Kama jambo hili halitadhibitiwa linaweza kusababisha kutupeleka kwenye kampeni kabla ya wakati," alisema Nape.
Hata hivyo, akijibu hoja hiyo, Kamishna wa NEC, Profesa Amon Chaligha, alisema hawaamini madai hayo ya Nape kwani wanachojua ni kwamba, kinachofanywa mfano na madhehebu ya dini ni kuhamasisha waumini wao kwenda kupiga kura siku ya uchaguzi na si vinginevyo. "Hawaendi kusema nendeni mkampigie kampeni mtu fulani," alisema Profesa Chaligha.

Wakati Profesa Chaligha akisema hivyo, viongozi wa vyama vya siasa wamepinga uamuzi wa NEC kuruhusu utoaji wa elimu ya mpigakura kupitia matangazo yatakayosomwa kwenye nyumba za ibada za waumini katika kila eneo unakofanyika uchaguzi.

Katibu Mkuu wa AFP, Rashid Rai, alisema kuruhusiwa kwa suala hilo ndiko kulikotoa mwanya kwa viongozi wa madhehebu moja kufanya kampeni kwa kuwataka wananchi wasikichague chama kimoja cha siasa katika kampeni za uchaguzi mdogo wa ubunge, uliofanyika katika Jimbo la Igunga, mkoani Tabora, mwishoni mwa mwaka jana.

TLP WAPINGA
Katibu Mwenezi wa TLP, Dominata Rwechungura, alisema iwapo utoaji elimu ya mpigakura wa aina hiyo utaruhusiwa, adui anaweza kupitia hapo na kuvuruga uchaguzi na kushauri kufikiriwa upya suala hilo kwa kuondoa utaratibu huo wa utoaji elimu ya mpigakura, badala yake viongozi wa dini waruhusiwe tu kuwatangazia waumini wao siku rasmi ya kupiga kura.

DEMOKRASIA MAKINI
Naibu Katibu Mkuu wa Demokrasia Makini, Nuru Kimwaga, alisema haoni sababu ya kuruhusu utaratibu huo wa utoaji elimu ya mpigakura kwa kuwa nchi imekwishapanga siku nyingi kwamba, siasa zisihusishwe kwenye dini.
Alisema athari ya kuhusisha siasa kwenye dini aliishuhudia katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 katika Jimbo la Gairo, mkoani Morogoro.

Kimwaga alisema katika uchaguzi huo, baadhi ya waumini wa dini ya Kiislamu walishuhudiwa wakiwahamasisha wananchi kumchagua aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Jakaya Kikwete kwa madai kwamba ni mwenzao na kuwazuia kumchagua aliyekuwa mgombea wa kiti hicho kupitia Chadema, Dk. Willibrod Slaa, kwa madai kwamba, ni kafiri.

"Hata mimi ambaye ni Muislamu, niligombea ubunge katika jimbo hilo kupambana na (Ahmed) Shabiby, katika urais nilimfanyia kampeni Dk. Slaa kwa kuwa chama changu hakikusimamisha mgombea urais, waliniita kafiri," alisema Kimwaga.

CHADEMA WEKA DINI MBALI
Naye Victor Kimesera kutoka Chadema, alisisitiza kutaka mambo ya dini kuwekwa mbali na siasa kwa maelezo kwamba, Tanzania haina dini.

Rais wa Tadea, John Chipaka, alisema pamoja na umuhimu wa elimu ya mpigakura, ana wasiwasi eneo la ibada kutumiwa kutoa elimu hiyo. Hakufafanua.

JAJI LUBUVA MIPAKA MUHIMU
Akijibu hoja hizo, Jaji Lubuva alisema ni jambo la kuzingatiwa kwa vile linaipa angalizo na tahadhari Tume yake na pia linaonyesha haja kwa asasi za dini kuwekewa mipaka katika mchakato wa uchaguzi.

BORESHA DAFTARI LA WAPIGAKURA
Mkurugenzi wa Masuala ya Bunge na Halmashauri wa Chadema, John Mrema, alionyesha masikitiko yake kwa vyama kwenda kwenye uchaguzi mdogo jimboni humo bila ya kuwapo uandikishaji mpya wa wapigakura.

Alisema uandikishaji mpya wa wapigakura ni muhimu kwa vile idadi ya wapigakura imeongezeka, kwani wakati wa uandikishaji uliofanyika mwaka 2010, kulikuwa na wananchi waliokuwa chini ya umri wa miaka 18 ambao sasa wametimiza umri huo unaowaruhusu kupiga kura.

Pia alisema kuna waliopoteza kadi za kupiga kura kwa njia mbalimbali, ikiwamo baadhi kuzitumia kama dhamana mojawapo ya kuchukulia mikopo, hivyo kwa kutokuwa na kadi hizo na kutokuwapo uandikishaji mpya, kunawafanya wapoteze haki yao ya kupiga kura.

Vilevile, alisema katika Jimbo la Arumeru Mashariki kuna vyuo vitatu vimefunguliwa, hivyo kuongeza idadi ya wapigakura, lakini kutokana na kutokuwapo uandikishaji mpya wa wapigakura, kutawafanya wakose haki yao ya kupiga kura.

Alisema kila mwaka NEC imekuwa ikisema itarekebisha baadhi ya kasoro zinazojitokeza kwenye Daftari la Kudumu la Wapigakura, hasa kwenye kipindi cha uchaguzi, lakini hakuna utekelezaji.
Alisema hata ukiangalia Daftari la Kudumu la Wapigakura wa Jimbo la Igunga la mwaka 2010 na lile la 2011 na kusema lina tofauti kubwa mno.

VITUO KUWA MBALI
Awali, Nape alishauri vituo vya kupiga kura kuwekwa karibu na wananchi akisema tatizo la vituo hivyo kuwa mbali na wananchi ndilo ambalo limekuwa likisababisha idadi kubwa ya wananchi kushindwa kupiga kura.

Akijibu hoja hiyo, Profesa Chaligha alisema ni kweli kumekuwa na malalamiko ya vituo kuwa mbali na wapigakura na kusema malalamiko hayo waliwahi kuyashuhudia katika Wilaya ya Mpanda, mkoani Rukwa.

Hata hivyo, alisema suala hilo linaungwa mkono na sheria, lakini akasema wanalifanyia kazi.Kuhusu uandikishaji mpya wa wapigakura alisema jambo hilo haliwezekani kwa sasa na kusisitiza kuwa watakaoruhusiwa kupiga kura ni wale tu waliomo kwenye Daftari la mwaka 2010 na kusisitiza kuwa jambo hilo ni la kisheria.

Awali, akiwasilisha mada hiyo kwenye mkutano huo, Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, Julius Mallaba, alisema kuanzia Februari 19 vifaa vya uteuzi vilianza kusafirishwa ili kuhakikisha kuwa vinafika kunakohusika kabla ya siku ya kutoa fomu za uteuzi kwa wagombea udiwani Februari 21 na kwa wagombea ubunge Februari 24.

Alisema kati ya vyama 19, ni vitano tu; AFP, APPT-Maendeleo, Chausta, NCCR-Mageuzi na UDP, havijasaini marekebisho ya maadili ya uchaguzi na kuvitaka viwe vimefanya hivyo ifikapo Machi 2, mwaka huu, vinginevyo havitaruhusiwa kushiriki kampeni za uchaguzi.

TENDWA AJICHIMBIA ARUMERU
Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa, amejichimbia katika Jimbo la Arumeru Mashariki kwa lengo la kutoa elimu ya sheria mpya ya gharama za uchaguzi ili wapigakura wasipewe rushwa.

Msajili Msaidizi wa Ofisi ya Msajili, Ibrahim Mkwawa, alisema jana jijini Dar es Salaam kuwa wamejipanga sawa sawa katika ofisi zote za Kanda kwa ajili ya kutoa elimu ya umma kuhusu sheria ya gharama za uchaguzi katika Jimbo la Arumeru Mashariki na Kata nane ambazo zinatarajia kufanya uchaguzi wa madiwani.

Alisema Tendwa ameondoka kwenda Arumeru kwa ajili ya kuongoza utoaji elimu kwa wapigakura kuhusiana na sheria hiyo ili kuhakikisha hawarubuniwi kwa kupewa rushwa.

Uchaguzi huo unaotarajiwa kufanyika Aprili mosi mwaka huu unafuatia kifo cha mbunge wake, Jeremiah Sumari (CCM), kilichotokea baada ya kuugua kwa muda.

Huu utakuwa ni uchaguzi mdogo wa ubunge wa tatu kufanyika baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010. Wa kwanza ulikuwa ni Igunga ambako CCM na Chadema walichuana kwa karibu sana, mgombea wa CCM, Dk. Peter Dalali Kafumu alishinda. Wa pili ulikuwa ni kujaza nafasi ya Baraza la Wawakilishi la Uzini, ambako mgombea wa CCM, Mohamed Raza, alishinda.

Imeandikwa na Samson Fridolin, Muhibu Said na Jimmy Mfuru. NIPASHE
 
Mbona Igunga mashehe walikuwa wanatangaza misikitini msimchague fulani hatukusikia malalamiko ya aina hii?

Nakumbuka Bakwata waliitisha mkutano na waandishi wa habari wakasisitiza hilo na tume ya uchaguzi ilikuwepo.
 
Mbona Igunga mashehe walikuwa wanatangaza misikitini msimchague fulani hatukusikia malalamiko ya aina hii?

Nakumbuka Bakwata waliitisha mkutano na waandishi wa habari wakasisitiza hilo na tume ya uchaguzi ilikuwepo.

Mbona wewe ulikuwa wa kwanza kulalamika hapa?
 
Easily, easily diverted from right focus to arumeru, easily
 
Mbona Igunga mashehe walikuwa wanatangaza misikitini msimchague fulani hatukusikia malalamiko ya aina hii?

Nakumbuka Bakwata waliitisha mkutano na waandishi wa habari wakasisitiza hilo na tume ya uchaguzi ilikuwepo.
Ni sawa na somalia. Dini moja, kabila moja, ila koo (clans) ndiyo tofauti.
Udini hautafanya kazi kwani almost 95% siyo tu ni wakristo, bali ni walutheri.
Ukabila hauna nguvu sana as long as wachaga na wanyiramba/warangi hawatahusishwa sana.
Hata NGOs nyingi ni church oriented.
All in all, I hope there will be two young gunners competing ..... and the better one will win.
 
Yangu macho, hungry stomarch + an empyty head sijui unapata nini, ndio nchi yetu ilivyo jamani.
 
Back
Top Bottom